Mzee Mwanakijiji
Platinum Member
- Mar 10, 2006
- 33,476
- 39,995
Migomo na migogoro mingi ambayo tumeiona ikitokea nchini kwa miaka kadhaa sasa hivi inachochewa na naweza kusema inasababishwa na Bunge letu. Wakati watu wengi walitilia mkazo kauli ya Mbunge wa Ubungo John Mnyika kuwa tumefikishwa hapa kwa sababu ya udhaifu wa Rais Kikwete mimi binafsi naamini uzito ulitakiwa kuwa kwenye ulegelege wa Bunge. Na bila yashaka hoja inaweza kujengwa kuwa upuuzi wa CCM nao umechangia sana kufika hapa. Hilo la upuuzi nitaliachia siku nyingine.
Bunge letu ndicho chombo cha juu kabisa ambacho wananchi wa Tanzania wanacho kuweza kusimamia watawala wao. Wananchi wanapoenda kupiga kura kuchagua mbunge hawaendi kumchagua mpiga porojo wa jimbo au bishoo wa Bunge. Hawaendi kuchagua mtu ambaye ataweza kuwachachafya wengine Bungeni au atakayeenda kulumbana kwa mipasho Bungeni na wabunge wa kambi nyingine. Wanapochagua wabunge wananchi wanachagua wawakilishi wao. Dhana hii ya wawakilishi nadhani inapotea sana hasa pale watu wanapoitwa wabunge.
Mtu anapoitwa Mbunge anakuwa na hisia kuwa kazi yake kubwa ni Bungeni wakati Mwakilishi anajitambua kuwa yupo pale mjengoni kwa sababu anawakilisha watu au kundi fulani. Mbunge anayejitambua kuwa ni mwakilishi anaposimama Bungeni anasimama akijua kabisa kuwa ni maslahi ya wale waliomtuma ndio anahitaji kuyatetea. Kusimamishwa kwake na chama cha siasa hakumfanyi Mbunge huyo kujifikiria ni mwakilishi wa chama kile cha siasa. Ni mwakilishi wa jimbo la uchaguzi.
Tukielewa hili upande mmoja tunaweza kuelewa kwanini sisi wengine hatuamini kabisa mantiki ya kuwa na viti maalum au wabunge ambao wanaingia Bungeni ati kwa vile wameshinda bila kushindanishwa! Wabunge wa viti maalum hawana mtu wanayemuwakilisha ambaye hawakilishwi tyayari na mbunge wa jimbo aliyechaguliwa. Siyo wanawake, vijana, au walemavu ambao wanahitaji MBunge wa kuwawakilisha zaidi ya wale wa Bunge. Lakini cha kuudhi zaidi ni watu ambao kwa kutumia mbinu mbalimbali au udhaifu wa washindani wao waliweza kujipatia ubunge wa jimbo bila kupigiwa kura hata moja na wengine wakaenda kushika nafasi za juu za nchi (Makinda na Pinda ni mifano ya viongozi wasio halali ambao wanawakilisha majimbo ambayo hawakuchaguliwa kwa mujibu wa katiba!)
Haya yote hata hivyo yanadokeza kitu ambacho naamini tatizo kubwa zaidi ukiondoa udhaifu huo wa muundo wabunge wameshindwa kusimamia serikali, kuliongoza taifa na sasa wananchi wetu wanalipa gharama ya ulegelege wao, uzembe na kwa kwa kila kipimo kuweka mbali vyama vyao kuliko majimbo wanayowakilisha. Migogoro yote ambayo tunaiona leo hii mgomo wa madaktari, tishio la mgomo wa wafanyakazi na ule wawalimu n.k ni matokeo ya kushindwa huku kwa bunge! Siyo tatizo la Kikwete peke yake!
Kikwete ameshindwa
Kwamba Rais Kikwete ameshindwa kuonesha uongozi wa kutatua matatizo haya zaidi ya kuwa na vikao visivyoisha na matumizi ya mikwara halina shaka. Kushindwa kwake huku wengine tulishakutarajia na kwa kweli kama wengine tulivyojenga hoja kabla ya uchaguzi uliopita ni bora wananchi tukubali tu yaishe. Lakini kama yeye kashindwa ina maana lazima na wengine nao washindwe? Rais Kikwete ni wazi anasubiri matukio ilia je nyuma yake badala yay eye kuyatangulia matukio na kuonesha uongozi. Nimewahi kusema zamani kwenye maandishi yangu kuwa usipoongoza utajikuta unafuata ni wazi kuwa sasa hivi serikali yetu hasa upande wa utendaji (executive) iko inafuata. Matukio yanatokea na wao wanakuja nyuma na kuzungumza kwa jazba zote!
Bunge limeshindwa zaidi
Hata hivyo kumlaumu Kikwete kuwa kashindwa kutatua mgogoro wa madaktari na masuala mengine kwa kiasi ni kumuonea. Kikwete kama Rais wa Kikatiba anafungwa na sheria ambazo Bunge linapitisha na anaweza kufanya yale tu ambayo Katiba na sheria inamruhusu kufanya. Hawezi kufanya zaidi ya vile kwani akifanya hivyo atashtakiwa na kuondolewa madarakani na Bunge kwa mashtaka ya kibunge (impeachment). Rais wetu kama nilivyokataa aliposema ana uwezo wa kuamuru Dr. Slaa akamatwe na akakamatwa hana nguvu zozote nje ya zile ambazo Katiba na sheria zetu zinampa. Hawezi kulazimisha kuingia ndani ya nyumba ya mtu, hawezi kuamuru mtu apigwe risasi au hata kuamuru boyfriend wa binti yake akamatwe na akakamatwa! Nguvu hizo hana! Ninachosema hapa ni kuwa anaweza kufanya kile tu ambacho wabunge wanamtaka afanye na wamemtengenezea sheria kufanyia.
Zipo sheria ambazo zimeundwa zenye kusimamia sekta mbalimbali ikiwemo ile ya afya na elimu. Sheria hizi ndizo ambazo zimezaa mfumo huu wa afya ambao unatusumbua sana. Ni bunge liliopitisha sheria hizo na kutaka serikali izisimamie. Kitu kinachonishangaza mimi kama mdadisi wa masuala ya utawala na demokrasia ni kuwa ni lini Bunge litaamua kuangalia sheria zake na kuona jinsi gani zinachangia migogoro kwenye elimu na afya? NI nani mwenye akili timamu Bungeni kama wote siyo legelege ambaye anaweza kuwasema sheria hii na hii ni mbaya tuzibadilishe? Ni wazi kuwa wabunge wa aina hiyo hawapo ndani ya CCM kwani na wao ukiwasikliiza utaona wanaililia serikali ifanye jambo moja, hili na jingine.
Wabunge hasa wa CCM (hata wa upinzani wako hivyo hivyo hawachoki kusema Miye naomba serikali au utawasikia Serikali iamue kuanzia sasa au Umefika wakati kwa serikali kufanya mambo elfu moja na moja. Wanachosahau ni kuwa ni wao bunge ndio wanaweza kusababisha kitu kifanyike ambacho hakifanyiki.
Kwa mfano, kama wabunge wanataka muundo wa jeshi la polisi libadilishwe hawawezi kuitaka serikali wao kama watunga sheria wanatumia raslimali zao na kuandika muswada wa sheria wa kufanya mabadiliko wanayoyataka. Jambo baya sana katika Bunge letu ni kuwa ukiondoa michango, hoja, na hotuba mbalimbali wabunge wetu hawaleti miswada binafsi ya sheria. Kuna mifano michache sana ya baadhi ya wabunge kujaribu kuleta miswada ya sheria Bungeni. Mara nyingi wabunge hawachoki kuiomba serikali ilete mswada Bungeni kana kwamba wao kule Bungeni ni vilaza wa kutupwa.
Hii ina maana kuwa kama wabunge wanaona kuna tatizo katika sekta ya afya hususan mfumo wa utendwaji kazi wa madaktari na malipo yao basi wabunge wanaweza kuingilia kati na kuleta mswada wa mabadiliko ya sheria ili kuipa serikali nyenzo fulani ya kuweza kufanikisha hilo. Bahati mbaya sana tangu Machi hadi leo hii na kama ilivyokuwa tangu mgomo wa madaktari wa 2006 hadi leo hii wabunge wetu legelege hawajajaribu kuleta mabadiliko ya sheria ili kuongoza sekta na ajira za madaktari na badala yake wote wamekaa kama wachovu wakisubiri Rais na Ikulu iandae mikutano ya kunywa juisi ili mambo yamalizwe kiutuuzima. Safari hii madaktari wamegoma na kwa haki wanaendelea kugoma na baadhii yetu tunawaunga mkono kwani wamefunua udhaifu mkubwa wa sekta hii. Sasa wabunge wanataka kujadili hotuba ya RAis, Waziri Mkuu au hali ya mgomo! Hawataki kuitana na kuandaa mswada wa dharura wa sheria ili kuokoa sekta hii na kuokoa maisha. Watu wamebakia kuwalaumu madaktari wakati ni wabunge ambao wametunga sheria ambazo serikali imezitumia dhidi ya madaktari! Hakuna mbunge wa CCM au wa upinzani ambaye amethubutu kuja na mswada wa sheria ya Afya ili kuleta mfumo mpya.
Wabunge ndio wanagawa fedha
Sasa inashangaza sana kuwa watu wamekaa na kumuangalia Rais kuhusu ongezeko la mishahara ya madaktari na maslahi ya watumishi wengine wa afya, elimu na kada nyingine. Wabunge wamekaa na kusubiri waziri alete bajeti yake ili waichambue. Bajeti nzima imeachwa iandaliwe na watu wa serikali kiasi kwamba wabunge wao wanakuwa wachangiaji bungeni. Hii inashangaza! Wabunge ndugu zangu ndio wanaamua fedha kiasi gani ziende wapi na kwanini! Serikali inakuja na mapendekezo na maombi. Labda nilieleze vizuri zaidi.
Serikali ni mtumishi wa wananchi. Kinadharia haiwezi na haipaswi kutumia fedha yoyote ya umma bila kupewa au kugawiwa. Fikiria unataka kujenga nyumba na ukatafuta wajenzi. Wakaja wajenzi mbalimbali wakitafuta kazi na kati yao ukawachagua wale ambao unaamini wana uwezo wa kufanya kazi husika. Mkakubaliana ramani ya nyumba (itakuwaje), bajeti ya vitu mbalimbali, na gharama za ufundi. Katika kukamilisha kazi hiyo wewe kama mmiliki ulijua kabisa bajeti yako ni kiasi gani na mafundi walielewa bajeti hiyo.
Sasa inakuja siku mafundi wanakuja na kusema wanahitaji fedha zaidi ya kununulia mchanga; unawauliza zile ulizowapangia kununulia mchanga wamezitumiaje wanakuambia ati wamenunua baskeli na viti vya kupumzikia! Na wewe kwa vile ni tajiri sana unawapa fedha nyingine za mchanga. Baadaye wanarudi tena na kusema wanahitaji fedha za kenchi! Unauliza vipi zile za kenchi ulizowapatia wanasema walijikuta wanapatwa sana na kiu wakaamua kununua mabox ya maji safi ya chupa! Utaendelea mpaka lini?
Mwisho wa siku utatakiwa kuamua ama kuendelea na wajenzi wale wale ama kuanza kuwakatalia; itakupasa uamue kama unataka kuendelea kuwatengea fedha za Big G na Ice Cream au kuhakikisha wanatumia fedha kwa kujenga mabomba na kuinua nyumba. Wewe mwenye nyumba ndio mwenye uamuzi wa mwisho kuhusu nini kifanyike na kwa gharama gani.
Sasa Bunge letu ndio wawakilishi wa sisi wananchi. Ndio maana Bunge linajadili bajeti, linapanga matumizi na hata kubadilisha vitu ambavyo serikali haijaviweka sawa. Bunge linafanya hivyo kwa sababu wao ndio wawakilishi wa sisi wananchi wote. Ni Bunge linalotakiwa kuamua nini kinafanyika nchini, kinafanywa na nani, na kwa gharama gani. Na ni hili hili Bunge linaloamua fedha hizo zinatoka wapi na kwa vipi! Siyo Rais Kikwete. Kwa mtindo wetu wa Kibunge, wabunge wanaweza kulazimisha serikali ibadili mipango yake au hata kutenga fedha (appropriate) zitumike vipi. Kama umefuatilia Bunge utaona kuna wakati Bunge linakaa kama kamati ambapo linapitia bajeti au mswada mstari kwa mstari (line items). Ni wakati huu bunge linafanya kazi yake hasa ya kutunga sheria na kupitisha bajeti.
Hii ina maana ya kwamba, kama kweli tunaona kuna tatizo kwenye sekta ya afya na tumegundua kuwa Ikulu (chini ya Kikwete) hawana uwezo wa kutatua basi tumaini la mwisho ni Bunge. Bunge letu bahati mbaya ni legelege siyo maneno yangu bali ya Mbunge mmojawapo na hayakutakiwa kufutwa! Ulegelege huu wa bunge ndio kweli umetufikisha hapa. Wabunge wa CCM wako makini kuona serikali na Rais wao hashambuliwi sana Bungeni. Tusiwategemee waamue kuingilia kati mgogoro tunaouoona sasa au ule mwingine (wa walimu). Wao wamelelewa katika fikra za chama kimoja ambapo wanaileza serikali na hawaishurutishi serikali yao. Hakuna mbunge wa CCM anayeweza kuleta mswada binafsi wa kuboresha sekta ya afya. HAKUNA!!! Wote wamekaa na kusubiria Serikali ilete mapendekezo au ilete mswada! Utasikia wanamuomba Mwanasheria Mkuu afanye hivyo. Kwanini kwa sababu wao wabunge ni legelege!
Wabunge wa upinzani nao wameingia kwenye mtego huu huu. Wanajitahidi kuikosoa serikali sana ili itawale vizuri. Matokeo yake na wao hawafikirii kuleta mswada binafsi wa kubadilisha na kuboresha sekta ya afya na kama ni mswada mzuri kutafuta ushirikiano na wale wa CCM. Ni wazi ni rahisi zaidi kwa mbunge wa CCM kufanya hivyo kuliko wa upinzani kwa sababu hata kama mswada wa upinzani ni mzuri kiasi gani CCM hawatoukumbatia kwa kuogopa kuwapa ujio wapinzani! Matokeo yake wapinzani hata kujaribu hawajaribu.
Lakini kutokujaribu kwao kunawaweka wao pabaya; kwani hadi hivi sasa hatujui ni sheria za namna gani upinzani wanaweza kuja nazo baadaye. Kwa mfano, je wanaweza kuandika sheria nzuri ya kusimamia sekta ya afya kuliko CCM? Je wanaweza kuandika sheria nzuri ya fedha kuliko ya serikali ya CCM? Ni bora wangekuwa wanajaribu na tuone miswada yao tuweze kupima kama itakuwa na unafuu kuliko kusubiri waingie madarakani ndio waanze kuhangaika na kuandika sheria. Lakini kwa mfano, wakiweza kuandika sheria mbalimbali (nzima au mabadiliko ya sheria za sasa) na zote zikakataliwa na CCM lakini zikapendwa na wananchi je siyo mtaji tosha kwao unapokuja uchaguzi mkuu kwani wananchi tayari wanajua ni sheria gani za kisekta ambazo zikutawepo chini ya chama cha upinzani!
Sasa tuna matumaini? Swali hili sijui jibu lake. Lakini kama nilivyowahi kusema mwanzoni kila uchaguzi una matokeo (every election has its outcome) na uchaguzi wa wale waliowarudisha hawa madarakani una matokeo na matokeo yake mengine ni haya. Safari ijayo ukipewa michongoma na mahindi chagua sahihi; haiwezekani kwa miaka 50 bado unachagua michongoma na ikikuchoma unalalamika. Bunge la michongoma huchoma!
Niandikie: mwanakijiji@jamiiforums.com