Chiriku yuko Tunduni

Mzee Mwanakijiji

Platinum Member
Mar 10, 2006
33,475
39,991
Chiriku wako ni wako, popote pale alipo,
Popote huko aliko, mawazoni kwake upo,
Ndege huyo ni wa kwako, Chiriku wa kwako yupo,
Chiriku yuko tunduni, mbona wewe humuoni?

Ni wewe ulimpata, Chiriku akawa wako,
Kama kalishwa limbwata, uliko wewe yeye yuko,
Wendako anakufuata, kama mwana na mbeleko,
Chiriku yuko Tunduni, mbona unamtafuta?

Ulimuahidi nini, Chiriku asubiria,
Ulisema siku gani, punje utamwagia,
Sasa kagoma tunduni, tenzi unamtungia,
Chiriku yuko tunduni, mbona unamlilia?

Chiriku kaimba nyimbo, na miluzi akapiga,
Muziki kama ulimbo, na wengine wakaiga,
Amekuwa ni makombo, kumbe wewe ulizuga,
Chiriku yuko tunduni, mbona wimbo hujajibu?

Chiriku ana huzuni, tunduni amejilaza,
Amefanya kosa gani, Chiriku ajiuliza,
Alalamika tunduni, nani atamtuliza,
Chiriku yuko tunduni, mbona kasahauliwa?

Beti zangu zinakoma, mapenzi ninakuasa,
Na ufanye wewe hima, Chiriku utamkosa,
Wengine waje jinoma, kwa yako wewe makosa,
Chiriku yuko tunduni, mbona akusubiria?!
 
Chiriku nimemtosa,mi alininyima raha,
Kwake raha nilikosa,ni maudhi Na karaha,
Imani nimeikosa,mi naisaka furaha,
Chiriku yuko tunduni,ye ataisoma namba.

Kupika wala hajui,we muulize mamaye,
Kupiga mie sijui,wamlaumu kungwiye,
Karudi kwao mwadui,kachakaa kama siye,
Chiriku yuko tunduni,ye ataisoma namba.

Chiriku ukijifunza,japo kupika ugali,
Mie utanipendeza,kwa kweli nitakujali,
Penda sana kujifunza,na mapishi mbalimbali,
Chiriku yuko tunduni,ye ataisoma namba.

Nakupa mezi mitatu,Ili wakufunde tena,
Ukileta utukutu,hatutoonana tena,
Na jifunze sana utu,uongee ya maana,
Chiriko yuko tunduni,ye ataisoma namba.

Najua mlimpenda,shemeji yenu chiriku,
Mwashangaa kwao kwenda,na begi tena usiku,
Ni mengi alinitenda,sikulalamika Huku,
Chiriko yuko tunduni,ye ataisoma namba.

Mi nisiongee sana,ngoja nimpe tu muda,
Nisije nikatukana,ikaja ikiwa shida,
Na namwomba maulana,aujali sana muda,
Chiriku yuko tunduni,ye ataisoma namba.



Sijui nimepatia au nimeharibu Ni shairi langu la kwanza kulitunga maishani mwangu.
Nalog off
 
>>Nahisi nipo peponi,nikiona sura yako.
Penzi lako la thamani,hakuna mfano wako.
Napata hamu moyoni,kushika kiganja chako.
Kilichokuwa laini,nalainika mwenzako.
Nikuonapo usoni,ni nyororo ngozi yako.
Sikuachi asilani,milele mimi ni wako.
Wewe ni wangu mwandani,nifanye chaguo lako.
Nitie ndani moyoni,nisije kufa mwenzako.
Kwani kwangu u moyoni,kukuacha mimi mwiko.
Sebuleni na chumbani,kwangu uje kuwa jiko.
Ni shuka langu la ndani,kwako sina hangaiko.
Nitatulia kitini,nije pata pumziko.
Nisemeze sikioni,linitoke sikitiko.
Mrembo hadi gizani,hata hujapakwa piko.
Ungelikuwa angani,malaika peke yako.
Utamu wako mezani,nilizuri pishi lako.
Oho malaika wangu,ipooze roho yangu.
Kwako sipati uchungu,upo kwenye moyo wangu.
Nishike mkono wangu,utazame mboni yangu.
Utajiona mwenzangu,wewe ulo chungu changu.
Ivisha chakula changu,kitamu kiso kichungu.
Zawadi toka kwa mungu,ilofika hapa kwangu.
Naapa haki ya mungu,paka kifo wewe wangu.
Niseme nini mwenzako,nahisi nipo peponi.
Mazuri mahaba yako,yasiyouzwa sokoni.
Mazuri mahaba yako, hayapo hata dukani.
Shairi:NAHISI NIPO PEPONI.
Mtunzi:Idd Ninga wa Tengeru Arusha.
0655519736.
 
Hata yule wa kilosa, eti chiriku apenda
hata yule mwenye kosa, chiriku anamlinda
humpa kwenye kisosa, chakula hata matunda
chiriku tunduni baki

Chiruki anastahili, amepata alotaka
Alikuwa mhimili, porini akatimka
Tena kwa punje viwili, bandani akajiweka
Baki tunduni chiriku

Sauti iso mithili, chiriku alipo gamba
maneno yenye mithali, porini alivyotamba
chiriku kawa muhali, na kelele kwa mjomba
chiriku baki tunduni

Porini vipi arudi, kundini Hawamtaki
bandani nako hasidi, ukimya hapati kiki
chiriku hana ahadi, fungeni banda abaki
baki tunduni chiriku

ngoja nianue jamvi, tundu niende lifunga
chiriku kawa mgomvi, alomweka Si mjinga
nisije ongeza chumvi, nafunga tena kwa ninga
Chiriku baki tunduni
 
Tunduni abaki sana,hili fundisho kwa wote,
Na bora iwe lawama,Mi siogopi chochote,
Mi nilimpenda sana,waulize watu wote,
Chiriku asoma namba,walobaki wanalia.

Walobaki wanalia,chiriku asoma namba,
Na machozi wanalia,msamaha kuniomba,
Mengi nimevumilia,kwa ndani ya ile nyumba,
Chiriku asoma namba,walobaki wanalia.

Chiriku hana mpango,kawaulize mafia,
Kidogo nipate pengo,yeye kumgombania,
Nilimpa Na mjengo,wa rangi ya kahawia,
Chiriku asoma namba,walobaki wanalia.

Mwaka Sasa unaisha,ninahitaji furaha,
Chiriku alinitisha,nilidhani Ni mzaha,
Naangalia maisha,sitaki fuga usaha,
Chiriku asoma namba,walobaki wanalia.

Nimelitumbua jipu,ni kwapani kwa chiriku,
Mi naumwaga u -pu- pu,pale kwenye mchiriku,
Ni bora Nile mapupu,kuliko mbovu kuku,
Chiriku asoma namba,walibaki wanalia.

Krismas peke yangu,nijiachie kwa hamu,
Mie sitaki majungu,mi nitatulia homu,
Bora niwale machangu,nagonga kila sehemu,
Chiriku aisoma namba,walobaki wanalia.


Mwaka waisha salama,namshukuru rabana,
Nawe pia pata mema,na ufurahi kwa sana,
jifunze mwaka mzima,Ili uwe wa maana,
Chiriku asoma namba walibaki wanalia.


Nitaimalizia natoka kidogo
Nalog off
 
Back
Top Bottom