Cameroon yaipigia kambi Stars Kenya

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,792
287,994
Cameroon yaipigia kambi Stars Kenya

na Makuburi Ally
Tanzania Daima~Sauti ya Watu

TIMU ya taifa ya Cameroon, ambayo awali ilikuwa ipige kambi ya muda nchini kujiandaa kwa mechi ya marudiano ya Jumamosi dhidi ya Tanzania, Taifa Stars, muda mfupi kabla ya mechi ya juzi, waliamua kwenda kupiga kambi nchini Kenya.

Hivyo, Cameroon namba moja kwa ubora wa soka Afrika, kwa sasa wako mjini Nairobi kwa kambi ya siku kadhaa kabla ya kurejea kwao kwa pambano dhidi ya Stars litakalopigwa Jumamosi wiki hii, mjini Younde.

Akithibitisha suala la Cameroon kupiga kambi nchini Kenya, Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Florian Kaijage, alisema msafara wa timu hiyo ulioondoka juzi usiku baada ya mechi, umepiga kambi nchini humo.

"Cameroon waliondoka juzi usiku ikiwa ni saa chache baada ya mechi… kwa sasa wako nchini Kenya ambako wamepiga kambi huko kwa ajili ya mechi ijayo dhidi ya Stars itakayopigwa Jumamosi," alisema Kaijage.

Alipoulizwa sababu zilizoifanya Cameroon kuamua kuondoka mara tu baada ya mechi wakati awali ilielezwa timu hiyo ingepiga kambi ya muda, Kaijage alisema hata wao TFF, walishangazwa na hilo.

"Nadhani ni mabadiliko ya kawaida, kwamba baada ya kupiga kambi hapa nchini kama walivyokuwa wamekusudia awali, wakaamua kupiga kambi Nairobi, Kenya. Ni vigumu kujua sababu.

"Kulikuwa na taarifa kuwa, wangepiga kambi ya muda nchini katika kujifua kwa mechi ya marudiano na sisi (Stars) hapo Jumamosi, lakini muda mfupi kabla ya kuanza kwa mchezo wa jana (juzi), wakasema wangeondoka baada ya mechi," alisema Kaijage.

Kuna uwezekano mkubwa kwa Stars kusafiri pamoja na Cameroon kwani Stars inaweza kuondoka kati ya Alhamisi au Ijumaaa wiki hii ikiwa ni siku mbili au moja kabla ya mechi hiyo ya marudiano.

Kuhusu Stars, Kaijage alisema kutokana na ugumu wa mechi ya Jumamosi, wachezaji walipewa mapumziko mafupi na leo wataripoti kambini kwa ajili ya maandalizi ya mechi ya Jumamosi.

"Hii ni mechi ngumu… hapa hakuna kulala, wachezaji wamepewa mapumziko mafupi tu na kesho (leo) wataripoti kambini kujiandaa na mechi ya marudiano dhidi ya Cameroon itakayofanyika Jumamosi," alisema Kaijage.

Alipoulizwa kuhusu kuondoka kwa timu, Kaijage alisema suala hilo bado linafanyiwa kazi kutokana na mazingira halisi yaliyopo, lakini suala hilo litajulikana leo.

Stars iliyo nafasi ya tatu katika kundi lake kwa pointi mbili, inalazimika kushinda mechi tatu zilizobaki ili kujiweka katika nafasi nzuri kwani tayari imetanguliwa na Cameroon na Cape Verde.

Cameroon ina pointi saba, Cape Verde imefikisha pointi sita, huku Mauritius ikiwa na pointi moja, iliyoivuna kwa Tanzania, kwani katika mechi ya juzi, ilifungwa 1-0 na Cape Verde.

Aidha, katika mechi za juzi, timu vigogo kama Misri, Angola, Ghana, Morocco na Afrika Kusini, zilipigwa mwereka katika kampeni za kusaka tiketi za kucheza Afrika Kusini na Angola.

Kama ilivyokuwa kwa Tanzania, Ivory Coast nayo juzi ilitoka sare huku Rwanda ikiifunga Morocco 3-1, Uganda iliichapa Angola 3-1, Sierra Leon ikiizima Afrika Kusini 1-0, Gabon ikiifunga Ghana na Misri ikilala kwa Malawi.
 
wallahi hiyo jumamosi hatutoki mulee...sijui labda sio cameroon niwajuao!!
 

Similar Discussions

0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom