China kutoa mikopo ili kuweka ‘mtego wa madeni’ kwa Afrika ni kauli za uzushi tu

ldleo

JF-Expert Member
Jan 9, 2010
1,006
1,026
NA PILI MWINYI

VCG111338665022.jpg
Hakuna ubishi kwamba China sasa ni nchi yenye nguvu kubwa duniani. na ni nchi ya pili kwa uchumi mkubwa duniani. Kwa nchi nyingi, kutoka Asia, Afrika hadi baadhi ya sehemu za Ulaya, China imekuwa mshirika muhimu na mkubwa wa kiuchumi. Mwaka 2009, China iliipindua Marekani na kuwa mshirika mkubwa wa biashara wa nchi za Afrika, pia ni mkopeshaji mkubwa wa sekta za umma katika Afrika. Lakini licha ya nchi hii kuwa kubwa kiuchumi, mara nyingi kumekuwa na taarifa chache au za kupotosha kuhusu utoaji wake mikopo au uwekezaji katika Afrika.

Oktoba 26, Ofisi ya Habari ya Baraza la Taifa iliitisha mkutano na wanahabari ambapo mkurugenzi wa Idara ya Taifa ya Ushirikiano wa Maendeleo ya Kimataifa Luo Zhaohui, na manaibu wake Zhang Maoyu, Zhou Liujun, na Deng Boqing, walitambulisha msaada wa China wa kupambana na janga la Corona na ushirikiano wa maendeleo ya kimataifa, pamoja na kujibu maswali ya wanahabari.

Katika majibu yake kwa wanahabari walioulizia kuhusu msaada wa China katika nchi za nje na masuala ya madeni katika nchi za Afrika, naibu mkurugenzi Zhou Liujun, alisema tatizo la madeni ya Afrika limefuatiliwa sana. Lakini pia kuna sababu za nje kama vile thamani ya sarafu.

Katika miaka miwili iliyopita, kutokana na athari za janga la Corona, matatizo ya madeni katika Afrika yamekuwa makubwa. China inatilia maanani sana shinikizo la madeni linalozikabili nchi za Afrika.

‘Siku zote tunaheshimu matakwa ya Afrika katika ushirikiano wa kifedha na Afrika ambao unafuata msingi wa mahitaji ya Afrika. Wakati tunapotoa mikopo isiyo na riba na ya upendeleo, tunazingatia kwa kina hali ya madeni na uwezo wa kulipa wa nchi zinazokopeshwa za Afrika, na kuzingatia sheria na kanuni, uwazi kwenye kazi yetu, na kamwe hatutafuti kujipatia manufaa binafsi ya kisiasa”. alisema naibu Zhou Liujun.

Lakini licha ya nia njema na juhudi zinazochukuliwa na China katika Afrika, kumekuwa na madai ya kwamba kitendo cha China kuikopesha Afrika, kimezilazimisha nchi za Afrika kuingia kwenye mitego ya madeni, kusema kweli madai haya hayana msingi wowote na ni ya uzushi tu. Imesahaulika kwamba matatizo ya madeni ya Afrika yameanzia tangu zamani na ni masuala ya kihisoria, licha ya hayo pia yanatokana na kuongezeka kwa hatua za kujilinda na sababu za thamani ya sarafu.

Janga la Corona limeziathiri sana nchi masikini za Afrika zenye madeni makubwa na kuziacha njia panda nchi hizo zisijue la kufanya. Kama alivyosema Waziri mkuu wa Ethiopia Abiy Ahmed, Aprili mwaka jana kwamba viongozi wa Afrika wamelazimika kuchagua moja, ama kuendelea kulipa madeni au kuelekeza moja kwa moja rasilimali zao ili kuokoa maisha ya watu wao. Na wakati wakichagua kuokoa maisha ya watu wao, mara nyingi wanapaswa kuiangalia China ambaye ni mkopeshaji wao mkubwa.

China ikiwa rafiki na mwenzi mkubwa wa nchi za Afrika haikuonesha hiyana wala uchu katika kipindi hiki kigumu, lakini badala yake ilitilia maanani kwamba China na Afrika zina mustakabali wa pamoja hivyo wangebeba taabu zote zinazotokana na janga la Corona kwa pamoja. Wakati huohuo Rais Xi Jinping na viongozi wa nchi husika za Afrika walifanya mkutano maalumu wa pamoja kati ya pande mbili ambapo lengo lake likiwa kuleta mataifa ya Afrika na China pamoja katika kupambana na janga la Corona, na rais Xi alitangaza hatua nyingi muhimu za kusaidia maendeleo ya nchi za Afrika, ikiwemo kupunguza madeni na kuongeza muda wa kulipa madeni.

Swali la kujiuliza ni kwamba je kama kweli China ilikuwa na nia mbaya ama kuitega Afrika kupitia madeni, ingethubutu kuchukua hatua kama hizi za kuisaidia Afrika katika wakati wa dhiki? China inahimiza kwa nguvu zote na kutekeleza Mpango wa Kupunguza Madeni wa Kundi la nchi 20 (G20). Pia imesaini mpango wa kupunguza madeni au kufikia makubaliano na nchi 19 za Afrika kwa ajili ya kusamehe nchi zote za Afrika zenye maendeleo duni, nchi masikini zenye madeni makubwa, nchi zinazoendelea zisizo na bandari na nchi za visiwa vidogo ambazo zilipaswa kulipa madeni mwishoni mwa mwaka 2020.

Kwa mujibu wa Zhou Liujun, ufumbuzi wa tatizo la madeni ya Afrika unategemea na maendeleo, na ni muhimu kwa nchi za Afrika kuongeza uwezo wao wa kujitegemea kimaendeleo na kupata maendeleo endelevu.

Wachina wana msemo “kama ukitaka kuwa tajiri, kwanza anza kujenga barabara”. Takwimu zinaonesha kuwa kupitia ushirikiano huu, China imejenga zaidi ya kilomita 6,000 za reli, zaidi ya kilomita 6,000 za barabara, bandari karibu 20, na zaidi ya vituo vya umeme 80 katika Afrika. Kwa maana hiyo hakuna nchi inayoendelea iliyojiingiza kwenye mtego wa medeni kutokana na mikopo ya China, bali shutuma kama hizi zinatolewa kwa lengo la kisiasa na kwa ajili ya kuvunja uhusiano wa kirafiki na ushirikiano kati ya China na Afrika.
 
Wachina wazamani sio wachina wa sasa.

Ili Afrika iendelee inahitaji kujiendeleza yenyewe bila kutegemea Mchina wala mzungu .

Iwekeze Kwenye sayansi na teknolojia
 
Bora mchina kuliko hao wazungu,wazungu hata chanjo tu wanashindwa kutupa,sembuse barabara ,wataweza kweli
 
Back
Top Bottom