CCM wachezeana rafu kumrithi Wangwe

Pdidy

JF-Expert Member
Nov 22, 2007
50,947
22,100
CCM wachezeana rafu kumrithi Wangwe



Na George John,Tarime

SIKU chache baada ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kutangaza rasmi ratiba ya mchakato wa kumpata mgombea wa chama hicho katika Uchaguzi mdogo wa Ubunge Jimbo la Tarime, zimeibuka shutuma zikielekezwa kwa viongozi wakuu wa chama hicho wilayani humo wakidaiwa kumbeba mgombea mtarajiwa mmoja.

Habari zilizopatikana juzi zinadai kuwa viongozi hao wa CCM ngazi ya wilaya wanatuhumiwa kupita kila kona ya jimbo hilo na kutangaza jina la mwana CCM huyo kama njia moja wapo ya kushawishi wajumbe kumpigia kura za maoni zitakazopigwa katika Mkutano Mkuu wa Wilaya Septemba 3 mwaka huu.

Habari hizo zinadai kuwa pamoja na kwamba jina la mwanaCCM huyo halijaingizwa katika vitabu vya chama hicho kama mmoja wa watu wanaowania nafasi hiyo kwa vile bado hajachukua fomu, lakini viongozi hao kwa nyakati tofauti wanadaiwa kunadi jina hilo ili lifahamike mapema kwa wajumbe.

Imeelezwa kuwa viongozi hao mbali na kufanya ushawishi huo kwa wajumbe, wameanza mbinu chafu za kuchafua baadhi ya wanachama walioonesha nia ya kugombea nafasi hiyo kwa kupanga kuwandikia rikodi mbaya kwenye ngazi mbalimbali za chama hicho.

“Juzi tu chama kimetangaza ratiba ya kuchukua fomu kwa wanaCCM wenye sifa kuwania ubunge lakini cha kushangaza viongozi wetu wa wilaya wanaonekana kulalia kwa jina la mgombea mmoja kwa vile tu mmoja wa viongozi wa chama wilaya wanafanya naye biashara,”kilisema chanzo chetu.

Kiliendelea kudai kuwa, vingozi hao baada ya kufanya tathimini na kuona jina la kipenzi chao si chagua la wana Tarime wameanza kutumia mbinu hizo chafu kitu ambacho alidai kisipoangaliwa, kinaweza kuigharimu tena CCM.

“Tarime wanataka mtu na si kuambiwa eti huyu ni mchumi au anafanya kazi katika mamlaka kubwa...hapa hatuna hilo hata ukileta mkulima au mfugaji sisi tutampa kura na wasipoangalia hapa na kutuchagulia mtu, yale ya mwaka 2005 ndiyo utakayosikia yametokea,”kilieleza chanzo hicho.

Mmoja ya viongozi wanaotuhumiwa kubeba jina hilo,Mwenyekiti wa CCM Wilaya, Bw. Museti Nyaronyo alipozungumza na Majira kwa njia ya simu,alikana kuwepo kwa mchezo huo na kusema huo ni huzushi wa kisiasa.

Alisema chama chake hakiwezi kumkumbatia mtu mmoja katika uchaguzi huo kwa vile maamuzi yote yatafanywa na Mkutano Mkuu wa Wilaya kwa kura za maoni na si viongozi wachache.

“Siwezi kumkumbatia mtu hata siku moja je huyo tunayemtaka akifa…CCM Tarime kwa sasa hatuna makundi hata kidogo, hao wanaosema ni wazushi tu tunaamini kila mwana CCM ana haki ya kuchukua fomu na kuchaguliwa,”alisema Bw. Museti.

Aliongeza kuwa viongozi wa wilaya na mkutano huo wa kura za maoni unachofanya ni mapendekezo tu kwenda ngazi za juu ya chama na si uteuzi wa mwisho.

WanaCCM ambao tayari wameonesha nia ya kugombe ni pamoja na Ofisa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) makao makuu,Bw. Ryoba Kangoye,Mtunzi wa vitabu Bw. Nyambari Nyangwine, Rais wa Shirika moja lisilo la kiserikali (SACHITA) Bw. Peter Mwera, huku zikiwepo taarifa za wanaCCM wengine zaidi wenye nia ya kuingia kwenye kinyang'anyiro hicho.

Kwa mujibu wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Uchaguzi huo mdogo unatarajiwa kufanyika Oktoba 12 mwaka huu kufuatia kifo cha aliyekuwa Mbunge wa Jimbo hilo marehemu Chacha Wangwe aliyefariki kwa ajali ya gari Julai 28 mwaka huu eneo la Panda mbili Kongwa mkoani Dodoma.
 
Sio jambo la ajabu kwa CCM kuchafuana maana huo ndio mtindo wao wa siasa chafu Tokea uchaguzi mkuu wa 2005 kwa ngazi zote.
Hili ndilo lililosababisha tuna viongozi wengi wa hovyo kabisa kupata kutokea katika historia ya nchi hii.
 
Back
Top Bottom