Rev. Kishoka
JF-Expert Member
- Mar 7, 2006
- 4,526
- 1,540
CCM Pambalama, CCM Pambalama, kocheleli CCM eee, kocheleli CCM Pambalama Kochelele...
Fukuto la fukuta, moshi wafoka, mapovu yanamwagika, CCM imefika njia panda! Ama isuke au inyoe!
Hili vurugu la Richmond, likizingirwa na BOT EPA, BOT CIS, BOT Minara, Rada, Kiwira, Buzwagi na moto kutoka Upinzani, unafanya mambo kadhaa tujiandee kutokea.
- Wabunge ambao si mtandao, wenye uchungu wa kweli wa CCM, kuendelea kusulubisha viongozi wao na Serikali yao iwe wazi. Hawa wabunge, mwokozi wao na nguzo yao ni Wastaafu Malecela, Kawawa, Mwinyi, Salim na Msuya. Huku wako hawa walioshupalia RDC;-Mwakyembe, Kilango-Malecela, Seleli, Kimaro, n.k.
- Team Mkapa; huku ni wale wajanja wa Che-Nkapa ambao bado wanatibu majeruhi ya mchakato wa kugombea Urais 2005 na kunyang'anywa tonge la Hatamu za Chama. Hapa kuna Mang'ula, Ngwilizi, Kigoda, Kinana, Warioba na Ruhinda. Katika kundi hili, pia wapo wale waliotajirika na mradi wa Ujasirimali Ikulu; Yona, Mramba, Mgonja, Mkono n.k.
- Mtandao; Kundi hili lina majeruhi wengi kutokana na kuvunjwa kwa baraza la mwazirina mwegemeo wa kashfa za ufisadi kuwa kwenye shingo zao. Kundi hili, limegawanyika katika sura mbili;
- Team Kikwete ambayo wamebakia Makamba, Chiligati, Membe, Migiro, Karume
- Team Rostwassa(Rostam/Lowassa); Karamagi, Msabaha, Nchimbi, Apson, Meghji, Kamala, Diallo, Chenge,
- Wasiofungamana lakini wana nguvu na ni tishio; Pinda, Mwandosya, Sumaye, Balali, Salmin, Magufuli, Msekwa na Sitta.
Nanukuu baadhi ya mambo ambayo yanaashiria kuwa huko CCM si salama, na hata kama wakitoka nje ya ukumbi wakiwa wamekumbatiana, tusiwaamini.
BAADHI ya wabunge wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), wamesema wakati umefika sasa wa kila mtu ndani ya chama hicho kubeba msalaba wake mwenyewe, na hawapo tayari kutumiwa tena kama mihuri ya kupitisha mambo ya Serikali ambayo mengine wanadai yamekuwa yakiwanufaisha baadhi ya watendaji serikalini.
Na kama hiyo haitoshi, baadhi yao wamesema watendaji wengine wa Serikali wangetumia busara kuachia nafasi zao kuliko kusubiri kuaibishwa na wanachama wenzao ndani ya Bunge.
Chini ya utaratibu wa three line whip uliozoeleka bungeni, wabunge wa chama fulani wanatarajiwa kukubaliana na mambo kadhaa ambayo wanayatetea kwa pamoja wakifika bungeni. CCM imenufaika ndani ya Bunge kwa utaratibu huo ambao hata hivyo, umewafanya wabunge wake kudharauliwa na wananchi katika majimbo yao.
Wakati hayo yakijiri, wabunge wa CCM walitarajia kukutana jana jioni, baada ya kuahirishwa kwa kikao cha Bunge, ambapo mkutano wao huo ulipangwa kufanyika kwenye Ukumbi wa Msekwa mjini hapa, bila shaka kuwekana sawa juu ya jinsi ya kujadili ripoti za uchunguzi wa Zabuni ya Kampuni ya Richmond (iliyowasilishwa bungeni jana), ubadhirifu katika Akaunti ya Ulipaji Madeni ya Nje (EPA) katika Benki Kuu (BoT), huku wakisubiri ile ya Kamati ya Rais ya Madini.
Habari zaidi zilisema jana kwamba, Rais Jakaya Kikwete mwenyewe alitarajia kuwasili mjini hapa jana, na kama hangehudhuria mkutano huo, basi angekuwa akifuatilia kwa karibu na kupewa taarifa ya kile kinachoendelea.
Hali imekuwa tete, na huenda ndiyo ilisababisha Spika wa Bunge, Samuel Sitta, aliyekuwa aanze ziara nchini Marekani kuifuta. Awali, aliagiza kwamba atakapokuwa huko, Bunge lisijadili masuala hayo ya BoT wala Richmond, bali wamsubiri hadi atakaporejea nchini. Ilikuwa arejee leo.
Kwa upande wa wabunge, Anna Kilango, mbunge machachari kutoka Same Mashariki, ameiambia Rai kwamba umefika wakati wa wana CCM kusafishana wenyewe kwa wenyewe ili kurudisha imani ya wananchi katika majimbo, hali ambayo anadhani imepotea.
Mimi nimegundua wananchi wangu wamepoteza imani na Serikali na wamekuwa wakinitupia mawe sana, huku wakidai hatuitendei haki Serikali. Hatufanyi kazi ndani ya Bunge na hatuwatetei wananchi ndani ya Bunge, alisema mbunge huyo na kuongeza:
Kuna mambo kweli tungependa yafanyike. Serikali ya CCM imechafuliwa na wana CCM. Na kama hivi ndivyo, huu mzigo hatuwezi kumtupia yeyote. Ni sisi wana CCM tunaotakiwa kuifanya. Basi tukosoane sisi wenyewe ili wananchi wa Tanzania warudishe imani kwani wametulalamikia vya kutosha.
Mbunge huyo aliwataka watu kutoilaumu CCM wala Serikali yake kwa makosa yanayofanywa na watendaji wake.
Lakini jambo ambalo ninawaomba Watanzania watenganishe ni Chama Cha Mapinduzi, Serikali ya CCM, wabunge wa CCM na viongozi ndani ya chama na ndani ya Serikali. Chama Cha Mapinduzi na Serikali wasivichanganye na watendaji na viongozi, kwani chama ni cha wana-CCM na chama kama chama hakiwezi kuiba, serikali kama serikali haiwezi kuiba wanaoweza kuiba ni watendaji au viongozi waliopewa dhamana ya kuwatumikia Watanzania ndani ya Serikali au ndani ya chama, anaeleza.
Anasema inapofikia wakati kwamba kuna wenzao wasio wazalendo na wala hawaipendi nchi bali maslahi yao, wanaibia wananchi. Ninawasihi sana Watanzania wajue kwamba ni watu na si Serikali. Na katika hali kama hiyo ni lazima sisi wabunge wa CCM, na ni jukumu letu kumsaidia Rais kuisafisha Serikali yake na chama chake kwa sababu Serikali ni ya CCM, anasema.
Dhamira hiyo ya wabunge ilijionyesha wazi katika semina ya wabunge iliyokuwa ifanyike Jumapili Februari 3, 2008 ambayo ilikuwa ijadili miswada ya umeme na mafuta. Katika semina hiyo, wabunge waligoma kumsikiliza Waziri wa Nishati na Madini, Nazir Karamagi, wakitaka kwanza Ripoti ya Bunge juu ya Mkataba wa Richmond pamoja na Ripoti ya Mikataba ya Madini viwasilishwe bungeni kabla ya kusikiliza chochote kutoka katika Wizara hiyo.
Aliyeanzisha hoja hiyo alikuwa Mbunge wa Vunjo, Aloyce Kimaro (CCM) ambaye alimtaka mwenyekiti wa semina hiyo kuahirisha hadi hapo Bunge litakapokuwa limejadili Ripoti ya Richmond.
Katika hoja zake, Kimaro alisema Wizara ya Nishati na Madini imepoteza sifa ya kuzungumza na wabunge. Tubadilike wabunge, si kila Serikali ikileta muswada tuukubali, tunaweza kuukataa na ndivyo tutakavyofanya sasa, alisema Kimaro. Baadaye alipofuatwa na Rai kumtaka afafanue kauli yake kwamba Wizara ya Nishati na Madini imepoteza sifa ya kuzungumza na wabunge, Kimaro alisema mwenye masikio amesikia.
Niliposema Wizara imepoteza sifa za kuzungumza na wabunge nilikuwa na maana pana. Bila shaka mwenye masikio amesikia. Na si lazima tufafanue kila kitu. Lakini nadhani bila shaka Waziri (Karamagi) alipata ujumbe wetu. Nina imani kwamba ametuelewa na yeye kama mtu mzima, bila shaka atachukua hatua haraka. Na hatua zenyewe ni kuachia ngazi, alisema.
Alipofuatwa Karamagi kuhusiana na hoja hiyo, aliiambia Rai kwamba alikuwa na shughuli nyingi nzito labda afuatwe baadaye. Hata hivyo, habari kutoka kwa watu walio karibu naye, zinaeleza kuwa Karamagi hana tatizo na kuachia ngazi, tatizo lake ni kuhusishwa na jambo la Richmond ambalo yeye amelikuta.
Karamagi yeye katika maongezi yake anasema hana tatizo na kuachia ngazi. Na hasa baada ya kauli ya Rais kwamba mawaziri na wabunge wenye biashara wachague moja. Karamagi hawezi kuchagua kuendelea na uwaziri na kuachia biashara zake, kilisema chanzo chetu cha habari kilicho karibu na Karamagi.
Bungeni kuna fukuto la aina yake kutoka kwa wabunge wa CCM. Tangu kuvunjika semina ya Jumapili, wabunge wanakaa katika vikundi wakijadili hatua za kuchukua bungeni wakati Ripoti za Richmond, ya Uchunguzi wa ubadhirifu kwenye Akaunti ya Malipo ya Madeni ya Nje (EPA) katika Benki Kuu (BoT) na ile ya Kamati ya Madini ya Rais zitakapowasilishwa. Ripoti kuhusu BoT na Richmond zipo tayari, wakati ile ya Kamati ya Madini bado wahusika wanaifanyia kazi.
Ukiachia wabunge wachache ambao walikuwa tayari kutajwa majina yao, wengi ambao hawakuwa tayari kutajwa majina yao wanaeleza kwamba kwa muda mrefu Serikali imekuwa ikiwalazimisha kuyabariki mambo ambayo wakati mwingine ni kinyume na dhamira yao.
Wabunge kadhaa wameiambia Rai kwamba kuna uwezekano wa ripoti mbili zitakapowasilishwa bungeni kuandika historia mpya ya nchi yetu katika Bunge na kusema watakaoanzisha jambo hilo ambalo hawakuwa tayari kulitaja, watakuwa wabunge wa CCM.
Mbunge mmoja akizungumzia yaliyotokea Jumapili, alisema wabunge wa CCM wamegundua kwamba utaratibu wa kuiunga mkono Serikali kwa kila inachokipeleka bungeni, umewafanya wapoteze imani kwa wananchi kiasi kwamba upinzani umekuwa ukiandaa watu wa kuchukua nafasi zao katika majimbo.
Wakati sisi tukiendelea na mambo haya, tumegundua kwamba wapinzani wanaandaa watu na wanatumia mambo haya haya ya Richmond, Buzwagi, Songas na IPTL. Na wananchi wameanza kuwaamini kwa sababu sisi mara zote bungeni tunaonekana kuunga mkono mambo haya ambayo yana utata, alisema mbunge mmoja mzoefu kutoka Mkoa wa Iringa, ambaye hata hivyo hakuwa tayari kutajwa jina lake gazetini .
Waziri mmoja wa Serikali ambaye naye hakuwa tayari kutajwa jina lake, alisema mambo yanayotokea ni kwamba watu ndani ya CCM wanatafutana wenyewe kwa wenyewe.
Leo hii tunamzungumzia na kumtupia lawama Karamagi katika suala ambalo wakati akiteuliwa kwenda Wizara ya Nishati tulimwona kama mwarobaini. Lakini leo hii tumemgeuka. Nasema hata akiondoka leo hii akaachia ngazi, tatizo lenyewe litaendelea kututafuna. Wasiwasi wangu ni kwamba wapo watu ambao malengo yao ya sasa ni tofauti na yale tuliyokuwa tukiyaeleza wakati wa kampeni. Ni jukumu la Rais Kikwete kuwabaini watu hawa na kuwaondoa. Asipofanya hivyo, atajikuta ana wabunge wachache katika kipindi kijacho na itamuwia vigumu kutenda kazi zake, alisema waziri huyo.
Kwa upande wake, Anne Kilango alisema kama kuna watu ndani ya Serikali wamehusika katika ripoti hizo za Richomond na Benki Kuu (BoT), wabunge watajua jinsi ya kufanya na wananchi wataridhika. Wabunge hawana nia ya kumuonea mtu ila tunataka kuona kama kuna watu wamehusika kuchafua jina la Serikali ya CCM au Serikali ya Kikwete tutawaweka sawa,alisema na kuongeza:
Niliwahi kuhojiwa na gazeti hili na ninakumbuka nilionyesha mlengo wangu, tena kwa hisia kwamba ninahisi umasikini walio nao Watanzania unatokana na rasilimali za nchi kuibiwa na baadhi ya viongozi wasio na uzalendo. Mpaka hapa utagundua zile hisia zangu ni za ukweli, kwamba haiwezekani nchi hii iwe na rasilimali kiasi cha kutisha na kisha iendelee kuwa na umasikini mkubwa kiasi hiki. Huo ulikuwa ni utafiti wangu ambao haukuwa rasmi.
Kilango alisema nia ya wabunge wengi walipokataa kujadili miswada hiyo miwili ilikuwa kutaka kupata majibu ambayo yatasaidia kuboresha miswada hiyo na ndiyo maana wameona haitakuwa busara kwao kuupeleka muswada huo wakati hawajui ni kitu gani kipo ndani ya Richmond na kwamba huenda kuna maswali mengi kuhusu TANESCO ambayo wabunge wamekuwa wakijiuliza ambayo majibu yanaweza kuwa kwenye ripoti ya Richmond.
Sipendi kusikia watu wakisema Serikali ya CCM ni chafu, lakini kuna watendaji ambao ni wachafu wanaoifanya Serikali iitwe chafu. Tuna uwezo wa kuwaondoa, rais ana uwezo wa kuwaondoa na sisi wabunge tuna uwezo wa kuwaondoa ili Serikali iendelee kuaminiwa na wananchi, alisema Kilango.
Akizungumzia uamuzi wa kuwandoa haraka wahusika wanaoendelea kuchafua Serikali na CCM, Kilango alisema kwamba si vyema kuwaondoa bila kufanya uchunguzi wa kina. Binafsi hata katika tuhuma za BoT anaamini wazi kwamba aliyekuwa Gavana, Dk. Daud Ballali hayupo peke yake.
Mimi mwenyewe binafsi siwezi kuamini kwamba Ballali yupo peke yake, kwani hawezi yeye kama Ballali akaiba zile fedha peke yake. Ni lazima kuna watu wengine alioshirikiana nao kuiba, hawezi kujiandikia barua mwenyewe akachukua fedha mwenyewe! No! Lazima kuna wadogo na wakubwa alioshirikiana nao.
Na ndiyo maana tunataka pia kuiona ripoti ya BoT ili kujua walioshirikiana na Ballali ni nani, basi tuwaeleze jamani kaeni pembeni msichafue hii Serikali ya CCM. Vile vile hata kwenye issue (suala) ya Richmond tunasubiri kupewa ripoti na tuisome kwa kina ili kujua nani alihusika katika lipi na ndiyo tujenge hoja ya yeye kuondoka, si hivi hivi, inakuwa si vizuri, anasema Kilango.
Wasiwasi wa wabunge hao, unatokana na msimamo wa watu wengi waliopo nje ya Bunge na wengine wakiwa ni watu mashuhuri waliowahi kushika nyadhifa za juu serikalini.
Mmoja kati ya watu hao ni Jaji Joseph Warioba aliyesema hivi karibuni kwamba Bunge la Tanzania limepoteza demokrasia yake ya kweli kwa sababu wabunge wa chama tawala, ambao ni wengi bungeni, wanalazimika kutimiza matakwa na maslahi ya chama chao badala ya kuangalia mambo kwa misingi yake.
Jaji Warioba aliyasema hayo katika mahojiano maalumu na Rai miezi miwili iliyopita na akapendekeza kwamba, ili kuliokoa Bunge, umefika wakati wa kupunguza nguvu ya Serikali bungeni kwa kuwaondolea mawaziri hadhi ya kuwa wabunge.
Alisema njia pekee ya kufikia suluhisho hilo , ni kufanya mabadiliko ya katiba yatayomtaka rais kufanya uteuzi wa mawaziri nje ya wabunge, au mbunge akiteuliwa na rais kuwa waziri, alazimike kujiuzulu ubunge wake.
"Idadi ya mawaziri ni kubwa. Kuna mawaziri nadhani zaidi ya 30 na naibu mawaziri kiasi kama hicho. Yaani ukichukua Serikali mle kwenye Bunge ni zaidi ya watu 60 wanaitwa wabunge lakini ni mawaziri au naibu mawaziri. Na kwa kuwa wapo katika executive na power wanayo, interest yao ni kubwa sana, kwa hiyo unaweza kufika mahali ukakuta jinsi Serikali ilivyoamua mambo yake, ndivyo Bunge litakavyoyapitisha. Ndiyo maana nasema itafika wakati Serikali itasimamia Bunge badala ya Bunge kusimamia Serikali.
"Nimesema na ninarudia, tutenganishe Serikali na Bunge. Ukirudi kule nyuma tulipokuwa wakati wa chama kimoja, utaona wabunge, yaani back benchers, walivyokuwa wakizungumza. Kuna tofauti na sasa. Wakati ule Bunge kweli lingeweza kuisimamia Serikali kwa sababu walikuwa hawafungwi na chochote. Kulikuwa na more democracy (demokrasia zaidi) kwenye Bunge wakati wa chama kimoja kuliko sasa.
"Kwa sababu tulikuwa na chama kimoja, hawa back benchers walikuwa wakiisukuma kweli kweli Serikali. Sasa hivi nguvu ya wabunge wa kawaida imepungua kwa sababu nguvu ya Serikali imekuwa kubwa zaidi Wabunge wabaki ni wabunge, Serikai iwe pembeni inatekeleza mambo yake. Mawaziri watakuwa wanaitwa kwenye Bunge kueleza jambo wakiitwa, lakini wasiwe wabunge na wala wasikae bungeni," alishauri.
Jaji Warioba, alisema kwa sasa, nguvu ya Waziri Mkuu bungeni ni kubwa sana . "Na zipo sababu zake. Kwanza, yeye ni kiongozi anayetoka chama tawala na wengi wa wabunge wanatoka katika chama kinachotawala. Kwa hiyo si tu kwamba anatumia rungu la kuwa mbunge, lakini pia anatumia rungu la Chama. Kwa hiyo analazimika kusimamia kile kinachoitwa whip system, kwamba kama suala limeletwa na Serikali hii, na hii ni Serikali ya CCM na wewe ni mbunge wa CCM, ni lazima uunge mkono lile jambo," anaeleza.[FONT=Arial, Helvetica, sans-serif]© Habari Corporation Ltd
[/FONT]