Chongolo: Msisitizo wa chama cha mapinduzi(CCM) katika maeneo muhimu kwenye mpango wa maendeleo na bajeti za Serikali kwa mwaka wa fedha 2021/2022

Baraka Mina

JF-Expert Member
Sep 3, 2020
581
574
Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi Ndg. Daniel Chongolo anafanya mkutano na waandishi wa habari katika ukumbi wa Halmashauri Kuu (NEC) Makao Makuu ya Chama jijini Dodoma.

=====
1621519414362.png
KATIBU MKUU CCM AWAONYA WENYE NIA OVU SUALA LA UMEME, ATOA MAAGIZO KWA WIZARA TATU

CHAMA Cha Mapinduzi CCM kimewaonya wale wote waliokua na nia ovu kwenye suala la umeme huku akiitaka Serikali kuwachukulia hatua za kisheria watakaothibitika kuhusika na jambo hilo.

Hayo yamesemwa leo na Katibu Mkuu wa CCM, Daniel Chongolo wakati akizungumza na wandishi wa habari jijini Dodoma ambapo ametoa maagizo kwa Serikali kupitia Wizara zake tatu.

Wizara ambazo Katibu Mkuu Chongolo amezitolea maelekezo ni pamoja na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Wizara ya Kilimo na Wizara ya Nishati.

Chongolo ameiagiza Serikali kupitia Wizara ya Nishati kuhakikisha inamaliza kwa wakati miradi yote ya Nishati ambayo imeanza kutekelezwa ukiwemo mradi mkubwa wa umeme wa Bwawa la Mwalimu Nyerere uliopo Rufiji mkoani Pwani.

Katibu Mkuu Chongolo amesema kumalizika kwa mradi huo kutaongeza megawati za umeme zipatazo 2115 na kusaidia kuwa na umeme mwingi jambo ambalo litakuza uchumi wa Nchi kupitia viwanda.

" Nionye wale wenye nia ovu na Nchi yetu ambao walitaka kutuweka gizani,niipongeze Serikali kwa hatua za awali walizochukua katika kuhakikisha wananchi wanaepukana na changamoto ya manunuzi ya umeme.

Lakini pia tunaiagiza Serikali kumalizia kuweka umeme vijiji ambavyo vimebaki kwani Ni vichache sana, lengo la Chama chetu ni kuona Nchi nzima inawaka umeme ili kuchochea kasi ya maendeleo kwa Taifa letu," Amesema Chongolo.

Kuhusu Wizara ya Ardhi, Chongolo ameielekeza Wizara hiyo kuongeza kasi yake ya utoaji hati kwa wananchi katika kumiliki ardhi hatua ambayo itasaidia kuwafanya wananchi kuwa na usalama na ardhi yao.

" Tunaelekeza wizara kuongeza kasi kwenye suala la umiliki wa maeneo, CCM kupitia ilani yake ibara ya 74 imeielekeza Serikali kuongeza kasi ya utoaji hati na sisi kama Chama tutalisimamia hili kwa weledi na tunataka kuona Wizara kupitia bajeti yake watueleze wamejipanga kiasi gani kuondoa adha hiyo ya kupoteza ardhi zao kwa kukosa hati.

Kwenye usaminishaji na fidia CCM inaielekeza Serikali kuwalipa wananchi stahiki zao kwa wale wote waliotwaliwa maeneo yao kisheria, na niwaagize viongozi wetu kuanzia ngazi ya Mitaa na Vijiji hadi Wizarani kutatua changamoto za ardhi,"Amesema Chongolo.

Kwenye sekta ya Kilimo, Katibu Mkuu Chongolo ameielekeza Wizara ya Kilimo kukamilisha ujenzi wa skimu katika wilaya ya Songea na Rungwe huku akiitaka Serikali pia kuongeza tija na faida katika uzalishaji.

" Kutokana na kuwa na changamoto ya mbegu Chama kinaielekeza Serikali kuongeza bajeti ya utafiti wa mbegu ili kuwahakikishia wakulima ubora wa mbegu wanazonunua," Amesema Chongolo.

FULL TEXT....

MSISITIZO WA CHAMA CHA MAPINDUZI KATIKA MAENEO MUHIMU KWENYE MPANGO WA MAENDELEO NA BAJETI ZA SERIKALI KWA MWAKA WA FEDHA 2021/2022

Naibu Katibu Mkuu – Bara, Christine Mndeme

Wakuu wa Idara, Unezi Shaka Hamdu Shaka, Organaizesheni Mouldline Castico, Uchumi na Fedha Dkt. George Hawassi, Suki – Col. Ngemela Lubinga

Ndugu Wanahabari,


Awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha kukutana hapa leo. Aidha, kwa niaba ya Wajumbe wenzangu wa Sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya Taifa, namshukuru Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kupendekeza majina yetu kwa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa na kutupitisha, nami nikiwa Katibu Mkuu.

Nawashukuru Watumishi wote wa Chama Makao Makuu Dodoma, Ofisi Ndogo Dar es Salaam, Afisi Kuu Zanzibar na Mikoa yote kwa kunipokea mimi na Wajumbe wenzangu wa Sekretarieti na ushirikiano wanaotupa tangu tulipongia ofisini.

Kwa kipekee kabisa napenda kuwashukuru ninyi Wanahabari. Tulikuwa wote kwenye kazi hii adhimu na muhimu kwa maendeleo ya nchi yetu. Kila ninayemwangalia hapa, anatabasamu kuonyesha kuwa hajanisahau, nikiwa hapa CCM na baadaye Serikalini. Karibuni sana.

Najua kila mmoja wenu na kila Chombo cha Habari kilitamani sana kuja kufanya mahojiano na mimi baada ya kuteuliwa kwangu kuwa Katibu Mkuu wa CCM. Na zaidi najua wengi wenu mlitamani pia kusikia Katibu Mkuu mpya na Sekretarieti yake kasema nini leo na kujiuliza hivi anafanya nini kwa sasa. Kwa kweli tulipoingia tu tulianza na kazi moja kwa moja. Mnajua kulikuwa na Uchaguzi Mdogo kule Muhambwe na Buhingwe, Pamoja na Kata 17 katika maeneo mbalimbali nchini. Wajumbe wa Sekretarieti walikuwa huko kuhakikisha majimbo yale yanabakia CCM na kazi hiyo wameifanya vizuri na kazi nyingine pia zinaendelea. Nichukue nafasi hii kuwashukuru viongozi na wananchi wote wa Buhigwe, Muhambwe kwa kuiamini CCM tena.

Lakini hapa jambo kubwa ambalo mnapaswa kulifahamu ni kuwa, Chama na Jumuiya zake kazi yake ni ya uongozi wa Wananchi kupitia Serikali zake. Sekretarieti ndiyo inayoratibu kazi za kila siku za uongozi wa Wananchi kwa Kamati Kuu na Halmashauri Kuu ya Taifa. Kwa kifupi kazi kubwa ya Chama na Jumuiya zake ni kuhudumia Wananchi na kushughulika na kero zao za kila siku. Kwa mfano, katika kipindi hiki, kuanzia mwezi Aprili, Bunge la Tanzania linajadili Bajeti za Serikali, kwa mwkaa wa fedha 2021/2022. Hivyo basi, ni jukumu letu kama Chama na Jumuiya zake, kuikumbusha Serikali kuzingatia vipaumbele na maeneo muhimu ya kuyashughulikia kwenye sekta mbalimbali ndani ya Bajeti hizo kama Ilani ya CCM 2020/2025 inavyoelekeza.

Kazi hii ya kuikumbusha Serikali kuyazingatia maeneo muhimu, tunaifanya kutokana na ukweli kwamba yamekuwapo manung’uniko kadhaa kutoka kwa Wananchi katika baadhi ya maeneo nchini licha ya Chama kuahidi kwenye Ilani yake.

Hapa nataka kuwaahidi wananchi kwamba CCM ndiyo iliyobeba dhimara kuwasemea wao na kwamba jukumu hilo tutalifanya kwa ustadi na ueledi kusimamia Serikali zote mbili kuhakikisha hili lina fanikiwa.

Aidha, niwaombe watanzania wote kuzitumia Ofisi za CCM kama kimbilio lao kwenye changamoto zao. Jukumu hili tutalitekeleza bila kumwonea aibu mtu yeyote.

Kwa hiyo, leo hii tumewaita ili kuwaeleza tulikuwa tunafanya nini tangu tulipoteuliwa kuingia kwenye Sekretarieti. Kwa kipindi kifupi tuliona tushughulike maeneo muhimu yanayoleta manung’uniko kwa Wananchi ili Serikali iyazingatie kwenye Bajeti zao kwa kuanzia na mwaka huu wa Fedha wa 2021/2022.

Kwa kuanzia, leo tutaangalia na kutoa msisitizo wa Chama kwenye Sekta kubwa tatu za Ardhi, Kilimo, na Nishati.

MSISITIZO WA CHAMA KATIKA MAENEO MUHIMU KATIKA WIZARA YA ARDHI

WIZARA YA ARDHI

Katika kipindi cha mwaka 2020-2025, CCM iliendelea kuendelea kutunza rasilimali ardhi ikiwa ni pamoja na kuzielekeza serikali zake mbili kutatua migogoro ya ardhi iliyopo, kuthamisha ardhi ili kuziongezea tija, pamoja na kuhakikisha wananchi wanamiliki ardhi kisheria ili kupunguza migogoro.
  • UMILIKI WA ARDHI
  • Kutokana na malalamiko ya wananchi wengi katika umiliki wa ardhi zao na kuwa na tija katika umiliki huo, Chama Cha Mapinduzi kupitia Ilani yake ya 2020-2025 Ibara ya 74, kimeielekeza Serikali ihakikishe inaongeza kasi ya utaoji wa hati miliki za ardhi mijini na hati za kimila vijijini kuwawezesha wananchi kumiliki kisheria maeneo yao na kutumia kama dhamana katika taasisi za kifedha. Hatua hii itasaidia kuwafanya wananchi wawe na usalama wa maeneo yao. Jambo hili ni muhimu sana hivyo, CCM italifuatilia kwa karibu utekelezaji wake.
  • UTHAMINISHAJI NA FIDIA
  • Chama kinaielekeza Serikali kuhakikisha inawalipa fidia stahiki na kwa wakati wananchi walio twaliwa maeneo yao kwa shughuli za umma, hivyo Chama kinaelekeza uimarishwaji wa mfuko wa fidia na Serikali.
  • Pia Viongozi wote wa serikali kuanzia ngazi za mitaa/kijiji mpaka wizara wahakikishe wanatatua migogoro ya ardhi kwa haki na kwa wakati, mathalani Chama kinaielekeza kumaliza haraka migogoro ya ardhi katika wilaya za Kondoa, Ngorongoro, Kiteto, Kongwa, Morogoro, Kinondoni na pembezoni mwa Hifadhi mbalimbali zitagusa na maeneo mengine.
  • MABARAZA YA ARDHI
  • Chama kinaelekeza serikali ipitie upya sheria za mabaraza ya ardhi kwa lengo la kuhuisha utendaji na ufanisi wa mabaraza hayo. Aidha mabaraza hayo yajihusishe na usuluhishi wa migogoro ya ardhi kuliko kuamua kimahakama, hatua hii itasaida kupunguza kwa kiasi kikubwa migogoro ya ardhi isiyo ya lazima
  • UPIMAJI ARDHI
  • Chama kinaielekeza serikali kuongeza kasi ya upimaji na upangaji wa matumizi bora ya ardhi ili kuepuka ukuaji holela wa miji, hasa katika miji inayokua kwa haraka ikiwemo maeneo ya majiji, Manispaa na miji midogo.
MSISITIZO NA MAELEKEZO YA CHAMA KWA SERIKALI KATIKA WIZARA MBALIMBALI

WIZARA YA KILIMO
  • UMWAGILIAJI NA MIUNDOMBINU YAKE
  • Kutokana na changamoto ya mabadiliko ya tabia ya nchi, kilimo cha umwagiliaji ndio kimbilio la wakulima wengi nchini, Ili kuongeza maeneo ya umwagiliaji nchini na kufikia malengo ya Chama ya angalau kuwa na hekta 1,200,000 za umwagiliaji ifikapo 2025, Chama kinaielekeza serikali kuhakikisha, kila mwaka wanatenga maeneo kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji, Chama kinaelekeza kwa mwaka huu wa fedha, Serikali ianze na maeneo kama vile skimu ya umwagiliaji ya Luiche-Kigoma, Kirya na Endagaw-Hanang, mabwawa ya Nyisanyi-Chato, Ilemba-Sumbawanga, Mkwale-Kyela, Ibanda-Geita, Mkombozi-Iringa, Ngomai-Kongwa na Idudumo-Nzega.
  • Chama kinailekeza serikali kukamilisha ujenzi wa Skimu za Mgambalenga-Kilolo, Mbaka-Busokelo na Muhukuru-Songea. Hatua hizi zitakwenda kuongeza wingi wa uzalishaji wa mazao ya kilimo. Chama kitafuatilia mpango huu kwa karibu ili kujiridhisha na mwenendo, tija, na ufanisi wa mipango hiyo. Maelekezo ya Chama Ibara ya 37 Ilani 2020-2025
  • KUONGEZA TIJA NA FAIDA KATIKA UZALISHAJI
  • Kutokana na changamoto ya mbegu ambayo imekuwa ikijitokeza kwa wakulima katika maeneo mengi, Chama kinaielekeza Serikali, kuongeza Bajeti ya Utafiti wa Mbegu. Taasisi zote zinazofanya utafiti zihusishwe kama zilivyoorodheshwa ndani ya Ilani Ibara ya 37 (B) (a). Aidha makampuni na taasisi za uzalishaji wa Mbegu Bora kama TARI, TOSCI na ASA ziwezeshwe ili kuongeza tija katika uzalishaji wa mbegu bora.
  • Mathalani mbegu za mafuta kama alizeti, tunaiagiza serikali kufungua mashamba mapya katika maeneo kama vile Msimba-Kilosa, Mwere-Mkinga, Bugaga-Kasulu, Kilimi-Nzega na Msungura-Chalize, hatua hii itasaida kuwa na uhakika wa utoshelevu wa mafuta ya kula nchini. Ongeza ufuta, maweze, karanga.
  • KILIMO BIASHARA
  • Ili kukuza masoko ya mazao yetu katika nchi jirani Chama kinaelekeza serikali kupitia wizara ya Kilimo, ujenzi wa ghala za kimkakati mipakani mfano katika mpaka wa Namanga na Mtukula ili kuimarisha uuzaji wa mazao nje ya nchi
  • Kutokana na uhaba mkubwa wa maghala ya kuhifadhia mazao kwa wakulima wetu nchini, CCM inaielekeza serikali kuanza ujenzi wa maghala katika wilaya za Chemba, Kiteto, Babati, Gairo, Namtumbo, Nanyumbu, Itilima, Kasulu, Kibondo, Buchosa, Bukombe, Kilosa pamoja Zanzibar. na Vihenge katika mikoa ya Dodoma, Mwanza, Katavi, Mtwara na Kigoma ili kukomesha changamoto ya uhifadhi wa mazao ya wakulima wetu.
  • Pia ili kukabiliana na uhaba wa masoko ya bidhaa zetu hasa za kilimo, Chama kinaielekeza serikali ihakikishe inafanya jitihada zote kupata eneo kwa ajili maonesha ya bidhaa za kilimo katika nchi kama vile Saudi Arabia na China na Nchi nyinginezo, serikali pia ijenge soko kubwa la kisasa katika wilaya ya Loliondo na maeneo mengine karibia na mipakani ili kukuza biashara ya mazao ya kilimo.
  • Ili kukabiliana na upungufu wa vitendea kazi kwa maafisa ugani wote nchini, Chama kinaelekeza Serikali ihakikishe kila Afisa Ugani anapatiwa usafiri kama vile Pikipiki ama magari kwa ajili ya kuwafikia wakulima na kuwapa elimu ili kukuza tija katika kilimo chetu nchini.
  • Ili kukuza wakulima wetu nchini, CCM inaielekeza Serikali ihakikishe inatoa mikopo ya pembejeo yenye masharti nafuu kwa wakulima, ikiwemo, mitambo ya mashambani, pembejeo za kilimo, matrekta ya mikono, zana za usindikaji matunda, mbogamboga na mazao mengine na vifungashio vya mazao, na Chama kupitia Halmashauri Kuu za ngazi mbalimbali kitafuatilia kwa karibu utekelezaji wake.
MSISITIZO NA MAELEKEZO YA CHAMA KWA SERIKALI KATIKA WIZARA MBALIMBALI

WIZARA YA NISHATI
  • UPATIKANAJI WA UMEME
  • Ili kuwa na nishati ya umeme ya kutosha, uhakika na bei nafuu Chama kinaielekeza Serikali, kupitia bajeti ya 2021/2025 kuhakikisha inakamilisha miradi yote ya uzalishaji, usafirishaji na usambazaji wa umeme nchini, hivyo serikali iendelee kutenga fedha za kutosha na kusimamia kikamilifu mradi wa umeme wa Mwl Nyerere ili ukamilike kwa wakati uliopangwa, na hapa nipongeze Serikali chini ya Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa namna inavyoupa kipaumbele mradi huu muhimu. Hatua hizi zitasaidia upatiakanaji wa nishati ya umeme ya kutosha, uhakika na bei nafuu nchini.
  • Chama kinaiagiza serikali ihakikishe vijiji vyote ambavyo havijapata umeme vinapata umeme mwaka huu wa fedha. Pia vijiji ama vitongozi ambavyo vilirukwa na awamu za usambazaji wa umeme zilizopita, navyo vinapata umeme, mathalani katika vijiji vya Chihanga, Nzasa na Kiterela mkaoni Dodoma,vijiji vya Asamba na Londono mkoani Songwe, vijiji vya Juani, Jibondo na Chole mkoani Pwani, vijiji vya Kiruku, Mgunduzi na Kibafuta Mkoani Tanga, vijiji vya Berega, Mabula, Itaragwe mkoani Morogoro, Vijiji vya Nanyindwa, Lilala, Chokoweti, Namajani, Nambawala, lukwika, Malumba, Mtawatawa, Chotowe, Namijati, Mitumbati, Njisa, Mbagala Mbuyuni na Nambaya Mkoani Mtwara, Vijiji vya Masimba, Mang’ole na Mlandala-Singida ili kushamirisha shughuli za maendeleo nchini.
  • Pia Chama kinaielekeza Serikali ihakikishe kuwa, kero zote na urasimu unaokera wananchi katika kuunganishiwa umeme unaondoshwa mara moja. Pia gharama za nguzo, mita na ankra za malipo ya umeme zinaondoshwa, kwani zimekuwa ni mzigo kwa wananchi.
  • UTAFUTAJI NA USAFISHAJI WA MAFUTA NA GESI ASILIA
Kwanza nianze kwa kumpongeza sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa kusimama imara na kuhakikisha hatua zote za ujenzi wa bomba la mafuta kutoka Hoima mpanga Chokoleani Tanga unakamilika kwa haraka.
  • Serikali ihakikishe inakamilisha mazungumzo kuhusu mradi wa usafirishaji wa gesi kutoka Tanzania kwenda Uganda, ambao utajengwa sambamba na Mradi wa Bomba la mafuta kutoka Hoima-Uganda mpaka Chokoleani- Tanga ili hatua za ujenzi wa mradi huo zianze mara moja. Mazungumzo hayo yazingatie malipo ya fidia kwa wananchi wanaopitiwa na mradi huo, Ili kuepusha usumbufu kwa wananchi wetu. Chama kinaelekeza pia, wananchi waishio pembezoni mwa mradi huo serikali ihakikishe wananufaika na uwepo wa maradi huo, kwa mfano katika masuala ya ajira, biashara, manunuzi na faida zingine.
  • USAFISHWAJI NA USAMBAZAJI WA UMEME
  • Kutokana na mahitaji makubwa ya umeme kwa wananchi, Chama kinaelekeza Serikali kukamilisha kwa haraka miradi ya usambazaji wa umeme ikiwemo miradi ya Rufiji – Chalinze-Dodoma, Mradi mwingine ni Kinyerezi hadi Chalinze, Geita, Nyakanazi hadi Kigoma, Singida na Arusha hadi Namanga.
  • Pia Chama kinaielekeza Serikali Kuhakikisha kunakuwepo na umeme wa kutosha na wa uhakika kwa ajili ya uendeshaji wa reli ya Kisasa (SGR).
HITIMISHO

Mahusiano ya CCM na Vyama vingine vya siasa Chama cha Mapinduzi kinavihakikishia vyama vyote vya siasa kutathmini vyama maelekezo ya Mwenyekiti wa CCM Taifa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, kuhakikisha vyama vyote vinafanya siasa safi zenye tija na maslahi mapana kwa Taifa.

Dhamira ya CCM bado iko pale pale ya kutoshiriki siasa za mti kwa macho, piga nikupige ama watu kuhasimiana kwa sababu za kisiasa. Hivyo tunawahimiza wanasiasa wenzetu kufungua milango ya utengamano, maelewano na siasa zenye mashiko na mantiki kwa mustkabali wa taifa.

Tunamshukuru Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Rais wa Zanziba kwa kazi nzuri inayoendelea tumepewa dhamana hii tunaahidi kusimamia kwa uadilifu, umakini, na ustadi wa hali ya juu. Tunaahidi kufanya sia safi zenye mashiko upeo na kubeba mustkabali mwema wa taifa katika katika kuwaunganisha watanzania bila kujali itikadi zao za vyama, Imani,

Kwa bahati mbaya ikitokea mtu ama kikundi cha watu wakafanya jambo katika njia yoyote kudhania wanaweza kumkwamisha Rais Samia Suluhu Hassan tunawahakikishia watanzania hawatamudu kumtikisa, kumvuruga na kumyumbisha. Chama cha Mapinduzi kikao mara na makini muda wote.

 
Hakuna jipya ataloongea huyu. Anauza sura tu.

Ataongea nn cha maana toka chama hiki chakavu?
 
Mheshimiwa Chongolo yupo mbashara muda huu kupitia Television ya Channel Ten akizungumza na Waandishinwa Habari

Tafadhali fuatilia na usisahau kumjulisha mwenzako
 
Ulikuwa ufanyike saa sita, halafu ukaingiliwa na ishu za bomba la mafuta
 
CCM ya Bashiru na CCM ya Chongoro wasipoangalia zinaweza kuwa CCM mbili, Mungu jalia iwe hivyo tuondokane na hii kitu inaitwa CCM
 
Nani ataweka bundle yake kumfuatilia huyo muhuni? Aende vijijini ambako huwa mnasema ndiko waliko wananchi wa kawaida, kwani huwa mnasema mitandaoni hakuna wapiga kura.
 
  • Thanks
Reactions: BAK
Mheshimiwa Chongolo yupo mbashara muda huu kupitia Television ya Channel Ten akizungumza na Waandishinwa Habari

Tafadhali fuatilia na usisahau kumjulisha mwenzako

Yaani watu wajulishane kuwa KM wa ccm anaongea!? Huyo asikilizwe na wazee ama watu wasiojitambua.
 
  • Thanks
Reactions: BAK
Back
Top Bottom