Pascal Mayalla
Platinum Member
- Sep 22, 2008
- 50,467
- 113,567
03/12/2017 Mchango wa Sekta Binafsi Kwenye Elimu, Wapongezwa
Mchango wa Sekta Binafsi kwenye utoaji wa Elimu ya Juu nchini Tanzania, umepongezwa na kuelezewa kuwa unalisaidia Taifa kukidhi mahitaji ya wataalamu wa fani mbalimbali, hivyo kusaidia kwenye maendeleo ya taifa.
Pongezi hizo, zimetolewa jana na Mkuu wa Chuo Kikuu cha Kumbukumbu ya Hubert Kairuki, Dr. Salim Ahmed Salim, wakati wa mahafali ya 15 ya Chuo hicho, yaliyofanyika jana chuoni hapo ambapo jumla ya wanafunzi 288 Walihitimu kozi mbalimbali za astashahada, shahada na shahada za uzamili katika fani ya uuguzi na udakitari wa binadamu, wakiwemo wanafunzi 136 waliohitimu udakitari wa binadamu wakiongozwa na mhitimu, Dr. Delilah Mwindadi aliyeibuka mwanafunzi bora wa udakitari.
Dr. Salim amesema, tangu chuo hicho kimeanzishwa, kimetoa madaktari wengi wanaolisaidia taifa hili, hii ikiwa ni ishara ya kutimizwa kwa azma ya muasisi wa chuo hicho, Marehemu Prof. Hubert Kairuki, la kuhakikisha chuo hicho kinatoa mchango kwa maendeleo ya taifa.
Mwenyekiti wa bodi ya Wakurugenzi wa Chuo hicho, Mama Kokushubira Kairuki, aliwataka wahitimu hao, kwenda kuyatumia mafunzo waliyoyapata kwa bidii, weledi na uadilifu, ili kuendelea kulinda sifa na heshima za wahitimu wa chuo, waliojinjengea kwa miaka mingi.
Makamo Mkuu wa Chuo, Prof. Charles Mgone, amesema wahitimu wa Chuo hicho, wamefunzwa kuweza kufanya kazi popote nchini Tanzania, na mrejesho wa wahitimu hao huko makazini ni mzuri kwa sababu ni wachapa kazi kwa kujituma kwa bidii, weledi na waadilifu sana. Kwa upande wa chuo hicho, kinaongeza kampasi nyingine, na kutanua wigo wa mafunzo na huduma za kusafisha figo, dialysis, na huduma za kupandikiza uzazi, IVF kwa wanandoa wenye matatizo ya kutopata watoto.
Mwenyekiti wa Baraza la Chuo hicho, John Ulanga, amesema, mahafali haya ya 15, ni kielelezo cha mchango wa sekta binafsi katika kusaidia maendeleo ya taifa, kwa upande wa sekta ya afya na tiba ya binadamu, hivyo akatoa wito kwa serikali na sekta ya umma, kuendelea kujenga mazingira wezeshi kuwezesha sekta binafsi, kukua na kutoa mchango wake kuisaidia serikali na sekta ya umma kuleta maendeleo ya taifa letu, kwa sababu maendeleo ya kweli, yatapatikana kwa ushirikiano wa sekta binafsi na sekta ya umma, pamoja, tutaweza.
Jumla ya wahitimu 288 walihitimu, kati yao wauguzi ni 49, shahada za uuguzi ni 22, shahada za udaktari 136, na shahada za uzamili kwenye udakitari, ni 21.