Na Fadhili Mpunji
Katika miaka ya hivi karibuni sekta ya Tehama imekuwa na maendeleo makubwa katika nchi mbalimbali za Afrika, maendeleo ambayo si kama tu yamekuwa na manufaa kwenye mawasiliano, habari na utangazaji, bali pia yamekuwa na manufaa makubwa kwenye sekta za afya, elimu, biashara na hata utawala bora. Licha ya kuwa kiwango cha maendeleo kiko tofauti katika viwango tofauti katika nchi mbalimbali, ukweli ni kwamba yanaleta mabadiliko chanya katika kila nchi.
Ripoti ya mwenendo wa maendeleo ya Afrika (Africa’s Development Dynamics -AfDD) iliyotolewa Januari 2021 kwa ushirikiano kati ya Umoja wa Afrika na kituo cha maendeleo cha Shirika la ushirikiano wa na maendeleo ya uchumi (OECD), inaonyesha kuwa katika kipindi cha miaka 10 iliyopita matumizi ya internet barani Afrika yameongezeka kwa zaidi ya mara 50, urefu wa mkonga wa mawasiliano umeongezeka kwa zaidi ya mara nne, idadi ya watu wanaoomba huduma ya simu za mkononi imeongezeka mara mbili, na asilimia 58 watu wa Afrika wanaishi kwenye maeneo yenye huduma ta 4G.
Kenya ni moja kati ya nchi zenye maendeleo makubwa zaidi ya sekta ya Tehama barani Afrika, na sasa inaongoza barani Afrika kwa kuwa na asilimia 85 ya watu wake wanatumia Internet, Rwanda asilimia 45, Uganda asilimia 39, na Tanzania asilimia 38. Takwimu hizo zinabadilika kila mwaka kutokana na kuendelea kwa juhudi za serikali za nchi za Afrika kueneza huduma ya Tehama, na kuongeza kwa idadi ya watu wanaonunua vifaa vya kutumia huduma ya internet.
Maendeleo haya sio kama tu yamekuwa na mchango mkubwa katika kuhimiza mawasiliano, bali pia yamekuwa na mchango mkubwa katika kuhimiza maendeleo ya kiuchumi na kijamii. Ripoti pia imesema kwa sasa barani Afrika kuna zaidi ya akaunti milioni 480 za pesa mtandao (mobile money accounts), na makampuni zaidi ya 500 yanayotoa huduma za fedha kwa kutumia tehama. Watu wenye mapato ya chini katika nchi mbalimbali za Afrika, sasa inawezekana kutokana na huduma matumizi ya huduma za pesa mtandao kama vile M-pesa au Tigo-Pesa. Huduma hii imefika hata kwenye maeneo ambayo ni vigumu kwa mabenki kutoa huduma kutokana na changamoto za miundombinu. Hali hii pia imewasaidia wajasiriamali kuweza kufanya shughuli zao bila vizuizi vya huduma ya fedha.
Tunaweza kuona pia jinsi sekta binafsi inavyoendelea kuchangamka kutokana na watu kutumia internet kujiajiri, iwe ni kwenye kufanya biashara, au kutumia majukwaa mbalimbali ya kimtandao kufungua shughuli zao kwenye sekta za habari, sanaa, utamaduni na hata mawasiliano.
Kwenye upande wa utawala bora, pia tumeshuhudia jinsi ushirikishaji wa umma katika kufuatilia utendaji wa idara mbalimbali za serikali kwa njia ya internet, kwa kuripoti mambo ambayo hatimaye yanafuatiliwa na kufanyiwa maamuzi na taasisi zisizo za kiserikali, watunga sera na hata watawala.
Licha ya kuwa haya ni maendeleo makubwa, ikilinganishwa na nchi zilizoendelea bado bara la Afrika liko nyuma, na pengo la kidigitali barani Afrika ni kubwa. Mara kwa mara tumekuwa tukisikia juhudi za kupunguza pengo hili barani Afrika. Hatuwezi kutaja maendeleo ya sekta hii barani Afrika bila kutaja mchango wa China katika eneo hili. Inakadiriwa kuwa karibu asilimia 70 ya mtandao wa huduma ya 4G barani Afrika umejengwa na makampuni ya China (Huawei na ZTE). Sehemu kubwa ya mkonga wa mawasiliano (optic fiber) katika nchi za Afrika Mashariki pia umewekwa na makampuni ya China. Hii ni mbali na vifaa vingi kama vile simu za mkononi, Kompyuta n.k.
Eneo la Tehama ni moja ya maeneo yenye mustakabali mzuri wa uwekezaji barani Afrika, na ni eneo ambalo bado lina changamoto. Tofauti na nchi za magharibi ambazo zimekuwa zikitoa kauli na takwimu za mara kwa mara kuhusu pengo la kidigitali barani Afrika, China imekuwa inatumia fursa za ushirikiano na nchi za Afrika kuendelea kupunguza pengo hilo.