nngu007
JF-Expert Member
- Aug 2, 2010
- 15,862
- 5,797
Sunday, 04 September 2011 21:49 |
0digg Boniface Meena na Joseph Zablon, Igunga VYAMA vya CCM na Chadema vimeingia katika msuguano mkali siku chache kabla ya kampeni za uchaguzi mdogo wa ubunge katika Jimbo la Igunga, Tabora kuanza baada Katibu wa Halmashauri Kuu, Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye kuvamiwa na baunsa mmoja maarufu wa chama hicho pinzani kutoka Dar es Salaam ambaye anatajwa kutumwa kufuatilia nyendo za katibu huyo jimboni hapa. Taarifa zilizopatikana mjini hapa jana zilisema kuwa Nape alivamiwa baada ya kutoka kutoa pole kwa familia ya mtoto Peter Ezekiel ambaye alifariki dunia papo hapo baada ya kugongwa na lori Ijumaa iliyopita alipokatiza barabara akitokea katika umati wa watu waliokuwa wakisubiri msafara wa mgombea wa CCM, Dk Peter Kafumu, alipokuwa akienda kuchukua fomu. Kutokana na msiba huo, CCM kilisimamia taratibu zote za mazishi yaliyofanyika juzi nje kidogo ya mji wa Igunga na kilitoa rambirambi ya Sh milioni moja, huku Chadema ambacho nacho kina mgombea jimboni hapa kikitoa Sh120,000. Nape msibani Nape aliwasili hapa jana saa 6:00 mchana na kwenda moja kwa moja nyumbani kwa wazazi wa marehemu Ezekiel... "Nisingependa kusema mengi hapa, lakini naomba niwaombe kuwa watulivu wakati huu mgumu kwa msiba wa mtoto wetu mpendwa. Hii ni mipango ya Mungu, nimeona nipite hapa kuwapa pole kwa kuwa nilipata habari za msiba huu," alisema Nape. Baba mkubwa wa mtoto huyo aliyefariki katika ajali hiyo, Joseph Mlewa alisema: "Wametufariji sana na ninaweza kusema kuwa ni vyama vyote viwili vya CCM na Chadema kwani ahadi zao zote ambazo waliahidi baada ya kifo cha mtoto wao wamezitimiza jambo ambalo linaonyesha ni jinsi gani siasa inaweza kuwekwa pembeni wakati wa matatizo ya kijamii kama hilo la msiba. Kwa upande wake, Dk Kafumu alisema ameguswa na kifo cha mtoto huyo: "Nashangaa watu kuhusisha kifo hiki na harakati zangu za uchaguzi kwani tukio hilo ni la kawaida kama mengine. Kilichotokea baa Wakati Nape akitoa pole Mratibu wa kampeni za Chadema, Mwita Waitara alionekana akirandaranda jirani na nyumba ya familia hiyo iliyopo mita 500 kutoka Barabara Kuu ya Singida-Igunga. Baada ya Nape kutoka kutoa pole alikwenda kwenye Baa ya Silver 'C' iliyopo jirani na nyumba ya familia hiyo ambako aliwakuta vijana kadhaa waliokuwa wakitaka kufanya naye mazungumzo. Katika eneo hilo, alikuwapo baunsa huyo wa Chadema ambaye inadaiwa alitumwa kumfuatilia katibu huyo tangu alivyotoka Dar es Salaam. Nape akiwa katika baa hiyo na wanachama hao waliodaiwa kuwa wa CUF na CCM, walimwomba baunsa huyo awapishe kwa kuwa hakuwa akihusika na mazungumzo yaliyokuwa yakifanyika lakini alikaidi na kuzusha tafrani na kufanya kikao kuvunjika. Baada ta mvutano huo, Nape aliamua kuelekea katika gari lake na hata alipofuatwa na kuulizwa kulikoni? Alijibu Napita njia tu, kisha kupandisha kioo cha gari lake na kuondoka. Katibu wa CUF Wilaya ya Igunga, Michael Maganga alipoulizwa kuhusu kilichotokea hakutaka kuzungumza muda mfupi baadaye aliondoka na vijana wake. Akizungumzia mvutano huo akiwa nje ya baa hiyo muda mfupi baada ya tukio, mlinzi huyo alisema alipata habari za Nape kufika na ndipo alipoamua kuungana na wanaCCM na CUF waliokuwa wakimsubiri katika baa hiyo tangu mapema asubuhi. Alisema akiwa kaunta ya baa hiyo akitaka huduma, alifuatwa na kijana mmoja ambaye alitoka katika mkusanyiko wao na kumtaka atoke kwani walikuwa na kikao jambo ambalo alikaidi akisema alikuwa amefika hapo kupata huduma kama wateja wengine. Chadema yairushia CUF kombora Muda mfupi baadaye, Katibu wa Sera na Utafiti wa Chadema, Mwikabe Waitara alifika hapo na kusema hashangazwi na kinachotokea kwani ndoa ya CCM na CUF bado ipo na ndiyo maana wana agenda moja Igunga. Waitara alisema watu hao wanazungumza lugha moja dhidi ya Chadema hali ambayo inaonyesha wazi kuwa wana mkakati wa pamoja na alisema ujio wa Nape ambao ulifuatiwa na gari la polisi la kumwaga maji ya kuwasha ambalo lilikuwa linazunguka mitaani likipiga ving'ora ni njia ya wa kuwatisha wananchi wasije katika mikutano ya chama chao. CUF waipuuza Chadema Akizungumzia tuhuma hizo, Naibu Katibu Mkuu wa CUF (Bara), Julius Mtatiro alipuuza madai hayo akisema ni propaganda za Chadema kupandikiza fitina za kisiasa; " Chadema tumewazidi karata sana hapa mjini jambo ambalo linawalazimu kutumia janja ya nyani ambazo hazitawasaidia." Mtatiro ambaye amepiga kambi jimboni hapa alisema kwa kipindi chote cha jana, timu nne za chama chao zilikuwa zimejikita katika Vijiji vya Nsimbo, Manonga, Igurubi na Mjini Igunga na kote huko walikuwa katika mikutano ya ndani na mkutano mmojawapo alikuwa akiusimamia mwenyewe. "Hivi sasa unaponipigia simu hii nimemaliza kikao dakika 15 zilizopita (saa 12 jioni) na huku tulikuwa tunapanga mikakati ya ushindi," alisema Mtatiro. Alisema haiwezekani wanachama wa CUF wakakutana na kiongozi wa CCM wakati kila mmoja anatafuta ushindi kivyake na kwamba hakuna mantiki kwa tuhuma zinazotolewa dhidi ya chama chao. "Safari hii chama chetu kimejipanga kwelikweli na hakuna mtu au chama chochote kitakachotuchezea na tulimaanisha tulipojitosa kwenye kinyang'anyiro, hao wanaotoa tuhuma ni lazima wathibitishe hayo wanayoyasema," alisema. Alisema katika kuongeza nguvu za mashambulizi, Katibu Mkuu wa chama chao, Maalim Seif Sharif Hamad atafika mjini Igunga kwa ajili ya shughuli za kuimarisha chama hicho baada ya kutoka Urambo ambako alikuwapo jana katika ziara za kuimarisha chama hicho. Gari la Maji ya kuwasha Gari la polisi linalotumika kurusha maji ya kuwasha jana lilionekana likizunguka katika viunga vya Mji wa Igunga huku likipiga vingora. Gari hilo lilikuwa likifanya mzunguko huo majira ya saa 8:00 mchana kitendo ambacho wananchi walioshuhudia walikitafsiri kuwa ni vitisho. Mmoja wa wakazi wa Igunga ambaye hakutaka jina lake litajwe gazetini, alisema hivyo ni vitisho kwa wananchi hasa ukizingatia kampeni zinatarajia kuanza hivi karibuni. Akizungumzia kuzunguka kwa gari hilo huku likipiga kingora, Kamanda wa Polisi wa Wilaya ya Igunga (OCD), Issa Muguha alisema lilikuwa likijaribiwa kwa kuwa lilikuwa halina mafuta na kuongeza kwamba majaribio hayo ni maandalizi ya uchaguzi unaotarajiwa kufanyika Oktoba 2. Hakuna tatizo mbona hayo mengine yakipita hamuulizi. Tunalifanyia majaribio kwa kuwa lilikuwa halina mafuta hivyo tunayaangalia magari yetu, alisema. Achukua fomu za ubunge kwa baiskeli Mgombea ubunge kwa tiketi ya UMD, Ndegeye Ernest jana alichukua fomu kuwania ubunge wa Igunga kwa kutumia baiskeli. Hakuwa na maandamano wala mbwembwe kama ilivyofanywa na vyama vingine kama CCM, CUF na Chadema. Akizungumzia hatua yake hiyo Ernest alisema chama chake ni cha wanyonge na hakina kitu ndiyo maana hana shamrashamra zozote na yeye anatumia aina hiyo ya usafiri hivyo ni wajibu wa wakazi wa Igunga kupima uzalendo wa waombaji wa nafasi hiyo. Alisema atakachofanya ni kuwaeleza ukweli wananchi na kuwataka watumie nafasi walizonazo kujiletea maendeleo na siyo kuitegemea Serikali kuu ambayo ila siku inalalamika kuwa haina fedha. Mgombea huyo alisema uzinduzi rasmi wa kampeni zake atautangaza hivi karibuni. Chama chake kinakuwa cha sita kusimamisha mgombea jimboni humo vingine vikiwa ni CCM, Chadema, CUF, Sau na DP. |