Chadema walivyowachanganya CCM uchaguzi mdogo Igunga

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797
Friday, 07 October 2011 19:52
Mwandishi Wetu mwananchi
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), kilipata wakati mgumu katika uchaguzi mdogo wa ubunge katika Jimbo la Igunga, licha ya mgombea wake, Dk Dalaly Kafumu kuibuka mshindi.Dk Kafumu alishinda kwa kupata kura 26,484 kati ya kura 52,487 halali zilizopigwa, sawa na asilimia 50.4, huku mshindani wake wa karibu, Joseph Kashindye wa Chadema akipata kura 23,260 sawa na asilimia 44.3.

Miongoni mwa mambo ambayo yalionekana kukichanganya chama tawala ni hatua ya Chadema, kubadilisha idadi kubwa ya mawakala wake wa usimamizi kwenye vituo vya kupigia kura hatua ambayo ilifanyika siku chache kabla ya uchaguzi.

Kadhalika, CCM kilikuwa na hofu ya wasimamizi wa vituo vya kupigia kura kwamba hawakuwa upande wake na badala yake kuwashutumu wasimamizi hao kwamba walikuwa na mapenzi kwa Chadema hivyo wangekisaidia chama hicho pinzani katika mpango wake wa ‘kuiba kura’.Hatua ya Chadema kubadili mawakala ilipewa tafsiri tofauti na viongozi wa CCM ambao walikuwa wakiipinga kwa maelezo kwamba chama hicho kilikuwa kimekiuka Sheria za Uchaguzi.

Hata hivyo, baada ya kushindwa kuishawishi Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), kuwakataa mawakala hao, CCM waliupa mpango huo sura ya kisiasa, kwamba Chadema walikuwa wamewadharau wapiga kura wa Igunga kwa kuwaleta mawakala kutoka nje ya jimbo hilo.

Oktoba Mosi, mwaka huu, siku moja kabla ya kupiga kura, Katibu wa Mambo ya Nje na Siasa wa CCM, January Makamba akiambatana na kada wa chama hicho ambaye pia ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), Stephen Wassira walikwenda katika Ofisi ya Msimamizi wa Uchaguzi wa Igunga, Protace Magayane kulalamikia mawakala wapya wa Chadema.

Habari kutoka ndani ya kambi ya CCM zilidai kuwa kabla ya January na Wassira kwenda katika ofisi hizo, kulikuwa na mjadala wa ndani kuhusu suala hilo lengo likiwa ni kukidhoofisha Chadema iwapo mpango wa kuwaengua mawakala wake ungefanikiwa.

Siku hiyohiyo mapema asubuhi, Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM), Martine Shigella alikuwa amekutana na waandishi wa habari katika Hoteli ya Peak, akisema kuwa Chadema hawakustahili kupewa kura kwani walikuwa wamewadharau vijana wa Igunga kwa kuleta mawakala kutoka nje ya jimbo hilo.

Shigella alidai kwamba Chadema walikuwa wamepanga kutumia mamilioni ya shilingi kuwalipa mawakala hao kutoka nje ya Igunga na kwamba kama wangekuwa wakiwathamini vijana wa jimbo hilo wasingekuchua hatua hiyo.

“Hawapaswi kupewa kura, fedha hizi ambazo ni ujira wa muda walipaswa kuwapa hawa vijana wa hapahapa, lakini wamekwenda kuwachukua ndugu zao huko Arusha, Mwanza na Mara, hawastahili kupewa kura,” alisema Shigella.

Hata hivyo, January alisema jana kuwa hatua yao hiyo haikutokana na woga kwamba wangeshindwa katika uchaguzi huo, bali CCM kilitaka kuona kwamba haki inatendeka kwa kila chama kuzingatia sheria na taratibu za uchaguzi huo uliokuwa na ushindani mkali.

Mbowe na mawakala
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe alisema hatua ya kuwaleta mawakala kutoka nje ya Igunga ilitokana na maombi wa makada wa chama hicho mkoani Tabora, kutokana na kutokuwa na vijana wa kutosha na wenye uzoefu wa kusimamia uchaguzi ambao ulikuwa wa ushindani mkubwa.

“Viongozi wetu wa hapa, wenyeji wetu wametuomba kwamba tuongeze nguvu kwa kuleta watu wengine, kwamba wao hawana (capacity ya ku – manage), uwezo wa kuhimili vishindo vya uchaguzi huu peke yao, sisi ndani ya chama tuliona kwamba ni busara kuchukua vijana ambao kwa kweli wametusaidia sana,” alisema Mbowe na kuongeza:

“Sasa kama hilo linatuathiri sisi kisiasa, wao linawahusu nini, labda wasema jingine sisi tuliwaita kwa manufaa ya chama chetu kwa hiyo wao haliwahusu na siyo juu yao.”

Kauli yake iliungwa mkono na Mwita Waitara ambaye alikuwa Mratibu wa Kampeni za Igunga wa chama hicho. Alisema hakukuwa na mpango wa malipo ya Sh300,000 kwa kila wakala kama CCM walivyodai na kwamba wengi wa vijana hao walikuwa wakijitolea.

“Si unawaona? Hapo kuna mtu aliyepewa 300,000? Hawa wamelala hapohapo usiku kucha, wengine hata maji ya kuoga hawajapata, wamekula chakula cha jumla kilichopikwa hapa, chai ndiyo hiyo hapo wanakunywa na mikate, sasa hizo 300,000 wamefanyia nini?” alihoji Waitara akiwa katika kambi ya vijana hao Igunga.

Hofu ya kushindwa
Hofu ya kushindwa ilitawala kambi ya CCM na mmoja wa viongozi wa chama hicho aliliambia gazeti hili siku ya uchaguzi Oktoba 2, 2011 kwamba chama chake kingekwenda mahakamani iwapo kingeshindwa katika uchaguzi huo.

Hofu hiyo ilitokana na kile baadhi ya viongizo wa CCM walichodai kwamba kulikuwa na mbinu za makusudi za wasimamizi wa uchaguzi kukisaidia Chadema ili kishinde uchaguzi huo isivyo halali.

“Ngoja nikwambie sisi tumefanya kampeni na tumejiridhisha kwamba tutashinda uchaguzi huu, lakini shaka tuliyonayo ni kuhusu usalama wa kura zetu, hawa wasimamizi hawapo upande wetu kabisa hivyo huenda wakashirikiana na Chadema kuiba kura,” alisema mmoja wa viongozi waandamizi wa CCM siku moja kabla ya kupiga kura.

Kiongozi huyo alisema sababu kubwa ya wasimamizi hao kuwa na kile alichokiita chuki dhidi ya CCM ni kutokana na matatizo ambayo alisema yamekuwa yakiwakabili watumishi wa kada za chini.

“Hawa wengi ni watumishi wa kada za chini, wengi wana chuki na CCM. Katika hali hiyo, tuna wasiwasi mkubwa na hiyo ndiyo hofu yetu katika uchaguzi mzima,” alisema.

Hii ni mara ya kwanza kwa chama hicho tawala kutoa shutuma kwa wapinzani kwamba wanataka kukiibia kura katika uchaguzi katika miaka ipatayo 20 ya siasa za upinzani nchini, hatua ambayo Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willbrod Slaa aliita kuwa ni hofu ya kushindwa uchaguzi.

Tuhuma dhidi ya wasimamizi wa uchaguzi ziliendelea hata baada ya uchaguzi huo, pale Katibu Mkuu wa CCM, Wilson Mukama alipowaambia waandishi wa habari kwamba chama chake kingepata ushindi mnono zaidi kama wasimamizi wasingekihujumu.

Hata hivyo, uchunguzi uliofanywa na mwandishi wetu ulibaini kuwa chimbuko la wasiwasi huo ni kitendo cha kundi la wasimamizi wa uchaguzi waliokuwa wakitoka kwenye mafunzo ya kusimamia kazi hiyo, kuunyooshea vidole moja ya misafara ya kampeni ya CCM viwili walipokutana. Vidole hivyo ni ishara ya Chadema.

“Hali hiyo iliporipotiwa hapa, wazee (wa CCM) walichanganyikiwa, ilibidi wakutane na kujadili kwa undani, ukweli ni kwamba kwa sasa Chadema siyo adui yao na wala chama hicho hakizungumzwi hapa, ila wasimamizi ndiyo maadui wakubwa na tishio la ushindi wetu,” alisema kiongozi mwingine siku chache kabla ya uchaguzi huo.

Aliyekuwa Mratibu wa Kampeni za CCM Igunga, Mwigulu Nchemba akizungumzia ushindi wa mgombea wa chama chake alisema: “Katika uchaguzi huu sitawasaau Chadema, lazima Watanzania wajue kuwa Chadema ni janga la kitaifa.”

Mbowe katika maelezo yake baada ya uchaguzi huo alisema kushambuliwa kwa chama chake kunathibitisha kwamba ni tishio kwa CCM na vyama vingine vya siasa nchini.

Tayari Chadema kimeeleza kusudio lake la kufungua kesi mahakamani kupinga ushindi wa CCM. Hata hivyo, inachopinga si matokeo kwa maana ya kura, bali ni kile kilichodai kuwa ni kukiukwa kwa taratibu za uchaguzi katika ngazi mbalimbali.
 
habari ndefuje ila ninavoipenda CDM imebidi niisome kwa utulive yote..........
ila mm cjafurai walivoshinda CCM kabisaaaaaaaaaaaaaa ila CDM wangekua makini zaidi wangelichukua jimbo sema betrayers wa CDM ndio wamewaangusha
 
habari ndefuje ila ninavoipenda CDM imebidi niisome kwa utulive yote..........
ila mm cjafurai walivoshinda CCM kabisaaaaaaaaaaaaaa ila CDM wangekua makini zaidi wangelichukua jimbo sema betrayers wa CDM ndio wamewaangusha

Bwana mdogo unatakiwa ufanye mazoezi ya kusoma habari ndefu. Usiwe kama Watanzania wengine wanaolaumiwa kwa kutokuwa na utamaduni wa kujisomea.
 
Back
Top Bottom