CCM yaonywa kuwa macho na wapinzani

Zak Malang

JF-Expert Member
Dec 30, 2008
5,404
234
* Ni kauli ya aliyewahi kuwa Katibu Mkuu Ikulu
* Asema wasipoangalia watashangaza Oktoba 31

Aliyewahi kuwa Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais na kushika nyadhifa mbalimbali wakati wa serikali ya wamu ya kwanza, Mzee Timothy Apiyo, ameitahadharisha CCM kuwa macho na wapinzani kwani wanaweza kushangaza kwenye matokeo ya uchaguzi mkuu Oktoba 31, mwaka huu.

Akizungumza katika mahojiano maalum na NIPASHE JUMAPILI nyumbani kwake Jijini Dar es Salaam jana, alisema CCM haina budi kuwa macho na pia kutompuuza mgombea urais wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk. Wilbroad Slaa, kwani anaweza kukishangaza chama hicho tawala kwenye matokea ya Uchaguzi Mkuu Oktoba 31.

Pia alizungumzia mambo mbalimbali yanayohusu nchi na maisha yake binafsi, Aidha, alimsifu mgombea huyo wa Chadema kuwa ni mtu mwenye ufahamu mkubwa wa mambo, msomi na mwenye uwezo mkubwa wa kujenga hoja zinazoweza kuwashawishi wananchi wakamchagua, hivyo CCM inatakiwa kulitambua hilo.

Mzee Apiyo ambaye alikuwa mmoja wa viongozi wa serikali walioaminiwa sana na Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere wakati wa utawala wake, alisema ingawa anaamini kuwa mgombea urais wa CCM, Dk. Jakaya Kikwete, atashinda uchaguzi huo, lakini anaweza kupata upinzani mkubwa kutoka kwa mgombea huyo wa Chadema, endapo chama hicho tawala hakitajipanga vizuri.

"CCM ikifanya mchezo itashinda kwa jasho jingi na wakizembea kidogo tu wanaweza kuwa 'suprised' (shangazwa) na matokeo".

"Slaa ni msomi na ni mwanasiasa machachari, ana uwezo wa kueleza mambo vizuri sana, kujenga hoja na kuwashawishi wananchi wamchague" alisema Mzee Apiyo ambaye alijitambulisha kuwa ni wanachama mtiifu wa CCM.

Mzee Apio ambaye kwa muda mrefu sasa hajasikika hadharani tangu alipostaafu kazi serikalini Julai, 1986, alisema CCM pia inatakiwa kuwa makini na Chadema kwa kile alichoeleza kuwa ni chama kinachoonekana kuwa na wasomi wanaojua kuchambua mambo na watu wenye uwezo wa kifedha wanaokiunga mkono.

Hata hivyo, alisema pamoja na uhodari huo wa Dk. Slaa, lakini anaamini kuwa CCM itashinda uchaguzi mkuu ujao kwa kuwa imewafanyia wananchi mambo mengi tangu Tanganyika ilipopata uhuru, mambo ambayo hadi leo yanaonekana kila kona ya nchi.

"Pamoja na yote hayo, CCM itashinda uchaguzi kwa sababu kipo kila kona ya nchi na kazi zake zinaonekana kila mahali na wananchi wanaona kazi za Kikwete alizozifanya katika kipindi cha miaka mitano ya urais wake," alisema.

Alimsifu Rais Kikwete kuwa amefanya mambo mengi mazuri katika awamu yake ya miaka mitano ya urais, ambayo yatambeba kuchaguliwa tena na wananchi, tofauti na wagombea wa vyama vingine ambao hawana cha kuonyesha.

"Wananchi watamchagua tena Kikwete kwani wanaona jinsi alivyoboresha sekta mbalimbali kama miundombinu na huduma za jamii ikiwemo ujenzi wa shule, wana macho wanaona mambo hayo" alisema Mzee Apiyo.

Akizungumzia kampeni za uchaguzi mkuu zinazoendelea nchini kote, Mzee Apio, alivitaka vyama vyote vinavyoshiriki uchaguzi huo kuendesha kampeni kwa amani na utulivu na kutumia fursa hiyo kuwaeleza wananchi ukweli wa nini vitafanya endapo vitachaguliwa.

Alisema kazi za vyama vya siasa wakati huu wa kampeni ni kuwaeleza wananchi vitasaidiaje kutatua matatizo mbalimbali yanayowakabili wananchi ambao ndiyo wapiga kura na kwamba vinatakiwa kueleza ukweli badala ya ahadi zisizotekelezeka ili tu viingie madarakani.

"Vyama vya siasa vieleze ukweli mtupu kwa sababu wananchi wanaona na wana ufahamu mkubwa sasa, vizingatie kunadi sera na ilani, hasa CCM wanatakiwa kuwaeleza wananchi wamefanya nini na watafanya nini wakichaguliwa tena kuongoza nchi, wasitishwe na Dk. Slaa kwani wana cha kujivunia, serikali imefanya mambo mengi mazuri ambayo wananchi wanayaona", aliongeza kusema.

Pia Katibu Mkuu huyo mstaafu wa Ofisi ya Rais, cheo ambacho kwa sasa kinatambulika kama Katibu Mkuu Kiongozi, alivitaka vyama vya siasa kujiepusha na kauli ambazo zinaweza kusababisha machafuko wakati huu wa kampeni na uchaguzi mkuu.

"Vyama visitufikishe mahali tukauana kama ilivyokuwa kwa wenzetu Kenya, suala hili liangaliwe sana kwani amani ni kitu muhimu kwa nchi yetu" alisema.

Alisifu kuwepo kwa mfumo wa vyama vingi nchini, ambao alisema umesaidia kuikosoa serikali iliyopo madarakani na kuifanya iwajibike zaidi kwa wananchi.

"Hata Mwalimu Nyerere hakupinga vyama vya upinzani kwa sababu alijua umuhimu wake, ni lazima tukubali kukosoana kwa manufaa ya nchi yetu?", alisema.

Katika mahojiano hayo maalum na gazeti hili, Mzee Apiyo, pia alizungumzia mambo mengine mbalimbali kama vile vita dhidi ya rushwa, uadilifu kwa viongozi, kubinafsishwa kwa mashirika ya umma, jinsi ya kuzuia viongozi kuingia mikataba mibovu na mambo mengine mengi. Jumapili ijayo tutachapisha mahojiano kamili kwenye gazeti hili.

CHANZO: NIPASHE JUMAPILI
 
Apiyo kasema ukweli kabisa -- maana kaona ufisadi, anasa na kutojali wananchi kunavyoipeleka CCM shimoini wasipojiangalia. Alishindwa tu kusema inabidi sasa CCM watumie dola, mabavu na wizi wa kura kushinda, kama nilivyosoma katika topic moja kuhusu uhamisho ghafala wa Mkurugenzi wa Arusha (ambaye pia ndiye msimamizi wa uchaguzi wa jimbo hilo ili tu kuhakikisha yule mama unpopular -- Batilda katika jimbo la Arusha.

Yeye Apiyo ni mfano mmoja wa viongozi wa zamani ambao hawakuwa na tamaa ya kujilimbikizia mali na nasikia anaishi kwa pensheni tu. Jee, lini Tanzania inaweza tena kupata viongozi kama hawa?
 
Back
Top Bottom