CHADEMA: Kauli ya Kikwete ni kilele cha ushahidi CCM kutumia polisi kuua

Chief Isike

JF-Expert Member
Jan 17, 2010
445
462
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

KAULI YA RAIS JAKAYA KIKWETE NI KILELE CHA USHAHIDI WA CCM KUHUSIKA NA MATUKIO YA MAUAJI YANAYOFANYWA NA POLISI

KAULI iliyotolewa na Mwenyekiti wa CCM, Jakaya Kikwete kuwataka viongozi na wanachama wa chama hicho waache kutegemea Jeshi la Polisi katika kukabiliana na wapinzani wao, bila shaka yoyote imetufikisha kwenye kilele cha juu cha ushahidi wa tuhuma ambazo Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) pamoja na Watanzania wengine wamekuwa wakitoa kuwa jeshi hilo linatumika kisiasa na CCM wanalitumia kutimiza matakwa yao kisiasa.

Kwa kuangalia muktadha wa mtiririko wa matukio ya kudhibiti upinzani kwa kuvuruga kazi za kisiasa za vyama vya upinzani na utoaji wa mawazo mbadala nchini yanayofanywa na vyombo vya dola, hususan Jeshi la Polisi, kwa kuua Watanzania wasiokuwa na hatia…

Halikadhalika kwa kuangalia mtiririko wa mantiki ya hoja mbalimbali za wajumbe wakiwemo viongozi waandamizi kama Rais Kikwete katika mkutano mkuu wa CCM uliomalizika karibuni, hitimisho la kimantiki katika kauli ya Rais Kikwete ni kwamba wapinzani anaomaanisha Rais Kikwete na kuwaambia wenzake kuwa wasitegemee polisi kupambana nao ni; CHADEMA, mtu, watu au makundi mengine ya kijamii ambayo kila yanapodai haki na uwajibikaji nchini, yamekuwa yakihusishwa na CHADEMA.

Kutokana na ukweli huo, Kurugenzi ya Ulinzi na Usalama ya CHADEMA imeona kwa sababu kauli hii sasa imesaidia kumaliza fumbo lililokuwepo juu ya madai ya muda mrefu kuwa Jeshi la Polisi linatumika kisiasa na viongozi wa CCM na watendaji wa serikali, ni muhimu kuweka kumbukumbu sawa.

Kauli hiyo ya Kikwete imetufikisha kwenye kilele cha ushahidi kuwa Jeshi la Polisi linatumika kisiasa kukabiliana na hoja na shughuli halali za kisiasa zinazofanywa na CHADEMA, chama mbadala kwa sasa kinacholenga kuiondoa CCM madarakani, kwa mantiki ifuatayo;

Kikwete amethibitisha pasi na shaka kuwa CCM waliwatumia polisi katika kumuua kijana Ally Singano Zona wakati wanachama na wapenzi wa CHADEMA walipofanya mapokezi ya viongozi wao wa kitaifa siku ya Agosti 27, 2012, mjini Morogoro. Itakumbukwa kuwa tukio hilo lilitokea baada ya mafanikio mazuri ya mikutano ya M4C iliyofanyika katika 95% ya kata na 83% ya vijiji katika majimbo yote mkoani Morogoro, ambako maelfu ya wananchi wasiokuwa na vyama na wengine walioiasi CCM na vyama vingine walijiunga na CHADEMA.

Kauli hii pia imesaidia kufumbua fumbo la kwa nini Jeshi la Polisi Mkoani Iringa, chini ya usimamizi wa RPC Michael Kamuhanda waliamua kutumia nguvu kubwa kuingilia shughuli halali ya CHADEMA kufanya mikutano ya ndani, ikiwemo ufunguzi wa matawi katika Kijiji cha Nyololo, mkoani Iringa, na hatimaye wakamuua Mwandishi wa Habari, Daudi Mwangosi, Septemba 2, 2012.

Kwa kuangalia mtiririko wa matukio ya huko nyuma kama ambavyo tumewahi kuyatolea kauli na taarifa huko nyuma na kuangalia ripoti za uchunguzi wa tukio la Nyololo hasa uchunguzi uliofanywa na Baraza la Habari Tanzania na Tume ya Utawala Bora na Haki za Binadamu (TUBHB), sasa ni wazi kila mmoja anaweza kuona kulikuwa na kila aina ya dalili ya maelekezo ya kisiasa kutumia polisi kuidhibiti CHADEMA.

Kikwete pia amewasaidia Watanzania kuanza kutafuta majawabu kwa nini watuhumiwa wa kesi ya mauaji ya aliyekuwa Kiongozi wa CHADEMA Kata ya Usa River, Msafiri Mbwambo, ambao katika tuhuma zao walishirikiana na viongozi wa CCM kuua, waliweza kutoroka mahakamani mikononi mwa polisi na hadi sasa hakuna hatua yoyote iliyochukuliwa.

itakumbukwa pia namna ambavyo mmoja wa viongozi waandamizi wa CCM ngazi ya taifa ambaye pia ni mbunge wa chama hicho, amekuwa katikati ya tuhuma za kuandaa kikundi cha vijana ili wavuruge mkutano wa CHADEMA katika Kijiji cha Ndago, wilayani Iramba, huku polisi wakiangalia vijana hao wakirusha mawe bila kuchukua hatua yoyote.

Mbali ya kwamba vurugu hizo zilifumbiwa macho na polisi waliokuwepo eneo la tukio wakiongozwa na Mkuu wa Kituo cha Polisi Ndago, zimekuwa zikihusishwa na kifo cha kiongozi mmoja wa UVCCM, aliyekutwa amefariki eneo jirani, baada ya mkutano wa CHADEMA kumalizika.

Aidha kauli ya Mwenyekiti wa CCM, Rais Kikwete imefumbua fumbo juu ya mazingira ya utata yanayozunguka kifo cha kada wa CHADEMA, Mbwana Masoud, kilichotokea Igunga baada ya uchaguzi mdogo, ambaye alikutwa ameuwawa kinyama baada ya kutekwa na kuteswa na vijana wa CCM waliopewa mafunzo ya kufanya kazi hizo katika makambi ya Ulemo, Iramba, Singida.

Itakumbukwa kuwa wakati wa uchaguzi mdogo wa Igunga, CHADEMA kilibaini na kuwasilisha ushahidi polisi ukidhihirisha pasi na shaka kuwa CCM walikuwa wameanzisha makambi wakiwafundisha vijana mbinu za kijeshi kwa nia ya kuteka, kutesa na kuua wanachama na viongozi wa CHADEMA. Vyombo vya dola, wakiwemo polisi na usalama wa taifa, walihusika kutoa mafunzo kwa vijana hao wa CCM.

Upo uthibitisho mkubwa, kama ambavyo umeelezwa na Katibu Mkuu Dkt. Slaa mara kadhaa sasa akimtaka Rais Kikwete kama mwenyekiti wa CCM atoe ufafanuzi, kuwa chama chake kimeingiza silaha za moto bila kibali na kuwapatia vijana wake katika mafunzo kwenye makambi maeneo mbalimbali nchini.


Tangu utolewe ushahidi huo, kwa kutaja aina ya bunduki, namba yake, uwezo wa kubeba risasi na ilikotengenezwa, mbali ya polisi kushindwa kufanya uchunguzi ili kuwaambia Watanzania kwa nini CCM wanaingiza silaha nchini, Mwenyekiti wa CCM, Rais Kikwete ambaye pia ni Amri Jeshi Mkuu, ameshindwa kutoa ufafanuzi wowote, hali ambayo inahatarisha ulinzi na usalama wan chi.


Tunaweza kutaja matukio mengi ambayo kauli ya Rais Kikwete imefunua ukurasa mpya wa kilele cha ushahidi namna ambavyo kuna ushirika kati ya CCM, serikali yake na vyombo vya dola, hasa Jeshi la Polisi, kushughulikia vyama vya upinzani, hususan CHADEMA kwa kuteka, kutesa na kuua raia wasiokuwa na hatia, lengo kubwa ikiwa ni kutimiza matakwa ya propaganda za CCM kuwa CHADEMA ni chama cha vurugu.


Lakini hapa tunaweza kutaja mengine machache. Matukio yote ya chaguzi ndogo na kwa kuanzia uchaguzi wa Kiteto, Busanda, Biharamulo, Igunga, Arumeru Mashariki na chaguzi za juzi za kata 29, upo ushahidi wa wazi namna ambavyo CCM wanashirikiana na polisi, mmoja akimtumia mwenzake kufanikisha malengo ya kisiasa kama ambavyo Rais Kikwete amethibitisha.


Matukio yote hayo hasa katika chaguzi ndogo za ubunge, ambapo viongozi wa CCM na polisi wameshambulia, wameteka na wametesa wanachama na viongozi wa CHADEMA katika shughuli halali za kisiasa, ushahidi wake umewasilishwa polisi kwa ajili ya uchunguzi na sheria ichukue mkondo wake, lakini mpaka sasa hakuna hatua wala taarifa zozote za maana. Hivyo kauli ya Rais Kikwete imefumbua fumbo na sasa Watanzania wanajua zaidi.


Hitimisho.


Watanzania wanajua kuwa matukio ya vyombo vya dola kuhujumu wapinzani na wakosoaji wa serikali ya CCM, kwa nia ya kuilinda CCM, yameanza kwenda mbali ya CHADEMA, kwa sababu sasa hata mtu, watu au makundi mbalimbali ya kijamii ambayo yanaonekana kutoa mawazo mbadala, kudai haki na uwajibikaji yameanzwa kuandamwa. Mifano mizuri hapa ni kufungiwa kwa Gazeti la Mwanahalisi na kutekwa na kuteswa kwa kiongozi wa madaktari, Dkt. Steven Ulimboka.


Rais Kikwete aoneshe dhamira yake kwa kutekeleza barua ya Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe, aliyemwandikia kutaka matukio yote ambayo vyombo vya dola, wakiwemo polisi, wametumika kuteka, kutesa na kuua kwa malengo ya kisiasa ya kupambana na wakosoaji wa CCM na serikali yake, vifanyiwe uchunguzi huru, kwa kuunda Tume ya Kimahakama/Kijaji ili ukweli ujulikane na haki ionekane ikitendeka badala ya kutoa lugha ya kisiasa kwa nia ya kujikosha mbele ya umma, lakini nyuma ya pazia CCM na polisi, wanakaa na kupanga mikakati inayopelekea kudhulumu haki na roho za Watanzania.


Aidha, wakati uchunguzi huo ukifanyika, watuhumiwa wote, wakiwemo viongozi wa CCM, serikali na watendaji wa Jeshi la Polisi waliokubali kutumika, hata kuvunja haki za binadamu, katiba na sheria, wanawajibika kwa wao kujiuzulu au kufukuzwa kazi na Rais Kikwete.



Imetolewa leo Novemba 16, 2012, Dar es Salaam na;



Wilfred Lwakatare


Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama CHADEMA
 
Naona kuna magazeti mawili na redio kadhaa ziliweza ku-cover hii stori;

Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema ) kumetoa tamko kumtaka Rais Jakaya Kikwete kuonyesha dhamira ya kushughulikia malalamiko waliyotoa kwake dhidi ya matumizi ya polisi kupambana na wakosoaji wa CCM na serikali.

Tamko hilo limo kwenye taarifa ya Chadema iliyotolewa na Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama Wilfred Lwakatare, iliyotolewa jana jijini Dar es Salaam.

Katika andiko hilo, walimtaka Rais Kikwete atekeleze mambo yaliyoandikwa kwenye barua ya Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, aliyetaka serikali ifanye uchunguzi wa matukio ya utesaji yaliyofanywa na vyombo vya dola dhidi ya wanaoipinga serikali.

Waraka huo ulitaka uchunguzi ufanyike dhidi ya polisi waliotumika kuteka, kutesa na kuua kwa malengo ya kisiasa ya kupambana na wakosoaji wa chama tawala na serikali yake.

Katika taarifa yake, Chadema ilisema walimwandikia Rais wakitaka kufanyike uchunguzi huru kwa kuunda Tume ya Kimahakama/Kijaji ili ukweli ujulikane na haki ionekane ikitendeka badala ya kutoa lugha ya kisiasa kwa nia ya kujikosha mbele ya umma, wakati CCM na polisi, wanakaa na kupanga mikakati inayopelekea kudhulumu haki na roho za Watanzania.

Aidha, wakati uchunguzi huo ukifanyika, watuhumiwa wote, wakiwemo viongozi wa CCM, serikali na watendaji wa Jeshi la Polisi waliokubali kutumika, hata kuvunja haki za binadamu, katiba na sheria, wanawajibika kwa wao kujiuzulu au kufukuzwa kazi.

Rwakatare alisema kauli iliyotolewa na Mwenyekiti wa CCM, Rais Kikwete kuwataka viongozi na wanachama wa chama hicho waache kutegemea Jeshi la Polisi katika kukabiliana na wapinzani ni ushahidi wa tuhuma ambazo Chadema imekuwa ikitoa dhidi ya chama hicho.

Hivi karibuni Rais Kikwete, alikitahadharisha chama hicho kuwa kikitegemea zaidi polisi kwamba ndiyo msaada kwake katika kujibu mapigo ya wapinzani kitashindwa.

Akizungumza wakati wa Mkutano Mkuu wa Nane CCM baada ya kuchaguliwa kwa mara nyingine kuwa Mwenyekiti kwa miaka mingine mitano, alisema viongozi wa CCM lazima wajipange na kuwa wepesi wa kujibu mapigo ya wapinzani.

Alisema jawabu la siasa siyo polisi bali ni wanasiasa wenyewe na kwamba polisi hawawezi kuwa jibu la suala la siasa lazima kila kiongozi ajitambue yeye mwenyewe ndiyo mwenezi katika eneo lake.

Chadema ilisema Watanzania wanajua kuwa matukio ya vyombo vya dola kuhujumu wapinzani na wakosoaji wa serikali ya CCM, kwa nia ya kuilinda CCM, yamekwenda kwa sababu watu na makundi ya kijamii pia wameanza kuandamwa.

"Mtu, watu au makundi mbalimbali ya kijamii ambayo yanaonekana kutoa mawazo mbadala, kudai haki na uwajibikaji yameanza kuandamwa. Mifano mizuri hapa ni kufungiwa kwa Gazeti la Mwanahalisi na kutekwa na kuteswa kwa kiongozi wa madaktari, Dk. Steven Ulimboka. " ilisema taarifa ya Rwakatare.

Chadema ilisema ukweli huo umesaidia kumaliza fumbo lililokuwepo juu ya madai ya muda mrefu kuwa Jeshi la Polisi linatumika kisiasa na viongozi wa CCM na watendaji wa serikali.

"Kauli hiyo ya Kikwete imetufikisha kwenye kilele cha ushahidi kuwa Jeshi la Polisi linatumika kisiasa kukabiliana na hoja na shughuli halali za kisiasa zinazofanywa na Chadema , chama mbadala kwa sasa kinacholenga kuiondoa CCM madarakani".

Aidha imesaidia kufumbua fumbo la kwa nini Jeshi la Polisi Mkoani Iringa lilitumia nguvu kubwa kuingilia shughuli halalli za Chadema kufanya mikutano ya ndani, ikiwemo ufunguzi wa matawi katika Kijiji cha Nyololo, mkoani Iringa, na hatimaye kusababisha kifo cha Mwanandishi wa Habari, Daudi Mwangosi, Septemba mwaka huu.




CHANZO: NIPASHE
 
Daima ukweli unamaisha marefu kuliko Uongo, yapo mengi ya uongo wao yatafikia kikomo cha maisha yao na ndipo watakapo saga meno!
 

JK kikaangoni



Mbali na msimamo huo uliotolewa na Wenje, CHADEMA pia kimemshukia Rais Kikwete na kumtaka awawajibishe mara moja maofisa wa serikali waliohusika kutekeleza amri za viongozi wa CCM za kuwapiga na kusababisha vifo vya wananchi.


Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jana, Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa CHADEMA, Wilfred Lwakatare amesema kauli ya Kikwete mjini Dodoma wakati akifunga mkutano mkuu wa CCM, imebainisha na kuweka wazi kuwa vyombo vya dola viliwakamata, kuwatesa na kuwaua wananchi hususan viongozi na wanachama wa upinzani kwa amri ya chama tawala.


Lwakatare alisema hoja ya Rais Kikwete ni jibu tosha kwa Watanzania kwamba CCM imekuwa ikilitumia Jeshi la Polisi kutimiza matakwa yao kisiasa.


"Kwa kuangalia muktadha wa mtiririko wa matukio ya kudhibiti upinzani kwa kuvuruga kazi za kisiasa za vyama vya upinzani yanayofanywa na vyombo vya dola, kwa kuua Watanzania wasiokuwa na hatia, kauli hiyo ya Kikwete imetufikisha kwenye kilele cha ushahidi kuwa Jeshi la Polisi linatumika kisiasa kukabiliana na hoja na shughuli halali za kisiasa zinazofanywa na CHADEMA.


"Kikwete amethibitisha pasi na shaka kuwa CCM waliwatumia polisi katika kumuua kijana Ally Singano Zona wakati wanachama na wapenzi wa CHADEMA walipofanya mapokezi ya viongozi wao wa kitaifa Agosti 27, 2012, mjini Morogoro," ilisema sehemu ya taarifa ya Lwakatare.


CHADEMA pia kimedai kuwa kauli hiyo ya Kikwete imefumbua fumbo la kwa nini polisi mkoani Iringa, chini ya usimamizi wa RPC Michael Kamuhanda waliamua kutumia nguvu kubwa kuingilia shughuli halali ya CHADEMA kufanya mikutano ya ndani, ikiwemo ufunguzi wa matawi katika Kijiji cha Nyololo, mkoani Iringa, na hatimaye wakamuua mwandishi wa habari, Daudi Mwangosi, Septemba 2, 2012.


"Kwa kuangalia mtiririko wa matukio ya huko nyuma kama ambavyo tumewahi kuyatolea kauli na taarifa huko nyuma na kuangalia ripoti za uchunguzi wa tukio la Nyololo, hasa uchunguzi uliofanywa na Baraza la Habari Tanzania na Tume ya Utawala Bora na Haki za Binadamu (TUBHB), sasa ni wazi kila mmoja anaweza kuona kulikuwa na kila aina ya dalili ya maelekezo ya kisiasa kutumia polisi kuidhibiti CHADEMA.


"Kikwete pia amewasaidia Watanzania kuanza kutafuta majawabu kwa nini watuhumiwa wa kesi ya mauaji ya aliyekuwa Kiongozi wa CHADEMA, Kata ya Usa River, Msafiri Mbwambo, ambao katika tuhuma zao walishirikiana na viongozi wa CCM kuua, waliweza kutoroka mikononi mwa polisi na hadi sasa hakuna hatua yoyote iliyochukuliwa," alisema Lwakatare.


Pamoja na kukumbusha vurugu za Ndago huko Iringa, CHADEMA kimezidi kudai kuwa kauli ya Mwenyekiti wa CCM, Rais Kikwete imefumbua fumbo juu ya mazingira ya utata yanayozunguka kifo cha kada wa CHADEMA, Mbwana Masoud, kilichotokea Igunga baada ya uchaguzi mdogo, aliyekutwa ameuawa kinyama baada ya kutekwa na kuteswa na vijana wa CCM waliopewa mafunzo ya kufanya kazi hizo katika makambi ya Ulemo, Iramba, Singida.


"Upo uthibitisho mkubwa, kuwa CCM kimeingiza silaha za moto bila kibali na kuwapatia vijana wake katika mafunzo kwenye makambi maeneo mbalimbali nchini.


"Tangu utolewe ushahidi huo, kwa kutaja aina ya bunduki, namba yake, uwezo wa kubeba risasi na ilikotengenezwa, mbali ya polisi kushindwa kufanya uchunguzi ili kuwaambia Watanzania kwa nini CCM wanaingiza silaha nchini, Mwenyekiti wa CCM, Rais Kikwete ambaye pia ni Amiri Jeshi Mkuu, ameshindwa kutoa ufafanuzi wowote, hali ambayo inahatarisha ulinzi na usalama wa nchi," alisema.


Lwakatare alizidi kuishambulia kauli ya Rais Kikwete akidai imefunua ukurasa mpya wa kilele cha ushahidi wa namna ambavyo kuna ushirika kati ya CCM, serikali yake na vyombo vya dola, hasa Jeshi la Polisi, kushughulikia vyama vya upinzani, hususan CHADEMA kwa kuteka, kutesa na kuua raia wasiokuwa na hatia, lengo kubwa ikiwa ni kutimiza matakwa ya propaganda za CCM kuwa CHADEMA ni chama cha vurugu.


Kutokana na hali hiyo, CHADEMA kimemtaka Rais Kikwete kutekeleza barua ya Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe, aliyemwandikia kutaka matukio yote ambayo vyombo vya dola, vimetumika kuteka, kutesa na kuua kwa malengo ya kisiasa ya kupambana na wakosoaji wa CCM na serikali yake, vifanyiwe uchunguzi huru, kwa kuunda Tume ya Kimahakama/Kijaji ili ukweli ujulikane na haki ionekane ikitendeka badala ya kutoa lugha ya kisiasa kwa nia ya kujikosha mbele ya umma.


Aidha, wakati uchunguzi huo ukifanyika, watuhumiwa wote, wakiwemo viongozi wa CCM, serikali na watendaji wa Jeshi la Polisi waliokubali kutumiwa na CCM, hata kuvunja haki za binadamu, katiba na sheria, wanawajibika kwa wao kujiuzulu au kufukuzwa kazi na Rais Kikwete.

Source; Tanzania Daima
 
Kama Ukimwi unao ni unao tu.Utakunywa dawa ipo siku zitagoma.Chadema mtahangaika sana kifo chenu hakipo mbali
 
Kama Ukimwi unao ni unao tu.Utakunywa dawa ipo siku zitagoma.Chadema mtahangaika sana kifo chenu hakipo mbali
Hizo dawa naona zimegoma kwa Magamba maana wameanza kupata opportunistic infections, wameanza kusema madhambi yao.
 
Kwa hakika huu ni ukweli mchungu,kitendo cha mh. Kikwete kuwataka wana ccm waache kuitegemea police ktk matukio mbalimbali ya kisiasa na kijamii,kinaonyesha sasa wanaanza kuropoka madhambi yao.siku zote ukweli huishi,na uongo hufa..damu za watanzania waliokufa bila hatia kwa kupigwa risasi hazitawaacha salama wale wote walio husika na vifo hivyo vya aibu.
 
Kama Ukimwi unao ni unao tu.Utakunywa dawa ipo siku zitagoma.Chadema mtahangaika sana kifo chenu hakipo mbali

kama CHADEMA ni ya kufa basi ingeshakufa siku nyingi,swali naomba unijibu,ni nani atakaye iua CDM??
 
Kama Ukimwi unao ni unao tu.Utakunywa dawa ipo siku zitagoma.Chadema mtahangaika sana kifo chenu hakipo mbali

Vipi ile dawa mliyosema iko jikoni inachemka kwa ajili ya kuwageuza magamba kuwa watu wa historia kwenye chama chenu, imemwagika nini au mpishi hajaivisha. Tupeni majibu bhna, inakuwaje mnafanya maazimio halafu jamaa wanapeta mpaka leo. Wengine mmeanza kuwarudisha kwenye circle, Vicious Circle of Fidasim, tehe tehe tehe, at the expense of justice, dignity of being and responsibility.
 
Mwenyezi Mungu huwa ana kawaida ya kuumbua au kulipiza hapahapa duniani, Mwenyezi Mungu huwa anasikia sauti za wanyonge wanao nyanyaswa na kuteswa, mwenyezi Mungu husikia sauti za wana walioko nyikani na kuomba msaada! Mateso yakizidi humpa moyo wa huruma mtesaji ili awahurumie wanao teseka! Ndio alicho kifanya kwa ccm! Aliwaangalia ccm kwa muda mrefu wakiwatesa na kuwauwa raia wasio na hatia kwa muda mrefu. Alikaa kimya akitegemea vyombo vinavyo husika na haki kuwa vingetenda haki. Alikuwa rahimu kuacha haki itendeke, ccm wameshindwa kuitenda haki ambayo ni tunu mbele ya macho ya mwenyezi Mungu na matokeo yake ccm haohao hutumia mikono yao kuingilia uhuru wa mahakama.

Mwenyezi Mungu ameamua kulitumia lililoitwa chagua lake (chaguo la mungu) huyu ni Jk, amemtumia yeye awaonee huruma raia wenzake wanaoteseka na dhambi ya kubaguliwa, kuuwawa na kuumizwa, haya yote ni kinyume na mapenzi ya Mungu. Mungu ameamua kumuwekea mkono Jk ili kuwakanya ccm wenzake kuacha kuwatumia polisi kutafuta uhalali wa kuungwa mkono, uhalali wa kuungwa mkono kupitia polisi kumesababisha mauwaji mengi ya raia (hasa kwenye mikutano ya vyama pinzani) hususani chadema.

Jk ameiona the hague? Amewahurumia watanzania wenzake kuuwa na polisi kwa sababu ya ccm kuidhibiti chadema? Nashindwa kupata majibu ya kina lakini jibu jepesi na rahisi ni kwamba " Mungu ameamua kumtumia yeye kuwaumbua ccm na kuwakanya waache kuuwa kwa kutumia polisi".
 
Labda alitakiwa kusema polisi waache kuitegemea CCM. Labda kuna a symbiotic relationship between the two that can not easily be broken.

A logical conclusion from the horses mouth, of which is valid and sound, kuna ushirika wa kutegemeana kati ya wote, maana nikikutuma kisha ukatekeleza ninayokutuma ninalazimika kukulinda ili usibwatuke kuwa nilikutuma...
 
Back
Top Bottom