Candid Scope
JF-Expert Member
- Nov 8, 2010
- 11,883
- 6,884
- Kada wa CCM ajeruhiwa kwa panga, bintiye abakwa
KADA wa CCM, Francisco Msalika amejeruhiwa kwa panga kichwani na binti yake kubakwa baada ya kuvamiwa nyumbani kwake Mtaa wa Benki ya zamani mjini Igunga na watu ambao walimtaka atoe pesa za kampeni. Akizungumza akiwa kitandani katika wodi ya majeruhi katika hospitali hiyo, kada huyo alisema tukio hilo lilitokea juzi kuamkia jana majira ya saa nane za usiku. Alisema alisikia kishindo ambacho kiliuvunja mlango wake wa chumbani na kisha watu hao kummulika kwa tochi kali usoni.
Alisema wakati akijaribu kuchukua panga lake ambalo alilihifadhi chini ya kitanda ili akabiliane na mhalifu huyo, alikatwa panga la kichwa ambalo lilimfanya aanguke chini na kishindo hicho kilimwamsha mkewe na mwanaye wa kike ambao nao walijikuta wakikabiliana na mvamizi huyo.
"Alininyang'anya panga nililokuwa nataka kuchukua na kusisitiza kuwa anataka simu na pesa nilizopewa za kampeni," alisema na kuongeza kuwa alimruhusu achukue suruali ambayo alikuwa ameining'iniza katika msumari ukutani ambayo ndiyo iliyokuwa na fedha.Msalika alisema mhalifu huyo alimtwanga panga jingine kichwani ambalo lilimfanya apoteze fahamu kwa muda na kisha kumshika mkono mtoto wake wa kike na kuondoka naye.
"Nilizinduka na kujikokota nikisaidiwa na mke wangu hadi kwa jirani zetu ambao wana pikipiki ili waniwahishe polisi na baadaye hospitali, lakini kabla hatujaondoka binti yangu akarudi," alisema Msalika. Alisema kuwa walimwuliza alipokuwa amemuachia akajibu kuwa ni jirani na mtoni. Msalika alisema kwa kuwa binti huyo hakuwa katika hali nzuri, hakuendelea kumhoji zaidi na badala yake alipelekwa polisi na kupewa PF 3 na kisha kupelekwa hospitali ya wilaya.
Msalika alisema kesho yake asubuhi alikuja mkewe na makada wengine wa chama hicho akiwamo mwanamke aliyemtaja kwa jina moja la mama Kashi walikuja kumletea chai ndipo mama wa mtoto alipomueleza kuwa binti yao katika kadhia ile alibakwa. "Mimi nashangaa huyo mtu kuja kutaka pesa kutoka kwangu wakati kampeni za safari hii sikushiriki kabisa tofauti na inavyokuwa miaka ya nyuma," alisema na kuongeza kuwa CCM huwa wanamtumia kutumbuiza kwa kwaya katika hafla tofauti.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tabora, Anthony Ruta alithibitisha kutokea kwa tukio hilo: "Ni kweli tukio hilo lipo na mtoto amethibitika hospitalini kuwa alibakwa na hali yake inaendelea vizuri na jeshi la polisi limefungua faili kuhusiana na tukio hilo la ubakaji na hakuna mtu ambaye ameshatiwa mbaroni kuhusiana na tukio hilo."
Hilo litakuwa ni tukio la pili ambalo linahusiana na masuala ya kampeni za kisiasa zinazoendelea mjini Igunga za kuwania kiti cha ubunge katika uchaguzi mdogo unaotarajiwa kufanyika Oktoba 2, mwaka huu. Katika tukio la kwanza, mtu mmoja, Mussa Tesha alimwagiwa tindikali na jeshi la polisi linamshikilia mtu mmoja kuhusiana na tukio hilo.
Mwananchi