Akiwasilisha Makadirio ya Bajeti Wizara ya Ujenzi Kambi ya Upinzani Bungeni jana jioni, Mh. Felix Mkosamali Amemlipua Waziri Mkuu Mizengo Pinda nanuukuu :
MAGARI YANAYOZIDISHA UZITO, MIZANI NA UHARIBIFU WA BARABARA
Mheshimiwa Spika, Uamuzi wa Waziri Mkuu Mizengo Pinda kuruhusu malori makubwa ya mizigo yaendelee kuzidisha uzito wa mizigo, umetajwa kuwa ni hatari na utaisababishia Serikali hasara ya mamilioni ya fedha.
Hasara hiyo inatokana na uharibifu wa barabara za lami ambao unachangiwa kwa kiasi kikubwa cha malori yanayozidisha uzito wa mizigo kinyume na kanuni 7 (3) ya Sheria ya Usalama Barabarani ya 2001.
Mheshimiwa Spika, Matakwa ya sheria Sheria Na. 30 ya 1973 na kanuni Namba 30 ya 2001 iliyotangazwa kwenye Gazeti la Serikali tangazo Namba 30 la tarehe 9 Februari , 2001 iliyoanza kutumika tarehe 24 Januari 2001 inafafanua uzito wa magari unaotakiwa. Kipengele cha saba cha sheria hiyo kinaeleza magari yote yenye uzito kuanzia tani 3.5 na kuendelea na aina ya makosa ya uzidishaji uzito, ambapo kifungu cha 2, 3 na 4 vinafafanua matumizi ya uzito uliozidi asilimia tano.
Mheshimiwa Spika, Waziri wa ujenzi Mhe. Magufuli aliwahi kunukuliwa akisema ataendelea kusimamia sheria ya barabara namba 30 ya mwaka 1973, hadi anaingia kaburini kwa kuhakikisha hakuna magari ambayo yanazidisha uzito na kuharibu barabara. Namnukuu Mh John Pombe MaghufuliNchini Ujerumani, uzito wa magari yote ni tani 40, Uingereza tani 40, Ufaransa tani 40, Urusi tani 38 lakini Tanzania tani 56, wakati mwingine tunakamata hadi tani 96, alisema,Magufuli.
Mheshimiwa Spika, Hata hivyo, ujasiri wa Dk Magufuli ulizimwa na amri ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda, aliyetengua agizo la waziri huyo na kuamua kuruhusu magari yenye uzito uliopitiliza kuendelea kuharibu barabara.
Mheshimiwa Spika, Ujenzi wa barabara unatumia gharama kubwa na hata ukarabati wake umekuwa ukitengewa mabilioni ya fedha za walipakodi kutokana na uharibifu unaofanywa. Mathalani katika bajeti yake ya 2013/14, Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi, ilitenga kiasi cha Sh bilioni 314.535 kwa ajili ya mpango wa matengenezo ya barabara kuu na
Barabara za Mikoa
Mheshimiwa Spika, Kiasi hicho cha fedha ambacho ni zaidi ya robo ya bajeti nzima ya wizara hiyo kwa mwaka, kinatosheleza kujenga barabara mpya ya lami yenye urefu wa kilometa zipatazo 315, kwa makadirio ya kilometa moja kugharimu Sh1 bilioni. Katika mwaka huu wa fedha, bajeti nzima ya Wizara ya Ujenzi ni Sh trilioni 1.226 .
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inapenda kuelewa hivi katika kuingilia tatizo hili la amri iliyotolewa na Mhe. Waziri mwenye dhamana ya barabara kulikuwa na mashauriano au ilikuwa ni wakubwa kuvuana ngua hadharani? Katika utendaji wa namna hii je watanzania watarajie tija kutoka kwa Serikali yao? Baba wa taifa aliwahi kusema serikali makini ni yenye kuwa na kauli moja na uwajibikaji wa pamoja(collective responsibility).
Mheshimiwa Spika, aidha kambi rasmi ya upinzani inamtaka waziri mkuu alithibitishie bunge kwamba yeye na marafiki zake na viongozi wa CCM wanamiliki maroli pia wana share katika makampuni mbalimbali na hivyo ndo maana imekua rahisi kwa yeye kuruhusu uzidishaji wa mizigo katika maroli na kuunga mkono uharibifu wa barabara zetu zilizojengwa kwa jasho la walalahoi ili yeye na marafiki zake wazidi kuneemeka na kukubali uhalibifu wa barabara kwa maslai yao binafsi na maroli yao