Elections 2010 CCM kufuatilia wanaojipigia kampeni za urais

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,314
33,108
Chama cha Mapinduzi Zanzibar (CCM) kimeanza kuwafuatilia kwa karibu wanachama wanaojipigia kampeni za Urais wa Zanzibar kabla ya muda na wakithibitika kitawafutia uteuzi.
Hatua hiyo imetangazwa na Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Saleh Ramadhan Ferouz alipokuwa akizungumza na Nipashe mjini hapa.
Alisema CCM haijalala na kinawafuatilia kwa karibu wenye tabia hiyo kuhakikisha maadili ya chama hicho yanalindwa.
Ferouz alisema wanachama wa CCM wanaruhusiwa kutangaza nia ya kuwania Urais lakini sio kufanya kampeni kabla ya wakati au kuwachafua wanachama wengine.
“Wale tutakaobaini walianza kampeni kabla ya muda tutawafutia uteuzi kwa vile maadili ya chama ndivyo yanavyotuongoza,” alionya Naibu Katibu Mkuu.
Alisema fomu za Urais wa Zanzibar zitaanza kutolewa Juni 21, ambapo wiki ijayo Kamati Maalum ya Halmashauri Kuu ya CCM itakutana kujadili watu watakaojitokeza kuwania nafasi hiyo.
Alisema awali utoaji fomu za kuwania Urais ulikuwa uanze Julai, lakini wamelazimika kubadilisha ratiba na kutoa fursa hiyo mapema zaidi kutokana na unyeti wa suala hilo.
Ferouz alisema kwamba mchakato huo umelazimika kuanza mapema zaidi ili kuhakikisha CCM inapata mgombea mwenye sifa na anayeheshimu maadili ya uongozi.
Tangu Rais Karume atangaze nia yake ya kutogombea tena nafasi ya Urais wa Zanzibar, viongozi na makada wa CCM wamekuwa wakiendesha kampeni kubwa za sirisiri kutaka kurithi nafasi hiyo.
Kampeni za Urais wa Zanzibar katika uchaguzi wa mwezi Oktoba zimekuwa ngumu na kuonyesha sura tofauti baada ya baadhi ya wagombea kuamua kuleta waganga wa kienyeji kutoka Nigeria na baadhi ya mikoa ya Tanzania Bara.
Hadi sasa ni mwana CCM mmoja tu, Balozi Ali Karume ambaye ameshatangaza hadharani azma yake ya kuwania nafasi ya Urais wa Zanzibar, ambapo vigogo wengine wamekuwa wakiahidi kujitangaza wakati utakapofika.
Hata hivyo, miongoni mwa watu wanaotajwa, Waziri Kiongozi Mstaafu, Dk. Mohammed Gharib Bilal amechukua nafasi kubwa ya mjadala ambapo wengi wanasema huenda akawa chaguo la CCM Zanzibar.
Dk. Bilal aliongoza katika kura za maoni za Kamati Maalum Zanzibar mwaka 2000.
Mwaka 2005 alionyesha ushindani kwa Rais Karume, akiwa amemaliza kipindi kimoja tu cha uongozi, ambapo baadaye aliombwa na wazee wa chama aondoe jina lake na amwachie mwenzake.
Hata hivyo, suala la mgombea wa Urais CCM Zanzibar linaonekana kuwapasua vichwa viongozi wa chama hicho, ambapo baadhi ya wanaotajwa kutaka kuwania nafasi hiyo wameanza kulegeza misimamo iwapo atajitokeza Makamu wa Rais Dk. Ali Mohammed Shein kutaka nafasi hiyo.
Tayari baadhi ya wazee kutoka Zanzibar wameombwa kwenda kumuomba kujitokeza kuwania Urais Zanzibar, kwa nia ya kupunguza siasa za makundi, lakini pia kudhorotesha ngome ya upinzani kisiwani Pemba.
Iwapo Dk. Shein atawania nafasi hiyo na wananchi Zanzibar kuamua kuwa na serikali ya mseto, Rais na Makamu wa Rais watatoka kisiwani Pemba.



CHANZO: NIPASHE JUMAPILI
 
Back
Top Bottom