"Comical Khatib" na Kwaheri 2007

Mzee Mwanakijiji

Platinum Member
Mar 10, 2006
33,461
39,928
Makala hii imetoka kwenye Tanzania Daima leo. Kwa bahati mbaya kwenye tovuti yao haionekani (kama ilivyo kwa makala nyingine). Kwa faida ya wasomaji, mashabiki na wakosoaji ninaiweka hapa kama ilivyo.

M. M. Mwanakijiji


Hii itakuwa ni makala yangu ya kufungia mwaka (isipokuwa kama kuna jambo la dharura kabla ya mwaka mpya). Katika kumaliza mwaka huu jambo ambalo limenigusa mno ni majaribio yasiyoisha ya kuzuga wananchi yaliyofanywa na serikali ya CCM na viongozi wake. Majaribio hayo dhaifu na yasiyoenda “shule” yalikuwa ni burudani tosha kwa wananchi hasa wale ambao hawakuwa tayari kuzugika.

Kuna matukio mengi ambayo tukianza kuyahesabu tunaweza kucheka lakini kwa hakika Watanzania wanakumbuka jinsi ambavyo viongozi wetu “walivyochemsha” mara kadhaa na kujikuta kuwa wananchi wamewashtukia. Binafsi nilifikia mahali pa kuweka manyanga chini na kukubali “yaishe” tu. Nilifikia mahali pa kuona kuwa serikali yetu imeziba masikio yake na ingawa inaimba wimbo wa “kukubali kukosolewa” kimsingi haina lengo la kusahihisha makosa au udhaifu wake na badala yake imejitahidi kuuelezea na kuuhalalisha.

Lakini ambacho kilinikera zaidi mwaka huu siyo masuala ya mikataba ingawa hilo lilinikera; siyo suala la nishati ingawa hilo lilinikera; siyo masuala ya wanafunzi wa Ukraine ambayo kwa hakika yalinikera sana; na kwa hakika siyo maamuzi mbalimbali ya kisiasa ambacho yamechukuliwa mwaka huu, ambayo nayo pia yalinikera. Binafsi kati ya yote ambayo serikali ya Kikwete imejitahidi kuyafanya na kushindwa vibaya sana ni uzugaji makusudi wa wananchi bila wananchi wenyewe kuzugika.

Tulipoanza na suala la vijana wetu waliokwama Ukraine ambao serikali iliwakubalia mkopo na kuwapa baraka zote waende kusoma huko kilichonisikisha na kunitisha siyo adha na matatizo ya watoto wetu wale hadi wakapiga kambi nje ya Ubalozi wa Uingereza bali ni majibu ya kizugaji ya serikali yetu. Licha ya kuwapa nafasi viongozi wote wakuu wa serikali yetu kuanzia Rais Kikwete hadi Wabunge wote kwa woga waligwaya kushughulikia suala hili na badala yake wakaja na majibu ya kizugaji.

Prof. Msolla na timu yake iliyojaa wazembe na viongozi wenye kujipenda wenyewe kuliko utumishi wao kwa taifa hili wakasema kuwa “tuliwapa ushauri wasiondoke, hawakusikiliza”. Hakuna kati yao kwa mwaka mzima aliyeweza kusema ni lini na ni nani aliyewapa vijana hao ushauri huo wa kutokwenda Ukraine lakini wakaenda. Na kwa kutumia ubavu mkubwa wakawalazimisha vijana wale kurudi nyumbani na kukatisha masomo. Wiki iliyopita Prof. Msolla bila soni anadiriki kuuambia ulimwengu kuwa Tanzania iko nyuma katika elimu ya juu!! Uzugaji juu ya uzugaji.

Rais Kikwete na Waziri wake Mkuu walipopewa nafasi ya kufanya maamuzi ya kijasiri na kishujaa wakagwaya na kuona kuwa tunashindana na serikali. Rais Kikwete yeye akasema “kama Wizara wangeshindwa wangeniambia” na Mhe Lowassa yeye alipopewa nafasi ya kuonesha uongozi akasema “ninaenda kula”. Bodi mbovu ya mikopo ambayo ni chanzo cha matatizo makubwa ya elimu ya juu na mfumo duni wa utoaji wa mikopo hiyo unaosimamiwa na Nyatega vyote bado vipo na mwaka ujao Watanzania muendelee kusubiri uzugaji juu ya uzugaji.

Tukawaonesha jinsi gani bodi ya mikopo inachota fedha na kushindwa kusimamia utoaji wa mikopo na hivyo kutengeneza mwanya mkubwa wa ufisadi na majina tukawapa. Kina Gesimba na wenzao wakakurupuka kutoka idara yao ya uzugaji na kujaribu kuelezea upotofu huo. Wakajaribu kutoa majibu ya nini kilifanyika kuhusu vijana wa Ukraine na tulipowabana wakaomba Taasisi ya Kuzuga kuwasaidia. Ndipo Bw. Edward Hosea na TAKUKURU wakajjitokeza na kusema kuwa “wanafanyia kazi” madai ya ufisadi kwenye Bodi ya Mikopo. Wananchi tukazugwa.

Wakati wa kikao cha bajeti Waziri Mkuu akiwa na jazba zake na akizungumza kwa sauti ya kupaa kama msanii wa bongo flava akatangaza Bungeni kwa mbwembwe zote kuwa “Tanzania imepaa” na wananchi tushangilie. Nikaandika wakati ule juu ya “Ndege ya Lowassa iliyopaa na abiria walioachwa wameduwaa” iliyoambatana na kikatuni kizuri kabisa. Mabingwa wa uzugaji wakakurupuka kuja na majibu yasiyo na kichwa wala mguu ambayo ndani yake wakatupa sisi wengine ukimbizi wa reja reja. Tukawajibu kimahiri bila kuwaonea soni kama vile kumkoma nyani giledi! Tukawaonesha kuwa wamekurupuka na waliposoma majibu yetu wakanywea na kuelewa kuwa uzugaji wao wa zamani hauna nafasi leo hii.

Yakaja masuala ya Buzwagi na Karamagi. Mjadala ukazuka na tukaona ni jinsi gani Taasisi yao ya Uzugaji imekosa nguvu kwani hata kitengo chao cha chama kinachoshughulikia Uzugaji kilishindwa kulitetea jambo hili. Walipomwadhibu Mhe. Zitto na kumfungia wao walitarajia wananchi watashangilia na Zitto aliposimamishwa kama shujaa katika Taifa hili wakajua uzugaji wao hatimaye umefikia kikomo. Wakawatuma kuanzia kina Mhe. Anna Makinda na wapambe wao toka Bungeni ili wawaeleweshe wananchi juu ya Adhabu ya Zitto na kwanini imestahili. Wakajaribu kuzuga weeeee lakini wapi, Zitto akawa Mzitto habebeki! Taasisi yao ya Uzugaji chini ya Hosea ikaingilia kati tena, wakasema “tunachunguza rushwa” wakati hakuna mtu aliyedai kulikuwa na rushwa!

Kabla hawajakaa sawasawa Ushirika wa wapinzani wakaja na kile ambacho naamini ni jambo kubwa kabisa katika historia ya nchi yetu mwaka huu nako ni kutajwa kwa orodha ya aibu ya ufisadi ambapo watumishi 11 katika serikali yetu wakatajwa kuwa “kwa namna moja au nyingine” wameshiriki katika ufisadi”. Alitajwa kuanzia Rais Kikwete hadi mtu wa mwisho. Kama vile mbogo waliojeruhiwa watawala wetu wakaanza kukurupuka na majibu ambayo kwa hakika mfano wake hakuna. Wakaanza kujaribu kutuzuga. Akatumwa Kingunge, Bomani, Warioba na wenzao huku watuhumiwa wakitishia kwenda mahakamani.

Watu tukashangazwa imekuwaje hadi Warioba kutumiwa katika uzugaji? Kumbe yalikuwa maji marefu. Walizoea kutuzuga sisi wananchi wa kawaida lakini mwisho “mjomba wetu” kule Ulaya akaingilia kati, uzugaji wao haukufanikiwa kama walivyotaka wakajikuta hawana budi kuruhusu uchunguzi “huru”.

Wakitumia ujuzi wao wa siku nyingi wa uzugaji wakaamua kutuma timu yao nzima kama kikosi kwenda mikoani kuzuga wananchi kwa kile ambacho wao walikiita “kuelezea bajeti”. Masikini wa Mungu wakajitahidi! Lakini wakienda huku wanazomewa, wakirudi kule wanazomewa! Hawakuelewa ni kitu gani kimewaingia Watanzania! Wakabakia wanaulizana ilikuwaje? Cha kusikitisha ni kuwa uzugaji wao ulifikia mahali pabaya hadi kuomba msaada wa mtuhumiwa wa mauaji Brother Ditto ambaye naye kwa kushindwa hoja akajikuta anatukana wake za watu! Kumbe cha kuvunjda hakina ubani!!

Wakiwa katika uzugaji huo ndipo kwa mara nyingine Watanzania tukaona jinsi gani nchi yetu imejaliwa wasanii. Kama ilivyokuwa wakati wa uvamizi wa Wamarekani nchini Iraq miaka karibu minne iliyopita, ambapo wananchi walishuhudia Umahiri wa Waziri wa Habari wa Saddam Bw. Mohammed Said al Sahaf. Waziri yule ambaye katika miaka ya hivi karibuni bila ya shaka anashikilia rekodi ya propaganda duniani aliweza kuiteka mioyo ya watu kwa kutumia kipaji chake cha maneno kuzuga watu. Mojawapo ya uzugaji wake mkubwa wakati wa vita ni madai kuwa “majeshi ya Marekani hayako Baghdadi na askari wa Marekani wanauliwa malangoni mwake”. Wakati anasema hayo majeshi ya Marekani yalikuwa mita chache toka alipokuwapo Waziri huyo. Ni kutokana na uzugaji huo magazeti ya magharibi yakampachika jina la “comical Ali” yaani mchekeshaji Ali wakimtofautisha na msaidizi mwingine wa Sadam aliyejulikana kama “Chemical Ali”.

Ndipo na sisi Watanzania wakati wa sakata la orodha ya ufisadi tukapata mchekeshaji wetu. Waziri wetu wa Habari na Utamaduni (cheo kama cha Comical Ali) Bw. Mohammed Seif Khatib alipoonesha uzugaji wake. Mheshimiwa huyo alikana kabisa kuwa “viongozi hawazomewi, zote hizo ni propaganda za Wapinzani”.

Uzugaji ukaendelea mwaka mzima na hasa pale ilipouunda Kamati ya Ushauri kuhusu Sekta ya Madini. Wananchi walifurahia kweli kuwa hatimaye Rais kafanya kweli. Wananchi wakadhania kuwa “sala zao zimejibiwa” kumbe walichoshuhudia ni uzugaji wa hali ya juu. Hisia hizo kuwa tumezugwa zikathibitishwa na idara ya CCM ya uzugaji wa Hali ya Juu inayoongozwa na Mhe. John Chiligati. Yeye bila wasiwasi akawaambia wananchi kuwa Rais hakuunda tume ya uchunguzi! Wakatuzuga tukazugika.

Sasa uzugaji huu ukaendelea kwenye mambo mengi na kama nilivyosema kuyaorodhesha yote tutakesha. Hata hivyo nimeshindwa kujizua kuelezea uzugaji uliofanywa na Comical Khatib wetu mara ya mwisho. Yalipotolewa matokeo ya utafiti wa REDET kuhusu serikali ya Kikwete vyombo mbalimbali vya habari vikaelezea ni jinsi gani matokeo ya utafiti huo siyo mazuri kwa CCM. Mheshimiwa Khatib akitumia mbinu ya “Comical Ali” akajaribu kuelezea kwanini matokeo hayo ni mazuri kwa CCM kwa kuangalia neno “kuridhika”. Akajaribu kutuzuga.

Sasa, CCM na wapambe wake wataendelea kutuzuga hadi lini? Hivi wanaposimama na kusema mambo ambayo hayana mantiki kweli wanafikiria wananchi hawatashtukia? Leo hii Ofisa Ugavi toka Ofisi ya Rais Menejimenti ya Umma anawatangazia madiwani kuwa kuanzia sasa wanaweza kuomba Tenda katika halmashauri zao na wasikataliwe kwa vile tu wao ni madiwani wa halmashauri hizo. Bw. Athuman Ngwalo amesema kwa vile wao madiwani siyo watumishi wa “umma” (msiniulize wanamtumikia nani) basi hata kama wana makampuni yao mbalimbali sasa wanaweza kushindanisha tenda kwenye halmashauri zao kwani hakuna sheria inayowakata kufanya hivyo. Kama vile Rais wao Mkapa alivyofanya akiwa Ikulu sasa halmashauri zetu zimepewa leseni za kutengeneza pesa! Kuzuga wanakotuzuga.

Sasa, tunapoelekea mwaka huu mpya nina ombi moja tu kwa CCM na watendaji wake. Chonde chonde sana na tafadhali mno, kuwa mwaka ujao wa 2008 mtakapoamua kutuzuga jaribuni kutuzuga tukazugika. Jinsi ambavyo mmejaribu mwaka huu kwa kweli mmefeli mno na kwa neno moja mmetia aibu. Kama uzugaji mliofanya mwaka huu ndio mtakaourudia mwakani basi kama watani zangu wanavyosema kule Mbeya “Mbombo ingafu”. Mna kazi mwakani kama uzugaji mtakaofanya unakaribiana kwa kiasi chochotena ule wa mwaka huu.

Mtakapoamua kutuzuga mwakani hakikisheni mnatuzuga hadi tunazugika maana mkituacha na maswali ya ziada au mkitoa majibu yanayozua maswali zaidi basi mtakuwa mmeshindwa katika fani uzugaji. Kama Rais ataamua kuunda upya baraza lake ni bora ahakikishe kuwa kitengo cha Uzugaji kina watu wanaoweza kuimuda nafasi hiyo na mtindo mlioanzisha sasa wa Mawaziri kuzungumza na wananchi ni mzuri. Ila nawashauri mwakani wale “wasemaji” wenu watakapokuwa wanatoa taarifa rasmi watengenezeeni beji zenye herufi ya “M” ili wananchi wajue. Haitoshi kumwaga takwimu, haitoshi kulalamika magazeti hayaandiki mazuri na haitoshi kujaribu kuvinyima vyombo vya habari vinavyowakosoa biashara toka serikalini kwa vile tu hawakubali uzugaji wenu. Mkiamua kutuzuga mwakani mtuzuge tuzugike!

Vinginevyo, mwaka ujao tutaendelea kuwakalia kooni kama nira na kama ndege wanavyotua juu ya wanyama malishoni ndivyo na sisi tutavyotua katika migongo yenu. Tutawadonoa kwahoja na kuwaparua hadi makupe na viroboto yaishe kati yenu. Kama mwaka huu mmetushinda kwa kuwarudisha vijana wetu toka Ukraine kusoma na kuwaacha Solemba, na mkatangaza ushindi, basi mwaka ujao ni zamu yetu! Tunawatangazia mapema kuwa kama mlifikiri Tanzania ni yenu peke yenu na sisi wengine ni wakimbizi tu na wahamiaji mjue kuwa wakati wa njozi yenu hiyo umefikia kikomo! Unapokuja mwaka mpya, hatutakubali tena kuzugwa kwani kuzuga kwa miaka 46 iliyopita kumetosha na wananchi wanajiandaa kwa mwaka 2010! Mmepewa nafasi nyingi ya kusahihisha na kujisahihisha na mara zote mmekuwa na majibu na mikakati ya kizugaji. Watanzania wamechoka, na wakati waja na tena upo ambapo wataonesha uchovu wao kwenye sanduku la kura. Safari ya kuelekea huko ndiyo imeanza. Mtatuzuga tena? I don’t think so!

Kwenu nyote wasomaji, Eid Mubarak, Heri ya Krismasi, na Fanaka za Mwaka Mpya usio na uzugaji wa 2008! Tukutane wiki ya kwanza ya 2008

Niandikie: mwanakijiji(at)jamboforums.com
 
mwanakiji wewe si mtu wa Usalama wa taifa?mbona nawewe unatuzuga hautaki kutuambia ukweli ..hauoni na wewe ni mzugaji?
kwa kifupi Dr. Muungwana ana cha kujitetea kwa leo,Nchi ilikaribi kudondoka,uchawi ndio umewasaidia na ushauri wa Mzee cheyo aliowapa wa kuunda kamati na kumshirikisha Zitto.
 
Nice overall check on the almost otherworldly-obscene carte blanche enjoyed by the powers that be in Tanzania.

Few problems though, maybe it is a matter of style and presentation but perception can turn into reality.Especially with the limited access provided by the written word.

Majaribio hayo dhaifu na yasiyoenda "shule" yalikuwa ni burudani tosha kwa wananchi hasa wale ambao hawakuwa tayari kuzugika.

Kuna matukio mengi ambayo tukianza kuyahesabu tunaweza kucheka ...

It would be funny if it wasn't so tragic.To convince me you are serious you have to recognize the gravity of the problem, if you find entertainment in any of this you are not seriously ticked off.

Kuna matukio mengi ambayo tukianza kuyahesabu tunaweza kucheka lakini kwa hakika Watanzania wanakumbuka jinsi ambavyo viongozi wetu "walivyochemsha" mara kadhaa na kujikuta kuwa wananchi wamewashtukia. Binafsi nilifikia mahali pa kuweka manyanga chini na kukubali "yaishe" tu. Nilifikia mahali pa kuona kuwa serikali yetu imeziba masikio yake na ingawa inaimba wimbo wa "kukubali kukosolewa" kimsingi haina lengo la kusahihisha makosa au udhaifu wake na badala yake imejitahidi kuuelezea na kuuhalalisha.

I read a sense of desperation and towel throwing.Where is the relentless pursuit of justice? If this is really the feeling then why bother write at all? This is exactly what "mafisadi" wants to hear, that their "dignified silence" is frustrating the people out of their wits to the extent they cannot even organize a serious article challenging the status quo.the opposition can do without this timid and pesimistic desperation.


Sasa, tunapoelekea mwaka huu mpya nina ombi moja tu kwa CCM na watendaji wake. Chonde chonde sana na tafadhali mno, kuwa mwaka ujao wa 2008 mtakapoamua kutuzuga jaribuni kutuzuga tukazugika. Jinsi ambavyo mmejaribu mwaka huu kwa kweli mmefeli mno na kwa neno moja mmetia aibu. Kama uzugaji mliofanya mwaka huu ndio mtakaourudia mwakani basi kama watani zangu wanavyosema kule Mbeya "Mbombo ingafu". Mna kazi mwakani kama uzugaji mtakaofanya unakaribiana kwa kiasi chochotena ule wa mwaka huu.

Is this sarcasm or what? If it is then this is not it's place, I believe the issues are far too serious to employ "the lowest form of wit".If it is not, once again you do not demonstrate a seriousness to address the issue and one can make an argument that you dabble in this a mental jujitsu while hardly connecting with the plight of the people you claim to speak for.

The dramatic sensationalism employed in the concluding paragraphs (after the above quoted) emphasize on your lack of focus on the issues and prioritizing a game type scenario for mental entertainment.

Other than further qualifying arguments with anecdotes and providing substantial objections to government moves (the involvement of local government officials in tender was an opportunity to point out our leadership's lack of restraint from conflict of interest prone matters), the rest of the meat is ditto, ditto and bravo bravo.
 
there is only one guy who would respond like that.. I love it na mchango wako kwa miaka kadhaa unahitajika.. remember YOU started it!
 
Daayum,

Didn't know my flow was fingerprinted.

Blew my cover I guess. Its all good.Pole naona wanakupachika vyeo lukuki, usalama wa taifa and all this other bs.

The struggle is not for the weary bro, keep it up and we are right by you.
 
Bravo Mkijiji!
Hapa aliyetoneshwa donda ni air Uchumi!,

I like the way you present your message, it comes like a story, every one would not risk of missing it!,

Soon the word ''kumkoma nyani.. '' litaingizwa kwenye kamusi! you sell it very well.

Nasikia Tanzania Daima jtano ni hot keki every one looking for Mkijiji makala!
Good job!
 
Rwabugiri.. kuna mtu kaniambia hivyo and I really don't get that part.. napokea kwa heshima na unyenyekevu tu na ninashukuru watu wa hapa ambao they have always been able to keep me grounded kabla libichwa halijagusa udongo!
 
mwanakiji wewe si mtu wa Usalama wa taifa?mbona nawewe unatuzuga hautaki kutuambia ukweli ..hauoni na wewe ni mzugaji?
kwa kifupi Dr. Muungwana ana cha kujitetea kwa leo,Nchi ilikaribi kudondoka,uchawi ndio umewasaidia na ushauri wa Mzee cheyo aliowapa wa kuunda kamati na kumshirikisha Zitto.

Nimeiona hiyo email inayotembea kwenye mtandao kuhusiana na Mkjj kuwa ni mtu wa usalama wa Taifa. Nilitaka kuiweka hapa lakini nikaona si ustaarabu. Kama watu wa usalama wa Taifa wangekuwa wanahoji usanii ulioshamiri kwenye siri kali kama anavyohoji Mkjj basi nchi ingekuwa imepiga hatua kubwa na kuuzika usanii uliokithiri.
 
dah mwanakijiji nimevutika sana na post ya makala yako uliyoiweka hapa.
nimeikomboa fikra yangu siku nyingi. Ninadhani hoja kuu hapa ni namna ambavyo muungwana ameshindwa kuiendesha nchi kiasi kwamba anafikia kusema anayo majina ya wabadhirifu, wasambaza madawa ya kulevya na wafadhili wa ujambazi na ufisadi nchini and suprisingly amekaa na majina hayo for two years, what went wrong?au ndo ule usemi kuwa fanya dhambi Mungu anakuona??? Mawziri wamechemsha kiasi hata heshima ya taasisi ya uwaziri imeshuka halafu muungwana bado anawakumbatia... Always naamini kuwa dawa ya tatizo ni kulitatua na siyo kulilea au kulikumbatia...

Jana ilikuwa sendoff ya wazirimkuu wa nyumba yangu na kufikia next week nitakuwa na rais wake.(sorry nimeiweka hapa)
 
Jana ilikuwa sendoff ya wazirimkuu wa nyumba yangu na kufikia next week nitakuwa na rais wake.(sorry nimeiweka hapa)

Kama nimekuelewa vyema,
Nikupe hongera za awali na kukukaribisha katika chama.

Labda tu kwa taarifa kwa vile ni mgeni, chama chetu hupenda wanachama wa kudumu mpaka maulana akipangua mwenyewe! so take care!
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom