Songaleli
JF-Expert Member
- Aug 6, 2022
- 322
- 302
Ma-Ded waanza kushushiwa moto,Sasa kuwapisha wenye uwezo wa kukusanya Mapato,
Wakati halmashauri 85 zikikusanya mapato chini ya kiwango zilichopangiwa, Serikali imeanza kuchukua hatua dhidi ya wakurugenzi wake (DED), ikiwataka watoe maelezo ya kilichotokea.
Katika halmashauri hizo, Bumbuli ya Mkoa wa Tanga imeshika mkia kwa kukusanya asilimia 58 ya mapato, huku Kibaha ya mkoani Pwani ikiibuka kinara kwa kukusanya asilimia 247.
“Nimeambiwa na wakubwa zangu, nitoe maelezo kuhusu kilichotokea, nitafanya hivyo baadaye ndipo nitakapotoa maelezo mahali pengine,” alisema George Haule, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Bumbuli.
Jana, alipoulizwa kwa njia ya WhatsApp kuhusu hatua dhidi ya halmashauri hizo, Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Profesa Riziki Shemdoe alisema mbali na vyanzo hivyo, hatua za haraka zinazochukuliwa ni kuzihimiza halmashauri kufanya vizuri na kuondoa uvujaji wa mapato.
“Kwa hatua hii tunaendelea kuwahimiza kufanya vizuri kwa kuongeza vyanzo vya mapato na kuondoa uvujaji wa mapato,” alisema Shemdoe.
Alipoulizwa zaidi kuhusu hatua za kinidhamu kwa watendaji wa halmashauri alisema, “matokeo si yametoka jana tu kaka. Nashauri tumia majibu niliyokupa hapo juu.”
Licha ya majibu hayo ya Profesa Shemdoe, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Bumbuli iliyokuwa ya mwisho katika makusanyo, Haule alisema ni vigumu kwa sasa kueleza sababu za kilichotokea.Alisema amepewa maelekezo na wakubwa zake kuandika maelekezo kuhusu sababu za kukusanya kiwango hicho na kufafanua kuwa atajibu maswali ya mwandishi iwapo atamaliza hilo.
“Nimembiwa niandike maelezo kesho tutakamilisha na kuyatuma, baada ya kufanya hivyo sasa nitakuwa tayari kuyatoa kwa wengine, lakini kwa sasa nimeelekezwa na wakubwa,” alisema.
Halmashauri ya Mji wa Nanyamba imekusanya asilimia 71 ikiwa nafasi ya nne kutoka mwisho.
Mkurugenzi wa halmashauri hiyo, Thomas Mwailafu alitaja hali duni ya usalama kuwa moja ya sababu za makusanyo hayo.
“Nanyamba ni moja ya wilaya zilizopo mpakani kabisa na Msumbiji, sasa kata zetu tatu tegemezi kwa mapato ndiyo hizo zilizoathiriwa na machafuko,” alisema.
Halmashauri hizo 85, baadhi ya wakurugenzi wake wanatizamwa kwa jicho la karibuni na Rais Samia Suluhu Hassan, ambaye Jumatatu hii alisema anakusudia kufanya mabadiliko ya wakurugenzi, wakuu wa wilaya na makatibu tawala wa wilaya.
“…nihimize sana ukusanyaji wa mapato, lakini pia kufanya mapitio ya viwango tunavyojiwekea vya ukusanyaji wa mapato,” alisema Rais Samia alipomaliza kuwaapisha wakuu wa mikoa na makatibu tawala wa mikoa
Rais Samia aliwahi kunukuliwa akisema, miongoni mwa vipimo vya wakurugenzi ni jinsi wanavyopambana kukusanya mapato na kuyatumia katika kutatua changamoto zinazowakabili wananchi.
Katika hatua nyingine, Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Omary Kumbilamoto alilipongeza baraza la madiwani la jiji hilo kwa kusimamia vema ukusanyaji mapato.
Katika mapato hayo ya mwaka wa fedha 2021/22, Dar es Salaam ilikusanya asilimia 108, Kumbilamoto alisema makusanyo hayo pamoja na mambo mengine, yalifanikisha ujenzi wa vituo vinne vya afya.
“Katika bajeti ya mwaka huu, tunatarajia kujenga vituo vitatu vya afya, kwa hiyo jumla tutakuwa na vituo saba vilivyotokana na mapato ya ndani ya halmashauri. Pia tunatarajia kujenga soko kwa ajili ya wafanyabiashara Ilala Boma,” alisema.
Halmashauri zilizokusanya chini ya asilimia 100 na asilimia ni Bumbuli asilimia 58, Korogwe (67), Bunda (70), Nanyamba (71), Madaba (77), Manispaa ya Mtwara (78), Gairo (79) na Liwale (80).
Nyingine ni Itigi (81), Kilolo (81), Longido (82), Ushetu (82), Mvomero (83), Kishapu (84), Mji wa Korogwe (84), Nachingwea (85), Pangani (85), Bahi (86), Manyoni (86), Mpwapwa (87), Kilwa (87), Musoma (87), Nzega (87) na Arusha (88).
Pia, Lushoto (88), Nkasi (88), Geita (88), Iringa (88), Hai (88), Kalambo (89), Ruangwa (89), Tandahimba (89), Manispaa ya Lindi (90), Itilima (91), Uvinza (91), Manispaa ya Morogoro (91) na Busokelo (91).
Halmashauri ya Nyang’hwale (91), Sengerema (91), Kibondo (91), Buchosa (91), Malinyi (92), Kwimba (92), Kasulu (92), Mbeya (92), Manispaa ya Singida (92), Chato (92), Kondoa (92), Uyui (93), Tarime (93), Mji wa Handeni (94) na Newala (94).
Moshi (94), Mtama (94), Msalala (94), Ikungi (94), Kilindi (95), Ukerewe (95), Songwe (95), Mji wa Tabora (95), Songea (95), Buatiama (95), Mji wa Makambako (95), Chalinze (95), Manispaa ya Kinondoni (96), Handeni (96), Manispaa ya Musoma (96), Kigoma (96), Manispaa ya Mpanda (97) na Same (97).
Manispaa ya Temeke (97), Ngorongoro (97), Mwanga (97), Mji wa Kigoma (97), Kilosa (97), Urambo (97), Masasi (98), Kyerwa (98), Mbogwe (98), Mji wa Nzega (99), Mji wa Tarime (99), Busega (99), Muleba (99), Mji wa Sikonge (99) na Nyasa (99).