CUF kutoshiriki sherehe za mapinduzi ya Zanzibar 12/1/2106

mashonga

JF-Expert Member
Nov 30, 2013
594
967
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Tokea yalipofanyika Mapinduzi ya tarehe 12 Januari, 1964, tumekuwa tukiadhimisha tukio hilo kubwa katika historia ya Zanzibar kila mwaka inapofika siku hiyo. Tukio hilo kubwa ndilo lililopelekea kutangazwa kwa Jamhuri ya Watu wa Zanzibar na Rais wa kwanza wa Zanzibar, Marehemu Mzee Abeid Amani Karume.

Chama Cha Wananchi (CUF) kimekuwa kikishiriki kikamilifu katika maadhimisho ya siku hiyo kila mwaka kwa kutambua kwamba Mapinduzi ya tarehe 12 Januari, 1964 ni Mapinduzi ya Wazanzibari wote. Malengo makuu ya Mapinduzi hayo yameelezwa na kufafanuliwa vyema kupitia Dikrii Nam. 6 ya mwaka 1964 iliyopitishwa na Baraza la Mapinduzi ambayo yanatajwa kwamba ni kuleta usawa, umoja na maridhiano baina ya Wazanzibari wote na kupiga vita aina zote za ubaguzi.

Tayari tumetangaziwa kwamba kuanzia tarehe 2 Januari, 2016 kutakuwa na shughuli mbali mbali zenye lengo la kuadhimisha Mapinduzi yetu na hatimaye, kama ilivyo ada na desturi, kufikia kilele tarehe 12 Januari, 2016 katika sherehe ambazo zitafanyika Uwanja wa Amaan, mjini Zanzibar.

CUF kama chama cha siasa kinawatakia kheri Wazanzibari wote katika kuadhimisha miaka 52 ya Mapinduzi yao.

Hata hivyo, tunatambua kwamba sherehe za mara hii zinafanyika wakati ambapo nchi yetu na watu wake wema wamo katika mtihani mkubwa kufuatia kitendo cha mtu mmoja, Jecha Salim Jecha, kuamua kwa utashi wake na waliomtuma kuiingiza nchi yetu katika msukosuko na taharuki kwa kudai kwamba eti ameufuta uchaguzi mkuu wa tarehe 25 Oktoba, 2015 na matokeo yake. Kwa kitendo hicho cha mtu mmoja ambaye amevunja Katiba, amevunja Sheria ya Uchaguzi na amevunja hata maadili ya kazi yake, mara hii nchi yetu itaadhimisha Mapinduzi huku Serikali ikiwa inaongozwa na viongozi ambao hawana uhalali na ridhaa ya wananchi.

CUF tumesisitiza mara zote kwamba hatukubaliani na uamuzi huo wa mtu mmoja kujinyakulia mamlaka ya wananchi wa Zanzibar yaliyowekwa kikatiba. Kwa msingi huo huo, tunapenda kutumia fursa hii kuwaeleza wananchi wa Zanzibar kwamba viongozi wetu hawatoshiriki katika shughuli walizopangiwa katika ratiba ya sherehe hizi kwa sababu zifuatazo:

1. Kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 (Toleo la 2010), Ibara ya 28, Ibara ya 42(2), Ibara ya 48(b), Ibara ya 90(1) na Ibara ya 92(1) Serikali iliyokuwepo madarakani na Baraza la Wawakilishi lililokuwepo katika kipindi cha miaka mitano iliyopita (2010 – 2015) vilimaliza muda wake wa uongozi tarehe 2 Novemba, 2015 kwa upande wa Serikali na tarehe 12 Novemba, 2015 kwa upande wa Baraza la Wawakilishi. Kwa sasa, hatuna viongozi wenye uhalali wa kikatiba kuweza kutekeleza majukumu ya kiserikali. Kwa hivyo, kushiriki katika ratiba hizo kwa kutumia nafasi ambazo hazina uhalali tena wa kikatiba ni kwenda kinyume na dhamira ya waasisi wa Mapinduzi, jambo ambalo hatuko tayari kulifanya.

2. Kiuataratibu, kilele cha sherehe huongozwa na Rais ambaye yupo kikatiba. Kwa mara ya kwanza tokea tarehe 12 Januari 1964, sherehe za miaka 52 zitaongozwa na Rais ambaye ameshamaliza muda wake wa uongozi kikatiba na ambaye hana uhalali na ridhaa ya wananchi wa Zanzibar. Kushiriki katika sherehe hizo ni kuhalalisha kipindi cha uongozi ambacho hakipo tena kikatiba. Maalim Seif Sharif Hamad na viongozi wenziwe ndani ya Chama waliokuweko Serikalini hadi tarehe 2 Novemba, 2015 hawako tayari kuhalalisha uvunjaji wa Katiba ya Zanzibar ambayo ndiyo sheria kuu ya nchi.

3. Viongozi wa CUF wakiongozwa na Maalim Seif Sharif Hamad wanaamini katika msingi mkuu wa Mapinduzi ya tarehe 12 Januari, 1964 chini ya uongozi wa Baba wa Taifa la Zanzibar, Marehemu Sheikh Abeid Amani Karume, ambao ni kuleta utawala wenye ridhaa ya wananchi walio wengi. Msingi huo umewekwa wazi na kutiliwa nguvu na Katiba ya Zanzibar ya 1984 (Toleo la 2010) kupitia Ibara ya 9(2)(a) ambapo inaelezwa kwamba, “Mamlaka ya kuendesha nchi ni ya wananchi wenyewe ambapo nguvu na uwezo wote wa Serikali kufuatana na Katiba utatoka kwa wananchi wenyewe.” Mamlaka hayo ya wananchi yalitekelezwa tarehe 25 Oktoba, 2015 kwa kuwachagua viongozi watakaoongoza Serikali yao kwa miaka mitano ijayo. Kitendo chochote cha kupindua mamlaka hayo ya wananchi ni kwenda kinyume na misingi ya Mapinduzi na misingi iliyowekwa na Baba wa Taifa la Zanzibar, Marehemu Sheikh Abeid Amani Karume. CUF hatuko tayari kushiriki katika kuisaliti misingi hiyo na kuisaliti dhamira ya Mzee Karume.

4. Sherehe za kuadhimisha Mapinduzi ya tarehe 12 Januari, 1964 zina lengo la kukumbuka malengo ya Mapinduzi hayo na dhamira ya waasisi wake wakiongozwa na Marehemu Sheikh Abeid Amani Karume katika kusimamia utawala wenye ridhaa ya wananchi walio wengi. Kuzitumia sherehe za Mapinduzi kuhalalisha utawala usio na ridhaa ya wananchi wa Zanzibar na ambao haupo kikatiba ni usaliti mkubwa wa dhamira ya kuwepo kumbukumbu hiyo. CUF hatuko tayari kuwa sehemu ya usaliti huo.

Kwa sababu hizo zilizoelezwa hapo juu, viongozi wa CUF hawatoshiriki katika ratiba walizopangiwa mpaka pale chaguo la wananchi wa Zanzibar walilolifanya tarehe 25 Oktoba, 2015 litakapoheshimiwa.

Tuweke wazi kwamba tulichoamua ni viongozi wetu kutoshiriki katika ratiba zinazohusisha viongozi wa Serikali ambao wamemaliza muda wao wa uongozi. Kwa hivyo, bado tunachukua nafasi hii kuwatakia wananchi wa Zanzibar maadhimisho mema ya miaka 52 ya Mapinduzi na kuwataka waendeleze umoja, mshikamano na amani katika nchi.

Mwisho kabisa, tunamuomba Mwenyezi Mungu awalaze mahala pema Peponi muasisi wa Mapinduzi yetu, Marehemu Mzee Abeid Amani Karume, na waasisi wenzake wote na awasamehe makosa yao.

Tunawaomba Wazanzibari wote kila mmoja kwa dini yake wamuombe Mwenyezi Mungu kuijaalia kheri na salama nchi yetu na kuyasimamisha yaliyo ya haki. Tukiishika kamba ya Mwenyezi Mungu hatutoanguka.

Tunawatakia wote kheri ya mwaka mpya wa 2016 na tunaamini unakuja na kheri kubwa kwa Zanzibar na watu wake. Ni mwaka ambao safari ya ujenzi wa Zanzibar Mpya itaanza.

MAPINDUZI DAIMA!

HAKI SAWA KWA WOTE

MANSOOR YUSSUF HIMID
MSHAURI WA KATIBU MKUU – CUF

31 DESEMBA, 2015
 
Cuf bwana!,toka lini wakayapenda mapinduzi?Huyo Himid anadai miaka yote walikuwa wanashiriki,amesahau kuwa cuf walisusa kipindi kirefu sana shughuli zote za serekali au kwa vile yeye alikuwa ccm na shemeji yake karume.
Kwetu sisi mapinduzi daima,ni kielelezo cha ukombozi kutoka kwa sultani,anaesusa asuse sisi tunasonga mbele
 
Mkuu waambie MODS wakurekebishie kichwa cha Habari umechapia badala 2106 ni 2016.
 
Back
Top Bottom