Luteni
JF-Expert Member
- Jan 9, 2010
- 2,274
- 301
Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimewasilisha utetezi wake rasmi dhidi ya pingamizi lililowasilishwa kwa Msajili wa Vyama vya Siasa, John Tendwa, na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kikitaka mgombea rais wa CCM, Rais Jakaya Kikwete aenguliwe kwenye kushiriki Uchaguzi Mkuu.
Akizungumza na NIPASHE jana, Mwenyekiti wa kampeni za CCM Abdulrahaman Kinana, alisema wamewasilisha utetezi wao kwa msajili kama walivyotakiwa na wamezijibu hoja zote (tuhuma) zilizowasilishwa dhidi ya mgombea wao Rais Kikwete. Kinana alisema utetezi huo uliwasilishwa na viongozi wa CCM kwenye ofisi za Msajili wa Vyama vya Siasa jana.
Alipoulizwa madai ya mgombea wao kuongeza mishahara ya wafanyakazi kwa kutumia fedha za serikali (OC) tena bila kupitishwa na Bunge, Kinana alisema suala hilo halina ukweli, kwa vile fedha zote zinazotumika zilipitishwa na Bunge wakati wa mkutano wa bajeti.
Hata hivyo, alisema haelewi ni kwanini kila kitu ambacho kinasemwa na mgombea urais wa Chadema, Dk. Willibroad Slaa, kinaaminiwa na kuonekana kuwa ndicho chenye ukweli.
Akifafanua alisema suala la fedha za nyongeza ya mishahara ya wafanyakazi kutoka kwenye fungu la OC, ni madai yaliyotolewa na Dk. Slaa, lakini hakuna uthibitisho.
"Slaa kusema fedha hizo zimetoka OC, sio issue (hoja), hayo ni madai yake isichukuliwe kuwa ndio ukweli, na sisi tumepeleka majibu yetu kwa Tendwa, ambayo yamejaa ukweli na uthibitisho usiokuwa na ushabiki wowote wa kisiasa wala kujitafutia umaarufu," alisema.
Alipoulizwa wamejibu nini hasa katika madai hayo, alidai hawezi kutaja majibu hayo kwenye vyombo vya habari, kwani kwa kufanya hivyo na yeye atakuwa mtovu wa nidhamu kama Chadema.
"Msajili ametutaka tupeleke majibu yetu, tutakuwa watu wa ajabu kuyasambaza kwenye vyombo vya habari, tutakuwa tumeingilia kazi yake, ngoja asome mashtaka na utetezi, kisha atatoa hukumu," alisema Kinana huku akisisitiza kwamba kama mwandishi anataka mengine kuhusu majibu hayo awasiliane na Katibu Mkuu wa CCM, Yusuf Makamba.
Akizungumza na NIPASHE, Makamba alisema wamewasilisha utetezi huo, lakini naye akasema utetezi huo ni siri. "Wewe usitake kuuliza juu ya waraka wetu kwa Msajili, ila kile tulichokisema naweza kukueleza na wewe, mimi ndio Katibu Mkuu wa Chama hiki," alisema Makamba.
Alisema suala la kuongeza mishahara lipo kwenye Ilani ya CCM ya mwaka 2005.
Vilevile alisema hata ahadi aliyotoa Rais Kikwete ya kununua meli, ni jambo ambalo lipo kwenye ilani hiyo.
"Tuliahidi kwamba tukichaguliwa tutaimarisha usafiri wa anga, ardhini na ule wa majini. Sasa kununua meli ni sehemu ya kuimarisha usafiri wa majini,"alisema.
Alisema hata suala la nyongeza ya mishahara licha ya kuwepo kwenye ilani, lakini Rais Kikwete amekuwa akilizungumzia kila mara na kusema wafanyakazi wataboreshewa maslahi kwa kadri ya uwezo unavyopatikana.
Alisema Rais kutekeleza ahadi alizotoa kwa wafanyakazi sio rushwa, kwa vile hata Dk. Slaa naye ametoa ahadi ya nyongeza ya mshahara mkubwa zaidi kwa wafanyakazi, kuliko wanaolipwa sasa.
"Vilevile Rais kusema serikali itachukua deni la Nyanza la bilioni tano, pia alikuwa anatekeleza ilani yake, kwa vile ndani ya Ilani hiyo tumeahidi kuimarisha ushirika,"alisema Makamba.
Awali akizungumza na gazeti hili kabla ya kupeleka majibu kwa Msajili, Makamba alikejeli pingamizi hilo la Chadema na kusema limeandaliwa kwa hoja dhaifu.
Jumatatu wiki hii Chadema kupitia kwa Kaimu Katibu Mkuu wa chama hicho, John Mnyika, iliwasilisha pingamizi hilo kwa Msajili wa Vyama vya Siasa, John Tendwa.
Pingamizi hilo lililenga kumzuia Rais Kikwete, asishiriki Uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka huu, kwa madai kuwa amekiuka Sheria za Gharama za Uchaguzi ya mwaka 2010.
Hata hivyo Makamba alisema baada ya chama chake kupokea na kupitia pingamizi la Chadema, imebainika kuwa hoja zilizowasilishwa na wapinzani hao ni dhaifu na hazina msingi.
Makamba alisema Rais Kikwete hafanyi kosa lolote kuwaeleza wananchi mambo yaliyofanywa na serikali yake katika kipindi cha miaka mitano iliyopita na matarajio yake kwa miaka mitano ijayo.
Makamba pia alisema katika ilani ya chama hicho ya mwaka 2005, waliahidi kuboresha usafiri wa anga na majini, hivyo Rais Kikwete alipoahidi ununuzi wa meli haipaswi kutafsiriwa kuwa rushwa.
"Tuliahidi kuboresha usafiri wa anga na majini sasa ukienda sehemu ukakuta wananchi wana shida ya meli, usiwanunulie kisa ni wakati wa kampeni," alihoji.
"Sisi tunatekeleza ilani na lazima tuwaeleze wananchi tumewafanyia nini na tutawafanyia nini,"
Alisema Dk. Slaa amekuwa akiahidi mambo mbalimbali katika mikutano yake ya kampeni, hivyo haoni sababu ya chama hicho kuendelea kumsakama Rais Kikwete.
Kuhusu hoja nyingine ya Chadema kwamba mgombea wa CCM anatumia wadhifa wake wa urais kutoa ahadi, Makamba alisema kwa mujibu wa Katiba, Kikwete bado ni Rais hadi atakapopatikana mwingine katika Uchaguzi wa Oktoba 31 mwaka huu.
Katika pingamizi hilo lililowasilishwa na Mnyika, chama hicho kinalalamika kuwa Rais Kikwete amekuwa akitumia madaraka yake ya urais kutoa ahadi kwenye kampeni jambo ambalo linakiuka kabisa sheria hiyo.
"Sheria inakataza mtu aliyeko madarakani kama Rais au waziri kutoa ahadi yoyote iwe ya mali au fedha taslimu kwa kutumia wadhifa wake kwenye kampeni, lakini tumeshuhudia Rais Kikwete akifanya hivi kila siku ina maana sheria aliisaini bila kuisoma," alihoji Mnyika.
Alisema nyongeza ya mshahara katikati ya kampeni ni rushwa ya waziwazi kwa mujibu wa kifungu namba 21 (1) (a) na (e) ya Sheria ya Gharama za Uchaguzi namba 6 ya 2010.