CUF: Sasa ni vita ya kudai katiba mpya na tume huru ya uchaguzi

Rutashubanyuma

JF-Expert Member
Sep 24, 2010
219,470
911,172
UCHAGUZI mkuu uliomalizika mwishoni mwa mwezi wa kumi ulikuwa wa upande mmoja, badala ya ushindani kama ilivyodhaniwa, watawala walitumia mamlaka zake kuibeba CCM ishinde Hili ni tamko la Chama cha Wananchi (CUF) baada ya kufanya tathmini ya uchaguzi mkuu uliomalizika mwishoni mwa mwezi Oktoba katika kikao chake cha baraza kuu la Uongozi

CUF imesema baada ya tahthimini yake, imeona na kuridhika kuwa mazingira ya uchaguzi hayakuwa shirikishi na kwamba vyama vya upinzani vilivyoshiriki uchaguzi, vilifanya hivyo kwa hofu ya kumsusia nguruwe shamba na sio kushinda.

Kufuatia madhaifu na mapungufu mbalimbali yaliyopo chama hicho kimesema bila mabadiliko ya katiba na kupatikana kwa tume huru ya uchaguzi, vyama vya upinzani haviwezi kuishinda CCM na vikiendelea kushiriki katika uchaguzi vitakuwa wasindikizaji.

Akitoa tathmini hiyo kwa gazeti hili Kaimu Naibu Katibu Mkuu wa Chama hicho, Julius Mtatiro aliyekuwa akizungumza kwa niaba ya mwenyekiti wake Profesa Ibrahim Lipumba, anasema Tumeamua kwa dhati kusimama kidete kudai katiba mpya, pamoja na tume huru ya uchaguzi ili tutakaposhiriki uchaguzi mwingine wowote tuweze kushiriki katika mazingira huru yasiyo na upendeleo kwa chama chochote

Anasema kupatikana kwa katiba mpya kutawezesha kuwa na Tume huru ya Uchaguzi na ambayo itatoa fursa kwa vyama vyote kutoa maoni yao hasa wakati wa uchaguzi, maoni anayosema yatasaidia kuondoa kasoro mbalimbali zinazolalamikiwa na vyama vinavyoshiri katika uchaguzi.

Miongoni mwa kasoro zinazolalamikiwa na ambazo CUF imeziainisha ni uwepo wa wasimamizi wote wa uchaguzi, tangu mwenyekiti wa NEC mpaka wasimamizi wa majimbo na kata kuteuliwa na rais ambaye wakati huo huo yeye (rais) na chama chake wanashiriki katika uchaguzi huo.

Anasema kwa vyovyote vile wasimamizi hao hawawezi kwenda kinyume na maagizo watakayopewa mwajiri wao ambaye ni kwa wakati huo anakuwa mshiriki au mgombea na kwamba kwa mazingira hayo uchaguzi hauwezi kuwa huru na vyama vya upinzani haviwezi kuishishinda CCM.

Kauli yao kuhusu matokeo
Anasema mbali na kasoro hizo, tathmini waliyofanya wameridhika pia kuwa kulikuwa na mapungufu makubwa katika suala zima la kufanya majumuisho ya kura za wagombea wake ambapo anasema kura za mgombea urais wake profesa Ibrahim Lipumba ziliibwa na wagombea wake wa ubunge katika majimbo 12 kunyanganywa ushindi wao makusudi.

Kwa idadi ya kura kutoka kwa mawaka wetu, mgombea wa nafasi ya urais kupitia CUF Profesa Ibrahim Lipumba alipata idadi kubwa ya kura kuliko ile iliyotangazwa na mwenyekiti wa uchaguzi. Tulishtuka kusikia wakitangaza eti, Profesa alipata kura laki sita, sio kweli, Profesa alipata kura nyingi, lakini uchakachuaji ule wote uliwezekana kutokana na mapungufu makubwa yaliyopo kutokana na muundo wa Tume ya Tume ya Uchaguzi ambayo imekuwa kiranja wa ukandamizaji anasema Mtatiro.

Anayataja majimbo ya Tandahimba, Mafia, Sumve, Newala, Masasi, Tunduru, Temeke, Tanga Mjini, Lindi, Mchinga, Kondoa Kaskazini na Mtwara Mjini kuwa ni majimbo ambayo wagombea wake waliishinda CCM mpaka dakika ya mwisho lakini hali ilibadilika pale wasimamizi walipokuwa wakitangaza matokeo ambapo anasema, CUF ilishangaa ikitangazwa kushindwa badala ya kushinda.

Matatizo ndio yale yale, msimamizi anamtangaza mtu waliyeelekezwa kumtangaza, sio mshindi, hii ni hatari na ili kumaliza matatizo ya namna hii, na ili kuondoa malalamiko kila unapomalizika uchaguzi wowote, serikali ikubali kufanya mabadiliko ya katika, sambamba na kuruhusu kupatikana kwa tume huru ya uchaguzi.

Mtatiro anasema, CUF imeona kuwa Uchaguzi Mkuu uliokwisha, ulitawaliwa na vitisho vya kila aina kwa washiriki wa uchaguzi, viongozi wa vyama vya siasa na wagombea wa nafasi mbalimbali na anatoa mfano wa wenyeviti wake wawili wa wilaya za Rorya na Meatu ambao walikamatwa wakati wa uchaguzi na mpaka sasa wanashikiliwa na polisi huku wakiwa hawajafunguliwa kesi.

Anasema kauli iliyotolewa na mkuu wa majeshi kupitia mnadhimu wake mkuu Luteni Jenerali Abdulrahman Shimbo ya kuvitaka vyama vya siasa kukubali matokeo baada ya uchaguzi mkuu wa Oktoba na kuonya kwamba vyombo vya ulinzi na usalama vimejiandaa kikamilifu kupambana na yeyote atakayejaribu kuyakataa matokeo ililenga kuwatisha wananchi na vyama vilivyokuwa vikishiriki uchaguzi.

Anasema, hakukuwa na sababu kwa jeshi la wananchi ambalo linayo majukumu ya kulinda nchi na mipaka yake kutoa kauli zile alizoziita za vitisho na kusema Mkuu wa jeshi anaposema amejiandaa kikamilifu kupambana na mtu, watu, kikundi, chama au taasisi yoyote itakayokwenda kinyume na sheria, unategemea nani ataenda kupiga kura, kwa vyovyote ushiriki lazima utakuwa mdogo kutokana na hofu, na ndivyo ilivyokuwa, umeona idadi ya waliojitokeza kupiga kura imekuwa ndogo kulinganisha na ile ambayo walijiandikisha lakini hawakujitokeza.

Maazimio ya CUF
CUF imeazimia kwa kauli moja. ili kukabiliana na mapungufu yaliyojitokeza na ambayo yanaweza kujitokeza katika chaguzi zinazokuja, tuje na kauli mbiu, kwamba tunaanza mapambano ya kudai katiba mpya sasa.

Tunataka na tunahitaji katiba mpya, tunataka tume huru ya uchaguzi ili tuingie kwenye uchaguzi katika mazingira huru na yenye ushindani ulio sawa kwa kila mshiriki na sio mazingira kandamizi yanayopendelea upande mmoja kama ilivyo sasa anasema Mtatiro.

Anasema CUF inaanza kampeni hiyo ya kudai katiba mpya na tume huru ya uchaguzi sasa na kusisitiza kwamba, imani yake ni kufanya kile walichofanya Zanzibar ambapo kwa shinikizo la chama hicho wamefanikiwa kufanya mabadiliko ya katiba na kuwezesha kuunda serikali ya umoja wa Kitaifa iliyokishirikisha chama hicho katika kuunda serikali hali anayosema imeiwezesha Zanzibar kufanya uchaguzi wa amani baada ya kuwa na migogoro na kukosekana kwa amani kwa zaidi ya miaka 15 iliyopita
 
Ninatofautiana na mitazamo ya akina Mzee Mwanakijiji ambao wanakerwa na watanzania wengine kama vile akina Mkpa na wengineo kwa kujitosa kudai katiba mpya. Mimi ninaamini kila Mtanzania atakaposhiriki kwenye zoezi hili litakuwa na manafanikio zaidi kulikoni tukianza kuwabagua baadhi ya wenzetu kutokana na hisia zetu za matendo yao ya awali katika kukwamisha katiba mpya. Wahenga walinena. PENYE WENGI HALIHARIBIKI NENO.
 
CCM: We’re ready for talks on Constitution
Tuesday, 14 December 2010 22:38

By Edward Qorro
The Citizen Reporter
Dar es Salaam. CCM yesterday expressed its willingness to meet with opposition parties and hold “sober” discussions on the Constitution.
However, CCM publicity secretary John Chiligati said the Opposition should come up with concrete proposals as opposed to the current clamour, which he dismissed as “mere political rhetoric”.
He told The Citizen that CCM was ready to have a dialogue with other parties if they pinpointed contentious sections of the Constitution.

“CCM is willing to sit with other parties but they should raise sensible arguments as to why we need to have a new constitution,” Mr Chiligati said by telephone from his Manyoni East Constituency.
He argued that debate on the Constitution should not be guided by public euphoria, but concrete arguments showing why a new set of laws was desirable.
“It is illogical if they are acting on pressure…we need to have a sober debate devoid of vested interests,” he said.

On why CCM was not represented at a forum organised in Dar es Salaam yesterday by the Tanzania Centre for Democracy, Mr Chiligati said he was not in a position to explain the party’s absence from the gathering. “I have been away for several days now, and I’m not sure whether the TCD sent an invitation,” he said.
Speaking during the forum, Registrar of Political Parties John Tendwa said those agitating for a new constitution had a point, but said any debate should be “sensible”.
“It is urgent that we review the whole Constitution and make amendments where necessary…we should leave no stone unturned in attaining this,” he said.

He said, however, that any changes should ultimately be geared at safeguarding national interests.
“We can sit down and brainstorm with one goal in our minds – safeguarding national interests,” Mr Tendwa emphasised. He added that there were some sections of the Constitution that needed to be reviewed such as that which gave the President powers to appoint members of the National Electoral Commission.

Yesterday’s forum brought together 17 political parties, and discussed the push for a new constitution in the wake of mounting pressure on the government by various sections of society.
The Minister for Constitutional Affairs and Justice, Ms Celina Kombani, recently challenged legal experts to come up with tangible arguments as to why it was crucial to overhaul the Constitution.
Several prominent personalities have added their voices to the debate. They include retired President Benjamin Mkapa and Chief Justice Augustino Ramadhani.
Mr Justice Ramadhani said people should be allowed to freely debate as to whether Tanzania needs a new Constitution.

Speaking in Dar es Salaam when launching the Tanzania Network of Legal Aid Providers’ five-year strategic plan for the poor and marginalised in society, the CJ said debate should be encouraged with a view to reaching common ground that would in Tanzania’s best interests.
He said allowing public debate was the best way of handling the matter.

The chairman of the Commission for Human Rights and Good Governance (CHRGG), Mr Justice (rtd) Amir Manento and Tanganyika Law Society (TLS) president Felix Kibodya are other notable personalities who have commented on the clamour for a new constitution.
 
Mabadiliko ya Katiba ni lazima

TOKEA kumalizika kwa Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu mwezi Oktoba, kilio cha kutaka Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kimesikika kwa sauti kubwa zaidi na kilio kinazidi kuenea kila kona ya nchi yetu kikihusisha watu wa kada mbalimbali.

Kilio hiki kwanza kilianzishwa tena na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) ambacho kilidai matokeo ya mgombea wake wa kiti cha urais wa Jamhuri ya Muungano yalichakachuliwa na kikapeleka malalamiko yake Tume ya Uchaguzi lakini hakikusikilizwa.

Chama hicho kikalalamika kwamba Katiba haiwaruhusu kudai haki yao mahakamani ingawa kinao ushahidi kwamba haki hiyo ilipokonywa waziwazi. Ni katika mazingira hayo ambapo wabunge wa chama hicho waliamua kutafuta njia mbadala ya kufikisha malalamiko yao kwa umma wa Watanzania na jumuia ya kimataifa kwa kususia hotuba ya Rais wakati akifungua Bunge.

Tokea hapo kilio kimezidi kupanuka ambapo sasa kimepokewa na majaji wastaafu (mfano Jaji Manento), Jaji Mkuu aliyepo Augustine Ramadhan, Rais mstaafu Benjamin Mkapa, viongozi wa dini, wasomi na wanazuoni mbalimbali, wanaharakati, na wengineo wengi.

Sisi wa Tanzania Daima Jumatano kama sehemu ya Watanzania, tunapenda kuikumbusha serikali kwamba kilio cha Katiba mpya nchini hakikuanza leo. Ni cha muda mrefu ila kilio cha sasa sauti yake imepaa mno.

Tunawashauri viongozi wetu kusikia kilio hiki na kuanzisha mchakato wa Katiba mpya kwa kuwa kunyamaza kwaweza kuleta maafa makubwa. Katiba ambayo mbali na mapungufu yake mengine mengi, haimruhusu raia ama kikundi cha raia wema kudai haki yao kwenye chombo ambacho Katiba hiyo hiyo inakiita chenye kauli ya mwisho kwenye utoaji haki nchini, si Katiba nzuri ya kujivunia na kuendelea kuiwekea viraka.

Ipo siku itatusababisha wote tuingie kwenye maafa na si kiongozi wa serikali ama wa chama tawala ama raia wa kawaida atapona. Tuepusheni na nusu shari kabla ya shari kamili.

Tungependa kuwashauri viongozi, kutopuuzia madai hayo ili kuepuka kile kilichotokea kwa jirani zetu wa Kenya wakati wa kudai Katiba au katika nchi zingine barani Afrika ambako watawala hawakupenda mabadiliko ya Katiba.
 
Katiba mpya Tanzania sasa haikwepeki-Tendwa


Na Tumaini Makene

WAKATI madai ya kuwepo kwa haja ya Tanzania kuwa na katiba mpya yakizidi kushika kasi kila kukicha kutoka kwa watu na makundi mbalimbali ndani ya jamii nchini, Msajili wa Vyama vya Siasa, Bw. John Tendwa naye ameweka bayana kuwa suala hilo
sasa halikwepeki.

Akizungumza na waandishi wa habari jana Dar es Salaam, mara baada ya kufungua mjadala uliokuwa na mada isemayo 'Je kuna umuhimu wa kuangalia upya Katiba ya Jamhuri ya Muungano?" ulioandaliwa na Kituo cha Demokrasia (TCD), Bw. Tendwa alisema "lini tutaanza kuongea ukweli...tusidanganyane kuwa hatuna matatizo...kwa nini tuseme mfalme yuko sawa wakati hajavaa nguo...hili halina ubishi...lakini liweje."

Bw. Tendwa ambaye kitaaluma ni mwanasheria, alisema kuwa madai ya katiba mpya isiyokuwa na ladha ya chama kimoja, ni kilio cha wadau wa demokrasia vikiwemo vyama vya siasa kwa muda mrefu sasa, tangu wakati ukiundwa mfumo wa vyama vingi nchini.

Alisema kinachotakiwa sasa ni kwa wadau hao ni kuyawasilisha madai hayo katika mfumo unaotakiwa ili yachukue mkondo wa kisheria, mathalani vyama vya siasa kulifikisha katika Baraza la Vyama ambalo linatambulika kisheria na serikali, ili yafanyiwe kazi.

"Watu wanataka mabadiliko ya katiba...ni kilio cha muda mrefu cha vyama vya siasa, kilianzia katika 'pressure groups' miaka ya tisini hata wakati tunaanza mfumo wa vyama vingi tayari kulikuwa na kilio cha watu kutaka katiba mpya isiyokuwa na ladha ya chama kimoja, karibu miaka 20 sasa kilio hiki kipo."Wenzetu Kenya wamekuwa na tatizo hilo la kuwa na msukumo wa katiba mpya...sisi pia tuna matatizo mengi katika nyanja nyingi, tusidanganyane kuwa hatuna matatizo...kama mmemsoma jana Jaji Kisanga nami ningependa kumnukuu alisema kuwa Serikali inapaswa kusikiliza kilio hiki cha wananchi isipofanya hivyo itajuta baadae.

"Hapa leo tuna-brainstorm (kujadili) tu, hakuna ubishi wa hilo, lakini liweje, huu si ndiyo wakati wake sasa...lakini hawa wanapaswa kulipeleka katika Baraza la Ushauri la Vyama vya Siasa ambalo ndilo litapeleka serikalini kisheria...suala hili likija officially (rasmi) lina mkondo wake," alisema Bw. Tendwa.

Naye Profesa Ibrahim Lipumba, ambaye alikuwa mwenyekiti wa mjadala huo kwa niaba ya Bw. Freeman Mbowe, alisema kuwa upo umuhimu sasa wa taifa kuwa na katiba iliyotokana na mapendekezo ya watu, ikiwa na misingi imara inayokubalika katika jamii nzima kwa mustakabali wa nchi yao.

Alisema kuwa katiba ya sasa iliandikwa 'kwa haraka haraka na kikundi cha watu wachache waliopewa kazi hiyo baada ya kuonekana wamefanya kazi nyingine vizuri ya kuunganisha vyama vya TANU na ASP, ili kupata Chama Cha Mapinduzi, ambapo katiba hiyo ilitumika kuweka hatamu za uongozi wa nchi ziliwekwa mikononi mwa chama hicho, badala ya kuwekwa kwa wananchi kupitia chombo kama vile bunge.

"Katiba hii iliyo na viraka karibu kumi na tano, ilikuwa katiba ya chama kushika hatamu za uongozi wa nchi, ambapo bunge halina mamlaka bali chama...Jaji Nyalali aliweka wazi mapema mapendekezo ya kuwa na katiba mpya, pendekezo hilo lilikataliwa, Jaji Kisanga pia katika tume yake ya White Paper, alieleza hilo, lakini likakataliwa.

"Tunataka katiba mpya inayotokana na mapendekezo ya watu, kwa kuwashirikisha wananchi, yenye misingi imara ya kidemokrasia kama vile masuala ya wagombea binafsi, haki za binadamu ziwekwe kisheria si jumla jumla tu," alisema Prof. Lipumba.Akiwasilisha mada ya uchokozi katika mjadala huo, mara baada ya kufunguliwa, Mwanasheria kutoka Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) Bw. Harlod Sungusia, alisema kuwa katiba ya sasa ina kasoro nyingi ambazo zinatia dosari nchi na kulifanya taifa kukosa dira ya wapi linaelekea.

"Nikianza mada yangu ya uchokozi kwa kumnukuu Rais Mstaafu Mkapa aliyesema hivi karibuni kuwa katiba ni moyo wa Taifa sawa na moyo katika mwili wa binadamu, sasa unaweza kujiuliza huu moyo wetu wa Taifa la Tanzania wenye viraka na matundu namna hii...maana yake Taifa litakuwa linaumwa sana kwa sababu moyo wake hauko sawa. Kama wagonjwa wa moyo wanapelekwa India kwa ajili ya upasuaji, taifa litapelekwa wapi kupasuliwa.

"Katiba hii ya mwaka 1977 iliyopo sasa pamoja na ubovu wake lakini bado imejaa viraka, mpaka sasa imefanyiwa marekebisho mara kumi na nne...ni katiba ambayo unashindwa kuelewa inamilikiwa na nani, maana wananchi hawakuwahi kushirikishwa katika mchakato wa kupatikana kwake...kwa uhakika katiba zote kuanzia ile ya mwaka 1961, 1992, 1964, 1965 na hii ya sasa ya mwaka 1977 wananchi hawajawahi kushirikishwa.

Huku akiweka bayana matatizo mengi yaliyoko katika ibara na vifungu, aliainisha maeneo kadhaa yanayotia kasoro katiba ya sasa kuwa ni pamoja na historia ya mchakato wake, umiliki, kutoweka bayana utaratibu wa kuibadilisha, uhusiano wake (hadhi yake) dhidi ya sheria zingine, uhusiano wake na Katiba ya Zanzibar na pia kutotoa dira ya taifa, ambapo bado inazungumza "Tanzania ni nchi ya kijamaa."Wakichangia katika mjadala huo, viongozi waandamizi wa vyama mbalimbali waliokuwepo, kila mmoja alionesha wazi umuhimu wa nchi kuwa na katiba mpya, huku wengine wakitoa mfano wa nchi ya Kenya, kuonya kuwa gharama za kutokuwa nayo zinaweza kuwa kubwa zaidi, zikiligharimu taifa.

Bw. John Cheyo ambaye ni Mwenyekiti wa Chama cha United Democtratic Party (UDP), alisema haja ya kuwa na katiba mpya i wazi, ambapo masuala mengi yanapaswa kufanyiwa kazi kama vile mfumo wa uchaguzi, kushirikisha wananchi katika utungaji "tunagalie upande wa pili wa shilingi, kutokuwa na katiba mpya gharama yake ni kubwa mno, hakuna jambo la kuogopa kudai katiba mpya, twende kwa wananchi kuwahamasisha wadai."

Naye Peter Mziray wa APPT-Maendeleo, alisema kuwa katiba iliyopo si wananchi, hivyo mchakato rasmi wa kudai mabadiliko ya wananchi uanze 'leo leo' kwa kukusanya majina ya ili papatikane mahali pa kuanzia.Bw. Benson Kigaila wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) alisema kuwa kuna ulazima wa TCD, ambacho ni chombo kwa ajili ya vyama vyenye wabunge, kuitisha kongamano kuwahusisha wadau wengine zaidi ili kupanua wigo wa madai hayo ya muda mrefu.

Pamoja na mjadala huo kuhudhuriwa na vyama vya siasa mbalimbali, bado hoja ya kuwa na katiba mpya ilionekana kutawala kwa kila aliyeinuka kuzungumza ingawa kulikuwa na tofauti kadhaa za njia zipi zitumike kulisukuma jambo hilo kwenda hatua iliyopo sasa ya kudai katika makongamano na mijadala, kwa takribani miaka 20 sasa.
 
CUF wapo madarakani, katiba mpya ya nini kwao? Ni vyema wangeungana na CCM kuzuia uundwaji wa katiba mpya, vinginevyo watanyang'anywa hata hiyo nafasi ya Makamu wa kwanza wa Rais Znz!
 
“UCHAGUZI mkuu uliomalizika mwishoni mwa mwezi wa kumi ulikuwa wa upande mmoja, badala ya ushindani kama ilivyodhaniwa, watawala walitumia mamlaka zake kuibeba CCM ishinde” Hili ni tamko la Chama cha Wananchi (CUF) baada ya kufanya tathmini ya uchaguzi mkuu uliomalizika mwishoni mwa mwezi Oktoba katika kikao chake cha baraza kuu la Uongozi
CUF imesema baada ya tahthimini yake, imeona na kuridhika kuwa mazingira ya uchaguzi hayakuwa shirikishi na kwamba vyama vya upinzani vilivyoshiriki uchaguzi, vilifanya hivyo kwa hofu ya kumsusia nguruwe shamba na sio kushinda.

Nimequote kifungu hiki hapa juu kwa kuwa kinabeba ujumbe wote. Ila naaimi dhamira ilimsuta Prof Lipumba na ndio maana hakuthubutu kuwasomea waandishi maazimio haya na kumtuma Mtatiro.

Swala la kwamba uchaguzi ulikuwa wa upande mmoja...

1. .Je ALIPOENDA KIMBELEMBELE KUMPONGEZA JK kwa ushindi alilijua hili?

2. Kama alilijua kuwa yeye hakuwa mshindani kwa nini aliwekwenda?

3. Kwa nii sasa yeye na KUB aliyepita wamesimama na kuishambulia CHADEMA kwa kuitoyatambua matokeo wanayosema ni ya tume na washirika walioteuliwa na JK?

4. Je, uchu wa madaraka ndio unamfanya Lipumba atamani serekali yaumoja wa kitaifa huku Bara?

Although it is too late, lakini imesaidia kuonyesha kuwa "CUF is consistent kwa wasichokifahamu" na kwamba wananchi tayari tumewajua kuwa ni WANAFIKI na WAROHO wa MADARAKA?

Nisaidieni

 
CUF wapo madarakani, katiba mpya ya nini kwao? Ni vyema wangeungana na CCM kuzuia uundwaji wa katiba mpya, vinginevyo watanyang'anywa hata hiyo nafasi ya Makamu wa kwanza wa Rais Znz!


CCM: We're ready for talks on Constitution
Tuesday, 14 December 2010 22:38

By Edward Qorro
The Citizen Reporter
Dar es Salaam. CCM yesterday expressed its willingness to meet with opposition parties and hold "sober" discussions on the Constitution.
However, CCM publicity secretary John Chiligati said the Opposition should come up with concrete proposals as opposed to the current clamour, which he dismissed as "mere political rhetoric".
He told The Citizen that CCM was ready to have a dialogue with other parties if they pinpointed contentious sections of the Constitution.

"CCM is willing to sit with other parties but they should raise sensible arguments as to why we need to have a new constitution," Mr Chiligati said by telephone from his Manyoni East Constituency.
He argued that debate on the Constitution should not be guided by public euphoria, but concrete arguments showing why a new set of laws was desirable.
"It is illogical if they are acting on pressure…we need to have a sober debate devoid of vested interests," he said.

Hivi hizi kauli kuwa CCM hawataki katiba mpya zinatoka wapi?................jamani tuzisome hizi habari kwa uangalifu mkubwa.............
 
Tatizo ni kwamba watu wanataka katiba mpya kweli ina nina wasiwasi mkubwa na baadhi ya wajanja na wahuni wachache wanataka kuingiza hili na kuichakachua na kuingiza vitu vya maslahi yao
 
Swala la kwamba uchaguzi ulikuwa wa upande mmoja...

1. .Je ALIPOENDA KIMBELEMBELE KUMPONGEZA JK kwa ushindi alilijua hili?

2. Kama alilijua kuwa yeye hakuwa mshindani kwa nini aliwekwenda?

3. Kwa nii sasa yeye na KUB aliyepita wamesimama na kuishambulia CHADEMA kwa kuitoyatambua matokeo wanayosema ni ya tume na washirika walioteuliwa na JK?

4. Je, uchu wa madaraka ndio unamfanya Lipumba atamani serekali yaumoja wa kitaifa huku Bara?

Although it is too late, lakini imesaidia kuonyesha kuwa "CUF is consistent kwa wasichokifahamu" na kwamba wananchi tayari tumewajua kuwa ni WANAFIKI na WAROHO wa MADARAKA?

Nisaidieni

Suala la Katiba Mpya si la mtu mmoja mmoja kupimwa kwa kile alichokifanya au alishindwa kukifanya................ni letu sote na la vizazi vijavyo..........................tusipoteze mwelekeo kwa kuwakuza watu hao wachache......................
 
ni swala la uamuzi tu,hakuna kinachoshindikana ktk hii tanzania,namshangaa sana mama buriani yeye hujibu kuwa serikali haina pesa kuandaa katiba mpya,nadhani hajui alisemalo labda wanahitaji nguvu ya wananchi ili waweze kutimiza tuyatakayo
umefika wakati sasa wa kufanya maamuzi yatakayo tuweka huru daima
katiba mpya ni kila kitu kwetu watanzani,tusirudi nyuma kwa hili

mapinduzii daimaaaa
 
Mabadiliko ya Katiba hayaepukiki
ban.kijiji.jpg

M. M. Mwanakijiji

amka2.gif
Ukiondoa maneno kama "uchakachuaji" na "tume ya uchaguzi" maneno ambayo yatakuwa yanajirudia rudia tena na kuanza kukera watu yatakuwa ni "Katiba Mpya". Hakuna wakati ambapo hoja ya "Katiba Mpya" inarudi kwa nguvu zaidi kuliko wakati huu unaofuatia uchaguzi kwani kwa upande mmoja haja ya kuwa na Katiba hiyo mpya imemulikwa kama taa kubwa ya usiku na kila mtu anaanza kuona. Hata hivyo nina uhakika mkubwa kuwa kwa wale wasiojua Katiba au ambao hawajawahi kukaa chini na kuisoma Katiba ya nchi yao wanaweza wasijue mambo fulani fulani ambayo hayaingii akilini na kwa pamoja yake yanapaza sauti kuita "tunahitaji Katiba Mpya".
Katika ukorofi wangu na uchokozi wa hoja naomba nidokeze kidogo juu ya mambo yafuatayo ili kuonesha kuwa Katiba yetu ilivyo sasa ina vipengele vya ajabu ambavyo haviwezi kuondoka kwa kuombea au kupuuzia bali kwa kukaa chini na kuvifungia kazi kuviondoa aidha kwa mabadiliko makubwa ya katiba au kwa kuamua kuandika upya Katiba yetu. Naomba nitaje mambo machache ambayo mengine nimeyajadili kwa kina kwenye mtandao wa Jamiiforums.com.
1. Rais Kikwete angekuwa mgombea pekee wa Urais bado angepigiwa kura na Watanzania wote?
Sijui kama unajua kwamba kama vyama vingine vyote visingesimamisha wagombea wa Urais kama kina Slaa na Lipumba na kumuacha mgombea wa CCM Dr. Kikwete bado Watanzania wangempigia kura kama tulivyofanya wakati wa chama kimoja?
Kwamba baada ya CCM kupata mgombea wake wa Urais na vyama vingine kwa sababu moja au nyingine kushindwa kusimamisha wagombea Tume ya Uchaguzi isingemtangaza Kikwete kuwa ni "Rais" bali ingeliweka jina lake kwenye karatasi za kura na wapiga kura wangetakiwa kupiga kura ya "Ndiyo" au "Hapana"?
Kama ulikuwa hujui basi habari ndiyo hiyo. Katiba yetu na sheria yetu ya uchaguzi inaweka utaratibu wazi kuwa endapo mgombea wa Urais atakuwa ni mmoja tu bado atapigiwa kura na wapiga kura kwa mtindo wa "ndiyo" au "hapana". Yaani hawezi kuwa Rais kwa kupitishwa tu na chama chake kuwa mgombea?
Kama tungekuwa na utaratibu wa Rais akikosa wapinzani basi anakuwa ni Rais bila haja ya kupigiwa kura unafikiri ni kiasi gani kingetumika kushawishi wagombea wengine wasijitokeze au kurudisha fomu ili mgombea wa chama kimoja abakie peke yake na kisha atangazwe kuwa ni Rais bila kuwapa wananchi nafasi ya kumkubali au kumkataa?
2. Wagombea wasio na wapinzani wanatangazwa ni wabunge bila kupigiwa kura yoyote?
Katiba hiyo hiyo inayosema kuwa mgombea wa Urais ambaye hana mpinzani bado atapigiwa kura ya "ndiyo" au "hapana" inanyima fursa hiyo kwa majimbo ambayo wagombea wake wamejikuta hawana wapinzani? Katika majimbo hayo sheria hiyo ya ajabu inasema ati kwa vile mtu hana mpinzani hadi siku ya mwisho ya kurudisha fomu basi mgombea huyo pekee "ataonekana kuwa amechaguliwa".
Yaani, kura za maoni za watu wa chama kimoja zinahesabikuwa kuwa ni kuchaguliwa na watu wote! Wamarekani wanasema "go figure" - nenda ukafikirie! Hii ina maana gani? Mgombea wa Ubunge au chama chake kinaweza kujitahidi kuzuia wagombea wengine wasiingie kwenye kinyang'anyiro kwa sababu wanajua dakika ya mwisho wakikosekana wagombea wengine basi mtu wao atakuwa amepita "bila kupingwa".
Ukiwauliza amepita vipi bila kupingwa wakati hakuna mwananchi hata mmoja aliyepewa nafasi ya kupinga kwenye sanduku la kura wanasema "ndiyo sheria ilivyo". Mfano mzuri ni Jimbo la Nyamagana. Mgombea wake baada ya kukosa mpinzani alijua tayari kapita "bila kupingwa" lakini aliporudishwa yule mgombea wa chama kingine mgombea wa chama tawala akaangushwa na wananchi waliopewa nafasi ya kupinga!
Je, majimbo mengine ambayo wananchi wake hawakupewa nafasi ya kumchagua Mbunge wake na badala yake kupewa mbunge kwa mtindo wa "kupita bila kupingwa" haki yao ya kuchagua mbunge wao itatetewa na nani?
3. Je umewahi kujiuliza ni nani anamuapisha Spika na kwanini?
Sote tunajua kuwa Rais huapa mbele ya Jaji Mkuu ndivyo katiba inavyotaka na Jaji Mkuu huapa mbele ya Rais. Lakini Spika wa Jamhuri ya Muungano anaapa mbele ya Katibu wa Bunge. Rais wa Muungano na hata yule wa Zanzibar wote wanaapishwa na Majaji wakuu na Majaji Wakuu nao wanaapishwa na Marais. Lakini linapokuja suala la Spika anaapa mbele ya Katibu wa Bunge kwa nini?
Yumkini ni kweli kuwa Spika wa Bunge si mkuu wa Mhimili kama ilivyo kwa Rais na Jaji Mkuu? Wenye hoja hii wanatudokeza (kama wengi tulivyosikia kufuatia sakata la wabunge wa CHADEMA kutoka Bungeni) kuwa "Rais ni sehemu ya Bunge kwa mujibu wa Katiba".
Kama hili ni kweli Spika anaweza vipi kuwa mkuu wa Mhimili wa Bunge wakati Mhimili huo unamhusisha Rais ambaye ni Mkuu wa Mhimili mwingine? Kama Rais ni sehemu ya Bunge kama Katiba inavyosema basi Spika hawezi kinadharia kuwa Mkuu wa Bunge kwani atakuwa ni Mkuu wa Rais ambaye ni Mkuu wa Utendaji.
Sasa, kama Spika si Mkuu wa Bunge na ni msimamizi wa mikutano ya Bunge tu na mijadala ya Bunge kama baadhi ya watu wanavyofikiri basi Bunge letu bado halijawa mhimili unaojitegemea nje ya Mhimili wa Urais. Kwa maneno mengine, kwa kadiri ya kwamba Rais ni sehemu ya Bunge basi Bunge SIYO mhimili wa mwingine wa serikali. Labda tuliweke hivi; kama Katiba ingesema Mahakama ina sehemu mbili na sehemu yake mojawapo ni Rais tunaweza kusema kuwa Mahakama hiyo itakuwa ni huru kutoka madaraka ya Rais? Hili linaonekana katika kuapishwa kwa sababu kama Wakuu wa Mihimili ya Mahakama na Utendaji wanaapa kwa nguvu iliyosawa nao (Jaji Mkuu kwa Rais, na Rais kwa Jaji Mkuu) kwanini Spika ambaye kimsingi ukifikiria anawajibu mkubwa tofauti kabisa na wa Rais na Jaji Mkuu aapishwe na Katibu tu wa Bunge ambaye yeye mwenyewe ni mtumishi tu.
Lakini labda cha kutukoroga zaidi ni kuwa Kanuni za Bunge (25:2) zinatuambia kuwa "Mbunge yeyote aliyechaguliwa kuwa Spika kabla ya kushika madaraka yake, ataapa Kiapo cha Spika mbele ya Bunge. Lakini endapo atachaguliwa Spika ambaye siyo Mbunge, basi ataapa Kiapo cha uaminifu kwanza kabla ya kuapa Kiapo cha Spika."
Kumbe utaratibu wa Bunge wenyewe hausemi kama Katibu ndiyo asimame kushuhudia kuapishwa kwa Spika (labda kama kuna mabadiliko ya kanuni hiyo). Kwa maneno mengine mama Anna Makinda alipochaguliwa kuwa Spika alitakiwa kusimama mbele ya wabunge na kuapa yeye mwenyewe.
Hili nalo lingetuletea matatizo kwanini Rais aapishwwe mbele ya Jaji Mkuu na asingesimama na kuapa tu mbele ya Watanzania? Au kwanini Jaji Mkuu aape mbele ya Rais badala ya kuapa tu mbele ya Watanzania?
4. Je unajua mgombea anayehisi kuonewa kwenye Ubunge au Udiwani anaweza kwenda mahakamani lakini wa urais hawezi?
Nadhani hili hapa sasa hivi kila mtu anajua. Kuwa kama mtu ni mgombea wa udiwani au Ubunge anayehisi kutotendewa haki katika kuhesabu kura au kutangazwa mshindi anaweza kwenda mahakamani na kudai haki yake na ushindi wa aliyeshinda unaweza kutenguliwa?
Hili linajulikana siyo kinadharia bali kihistoria kwani tumeshawahi kuwa na wabunge ambao Ubunge wao ulitenguliwa baada ya ushahidi kuonekana haukuwa wa haki. Kuanzia mwaka 1995 katika mfumo wa vyama vingi tuna wabunge waliopoteza viti vyao baada ya mahakama kuona kuwa hawakuingia madarakani kihalali.
Lakini cha kushangaza ni kuwa Katiba hiyo hiyo inayotambua "haki" za waliodhulumiwa katika Ubunge na Udiwani kudai mahakamani inakataza waliodhulumiwa katika Urais kuhoji mahakamani au kwenye "chombo kingine chochote". Kwa maneno mengine, hata mgombea wa Urais akiingia kwa mbinde na kwa upinde na akatangazwa kuwa ni Rais huku kuhesabu kura kwake kukiwa na matatizo au kutangaza matokeo kukawa kwa matatizo lakini akishatangazwa hakuna namna yoyote ya kupinga na kuwa utaratibu umeweekwa kuwa akitangazwa tu basi ndani ya siku saba lazima aapishwe na hivyo kuondoa uwezekano wowote wa mtu kuandaa kesi yoyote ya kupinga ushindi huo.
Hapa mtu mwenye uwezo wa kufikiria atajiuliza kama aliyedhulumiwa Ubunge na Udiwani anaweza kupinga na akashinda mahakamani kwanini aliyegombea Urais hawekewi utaratibu wa kulalamika ushindi wa aliyetangazwa na kupewa nafasi ya kuleta ushahidi wake mahakamani?
Kwenye nchi inayodai kuwa inataka kujenga jamii yenye "haki" hivi hawa wanaoonekana kudhulumiwa kwenye kura za Urais walalamike wapi? Ndio maana binafsi nachukulia kitendo cha Wabunge wa CHADEMA kutoka ukumbini kuwa ni kitendo kidogo sana wala hakihitaji watu kuruka roho zao wala kumuudhi rais bali kukubali tu kuwa ndio njia pekee ya wao kuonesha malalamiko yao.
Sielewi kwanini watu wengine wamekwazika kiasi cha wengine kuanza kumfikiria Rais wa Tanzania kama "baba" yao! Jamani hii ni demokrasia na wakati mwingine demokrasia inakera na kuudhi.
Tujifunze kuvumilia demokrasia na gharama yake. CHADEMA wangeweza kumzomea, wangeweza kupiga kelele, wangeweza kujilaza ukumbini pale, au wangeweza kusimama nje na mabango pale Bungeni yenye maneno ya kila namna lakini wakaamua kutoka nje kwa heshima, bila kunyosha vidole, bila kumtukana mtu na kilichonifurahisha ni kuwa wabunge wa CCM wakazomea na kuguna wengine lakini hakuna mtu anayeona kitendo chao ni cha kukosa heshima kwa wabunge wenzao.
Lakini walichofanya ni kuinuka na kutoka ukumbini na kama Waziri Mkuu alivyosema yawezekana wabunge hao walikuwa wanaangalia hotuba ya Rais kwenye runinga. Kama hilo ni kweli, kwa nini watu wengine wamekwazika kiasi cha wengine kukasirika kabisa!
Wabunge hao wamefanya walichofanya kutuma ujumbe wao juu ya ubovu wa tume ya uchaguzi na tatizo la Kikatiba, watu wanazungumzia suala la Katiba na nilitegemea viongozi wa serikali badala ya kuanza kupiga mikwara wangesema tu kuwa wako tayari kusikiliza manung'uniko ya CHADEMA na jambo hilo lingeisha. Kwa sababu hakuna kitendo cha kumkataa kumtambua Rais au kukataa kutambua matokeo ya Urais ambacho kinabadiliki kuwa Kikwete ni Rais.
Hivyo, tuangalie suala hili kuwa ni la kidemokrasia na binafsi sitashtuka huko mbeleni wabunge wengine wakitoka wakiona hawajaridhishwa na jambo fulani.
Tunataka demokrasia, tuwe tayari kuishi nayo! Isiwe ni demokrasia ya kwenda kupiga kura tu lakini bila kujali matokeo yake!
5. Je unajua Waziri Mkuu akijiuzulu au kufa Baraza la Mawaziri nalo linavunjika japo yeye hakuliunda?
Mojawapo ya maajabu ya mfumo wetu ni kuwa Baraza la Mawaziri linaundwa na Rais baada ya kushauriana na Waziri Mkuu. Mawaziri hao hata hivyo hawali kiapo chochote mbele ya Waziri Mkuu isipokuwa wanaapa kwa Rais.
Kwa maneno mengine mawaziri wote na manaibu wao kihaki kabisa wako chini ya Rais na si chini ya Waziri Mkuu japo kiutendaji wanaweza kupokea maagizo toka kwa Waziri Mkuu. Lakini Waziri Mkuu hawezi kumfukuza Waziri au Naibu Waziri hata mmoja.
Lakini cha kushangaza ni kuwa Waziri Mkuu akijiuzulu na baraza la mawaziri linavunjika na vile vile Waziri Mkuu akifa baraza la Mawaziri nalo linavunjika.
Lakini kwanini linavunjika wakati yeye hakuliunda. Nchi nyingine baada ya Waziri Mkuu kuteuliwa na Rais na kuapishwa yeye ndiyo aidha anunda baraza la mawaziri au anapendekeza majina ya baraza la mawaziri kwa Rais ambaye anaweza kuyakubali.
Katika mifumo hiyo ni wazi kuwa Waziri Mkuu na baraza lake nalo ni kwishnei.
Lakini katika mfumo wetu Waziri wetu mkuu haundi wala kupendekeza baraza la mawaziri sasa kwanini livunjike kama Waziri Mkuu ndiye mwenye makosa?
Kuwakumbusha vizuri ni kuwa Waziri Mkuu Lowassa alipojiuzulu na kukubaliwa basi baraza la Mawaziri lisingeweza kuendelea kuwepo.
Ndio maana tuliwasahihisha wale waliotangaza kuwa "Rais kavunja baraza la Mawaziri kufuatia kujiuzulu kwa Lowassa". Ukweli ni kuwa Rais hakuvunja baraza lile bali lilivunjika automatically baada ya kukubaliwa kujiuzulu kwa Lowassa.
Je ulijua na hilo?
Kwa ufupi ni maswali hayo machache naomba tuyafikirie na tujiulize kama kweli tunahitaji Katiba mpya au la. Yapo na maswali mwengine vile vile ambayo tunaweza kujiuliza. Yapo maswali yanayohusu Zanzibar na viongozi wake na yapo maswali yanayohusu masuala ya dini na imani na Katiba yetu.
Yapo maswali yanayohusu mamlaka mbalimbali ya Rais na viongozi wengine na yapo maswali yanayohusu Bunge na wabunge. Tukianza kuyauliza yote hapa wengine tunaweza kuitwa "wachochezi, wasaliti na wanaotaka kuligawa taifa letu". Lakini, ni mwanadamu ambaye hataki kutumia ubongo wake kufikiri?
Kama hatia basi itakuwa ni hii ya kuwafanya watu wafikiri hatia ambayo tunasema tunaikubali. Tutaendelea kuwafanya watu wetu wafikiri nje ya kawaida. Kwani tayari mapambano ya kifikra tuliyoyaasisi miaka mitano iliyopita yanasimama kama ushahidi wa mwamko mpya wa taifa.
 
4. Je unajua mgombea anayehisi kuonewa kwenye Ubunge au Udiwani anaweza kwenda mahakamani lakini wa urais hawezi?
Nadhani hili hapa sasa hivi kila mtu anajua. Kuwa kama mtu ni mgombea wa udiwani au Ubunge anayehisi kutotendewa haki katika kuhesabu kura au kutangazwa mshindi anaweza kwenda mahakamani na kudai haki yake na ushindi wa aliyeshinda unaweza kutenguliwa?
Mwaka 1995 Mrema na wenzie walienda Mahakama Kuu kupinga Mkapa kutangazwa kuwa Raisi na Mahakama hiyo ilisema penye ushahidi wa ya kuwa NEC haikufuata sheria ya uchaguzi katika kumtangaza Raisi kama Ibara Na. 41 (5) inavyoelekeza Mahakama kamwe haitafumbia macho kutokana na maangalizo ya Ibara Na. 41 (7).........................

Mnaposhauri jamii muwe mnajishughulisha kujisomea somea hata hizi hukumu vinginevyo mtakuwa mnaipotosha jamii...........................
 
Haki ya kupiga
kura
Sheria ya 1984
Na.15 ib.6
Sheria ya 2000
Na.3 ib.4​
5​
.-(1) Kila raia wa Tanzania aliyetimiza umri wa miaka
kumi na minane anayo haki ya kupiga kura katika uchaguzi
unaofaywa Tanzania na wananchi. Na haki hii itatumiwa kwa
kufuata masharti ya ibara ndogo ya (2) pamoja na masharti
mengineyo ya Katiba hii na ya Sheria inayotumika nchini
Tanzania kuhusu mambo ya uchaguzi.
(2) Bunge laweza kutunga sheria na kuweka masharti
yanayoweza kuzuia raia asitumie haki ya kupiga kura kutokana
na yoyote kati ya sababu zifuatazo, yaani raia huyo-
(a) kuwa na uraia wa nchi nyingine;
(b) kuwa na ugonjwa wa akili;
(c) kutiwa hatiani kwa makosa fulani ya jinai;
(d) kukosa au kushindwa kuthibitisha au kutoa
kitambulisho cha umri, uraia au uandikishwaji kama
mpiga kura,
mbali na sababu hizo hakuna sababu nyingine yoyote
inayoweza kumzuia raia asitumie haki ya kupiga kura.
(3) Bunge litatunga Sheria ya Uchaguzi na kuweka
masharti kuhusu mambo yafuatayo-
(a) kuanzisha Daftari la Kudumu la Wapiga kura na
kuweka utaratibu wa kurekebisha yaliyomo katika
Daftari hilo;
(b) kutaja sehemu na nyakati za kuandikisha wapiga
kura na kupiga kura;
(c) utaratibu wa kumwezesha mpiga kura
aliyejiandikisha sehemu moja kupiga kura sehemu
nyingine na kutaja masharti ya utekelezaji wa
utaratibu huo;
(d) kutaja kazi na shughuli za Tume ya Uchaguzi na
utaratibu wa kila uchaguzi ambao utaendeshwa
chini ya uongozi na usimamizi wa Tume ya Uchaguzi.

je hiyo katiba iliyopo inatekelezwa hilo lililotiwa kivuli limefanyika?

 
Hivi hizi kauli kuwa CCM hawataki katiba mpya zinatoka wapi?................jamani tuzisome hizi habari kwa uangalifu mkubwa.............

Mkuu,

Vuguvugu la katiba mpya ..sasa lapamba moto na CCM wanajaribu kumwagilia maji ili lizimike.

Kwa CCM na wanaCCM kusema wanaunga mkono katiba mpya ni sawa na kuwakejeli waTZ. Wanachokifanya sasa hivi kuja mmoja mmoja kusema kuwa wao pia wanataka mabadiliko, wanaafiki katiba mpya, wanaposema ya katiba mpya yanazungumzika and then kesho yake wanasema Mapinduzi daima!! Au hakuna hela ya kuanzia mchakato, au tutatia viraka inapobidi…nk ni kuwakejeli WaTZ.

CCM wanachofanya ni kuuteka nyara mjadala wa Katiba mpya. Na kujaribu ku-buy time ili siku zisonge mbele hadi 2015. Ikifika 2013, watasema muda sasa hautoshi, tutashughulikia hili la katiba mpya baada ya uchaguzi mkuu wa 2015.

CCM wanajaribu kuupiga dana dana kwa ustadi mkubwa huu mjadala wa katiba mpya na sisi wengine tunaanza ku-sympathise nao. Propanganda kwa CCM ni kitu wanachokijuwa kwa uzuri sana. Be aware, they are hypnotizing us.

Kama wana ujasiri CCM wanaweza kupeleka hoja bungeni kwa haraka, au kama kweli wanaitakia nchi hii iendelee kuwa na amani na utulivu, kwa maslahi ya Taifa, baada ya madudu yaliyofanyika katika uchaguzi huu hawakuwa na sababu ya kusubiri waambiwe kuwa tunahitaji katiba mpya au mabadiliko ya maana ya tume ya uchaguzi na sheria za uchaguzi. Wangeonesha kwa vitendo na siyo kauli kuwa wanaunga mkono. Wao ndio wanaoendesha wizaya ya sheria na mambo ya katiba, wao ndio wenye wabunge wengi kama wana nia njema na nchi hili la katiba hawawezi kulifanyia utani.

Wangeshauriana na kukubaliana na vyama vilivyowasindikiza katika uchaguzi wa 2010 na wadau wengine na siyo kusubiri wasukumwe.

Pia wanaibuka mjadala ,jee inayohitajika ni katiba mpya au mabadiliko ya katiba kukidhi tume huru na sheria za uchaguzi?
 
CUF wapo madarakani, katiba mpya ya nini kwao? Ni vyema wangeungana na CCM kuzuia uundwaji wa katiba mpya, vinginevyo watanyang'anywa hata hiyo nafasi ya Makamu wa kwanza wa Rais Znz!
Wewe usiwe conservative kiasi hicho. Hebu angalia mawzo waliyosema kama ni ya msingi tuungane nao kuliko kumuattack mtu hata km anatoa mawazo ya kujenga. Usitake kufanya suala la kudai Katiba mpya ni la chama fulani au mtu fulani. Hili ni la kila Mtz mpenda mabadiliko. Hata Mkapa alipoliunga mkono tumempongeza. Usikae kukosoa hata yale mambo ya msingi, otherwise wewe umekaa hapa labda kutofautiana na watu kwa kila jambo.
 
Hii ni kauli ya Mtatiro au ya Chama? kama ni ya chama kwa nini Mwenyekiti wa CUF ambaye alikuwa mgombea hakuwahi kuhoji chochote kinachohusiana na kura alizopata? haya majimbo waliyonyimwa ushindi wamefungua kesi mahakamani au wamekubaliana na aliyetangazwa mshindi?
 
Ruta.
Nikupongeze kwa jitihada zako ambazo unazifanya. Mimi maoni yangu ni kuwa jambo hili tulisukume bila kuwa na tashwishi za kisiasa. Kila mtanzania mzalendo ashirikishwe katika mjadala huu. Watu binasfi kama tunavyoona, asasi za kiraia, vyama, na mashirika yasiyo ya kiserikali pamoja na serikali yenyewe washirikishwe. Kusiwe na msukumo wa kisiasa kwani itajenga taswira ya kuchukiana na kubezana.
Kama sijakosea nadhani kuna baadhi ya vyama huko nyuma tayari vilikwisha andika kasimu ya katiba mpya. Hebu tuipitie na tuangalie pia maeneo mengine yanayoweza kuboreshwa katika katiba mpya tunayoihitaji.
Pamoja na hayo pia zipo sheria kandamizi ambazo si asili yetu nazo tunahitaji kuitisha mijadala ili nazo zifutwe.
Mfano ni ile sheria ya ugaidi ya mwaka 2002 na sheria ile inayompa kibali askari wa kimarekani kutoshitakiwa nchini ikiwa amekamatwa kwa kosa la kuuwa. Nchi huru kama tanzania hatupaswi kuwa na sheria kandamizi kama hizi. Wenzetu kenya walizikataa katakata.
Nachangia!
 
Jamani nawapongeza wote mnaochangia hii post. Naomba kama kuna uwezekano wana jf tutoe tamko kusisitiza uundwaji wa katiba mpya, ili tusiwe kama yale maswali ya kipindi cha kipima joto kufichua madudu yaliyomo kwenye katiba bila kuonyesha tunahusikaje na mabadiliko ni hayo tu
 
Ruta.
Nikupongeze kwa jitihada zako ambazo unazifanya. Mimi maoni yangu ni kuwa jambo hili tulisukume bila kuwa na tashwishi za kisiasa. Kila mtanzania mzalendo ashirikishwe katika mjadala huu. Watu binasfi kama tunavyoona, asasi za kiraia, vyama, na mashirika yasiyo ya kiserikali pamoja na serikali yenyewe washirikishwe. Kusiwe na msukumo wa kisiasa kwani itajenga taswira ya kuchukiana na kubezana.
Kama sijakosea nadhani kuna baadhi ya vyama huko nyuma tayari vilikwisha andika kasimu ya katiba mpya. Hebu tuipitie na tuangalie pia maeneo mengine yanayoweza kuboreshwa katika katiba mpya tunayoihitaji.
Pamoja na hayo pia zipo sheria kandamizi ambazo si asili yetu nazo tunahitaji kuitisha mijadala ili nazo zifutwe.

Thank you for this useful post...................
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom