Doto James, Bwana Malipo Mkuu wa serikali
Ni kaa la moto!
Hakuna mtu anaetaka kuligusa.
Wazungu wanaita "third rail," kwa sababu reli ina mitarimba mitatu: miwili inatambaa sambamba ardhini, yenyewe unaweza kuigusa, kuichezea na hata kuing'oa wakati wowote ili mradi treni halipiti na serikali haikuangalii. Mtarimba wa tatu wa reli unatembea hewani sambamba na ile mihimili ya ardhini, lakini mhimili huu umebeba umeme! Treni liwe linapita, treni halipiti, serikali wanakuangalia au hawakuoni, huthubutu kugusa huu waya muda wowote!
Kwa mara ya kwanza raia Tundu Lissu aligusa huu mtarimba, masaa mawili baadae akamwagiwa risasi 16 kena kena (point blank range)!
Ni mtarimba wa Doto James, mtoto wa dada yake Rais Magufuli ambae ni katibu mkuu Hazina aliyeteuliwa na mjomba wake akitokea Tanroads mkoani. Ndie Mtanzania peke yake ameiona na kuidhinisha mikataba ya manunuzi wa ndege, bwawa na rufiji, na reli ya SGR zaidi ya Rais Magufuli.
Majuzi kwenye kampeni, mgombea Urais, raia Lissu akiwa Mbarali, ameibua timbwili pacha lingine ambalo tulikuwa hatujawahi kulisikia: Aliyepewa zabuni ya kujenga airport Chato ni mme mwenza wa Rais Magufuli, Mayanga Construction. Na aliyeidhinisha hela ni mtoto wa dada, Doto James.
Mpaka sasa wameibuka makada wa CCM kujibu hoja za upinzani, Spika Ndugai, Mstaafu Makamba, Mwenezi Polepole, Msemaji Abbasi na wengine, lakini hakuna aliyethubutu kugusa waya wa Doto James wala Mayanga construction. Msemaji Abbasi kajaribu kusogelea suala la gharama za miradi kujulikana lakini hakusema mikataba iko wapi na nani kawahi kuiona zaidi ya Rais na Doto James ambae anasaini hundi za malipo. Sheria ya mikataba iliyosainiwa na Magufuli mwenyewe inataka mikataba iwe wazi kwa umma kupitia bunge.
Raia Lissu anasema Baba wa Taifa amekaa Ikulu miaka 24 hajawahi hata kufikiria kufanya manuva za kuweka ndugu zake wa damu kwenye nafasi nyeti ili wapitishe mahela ya kujenga airport kijijini kwake kama Mobutu Sese Seko, wala kuidhinisha miradi ya usiri.
Sasa makada wamemwachia Rais Magufuli apambane na hilo fupa alilorushiwa na raia Lissu. Wanaogopa kulikoroga zaidi, maana hawajui Rais JPM mwenyewe anafikiria nini. Wamezoea kuongea kwa kupata cues ( ishara) kutoka kwa Rais. Wanamuiga mpaka kuongea vilugha vyao kwenye halaiki za umma wenye makabila mengi, kitu kipya katika nchi. Lakini kwa hili la Doto James na Mayanga Construction Rais JPM kimywa! Makada hawajui cha kusema. JPM anaweza kulitafuna hilo fupa mwenyewe au ataendelea kuliacha limtafune yeye ?