Elections 2010 CCM Kuchafua Uchaguzi Z'bar: Mkakati Wa Kupunguza Majimbo Ya Uchaguzi Pemba Waja.

Junius

JF-Expert Member
Mar 11, 2009
3,181
139
Na Salim Said Salim
KIFUPI cha marefu, mkato wa maneno na kurahisisha magumu yawe mepesi, nasema Zanzibar hakuna uchaguzi bali "uchafuzi."
Inazoeleka kuwa kupiga kura si haki kwa raia, bali zawadi inayotolewa na Tume ya Uchaguzi (ZEC) kwa wale inaoona wanafaa kutunukiwa.
Mamia ya watu waliozaliwa kisiwani Pemba, baadhi yao wakiwa hawajawahi kuvuka bahari kufika Unguja wamenyimwa haki hii na wanalalamika wamedhulumiwa.
Wananchi hao wanaodai haki ya kikatiba, sasa wanaitwa wachochezi lakini wale waliojenga mtandao kuwanyima haki hiyo, ndio huitwa kuwa wanapenda amani na utulivu.
Zipo habari kuwa kama ilivyotokea katika uchaguzi mwingine uliopita, idadi ya majimbo kisiwani Pemba, ngome isiyotetereka ya Chama cha Wananchi (CUF) itapunguzwa zaidi na kwamba huu mkakati wa kuandikisha watu wachache ni hatua moja ya kufikia huko.
Nia ya watawala ni kutaka ionekane kuwa kisiwani Pemba hakuna wapiga kura wa kutosha majimbo 21 ya uchaguzi yaliopo sasa.
Kisingizio cha kukatalia watu kuandikishwa kupiga kura ni kwamba hawana kitambulisho cha Mzanzibari mkaazi. Juhudi zao za kupata kitambulisho hiki kinachodhihirika kuwa kinatolewa kwa ubaguzi na kwa watu maalum, zimegonga ukuta.
Masheha, wengi wao wakiwa wastaafu wa Jeshi, Polisi, Usalama wa Taifa, Uhamiaji na vikosi vya ulinzi vya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), wanadai hawawajuwi.
Hawa katika uchaguzi wa huko nyuma, walikuwa wanakataa hata watoto na jirani zao, wakiwemo wale wanaofanana nao kwa sura na tabia na kutofautiana tu kwa mtazamo wa kisiasa.
Uongozi wa Zanzibar ambayo imejijengea sifa ya kufanya mambo ya ajabu yasiyotendeka kwingineko duniani, hata Tanzania Bara, hautaki kutambua kuwa cheti cha kuzaliwa ni uthibitisho wa uraia na kupiga kura ni haki ya raia.
Lakini inasemekana adha ya kuandikishwa haiwapati wale wenye kadi za Chama cha Mapinduzi (CCM) maana chao ni chama "nambari wani" na ndio uthibitisho wa Mzanzibari!
Utadhani ni kichekesho, lakini ni cha hatari.
Niliwahi kueleza kwamba binaadamu ana kiwango cha kuvumilia kile anachokiona ni uonevu na unyanyasaji. Watu wa Pemba wamekuwa wakilalamika kubaguliwa, kunyanyaswa na kutotendewa haki.
Baadhi ya wanazungumzia kutaka kuruhusiwa kujitenga kisheria kwa kuwa wanaamini hawatakiwi na Serikali ya Jamhuri ya Muungano baada ya kwishathibitisha msimamo huo upande wa SMZ.
Hamad Ali Mussa, aliyewahi kuwa mbunge bunge la 1995, anaongoza kundi la wazee wanaojitambulisha kuwakilisha wenzao wa Pemba, anaendelea kupigania kujitenga na anaendeleza mawasiliano na Umoja wa Mataifa kutaka wasikilizwe.
Hata kama Umoja wa Mataifa utapuuza madai yao, kama yanavyobezwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano, umoja huo wanapaswa kufahamu kuwa wanachokifanya ni sawa na kutosikia la mkuu, watakuja kuvunjika guu pale wanaodhani ni moshi tu utakaporipuka na athari zake kuenea.
Kinachoonekana Pemba sasa ni mwanzo wa mripuko unaoashiria balaa usoni. Baada ya mamia ya watu kukataliwa kuandikishwa, na wengine kudai wametishwa na kuambiwa wasionekane tena kwenye vituo vya uandikishaji, jimbo la Ole wamegoma kuandikishwa mpaka pale mamia ya wenzao waliokataliwa bila ya sababu za msingi, waandikishwe.
Upo mgogoro, iwe wa kisheria, wa kisiasa, au mizengwe. Inategemea mtu anavyoangalia suala hili. Niliwahi kushauri kama SMZ na Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) wanaona kupiga kura si haki ya kila mtu, bali ni msaada, zawadi au ihsani, ni vizuri ielezwe wazi.
Ielezwe wazi ili kama inavyosemwa kuwa CCM ina wenyewe, basi na haki ya kupiga kura ionekane na wenyewe hasa, Wapemba wakiwa si miongoni mwao.
Sielewi na sitafahamu wala sitakubali kuona mtu amezaliwa Zanzibar, anaishi Zanzibar na hajawahi kutoka nje yake, na si kichaa, ananyimwa haki ya kupiga kura katika uchaguzi wa Zanzibar.
Kama ni suala la ukaazi basi ana haki ya angalau kumchagua Rais wa Zanzibar ambaye jimbo lake la uchaguzi ni Zanzibar nzima.
Lakini lililo baya zaidi ni kudharau malalamiko yao na kuchukulia kuwa "watasema mchana na usiku watalala." Kuamua kwao kugomea uandikishaji wa kibaguzi ni ishara kuwa Wapemba hawataki kulala na hawaonyeshi dalili za hata kusinzia. Wanataka haki yao.
Yapo madai ya mamia ya wapiga kura mamluki kupelekwa Pemba kutoka Bara kwenda kujiandikisha. Sina hakika, lakini katika uchaguzi uliopita wasichana waliokuwa wamewekwa kambi katika Kiwanda cha Viatu Mtoni, waliniambia waliletwa kutoka Kawe na Bunju kwenda Zanzibar kupiga kura. Nani aliwapeleka, wanajuwa wenyewe.
CCM wamekanusha kuhusika na Chama cha Wananchi (CUF) wanasema hawana ubavu huo na zaidi kwa vile wanajuwa hawana shida ya wapiga kura Zanzibar.
Serikali nayo inasema haikuhusika. Labda wasichana hao walipelekwa na mashetani. Mamluki kama hao wamepenyezwa sana kwenye uchaguzi Zanzibar. Ni uthibitisho wa mwenye haki kunyimwa na asiyenayo kupewa.
Ndipo nikasema Zanzibar hakuna uchaguzi bali uchafuzi. Wala si ajabu mtindo wa kuingiza mamluki katika uchaguzi ukaendelea 2010 kama ilivyozoeleka mtu mmoja kupiga kura hata mara sita na asiwepo aliyeshitakiwa. Hadi sasa hakuna kesi mahakamani ingawa Tume ilithibitisha zaidi ya watu 6,000 walijiandikisha zaidi ya mara moja.
Viongozi wa SMZ inaoenakana hawajajifunza chochote kuhusu yaliyokwishatokea Zanzibar kabla, wakati na baada ya uchaguzi. Wamesahau kamwe mauaji ya 26-27 Januari 2001.
Kawaida yule asiyekuwa tayari kujifunza na yanayotokea nchini kwake, atafunzwa na ulimwengu na mafunzo yenyewe huwa ni machungu. Wiki iliyopita, Mjerumani aliyekuwa mwanajeshi wakati wa vita vya pili vilivyokoma mwaka 1945, alitiwa hatiani kwa kushiriki mauaji ya vijana nchini Italia.
Dawa na matatizo ya Zanzibar ni utawala chini ya CCM, kukubali kuwa chenye mwanzo kina mwisho. Na mtu anapolazimisha ngumi yake ivunje ukuta, ataumia mwenyewe.

SOURCE: MWANAHALISI.
 
mashaka makubwa haya. lakini pamoja na yooooote hayo wanafunga bao la kuotea
 
Kama kuna majimbo mengi yasio na ufanisi, ni bora yakaunganishwa... Ni wazi zuri na sio la kulibeza
 
Kama kuna majimbo mengi yasio na ufanisi, ni bora yakaunganishwa... Ni wazi zuri na sio la kulibeza
Basi yaunganishwe majimbo ya Makunduchi, Muyuni, Chwaka liwe moja na Kaskazini Nungwi na Mkwajuni na Tumbatu liwe moja. Bado sijaona umuhimu wa kuwa na jimbo la Kikwajuni hapo hapo pana jimbo la Miembeni na hilo hilo limelaliana na Rahaleo. Kwanini Pemba tu?
Walipoona jimbo la Mlandege lina wafuasi wengi wa CUF wameliunganisha na Gulioni na Makadara ambayo yalikuwa jimbo moja, walipoona na Gulioni hakuna CCM hata mmoja(kabaki Mshenga tu peke yake) wakaliunganisha na Rahaleo ambako kuna CCM kiduchu tu sasa, sijuwi wataunganisha wapi tena maana kulikobaki ni Mwembetanga ambako weshakusogeza Rahaleo na hapo watu wote CUF. Nshaona wakizidiwa wataifanya Zanzibar yote jimbo moja,wawape maadui zetu faida.
 
Back
Top Bottom