CHADEMA yaitaka serikali ibadili haraka Katiba

nickname

JF-Expert Member
Dec 20, 2009
544
147
Kamati Kuu (CC) ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), imeitaka serikali kuchukua hatua za haraka kufanya mabadiliko makubwa ya Katiba ya nchi kwa kuwashirikisha wadau wote, vinginevyo chama hicho kitaendeleza hatua za kudai suala hilo.


Imesema hatua hiyo ni muhimu kwa vile itasaidia kuepuka dosari zilizojitokeza katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu zisijirudie tena katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 kwa maslahi ya taifa.
Tamko hilo lilisomwa na Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Willibrod Slaa alipozungumza na waandishi wa habari, jijini Dar es Salaam kuhusu maazimio yaliyofikiwa na CC-Chadema katika kikao chake kilichofanyika jijini Dar es Salaam, Jumamosi wiki iliyopita.


Kikao hicho kilifanyika kwa lengo la kutathmini Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 31, mwaka huu baada ya kupokea mapendekezo kadhaa yaliyowasilishwa na Sekretarieti ya chama hicho.
"Kwa maana hiyo basi tunataka serikali ichukue hatua ya haraka kufanya mabadiliko makubwa ya Katiba. Labda kushirikisha wadau. Kama serikali haitachukua hatua, Kamati Kuu imeridhia Chadema tuendeleze hatua za kudai Katiba kwa njia zote zinazoweza kupatikana za amani," alisema Dk. Slaa.


Alizitaja njia za amani kuwa ni pamoja na kutoa elimu kwa wananchi, kufanya maandamano ya kudai Katiba, nakushirikisha wadau katika mikutano na semina mbalimbali.
Alisema Chadema ni chama kisichopenda vurugu na kwamba, jambo hilo walilitangaza toka mwanzo kwamba, hawataki damu ya Mtanzania hata mmoja imwagike.


Hata hivyo, alisema matokeo ya tatizo hilo, hasa baada ya taarifa iliyosomwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kugongana na ile ya wasimamizi wilayani, ilisababisha watu kutoka mitaani katika maeneo ya Geita, Shinyanga, Mbeya, Mbozi, ambako baadhi yao walipigwa mabomu na polisi.


Alisema hali hiyo iliashiria kwamba, kama watu hao wangeendelea kuingia mitaani, basi ingetokea hali ya uvunjifu wa amani na hata damu kuweza kumwagika.
Aliongeza: "Sasa kama haya yangetokea na sisi tungekubaliana na wale wananchi, maana yake ingetokea hali kama ya Ivory Coast. Chadema tumesema hapana. Toka siku ya kwanza tumesema hatutaki uchaguzi urudiwe, kwa sababu tumeshaona kabisa Katiba yetu inasema huwezi kwenda ku-challenge mahali popote."


Alisema jambo la pili lililoridhiwa na CC-Chadema katika kikao hicho, ni kuitaka serikali kuunda haraka tume huru kuchunguza nini kilitokea kwenye matokeo ya Uchaguzi Mkuu yaliyompa ushindi na kumwingiza madarakani Rais Jakaya Kikwete.
Dk. Slaa alisema Rais Kikwete hayuko kihalali kwenye utawala kwa madai kwamba, matokeo ya uchaguzi yaliyompa ushindi na kumwingiza madarakani yalichakachuliwa na kwamba, msimamo huo haujabadilika na Kamati Kuu imeridhia na kuukazia.


Source : Nipashe


 
Back
Top Bottom