nngu007
JF-Expert Member
- Aug 2, 2010
- 15,862
- 5,797
Thursday, 12 May 2011 19:11 newsroom
* Mwakani mwisho wa mafisadi dagaa
* Asema CCM itabaki na waadilifu tu
NA BASHIR NKOROMO, SINGIDA
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), kitatumia uchaguzi mkuu wake kuwaengua viongozi wote wasio waadilifu na mafisadi. Uchaguzi huo unatarajiwa kufanyika baadaye mwakani na kwamba, utatumika kusafisha masalia ya watuhumiwa wa ufisadi, ambao watakuwa bado hawajajiondoa. CCM imewataka watuhumiwa wa ufisadi kujiondoa wenyewe, vinginevyo nguvu itatumika wakati wa kikao cha NEC ya CCM, kinachotarajiwa kuketi Julai au Agosti, mwaka huu. Hata hivyo, CCM imesema kuwa ikilazimu kinaweza kuitisha mkutano wa dharura na kutekeleza agizo hilo kwa maslahi ya Chama na Watanzania kwa jumla. Hayo yalisemwa na Naibu Katibu Mkuu wa CCM (Bara), John Chiligati, wakati akizungumza na wajumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM mkoani hapa katika Ukumbi wa
FDC, jana. Chiligati, ambaye alikuwa Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi katika Sekretarieti iliyopita, alisema CCM imedhamiria kuwasafisha wanachama na viongozi wasio waadilifu. Alisema, hiyo ni miongoni mwa mikakati ya wazi iliyopitishwa na CCM mjini Dodoma, wakati ikiwa katika mchakato wa kujivua gamba kulikosababisha Kamati Kuu na Sekretarieti yote kujiuzulu na kuundwa mpya.
Chiligati alisisitiza kuwa watuhumiwa wa ufisadi ndani ya CCM wajitafakari wenyewe na kuchukua hatua, kinyume na hapo watangolewa. Pia, alisema ikionekana muda wa kufikia kikao kingine cha NEC ni mbali, mkutano wa dharura unaweza kuitishwa ili hatua za haraka zichukuliwe ili kukiacha Chama kikiwa safi mbele ya jamii. Alisema CCM imedhamiria kuwa na wanachama na viongozi wenye maadili safi mbele ya jamii na ndiyo, msingi wa kujivua gamba ili kusafisha wachafu. Hatutawavumilia wanachama na viongozi wachafu wanaotumia mgongo wa CCM na vyeo walivyonavyo ndani ya Chama na serikali kujilimbikizia mali, alisema.
Alisema ili kufikia malengo hayo, NEC ilipitisha uamuzi wa kuwepo kamati maalum ya udhibiti ili kurejesha nidhamu ndani ya Chama na kwamba, itakuwa na jukumu la kuzuia mpasuko wakati wa uchaguzi. Kuhusu kura za maoni, alisema zitakuwa zikipigwa na wananchi mapema ili kupata muda wa kusikiliza malalamiko, rufani, uchaguzi uliopita CCM haikuwa na muda wa kutosha ndiyo sababu zilijitokeza kasoro nyingi.
Pia, alisema uchaguzi huo utakuwa na uchujaji wa awali, na kwamba si kila anayechukua fomu atagombea, kwani itakuwa nafasi moja kwa watu watatu, anayeshinda lazima apate nusu ya kura.
Katika hatua nyingine, Chiligati aliongeza kuwa CCM imepitisha utaratibu wa kutoruhusu mwanachama wake kuwa na vyeo vingi kiutendaji, kwani hali hiyo imesababisha kasoro nyingi.
Chiligati yupo mkoani hapa katika ziara ya kuitambulisha Sekretarieti mpya ya CCM, ambapo amefuatana na Katibu wa NEC, Itikati na Uenezi, Nape Nnauye, Katibu wa NEC, Uchumi na Fedha, Mwigulu Nchemba na Katibu wa NEC, Oganaizesheni Asha Juma Abdallah.