Chama Kipya (CCJ) na Hatima ya CCM - lisemwalo...

Boramaisha

JF-Expert Member
Apr 29, 2009
820
18
  • Mshindo wake kuiyumbisha nchi
  • Kinaitwa Chama cha Jamii (CCJ)
  • Ni matokeo ya mitafaruku CCM
Mpasuko%5B1%5D%5B1%5D.jpg


NA MWANDISHI WETU
CHANZO: Gazeti la Raia Mwema

HUENDA sasa utabiri wa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, ukatimia kwa habari kwamba chama kipya cha siasa ki mbioni kuanzishwa kikihusishwa na vigogo wa serikalini na wa ndani ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Raia Mwema imebaini.

Uchunguzi wa Raia Mwema umethibitisha kufanyika kwa maandalizi ya kuanzishwa kwa chama hicho: Chama Cha Jamii (CCJ); ambacho rasimu ya katiba yake inadai kuwa kinakuja kukidhi kiu kubwa ya Watanzania wengi waliochoshwa na hali mbaya ya mahusiano ndani ya CCM na mitafaruku isiyoisha ndani ya vyama vya Upinzani.

Raia Mwema imethibitishiwa na watu wazito ndani ya Serikali na ndani ya CCM kwamba tayari kulikuwa na maandalizi ya kuanzishwa kwa chama kipya kama hatua mojawapo ama Mpango A, au kama itabidi basi vigogo hao wajitose katika chama kimoja cha siasa katika Mpango B.

Raia Mwema imearifiwa kwamba Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete, ana habari na mipango hiyo yote miwili na amenukuliwa akisema kwamba hatakubali CCM kumpasukia mikononi, kama ambavyo alipata kusema kwamba hatakubali Muungano wa Tanganyika na Zanzibar wa mwaka 1964 kuvunjika mikononi mwake.

Taarifa nyingine zinasema baadhi ya vigogo wanaotajwa kuhusika na chama hicho wamekwisha kuhojiwa na vyombo vya dola na hakuna kati yao aliyekana kufahamu uanzishwaji huo, japo walikwepa kuhusika moja kwa moja huku mmoja wao akinukuliwa kwamba: "Hatuwezi kuacha tunadhalilishwa kiasi hiki, ikibidi tutatumia haki yetu ya kikatiba kuunda chama. Tunaomba mtuunge mkono na si kutuzuia."

Kwa mujibu wa habari hizo, kuzinduliwa kwa chama hicho kipya kumecheleweshwa ama kuahirishwa kutokana na sababu kadhaa za kisiasa ikiwamo mkakati wa kuangalia "mwelekeo wa kisiasa na kusoma alama za nyakati kabla, wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2010," kinaeleza chanzo maalumu cha Raia Mwema.

Raia Mwema linalo majina ya wanasiasa maarufu nchini wanaoratibu mchakato wa kuanzisha chama hicho hadi kukisajili; lakini kwa sababu za kitaaluma haliwezi kutaja majina hayo kwa sasa.

Katika Mpango B, vyama vya Upinzani ambavyo vinatajwa sana kuwa huenda vikatumika na vigogo hao wa CCM kujiunga navyo ni pamoja na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Chama cha Wananchi (CUF) na NCCR-Mageuzi, kila chama kikiwa tayari kinacheza karata zake kuhakikisha kinawanasa.

Kwa haraka haraka inaelekea kama ikibidi vigogo hao kujiunga na Upinzani, uwezekano mkubwa utakuwa ni kwenda CHADEMA chenye viongozi wanaoonekana kuwa karibu na makundi kadhaa ya vigogo ndani ya chama tawala. CUF kinapewa nafasi ya pili kutokana hasa na nguvu yake Pemba kinakoshikilia usukani.

Bado si wazi hasa CCJ kitachota wana-CCM wa kundi gani kati ya mawili makubwa yanayosuguana ndani ya chama hicho. Hata hivyo, kwa kiasi kikubwa itategemea uamuzi wa mapendekezo ya Kamati ya Rais Mstaafu, Ali Hassan Mwinyi iliyoundwa kuchunguza mgongano miongoni mwa wabunge wa CCM na wajumbe wa Baraza la Wawakilishi.

Raia Mwema imefanikiwa kupata nakala ya rasmu ya katiba ya CCJ ambayo katika sehemu ya utangulizi inakipamba chama hicho kuwa na malengo ya kutetea haki za wananchi, matumizi sahihi ya raslimali za kitaifa na msisitizo katika suala la elimu.

Baadhi ya sehemu za utangulizi wa rasimu ya katiba hiyo zinasomeka: "Kwa kuwa uhuru tulioupata ulitupa fursa ya kujenga Nchi na Taifa lenye kubeba matumaini ya wananchi wote kwa ujumla kwa kuweka misingi imara ya kuheshimu na kuzingatia usawa wa binadamu, utawala bora, utawala wa sheria, haki za binadamu, hifadhi na ustawi kwa wananchi wote na utaifa wetu; na

"Kwa kuwa ukombozi kamili wa mwananchi kisiasa, kiuchumi na kijamii unahitaji juhudi, maarifa, moyo wa kujituma na ujasiri wa kuthubutu kwa upande wa viongozi, vipaji ambavyo bado kuviona vikitumika nchini; na

"HIVYO BASI, SISI WANANCHI WAZALENDO tuliokutana hii leo tarehe ... ... ... jijini Dar es Salaam kutekeleza wajibu wetu kikatiba wa kuunganisha pamoja mawazo yetu na kuunda chama cha siasa kinachozingatia changamoto zote zinazoikabili nchi yetu tangu baada ya uhuru na kinachobeba matarajio ya wananchi ya leo na kesho, kwa jina la CHAMA CHA JAMII, kwa kifupi CCJ, ambacho lengo lake kuu ni kuleta mageuzi ya kitaifa ya kidemokrasia, kiuchumi, kijamii na kisiasa kwa faida yetu sote sasa na ya vizazi vijavyo."

Kwa mujibu wa rasimu hiyo, chama hicho kinatarajiwa kuwa na bendera yenye rangi tatu na nembo ya mikono iliyoshikana pamoja ambayo ni ishara ya nguvu ya umoja.

"Bendera ya chama itakuwa na rangi kuu tatu ambazo ni Kijani, Nyeusi na Dhahabu. Kijani inaashiria kilimo, mazingira na uoto wa asili; Nyeusi inaashiria watu wa Tanzania; na dhahabu inaashiria raslimali nchi," inaeleza sehemu ya kwanza ya katiba hiyo na kubainisha kuwa itikadi ya CCJ itakuwa ustawi na hifadhi ya jamii (social welfarism), itikadi inayotajwa kuambatana na demokrasia ya kijamii na utawala wa katiba na sheria.

Chama hicho pia kimepangwa si tu kuwa na malengo na madhumuni lakini pia kitakuwa na imani yake. Imani ya chama hicho inatajwa kuwa ni; "Binadamu wote huzaliwa huru, na wote ni sawa;

Kila mtu anastahili heshima ya kutambuliwa na kuthaminiwa utu wake;

"Hifadhi na ustawi wa jamii yetu vitapatikana kwa matumizi bora na endelevu ya utajiri wa rasilimali tulizonazo, serikali kuwajibika kwa wananchi ambao ni msingi wa mamlaka yote katika nchi, na kupiga vita ufisadi kwa nguvu zetu zote," inaeleza sehemu ya imani za CCJ.

Malengo na Madhumuni ya chama hicho ni pamoja na kuhakikisha uwekezaji unatekelezwa kwa kumnufaisha mwananchi kutokana na rasilimali alizonazo na zinazomzunguka na kamwe usitoe fursa kwa wageni kuhodhi rasilimali hizo bila ushiriki wa wananchi na pia kuhakikisha shughuli za uchumi haziruhusu ulimbikizaji wa mali au njia kuu za uchumi katika mamlaka ya watu wachache binafsi;

"Kujenga umoja wa kitaifa kwa kutoa fursa sawa na za kutosha kwa wananchi wote wake kwa waume bila kujali rangi, kabila, dini au hali ya mtu; Kuhakikisha kwamba aina zote za dhuluma, vitisho, ubaguzi, uonevu, rushwa au ufisadi zinatokomezwa nchini; Kuhifadhi na kuendeleza mazingira kwa ajili ya uhai na afya ya binadamu na viumbe vingine na kwa faida ya vizazi vijavyo ;

"Kulinda haki ya kila raia ya kujielimisha au kutafuta elimu katika fani anayopenda hadi kufikia upeo wowote. Kuhakikisha kuwa mfumo wetu wa uchaguzi ni huru na unaotoa fursa stahili kwa wananchi kuchagua viongozi wanaowataka bila kurubuniwa kwa rushwa na takrima za aina yote yote ile;

Kudumisha maadili ya uongozi (uadilifu, uwajibikaji kwa wananchi na kutenda haki) katika chama na serikali kama yalivyoainishwa na kusimamiwa na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere katika uongozi wake kitaifa uliotukuka.

Malengo mengine ya chama hicho yanatajwa kuwa ni kushinda katika chaguzi zote zinazofanyika nchini kwa kutumia ushawishi wa nguvu ya hoja na kuunda Serikali Kuu na Serikali za Mitaa katika pande zote mbili za Muungano ili kuiwezesha CCJ kutafsiri malengo na madhumuni yake kama yalivyoainishwa kwenye ibara hii kwa vitendo.

Sifa za uanachama katika chama hicho ni kuwa raia wa Tanzania; umri usiopungua miaka 18, awe na akili timamu; kuikubali, kuiamini na kuitii Katiba ya CCJ na kanuni zilizotungwa chini yake; kuwa na kadi iliyolipiwa ada stahili za chama; asiwe mwanachama wa chama kingine cha siasa;

Msajili wa wa Vyama vya Siasa nchini, John Tendwa, hakuweza kupatikana jana kuzungumzia kuanzishwa kwa chama hicho kipya, lakini sheria inakilazimu chama kipya kuanza kwa kupata usajili wa muda kabla ya kulazimika ndani ya miezi sita kupata wanachama angalau 200 katika mikoa 10 angalau minane ya Tanzania Bara na miwili ya Zanzibar.

Masharti mengine ni pamoja na kuwa na katiba ambayo inaendana na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania isiyokiuka sheria na ambayo haihamasishi ukabila, udini, fitina, vurugu na uhasama.

Tayari kumekuwa na misuguano mikali ndani ya CCM na hata ndani ya baadhi ya vyama vya upinzani, hali ambayo inawafanya baadhi ya wananchi wakiwamo watendaji serikalini wanaokusudia kuingia katika siasa kuwa katika kigugumizi cha chama gani wanachoweza kujiunga nacho.

Kutokana na misuguano hiyo, hali ya kisiasa kuelekea uchaguzi wa mwaka huu imekuwa haitabiriki hasa kwa kuwa baadhi ya watu ndani ya CCM wamekuwa wakidaiwa kuweka mikakati ya kuwania urais kupitia chama hicho, jambo ambalo linakwenda kinyume na utamaduni ambao chama hicho kimejiwekea wa Rais aliye madarakani kuendelea kugombea kwa vipindi viwili.

Hatua ya wanasiasa hao, imeibua mjadala mpya uliohusisha hadi viongozi wa dini na watabiri akiwamo mnajimu Sheikh Yahya Hussein ambaye ametoa kauli ya kitisho kwamba atakayegombea na Kikwete atapoteza maisha, kauli iliyoibua mjadala na kupingwa na wengi wakiwamo Mbunge wa Maswa, John Shibuda, ambaye amesema atagombea na hatoogopa kifo. Shibuda alikuwa mmoja wa wagombea urais wa 11 wa CCM mwaka 2005.

Ndani ya CCM nako hadi sasa kumekuwa na mgawanyiko mkubwa juu ya kuunga ama kutounga mkono uamuzi wa kuzuia wanachama wengine kugombea urais mwaka huu, hali ambayo imeelezwa kuwagawa viongozi wa chama hicho mkoani Dar es Salaam, ambao wanapingana kuhusu kuandaa maandamano kuhusiana na suala hilo.

Karibu na Uchaguzi Mkuu wa mwaka 1995, Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere aliwahi kuweka bayana kuwa upinzani wa kweli utatoka CCM na hasa baada ya chama hicho kumeguka.

Kwa mujibu wa mtazamo huo wa Mwalimu Nyerere, kumeguka kwa CCM kunakoweza kuunda upinzani wa kweli nchini kunasindikizwa na hoja kwamba chanzo cha mmeguko kitakuwa tofauti ya makundi yanayopigania asili ya chama hicho na kundi jingine linalopigania maslahi binafsi, hali ambayo imejionyesha wazi kwa wakati huu.

Hali hiyo ya mgawanyiko wa makundi moja likipigania misingi ya kuanzishwa kwa chama hicho na jingine likipigania maslahi binafsi ya kisiasa, kumejitokeza miongoni mwa wabunge wa chama hicho kiasi cha kuundiwa Kamati maarufu kwa jina la Kamati ya Mwinyi.

Kamati hiyo iliundwa ndani ya Halmashauri Kuu (NEC) ya CCM katika kikao chake kilichopita, ikiwahoji wabunge ambao baadhi walifikia hatua ya kutoleana maneno ya kashfa na hata matusi, wakiwa pamoja na baadhi ya mawaziri.

Ripoti hiyo ya Kamati ya Mwinyi inatarajiwa kuwasilishwa katika kikao kijacho cha NEC kinachotarajiwa kufanyika Jumatatu na Jumanne, wiki ijayo, mjini Dodoma kikitanguliwa na kikao cha Kamati Kuu kinachotarajiwa kuketi Jumamosi, wiki hii.

Kati ya mapendekezo yanayotarajiwa ni pamoja na kuwavua madaraka viongozi watuhumiwa wa ufisadi, uamuzi unaotarajiwa pia kukumbana na upinzani mkali kutoka miongoni mwa haohao wanaCCM.

Kamati ya Mwinyi inawajumuisha Makamu Mwenyekiti wa CCM-Tanzania Bara, Pius Msekwa na Spika wa zamani wa Bunge la Afrika Mashariki, Abdulrahman Kinana.

 
Hii inaonekana kama zao la wakereketwa wa CCM asili ile ya Nyerere, hata mengi ya maneno yaliyotumika kwenye katiba yake yanaonekana yamechotwa kutoka ile iliyokuwa TANU
 
Ni wale wale tu,hakuna mpiganaji katika ufisadi................Wa tanzania tutaendelea kuliwa mpaka siku ya mwisho!!!
 
Haya kumekucha sasa wana CCM,Mbona gazeti halikutaja waasisi tuanze kuchukua kadi?Kama ni kizazi kipya nipo tayari saa na wakati wowote,Ila kama ni masalia ya Chama tawala-HAKUNA JIPYA -Ni ngonjera tu mvinyo ulele bali chupa safari hii ni mpya! Leteni habari za kutosha tupo wanachama watarajiwa kibao,Kwani huu utitiri wa vyama uliopo umeshindwa kukidhi haja zetu,
 
Kama wao M sisi J kaazi kweli kweli, sisiM (CCM) na sisiJ (CCJ).
 
Hakuna kitu hapo.. ni propaganda tu!!! hao wanaotoka ccm watakuwa kama mbeki na wenzake!!! ni tamaa tu ya uongoza sasa wanaona wanatishiwa huko majimbo ndio wakaona waanza zengwe jingine

mimi naamini hakuna kongozi au mbunge wa sasa wa ccm aliye msafi kiasi cha kunyooshea kidole mtu yeyote... yaani walikuwa wapi 2007 wakati moto unawaka? hadi waone kampeni za ccm zimewakalia vibaya ndio wanatupa kiini macho

ccj mai fut!!
 
mhhhh!! kazi kweli kweli... isije ikawa ni chama wale makada wa chama (ccm) waliohisi kutoswa na kupuuzwa baada ya 2005 wamekitegesha hicho, just in case.

Mkuu bora maisha, weka hiyo article tusome bana...
 
Yaani Raia Mwema ajue kabla JF haijajua?? sidhani kama hii habari ni genuine
 
Nimeisoma hii habari kwenye gazeti it is so interesting,halafu habari hii inaoana na stori ya Kubenea kwamba JK njiapanda,CCM kumfia mkononi,vigogo kibao kutimka.I wish this could real happen kwenye hiki chama.Ila siungi mkono hoja ya kuanzishwa chama kipya,Tanzania inavyama vingo mno kwa kweli.Wangechukua tu huo mpango wa pili wa kuhamia kwenye chama mojawapo cha upinzani na kuongeza nguvu huko.
 
Masaki, I thought so too!!

Kina-sound ki- freemasons freemasons, sije kikawa na code za Dan Brown kuchukua kura toka kwa CHADEMA na CUF, halafu inakuja ile hadithi ya mzee kobe (CCM) kushinda mbio za uchaguzi kwa vile sungura alivyofika katikati ya mbio za uchaguzi akaamua kulala kwa vile mzee kobe(CCM) wamemuacha mbaliii kabisa, usingizi ukamkolea sungura huku mzee kobe akijikongoja akapita kwa hatua za kunyata zisizo na mshindo, sungura alivyozinduka mbio zimekwisha mshindi mzee kobe.

Hizi ni alama za nyakati kwa wapiga kura na CHADEMA/CUF kushikilia uzi ule ule, maana mzee kobe kesha ona mambo magumu na kuleta chama feki miezi 9 kabla ya uchaguzi. Si ajabu Maalim alishastuka ndo maana anaona CCJ inakuja hivyo na wao wameweka mkakati w kuruka mtego.

Hivyo hao freemasons -CCJ wakija tuwaambie wavute suruali zao juu mpaka magotini tuone kama hakuna alama za ki-freemason basi watakuwa CCJ kweli.
 
Kina-sound ki- freemasons freemasons, sije kikawa na code za Dan Brown kuchukua kura toka kwa CHADEMA na CUF, halafu inakuja ile hadithi ya mzee kobe (CCM) kushinda mbio za uchaguzi kwa vile sungura alivyofika katikati ya mbio za uchaguzi akaamua kulala kwa vile mzee kobe(CCM) wamemuacha mbaliii kabisa, usingizi ukamkolea sungura huku mzee kobe akijikongoja akapita kwa hatua za kunyata zisizo na mshindo, sungura alivyozinduka mbio zimekwisha mshindi mzee kobe.

Hizi ni alama za nyakati kwa wapiga kura na CHADEMA/CUF kushikilia uzi ule ule, maana mzee kobe kesha ona mambo magumu na kuleta chama feki miezi 9 kabla ya uchaguzi. Si ajabu Maalim alishastuka ndo maana anaona CCJ inakuja hivyo na wao wameweka mkakati w kuruka mtego.

Hivyo hao freemasons -CCJ wakija tuwaambie wavute suruali zao juu mpaka magotini tuone kama hakuna alama za ki-freemason basi watakuwa CCJ kweli.

Eric Shigongo ameyatungia nahau yale mapendekezo ya Maalim Seif kuwa Karume aongezewe muda wa urais, ati kasema 'paka kakubali kulala chali...' Hii ya CCJ inawezekana ni paka mwingine. Paka wa Zenj kalala chali, sasa huyu wa huku bara sijui ndio kafanyaje, lakini nahisi bado ni paka.
 
Naona hizi ni propaganda kuelekea October 2010, na bado, mwaka huu tutaona mengi!
 
Gazeti zima linaweka blah blah tupu halafu linasema majina tunay? Msingi wa habari hii ni nini, kama hataunaweza kuiita habari?
 
Chama cha jamii gani/ipi? Hizi CC ambazo zilikuwa kule kwenye nCCr huwa wazipendea nini?
 
Tuna chama wadau, kwa mujibu wa redio mbao. Wanabodi wote wenye post zaidi ya 10,000 wana candidacy ya ubunge sehemu wanapotaka, wakigongana mwenye posts zenye thanks nyingi anashinda.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom