Bomoa Bomoa Tabata Nani Ajiuzulu?

Mkombozi

JF-Expert Member
Feb 19, 2008
806
426
Ndugu wana JF,nimesoma habari hii kutoka gazeti la Mtanzania na kuhisi kua hela zimeniishia mfukoni gafla. Najiuliza hivi uzembe serekalini utaisha lini? Bomoa bomoa hii ilikiuka mambo mengi ya kimsingi kama inavyojieleza hapo chini. Kulipa kifuta jasho kwa Serikali cha Jumla ya TShs 1.76 billion kwa hasara ambazo ni za kukiuka maadili na kutofuata sheria ni hasara kubwa kwa Taifa. Hizi hela ni za walipa kodi & wananchi kwa kujumla. Mimi nadhani viongozi waliohusika kwa njia moja ama nyingine wawajibike sio mpaka tume iundwe kuwachunguza tena.

Mimi nadhani imefika wakati kuwa na ustaarabu wa kujiuzulu au kuwajibika kwa kutotimiza wajibu. Hivi inaingia akilini bomoa kubwa kiasi hiki inafanyika ndani ya mkoa wenye wilaya tatu halafu mkuu wa mkoa asifahamu? Basi ni wakati wa Yeye mwenyewe kupima na kuona uzito na kuamua atajiwajibishaje. Hapa tunaendelea kuutumia mfano Wa aliyekua waziri mkuu Edward Lowasa kuwajibika kwa makosa ya watendaji wake na Pia Mzee Mwinyi miaka ya 1980s’, kwa hiyo nae awajibike,pia madiwani & wakurugenzi wa wote wa Ilala. Wasipojiwajibisha ina maana kuwa siku nyingine wanaweza kurudia makosa kama haya ya kutofuata kanuni na sheria za nchi. Hizi fedha za fidia zingeweza kutumika sehemu nyingine. Nchi ni masikini kila kukicha tunaomba ufadhili lakini baadhi ya viongozi hawatekelezi wajibu wao ipasavyo. Nadhani pia imefika wakati sasa serikalini kuiga mfumo wa Makampuni Binafisi ambapo mtu huendelea kuwepo kazini,kupandishwa cheo & nyongeza ya mshahara kutokana na ufanisi wake wa kazi. Kila kiongozi anaweka malengo yake ya mwaka, kwamba atafanya nini & mwisho wa mwaka anapimwa kama ameyatekeleza ipasavyo kama sio anaondolewe, wapo watu wengi wachapa kazi



Waliobomolewa Dar wapewa kifuta machozi Sh.1.76 Billions-Mwananchi

Wao wazikataa, wamtaka Waziri Wassira
Ramadhan Semtawa na Kizitto Noya
SERIKALI imetangaza neema ya kifuta machozi cha Sh1.7 bilioni kwa wakazi Tabata Dampo, jijini Dar es Salaam kufuatia ubomoaji haramu wa nyumba 88.
Uamuzi huo wa serikali wa kujikuta katika hasara hiyo, umetokana na kubaini uzembe wa baadhi ya maafisa wake kushindwa kusimamia kanuni na taratibu katika zoezi zima la ubomoaji wa nyumba hizo.
Kutokana na uzembe huo wa ukiukwaji wa taratibu na kanuni za notisi kuhusu ubomoaji nyumba unaohusishwa na ufisadi, serikali italazimika kulipa Sh 20 milioni kwa kila nyumba iliyobomolewa na kutoa kiwanja bure eneo Buyuni, Wilaya ya Ilala, kwa kila mkazi.
Akisoma Tamko la Serikali jijini Dar es Salaam jana kufuatia matokeo ya Tume Maalumu ya Kuchunguza Ubomoaji wa Nyumba hizo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Tamisemi), Stephen Wassira, alisema uamuzi huo wa serikali unatokana na kubaini kwamba ubomoaji huo haukuzingatia uamuzi wa Baraza la Ardhi.
Wassira alifafanua kwamba, uamuzi wa Baraza la Ardhi ulitaka Halmashauri (Ilala) iangalie taratibu zilizopo katika kuwaondoa wavamizi katika eneo husika.
Akifafanua kuhusu hilo, Wassira alitaja taratibu hizo ambazo zilipaswa kuzingatiwa kwamba ni kufikisha dhamira hiyo ya ubomoaji kwanza katika vikao vya juu vya timu ya menejimenti na vikao vya Baraza la Madiwani.
Wassira aliongeza kwamba, taratibu nyingine zilizokiukwa, ni wananchi kutoshirikishwa katika azma ya ubomoaji huo kitu ambacho ni kinyume cha misingi na kanuni za utawala bora huku kukiwa na harufu ya rushwa.
"Kuwepo kwa viashiria vya vitendo vya rushwa japo haikuweza kuthibitishwa," alikiri ufisadi katika ubomoaji huo ambao hata hivyo, alipobanwa alishindwa kufafanua waliohusika.
Alisema taratibu zinataka notisi ya ubomoaji wa nyumba za makazi uwe siku 30, lakini katika ubomoaji wa Tabata notisi ilitolewa Febrari 27 na utekelezaji ukaanza Februari 29, ikiwa ni siku mbili.
Alisema uamuzi wa serikali kulipa fidia hiyo, haukuzingatia kama wakazi hao wanaishi kihalali au haramu bali umetokana na kubaini ukiukwaji wa taratibu ambazo zilitokana na maafisa wake kushindwa kuzisimamia.
Waziri Wassira aliweka bayana msimamo wa serikali kwamba, malipo hayo hayahusiani na nyumba ambazo hazijabomolewa kwani wakazi hao hadi sasa wamefungua kesi Mahakama Kuu kupinga kuondolewa katika eneo hilo.
Hata hivyo, alitoa ushauri wa bure kwa wakazi hao kuachana na ujenzi katika eneo hilo badala yake watumie fedha hizo kujenga nyumba eneo la Buyuni ambalo serikali imewatengea ili kuepuka uwezako mwingine wa kupoteza mali iwapo Mahakama Kuu itaamuru waondoke.
Eneo la Tabata Dampo liko katika mvutano kati ya wananchi na Kampuni ya Allied Cargo, hali ambayo ilisababisha nyumba 88 kuvunjwa hapo Februari 29.
Hata hivyo, Mahakama Kuu haijatoa uamuzi wa kesi namba 18, 2008 kuhusu mgogoro huo.
Tayari baadhi ya watendaji wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilala akiwemo aliyekuwa Mkurugenzi Mtendaji John Lubuva, wamesimamishwa kazi, huku serikali ikielezwa kutumia Sh 600,000 kila mwezi kwa ajili ya chakula cha watu hao.
Katika hatua nyingine, waathirika wa bomoa bomoa ya Tabata wamesema hawatachukua hundi wala kiwanja mpaka waonane na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) kwa kuwa hawana imani na matokeo ya tume yake.
Mwenyekiti wa Kamati ya Maafa, Said Masoud alisema jana kuwa msimamo wa waathiri hao ni kutochukua fidia yoyote mpaka serikali iseme malipo hayo ya Sh20milioni ni ya kitu gani.
?Kimsingi sisi hatuchukui hela wala kiwanja mpaka Wassira atueleze ametulipa kitu gani. Kwanza malipo yenyewe ni kidogo na pia hayaelezi ni ya kitu gani,?alisema Masoud akizungukwa na wakazi wengine wa eneo hilo waliokuwa katika mkutano kuhusiana na suala hilo.
Masoud alisema mbali na mapungufu mengine, tume aliyoiunda Waziri Wassira kuchunguza maafa hayo imepoteza uaminifu kwa kuficha ukweli kuhusu rushwa na imewadhalilisha kwa kuwaita wavamizi katika eneo hilo.
Alisema ni udhalilishaji kuwaita wavamizi kwani wamekuwapo katika eneo hilo tangu mwaka 1964 na serikali imewatambua kwa kuwapa hati za makazi kwa malipo halali yaliyofanywa kiofisi.
?Sisi tumedhalilishwa kuitwa wavamizi, lakini pia ripoti imeshindwa kusema ukweli kwamba kulikuwa na rushwa katika zoezi zima hilo, rushwa ambayo sisi tumeiona katika hatua mbalimbali kabla ya zoezi lenyewe,?alisema Masoud
Alitaja mapungufu mengine katika ripoti hiyo kuwa ni kutoweka bayana malipo ya Sh1.7 bilioni yanahusu fidia ya jambo gani wakati madai yanayoendana na mali iliyoharibiwa katika zoezi hilo ni Sh5.7bilioni.
Alisema mbali na fedha hiyo kutokidhi haja, bado kuna upungufu wa wapangaji walioharibiwa mali zao katika bomoa bomoa kutolipwa chochote wakati nao ni waathirika.
Masoud alimwomba Rais Jakaya Kikwete kuingilia kati suala hilo na kuunda tume nyingine huru zaidi kama alivyofanya katika matukio mengine ya kitaifa ili kubaini ukweli na kuhakikisha haki inatendeka kwa waathirika wote.
?Kuanzia leo tunakutana na kutafuta namna ya kuwapata viongozi hao wa serikali lakini ni vema rais akaunde tume nyingine ili kubaini ukweli kuhusu tukio hilo kwani matokeo ya tume ya Wassira hayana ukweli.
 
Back
Top Bottom