Analogia Malenga
JF-Expert Member
- Feb 24, 2012
- 5,006
- 9,872
CHAMA CHA DEMOKRASIA NA MAENDELEO (CHADEMA)
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI NA UMMA
Wakati tukielekea mwisho wa ratiba ya kuchukua, kujaza na kurejesha fomu za uteuzi wa kugombea Uchaguzi wa Serikali za Mitaa, Vijiji na Vitongoji wa Mwaka 2019, ambao unatarajiwa kuwa leo jioni saa 10.00, Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kinahoji uthubutu walionao baadhi ya Wasimamizi/Wasimamizi wa Uchaguzi wanaoendelea kukaidi maelekezo ya kikanuni yanayotolewa na Waziri wa Tamisemi hasa kuhusu kufungua ofisi, kutoa na kupokea fomu za wagombea kama taratibu zinavyoelekeza.TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI NA UMMA
Aidha, Chadema kimepata taarifa za kuwepo vikao vya siri vinavyowahusisha Watendaji wa Vijiji/Mitaa, Kata na Waratibu wa Elimu Kata, Wasimamizi Wasaidizi na Wasimamizi wa Uchaguzi vinavyolenga kuwapatia maelekezo ya kuwaengua wagombea wa Chadema kinyume cha taratibu zilizowekwa.
Kupitia taarifa hii, Chadema inawataarifu wahusika wote (mamlaka) wa uchaguzi huu, vyombo vya habari na umma wa Watanzania kwa ujumla kuwa;
1. Mwenendo wa shughuli ya uchukuaji, ujazaji na urejeshaji wa fomu bado unakabiliwa na matatizo mengi ambayo Chadema imeyabainisha na kuyawasilisha kwa barua rasmi kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais- Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Ndugu Seleman Jafo. Ubainishaji wa matatizo hayo umeenda sambamba na taarifa za kina za maeneo husika na wahusika. Hadi muda huu wa asubuhi ya siku ya mwisho, katika maeneo mengi Wasimamizi/Wasimamizi Wasaidizi wa Uchaguzi hawajafungua ofisi zao kwa ajili ya wagombea kuchukua, kujaza na kurejesha fomu kama Mwongozo wa Waziri unavyoelekeza. Mifano wa maeneo hayo ni; majimbo yote mawili katika Wilaya ya Maswa (mkoani Simiyu), yenye kata 33, vijiji 111, Wasimamizi Wasaidizi hawajafungua ofisi tangu Novemba 1 hadi leo. Msimamizi Mkuu Joyce Nduguru amegoma kutoa ushirikiano hata kwa vyombo vya habari kutoa ufafanuzi kwa nini wasimamizi wasaidizi wamefunga ofisi na hawapokei fomu. Hali hiyo pia iko sehemu zingine; Kata za Ibindi, Masewela, na Muungano, (Nsimbo-Katavi), Kata za Kongolo, Nyigogo, Kandawe, Sukuma, Buhumbi, Ng’haya, Mwabulenga (Magu-mkoani Mwanza), kwa kutaja kwa uchache.
2. Kuna maeneo zinafanyika njama za makusudi kutofungua ofisi, kutopokea fomu za wagombea wa Chadema au kutowapatia nakala baada ya kurejesha au vitendo vingine kinyume cha kanuni kwa sababu katika sehemu husika CCM imekosa/haina wagombea, hivyo Wasimamizi/Wasimamizi Wasaidizi wa Uchaguzi katika maeneo hayo hawataki kutenda haki kwa kuwa wagombea wa Chadema watapita bila kupingwa. Mathalani kwenye maeneo ya Mikoa ya Simiyu na Shinyanga ambako kuna madai ya wakulima kutolipwa malipo ya mauzo ya pamba.
3. Yapo maeneo ambako Wasimamizi Wasaidizi wa Uchaguzi wamepokea fomu na kuziharibu kwa makusudi, mfano katika vijiji vya Kata za Kabila, Shishani huko Magu, Mwanza.
4. Kuwepo kwa taarifa za vikao vya siri vinavyowahusisha VEOs, MEOs na WEOs, Wasimamizi/Wasimamizi Wasaidizi na makada wa CCM katika kata husika ambao wameahidiwa ahadi mbalimbali pamoja na maagizo, ili wawahujumu wagombea wa Chadema hasa kwa kuwaengua mapema kabla ya muda uliowekwa mahsusi kwa ajili ya kuweka mapingamizi na uteuzi wa wagombea ambao ni Novemba 5- 7, 2019. Maeneo ya Rorya, Tarime na Manisapaa ya Morogoro tayari vikao hivyo vimekaa kuengua wagombea.
Chadema inaendelea kusisitiza wito wa kumtaka Waziri wa Tamisemi, kufuatilia na kuchukua hatua kwa mujibu wa mamlaka aliyonayo kikanuni ili wagombea wote wapate haki ya Kikatiba ya kugombea badala ya kuwekewa vikwazo vya kuwazuia, kinyume cha taratibu ambazo anapaswa kuhakikisha zinatekelezwa, tukimkumbusha pia kuwa Chadema imemwandikia kutaka ratiba ya kutoa, kujaza na kurejesha fomu isogezwe mbele katika maeneo yote ambako kumekuwa na ukiukwaji wa kanuni katika zoezi hilo.
Imetolewa leo Jumatatu, Novemba 4, 2019 na;
Tumaini Makene
Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano