CCM yabadilisha taratibu kugombea urais 2015

Mahesabu

JF-Expert Member
Jan 27, 2008
5,970
3,821
Thursday, 14 April 2011

* Lengo kudhibiti matumizi ya fedha
* Mukama: Mabadiliko si kujipodoa
* January: Kuvaa magwanda si ujemadari
* Nape ataka wapinzani kufungasha virago


Joseph Damas na Theodos Mgomba, Dodoma

UTARATIBU wa kumpata mgombea urais katika uchaguzi wa mwaka 2015 ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), umebadilishwa.

Hatua hiyo ni sehemu ya mageuzi makubwa yanayoendelea kufanywa ndani ya Chama. Mabadiliko hayo yanalenga kudhibiti wagombea wenye matumizi makubwa ya fedha kwa nia ya kununua kura za wajumbe wa vikao vya uchujaji na uteuzi wa majina.

CCM pia imetangaza kubadili utaratibu wa uteuzi wa wagombea ubunge na udiwani, ambapo sasa watachujwa kwanza ili kuwapata watatu, ambao watapigiwa kura ya maoni na wanachama.

Hayo yalielezwa jana na Makamu Mwenyekiti wa CCM (Bara), Pius Msekwa, alipohutubia wana-CCM na kuitambulisha sekretarieti mpya ya Chama kwenye viwanja vya Nyerere Square, mjini hapa.

Alisema katika kuhakikisha hilo linatekelezwa kwa mafanikio, Chama kitarekebisha kanuni juu ya watendaji na viongozi wanaogombea nafasi za kisiasa, ambazo wao pia wanahusika katika vikao vya maamuzi ya juu.

Msekwa alisema mbio za urais katika uchaguzi wa mwaka 2015 zimekuwa zikiwaumiza vichwa kutokana na makundi yanayojipanga kuwania kuwagawa wanachama na kuathiri umoja na mshikamano.

"Kiini cha tatizo hili ni utaratibu wa kupata wagombea wa CCM unaotumika sasa, hivyo tumeamua kuubadilisha ili kudhibiti matumizi ya fedha," alisema.


Kuhusu suala la rushwa na ufisadi, Msekwa alisema limekuwa mzigo mkubwa kwa CCM licha ya juhudi zinazoendelea kuchukuliwa na serikali.

Alisema Chama kimejipanga kuhakikisha kinafanya mageuzi makubwa ili kuondoa muonekano huo na kuwa ni Chama kinachopambana na rushwa kwa vitendo.

"Taswira ya Chama imeathiriwa mbele ya umma na migogoro ya viongozi kutokana na makundi yaliyopo. Tumebebeshwa mzigo kuwa tunakumbatia mafisadi," alisema.

Msekwa alisema CCM imepoteza sifa ya awali ya kuwa Chama kinachojali maslahi ya wanyonge, na sasa kinabebeshwa mzigo wa kuwa Chama cha matajiri.

Alisema mageuzi hayo makubwa yatadhihirisha kuwa CCM ni chama cha wanyonge na kwamba, hakikumbatii wala rushwa na mafisadi.

Kuhusu viongozi ndani ya CCM wanaotuhumiwa kwa ufisadi, Msekwa alisema wametakiwa kupima uzito na kuchukua hatua wenyewe.

Msekwa alisema Chama kina viongozi wengi, hivyo wote wanaotuhumiwa kwa ufisadi na rushwa watajulishwa kwa barua na Katibu Mkuu wa CCM, Wilson Mukama ili wajitambue na kuchukua hatua ya kujivua uongozi kwa maslahi ya Chama.

Hata hivyo, alisisitiza iwapo wahusika watashindwa kuwajibika, Chama kitawatimua na hilo litafanyika wakati wa Kikao cha Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM kinachotarajiwa kuketi miezi mitatu ijayo.

Kwa upande wake, Mukama alisema Chama ni imara na kimeweza kufanya mabadiliko makubwa bila nchi kutikisika.

Alisema hilo linaonyesha ukomavu wa kisiasa ndani ya Chama tofauti na vingine, ambapo hata akijiuzulu kiongozi mmoja mambo hubadilika na vyama hivyo kuyumba.

"Mabadiliko haya si nguvu ya soda, ni endelevu na Chama kimekusudia hilo kwa lengo mahsusi. Si mabadiliko ya kujipodoa kwamba kesho ukikosa vipodozi unarudia sura yako ya zamani," alisema Mukama.

Mukama alisema CCM imedhamiria kurudisha imani ya wananchi kwa Chama, kwa kuwa uongozi hauwezi kuganda kama barafu na ndiyo maana hilo limefanyika.

Naye Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, aliwataka wapinzani kuanza kufungasha virago. Alisema amerejea nyumbani kwa kishindo.

Alisema serikali ilimuazima kwa kipindi cha miezi minane, lakini sasa amerejea akiwa na nguvu mpya na moto aliouanzisha utaendelea kushika kasi mikoa yote.

Katibu wa NEC, Siasa na Uhusiano wa Kimataifa, January Makamba, alisema hotuba zake hazitakuwa na vifungu vya Biblia wala Kurani kwa kuwa kazi zake kikatiba ni kufuatilia hali ya siasa nchini.

Amesema jukumu lake lingine ni kufuatilia vyama vya siasa na kwamba, kazi hiyo anaimudu na kuwataka wana-CCM wasiwe na shaka hata kidogo.

"Kazi ya kuwabomoa wapinzani ni rahisi kwangu, nitaifanya kisayansi na wala msiwaone wamevaa magwanda mkaona ni majemedari... wale ni wapesi. Hakuna sababu ya kuwaiga kwa kuwashawishi vijana wa vyuo vikuu kuzomea.

"Jukumu letu ni kuwaeleza wanafunzi wasikileze hoja na baadae kujibu," alisema.

CHANZO: Gazeti la Uhuru
 
Katibu wa NEC, Siasa na Uhusiano wa Kimataifa, January Makamba, alisema hotuba zake hazitakuwa na vifungu vya Biblia wala Kurani kwa kuwa kazi zake kikatiba ni kufuatilia hali ya siasa nchini.

Amesema jukumu lake lingine ni kufuatilia vyama vya siasa na kwamba, kazi hiyo anaimudu na kuwataka wana-CCM wasiwe na shaka hata kidogo.

"Kazi ya kuwabomoa wapinzani ni rahisi kwangu, nitaifanya kisayansi na wala msiwaone wamevaa magwanda mkaona ni majemedari... wale ni wapesi. Hakuna sababu ya kuwaiga kwa kuwashawishi vijana wa vyuo vikuu kuzomea.

"Jukumu letu ni kuwaeleza wanafunzi wasikileze hoja na baadae kujibu," alisema.

Kweli kazi ipo January anasema yeye atawabomoa wapinzani. Hajui tatizo ni kubwa kuliko anavyofikiri, CCM sisi wananchi tuna njaa, hatuna uhakika wa kesho. Baba zetu hawana madaraka nasi tukaachiwa hazina, tupeni hizo mic nasi tuseme shida zetu kama mtasimama, na shida hzi tunazo kwa miaka hamsini.

Kubomoa upinzani ni kutekeleza ahadi zenu za miaka hamsini sasa. tuanataka ajira, elimu bora, haki mbele ya sheria, barabara nzuri na wezi wote wafikishwe mahakamni na wataifishwe vyote walivyotuibia. Bila hayo yote ni ngonjera tu.

Hatujachoka kuiona CCM tu hata kusikia pumba mnazoongea kana kwamba hamjui tatizo.
 
Hao wanatapatapa tu hata wafanye nini hatudanganyiki.Ka makamba kadogo nako kashaanza kuleta ujeuri.CCCM Kwishney haturudi ng'o.
 
ama kweli siasa ina mizaha mingi sana!

na hao wagombea ubunge watakaokuwa wanachujwa na kubaki watatu, nani atafanya kazi ya kuwachuja? hawaoni wanatengeneza mwanya mwingine wa rushwa? wanaenda nbele hatua moja wanarudi nyuma hatua kumi!
 
Waje arusha tunawakaribisha sana...

Wamtuoe jk na wamfukuze ccm kama kwa hao wengine..

Pia kwanini wasi wataje hao mafisadi ndani ya ccm kama wanawajua??? Waache unafiki hawawezi kuwatoa kamwe..

January anapiga kelele wakati rostam alimdhamini kwenye kampeni yake ya ubunge???

Ccm ondokeni we are tired of you!!!!!!!!!!!!!!
 
Mimi na naamini mwananchi yeyote yule muelewa hakuna anayejali nani analeta mabadiliko ya ukweli na endelevu ya matatizo yetu sugu ya umasikini, wizi na ubadhirifu wa mali ya umma na ukandamizaji wa wanyonge katika haki zao.

Na naona bado matatizo kama chama (Kamati yake) kitatupa majina 3 ya wa kuwapigia kura -maana wote watajieleza huko sisi wananchi tutanyimwa nafasi ya kusikia na kujua nani amejieleza vizuri. Utaratibu huu haufai kwa sababu kwa mbinu hii chama kina mwanya mkubwa kuliko sasa wa kutuletea kinayemtaka kwa kumpa weeker opponents (wananchi watakuwa hawajui CV za walioachwa, siri kwa faida ya nani).

Tukumbuke tatizo la sasa ni kwamba chama ni pale kataa maoni ya wananchi na kuwapelekea wanayemtaka na ikiwa ni pamoja na kuchakachua kura za wananchi hata ndani ya chama chenyewe. Kama watatafasiri kujivua gamba 'literally' yaani nyoka akijivua gamba mengine kama maeneo ya mawindo, ya kulala, nk. yanabaki vile vile ila anaweza kuongeza kuwa mwepesi wa kuongeza kasi ya kufanya aliyokuwa anafanya (e.g. kunasa mawindo yake na kuwakwepa maadui wake) Kama ni hivyo ndiyo indicator ya awali ya tutazamie nini I can only see signs of change for worse.

Hivi sasa walikuwa wanaingilia uhuru wa watu kuchagua wanayempenda kwa kuchakachua maoni na kura mbele ya pazia na kuweza kulalamikiwa kwa ushahidi (kwa hasira ya wananchi hasara imeonekana kupoteza eneo kwenda upinzani -CCM ndiyo imeimarisha upinzani).

Sasa watapata kile kile ki-system au kwa utaratibu alioupendekeza Mh Msekwa ni iwe rahisi kwa chama kujitetea kwamba si mtu mmoja anayeteua majina 3 bali ni kamati inayotokana na watu tuliowachagua wenyewe na kwahiyo ni kwa maslahi ya chama na wananchi (kwangu maslahi ya chama siyo lazima iwe maslahi ya wananchi). Kwa mazoea watu hasa wazamani (ambao wanazidi kupungua) hulazimika tu kuhama CCM. CCM isome alama za nayakati leo wananchi wengi ni wasomi wa kiwango kikubwa na itakuwa zaidi hivyo hiyo 2015.

CCM inahitaji vitu viwili TU TRANSPARENCY NA KUWA PEOPLE CENTERED (mengine hayo wawaachie wananchi na wataalamu wao).
 
January huwezi kutushawishi maana mnapokezana uongozi kwa Familia zenu, sisi sio wajinga tunawaelewa sana! Uchungu wa maisha tuliyonayo hamjui hata kidogo maana ninyi na wenzako mlioko katka daraja la utawala mumeanzisha Dini yenu au tuseme kabila lenu la watawala na hivyo mnapokezana madaraka huku mkituchonganisha sisi huku chini mara udini mara ukabila ili muendelee kutunyonya siku zote.

Tumewashtukia! kizazi hiki cha Technologia ya habari na mawasiliano kimebadilika sana! Desturi pia zimebadilika,ulimwengu umekuwa kama kijiji siku hizi ,tunaona wenzetu wanafanya nini na tumeanza kuwa na global culture na hivyo mabadiliko lazima na siasa za kale zinaisha maana ahazina nafasi ktk kizazi hiki!. Sasa mmemamua kuipromote JamiiForum watu wengi sasa watajiunga zaidi, vita ya kwenye Cyberspace ni ngumu sana,maana ndani ya cyberspace hakuna mipaka!

Ushauri! boresheni Maisha yetu kwa serikali kuwajibika ipasavyo kwa kuondoa Rushwa bila kuogopa watu,huduma za jamii nzuri.Elimu Bora na mambo mengine mengi ambayo ni majumu ya serikali na uone kama mambo hayatainyookea CCM lakini bado swali moja Gumu Mtaweza sasa wakayi miaka 50 Mmeshindwa?
 
kutoka Yusuf Makamba kuingia January Makamba
kutoka Moses Nnauye kuingia Nape Nnauye
Kutoka Ali Hassan Mwinyi kuingia Hussein Mwinyi nk.
Huko ndiko kuivua gamba. Unavua gamba baba unaingiza gamba mtoto; halafu mnatudanganya eti kuna mabadiriko ya mingi!
Tumechoka kuwa wadanganyika.
 
Sikujua kuwa huyo makamba jr ni mtupu kiasi hicho, yaani kwa akili zake za kukaririshwa anajua wanavyuo wakizomea wameshawishiwa na wapinzani!! Na je, wabunge wa ccm wanapowazomea wapinzani huwa wameshawishiwa na nani???
 
Tatizo ni mtazamo. CCM wanfikiri "wapinzani ni kitu" kumbe ni watu walio na akili na utashi. Wanafikiri mtu anabadilishwa kama kitu. Hilo ni kosa kubwa. Wajiulize kuwa Chama kama CHADEMA imetumia muda gani kutengeneza taswira yake ya sasa. CCM watatumia muda kama huo au zaidi kurudisha taswira nzuri kwa jamii. Kumbuka kubomoa ni rahisi kuliko kujenga. Wakati wanajibomoa kwa ufisadi wenzao walikuwa wanajijenga. Wasigetemee urahisi wa mambo. Inabidi wajenge hoja nzito zinazotelekezeka la sivyo wataendelea kuzomewa.
 
Tunawatakia kila laheri CCM sote lengo letu ni kutumikia wananchi ktk uadilifu; kama kuna nia ya dhati kwa CCM kujikosoa na kunyoosha mambo...well and good, lakini sisi tunatoa muda baada ya muda tutaliona kama ni la uongo au kweli....ulimwengu wa kudanganya watu sasa kwishilia mbali watakuwa wanajidanganya wao wenyewe
 
Tatizo hawa jamaa wanawaza urais 2015, kubomoa Chadema basi! hawafikirii kuondoa kero za wananchi na ufisadi uliopitiliza, kwa mtaji huo tusubiri tarumpeta saba zianze kuwagonga, Chadema kitapasua anga maradufu kwa mtaji huu wa sasa wa CCM. tusubiri tuone.
 
Gamba la CCM ni kamati yao walioivunja LAKINI GAMBA la watanzania ni CCM yenyewe ni lazima Tujivue nalo kwa nguvu zote.
1. Elimu duni
2. Umeme hakuna miaka yote hamsini ya utawala wao.
3. Miundombinu hakuna ya kuridhisha hakuna
4. Jiji kubwa kama DAR hakuna maji
5. EPA, Meremeta, IPTL, BoT twin tower, Dowans. Deep green, Alex stewart, Kiwira, TRC ukosefu wa ajira nk, leo wanatuambia wameanza upya - Shida ya CCM ni kudanganya umma wa watanzania ili waendelee kutawala kulinda uozo wa watangulizi wao

Ninashukuru Chadema kwa kuwafungua watanzania macho hata mwanangu wa miaka minne alipoona msafara wa watu kwa babu loliondo kwenye Tv akasema baba ona Chadema. kazi yenu si ndogo.
 
Wanahaha tu hawa hawajui watendalo mara wameshika hili mara wameshika lile na yote hayafanikiwi, kiwewe kinazidi kuwapanda.
 
ama kweli siasa ina mizaha mingi sana!

na hao wagombea ubunge watakaokuwa wanachujwa na kubaki watatu, nani atafanya kazi ya kuwachuja? hawaoni wanatengeneza mwanya mwingine wa rushwa? wanaenda nbele hatua moja wanarudi nyuma hatua kumi!
hawawezi kuona, ukishakua kiongozi unapata kama upofu wa aina fulani,
 
watahangaika sana.. sisi tunasubiri katiba mpya tu ili uchaguzi ujao tuchukue nchi kwa landslide
 
Back
Top Bottom