Binamu yangu

Mpauko

R.I.P
Jan 19, 2019
2,323
3,353
BINAMU YANGU-01

ROBIN MIHO

0776741545

Ni saa tatu usiku mvua ya wastani ilikuwa ikinyesha taratibu huku upepo ukivuma hapa na pale,nilifumbua macho kivivu na kugundua ya kwamba nilikuwa nimesinzia kochini sebuleni kwangu,nikatupa mkono kujaribu kumpiga mbu aliyekuwa akijipatia shibe mguuni lakini bahati ilikuwa ni yake nikamkosa na kuachia msonyo mdogo huku nikijikuna.

Nikajizoa zoa kuingia chumbani na kujibwaga kitandani,zilipita dakika chache tu kabla simu yangu haijaanza kuita kwa fujo nikafumbua jicho moja na kutupa mkono chini ya mto kuitafuta simu yangu nikaipeleka sikioni bila hata ya kutazama mpigaji ni nani,chezea usingizi wewe!

"Haloo" niliita

"Haloo hujambo mwanangu?"

"Sijambo mama shikamoo"

"Marahaba mwanangu umeshaanza likizo?"

"Ndio mama nineanza jana"

"Oohh mwanangu kesho uje nyumbani mara moja"

"Kuna nini tena mamaaa"

"Baba yako anataka umsindikize nyumbani kwa babu yako maana anaumwa"

"Lini mama?"

"Keshokutwa mwanangu anahitaji kuwahi kumuuguza babu yako na huu uzee wa baba yako hatoweza kuendesha gari hadi Mufindi"

"Sawa mama basi nitakuja kesho"

"Sawa mwanangu uwe na usiku mwema"

"Nanyi pia mama"

Baada ya simu kukatika na usingizi ukawa umeshakata hivyo nikaamua kuanza kupanga nguo zangu kwa ajili ya safari ya ghafla ya Mufindi.

Ni takribani miezi nane tu tangu niajiriwe katika benki ya National Microfinance Bank (NMB) kama meneja mwandamizi hivyo nikahama kwa wazee wangu mtaa wa uhuru na kupanga nyumba ndogo ya vyumba vitatu mtaa wa Mbuyuni.

Baada ya kuridhishwa na maandalizi yangu nikatoka kwenda kutafuta chakula maana nilikuwa mvivu kweli kweli kwenye suala la kupika chakula,nilijizoesha kupikiwa na mpenzi wangu Ezelina ambaye tuliachana baada ya kukorofishana hapa na pale tukaamua tu kusitisha mahusiano ingawaje nilikuwa bado nanpenda lakini glasi ikivunjika hata iunganishwe vipi bado haitoweza kuwa kama ilivyokuwa mwanzo.

Hatimaye siku ya safari ikawadia,tuliamua kuondoka saa nne asubuhi kwa gari ndogo ya baba yangu mzee Maliki aina ya Rav 4 old model nyeupe,niliendesha kwa umakini wa kutosha uliotufikisha Mufindi saa mbili na dakika kadhaa usiku,tulifikia kwa babu na bibi mzaa baba,ingawaje babu hakuwepo,alikuwa hospitalj na tukapanga kwenda kumuona kesho yake.

Nyumba ya babu ilikuwa ni kubwa na yenye vyumba vingi vya kutosha,mimi nilipewa chumba kilichojitegemea kwa nje huku baba yangu Mzee maliki akilala katika vyumba vilivyopo ndani kabisa ya jengo lile kubwa la matofari ya kuchoma,pengine inaweza kuwa nyumba nzuri kuliko nyingi ya nyumba kadhaa za kijiji hiki.

Asubuhi ya siku iliyofuata tulijihimu kwenda hospitali kwani ilikuwa mbali takribani mwendo wa masaa matatu hivi,tuliondoka watu watatu mimi baba na bibi mzaa mama,saa tatu kasoro ilitukuta mbele ya hospitali ya mafinga,hali ya babu haikuwa ya kuridhisha sana ingawaje ilikuwa nafuu ya jana,hadi inatimu saa tisa mchana,baba yangu mzee Maliki aliamua kubaki hospitali na kuniambia nitangulie kijijini pamoja na bibi mzaa mama.

Baada ya kuondoka hospitali masaa mawili tu yalitosha kutufikisha Igowole ambapo bibi aliomba nimuache pale akamsalimu mjomba,ilikuwa ni takribani dk 40 hivi kwa gari kabla ya kuingia kijijini kwetu,baada ya kumwacha sasa nilikanyanga mafuta kuwahi kijijini.

Sijui ni nini kilichonisukuma kuyatupa macho yango pembeni ya barabara alikuwepo binti mmoja mrefu kiasi,maji ya kunde,kifua kidogo na kalio la kutosha kumvutia mwanaume yeyote yule rijali,alikuwa amejitwisha kiroba akitembea kwa haraka kuelekea kule kule nilikokuwa nikielekea.

Nikajikuta nikipunguza mwendo na hatimaye nikasimama na kushusha kioo,nikampungia mkono wa kumwita,mwanzo alisita lakini akasogea dirishani na kunikazia macho kumaanisha alikuwa akinisikiliza.

Ukweli alikuwa ni mzuri sana,midomo minene iliyoumbika vizuri,macho makubwa na uso wa mviringo ulionakshiwa na muonekano wa hurumahuruma hivi,namna gani sasa nilijikuta nikiduwaa kwa sekunde chache huku mapigo ya moyo yakinienda mbio.

"Shikamoo" binti alisalimia baada ya kuona nikiwa nimezubaa.

"Eh.. Marahaba hujambo"

"Sijambo"

"Samahani hivi hospitali ya wilaya iko wapi?"

"Mmh iko hukohuko ulikotoka mbona"

"Eeh ni huku aisee... Inachukua muda gani kufika huko?"

"Ni kama masaa matatu hivi" alijibu huku akikwepesha macho yake baada ya mimi kunkazia sana macho.

"Aaah aise muda umekwenda saa kumi na nusu saizi nitaenda tu kesho!... Unaelekea wapi?" Nikamtupia swali.

"Hapo kihanga"

"Nami naelekea huko ingia nikusogeze mbele kidogo" nilimuona akisita huku akijifikiria na kukuna mikono yake asijue ama akubali au akatae ofa ile,nikashuka na kwenda kumpokea kiroba chake na kukitia kwenye buti,nilibaini ulikuwa ni unga,bila shaka alikuwa akitoka mashineni.

Tukaingia garini na safari ikaanza,nilitembea taratibu huku nikimfikiria binti huyu,sikujua hasa kwanini alinifanya nimfikirie kiasi hiki,mwisho nikavunja ukimya.

"Naitwa Aloyce Jacob Maliki" nikamtupia macho.

"Naitwa Helena Mtavangu"

"Una jina zuri Helena,nami nikijaaliwa mtoto nitamuita Helena"

"Ha ha ha asante bwana"

"Je! Unasoma?"

"Hapana,nimemaliza form six mwaka jana"

"Kwahiyo unaenda chuo sio?"

"Mmmh hapana,matokeo yangu hayakuwa mazuri sana,nitaenda kusomea ufundi cherehani mwezi ujao"

Tayari tulikuwa tumeshafika kijijini,Helena aliomba nimshushe mbali kidogo ingawaje nilibaini ya kwamba aliishi jirani tu na yalipokuwa makazi ya baba na bibi,yaani mwendo wa dakika nne au tano tu kwa mguu,niliwasili nyumbani na kukuta tayari nimeshaandaliwa maji ya kuoga,nilioga na kujivutia jikoni kuota moto maana baridi lilikuwa ni kali kwelikweli,hadi ilipotimu saa nne nikaagana na waliokuwepo jikoni na kwenda kujipumzisha.

Nikiwa kitandani akili yangu ilitawaliwa na picha ya Helena tu,nilimfikiria kwelikweli huku wakati mwingine nikijishitukia na kujiuliza sababu ya kumfikiria kiumbe huyu ni nini hasa? Je nilikuwa nimempenda? Lakini nampendaje mtu nimemuona siku moja? Au namtamani...niliwaza na kuwazua pale kitandani,sikumbuki ni muda gani usingizi ulinipitia nilikuja kugutuka tayari ni saa mbili asubuhi.

ITAENDELEA...
 
BINAMU YANGU-02

ROBIN MIHO

0776741545

Niliamka na kuingia maliwatoni,dakika kumi tu zilitosha kujimwagia maji,nikaelekea uwani kujumuika na wanafamilia wengine akiwemo shangazi,bibi mkubwa,wajomba na ndugu wengine wengi walioishi pale na waliokuja kusalimia.

Ingawaje nilikuwa pale bado akili yangu ilikuwa ikimuwaza mtu mmoja tu,Helena nilitamani sana japo kumtia machoni angalau hata niisikie sauti yake.


Nikaamua kutoka na kwenda kwa mpwa wangu ambaye tulipishana miaka mitatu tu yaani alikuwa na miaka ishirini na nne pungufu ya miaka minne tu kunifikia mimi,yeye aliitwa Masudi na nikiri wazi ndiye aliyekuwa kampani yangu kila nijapo kijijini,ni bahati mbaya nilipoteza mawasiliano naye miaka saba iliyopita mara ya mwisho kuwepo hapa.


Sikuwa na uhakika wa kumkuta na sikutaka kumuuliza yeyote kwani sikutaka mtu ajue kama naelekea kwake,Masudi alikuwa ni kijana mtukutu na mbabe kwelikweli kutokana na kuwa na umbo kubwa lililoshiba kazi ngumu za kubeba magogo na kupasua mbao.


Niliwasili kwa kina Masudi na kumkuta mama yake pamoja na wadogo zake masudi wakiwa wanapata sitafutahi ya viazi mviringo vya kuchemsha vilivyochanganywa maharage na mboga ya majani ambayo sikuitambua ni mboga ya aina gani.


"Karibu mwanangu karibu sana" Mama Masudi alinikaribisha kwa furaha iliyochanganyika na mshangao.

"Ahsante mama za hapa"

"Nzuri tu mwanangu Mungu anasaidia sana"

"Aisee vipi Masudi nimemkuta?"

"Ingia ukae kwanza mwanangu upate kifungua kinywa kwanza waongelea mlangoni kama mtoza kodi heheheee.."


Aliongea huku akipakua viazi na kuvitua kwenye meza,vilikuwa ni viazi vilivyochemshwa na kuchanganywa maharage na majani ya maboga "pure natural" nilijisemea huku nikitabasamu.


Baada ya kupata chai ya nguvu mama Masudi alinieleza kwamba Masudi alikuwa Mafinga mjini baada ya kukimbia kijijini kutokana na kumpa ujauzito mtoto wa chifu.


Ieleweke kuwa utamaduni wa wahehe kutawaliwa na chifu ulikuwa bado unaendelea ingawaje tawala za kiserikali kama vile mwenyekiti wa mtaa na diwani walifanya kazi zao kama kawaida,lakini Chifu alikuwa ni mjumbe mwenye sauti katika maamuzi mengi yahusuyo kijiji.


Kitendo cha Masudi kumpa ujauzito binti mkubwa wa chifu kilimuingiza katika matatizo makubwa kwani alisakwa kwa udi na uvumba ili ashitakiwe ingawaje binti wa chifu hakuwa mwanafunzi bado nguvu na mamlaka ya chifu vilitosha kufungua kesi ya kumpa ujauzito mwanafunzi.


Hii ilimlazimu Masudi kukimbilia Mafinga baada ya kukoswa koswa na walinzi wa kijiji,aliharibu zaidi baada ya kuwashushia kipigo mgambo wa kijiji, chifu aliapa kumshikisha adabu.



Baada ya mazungumzo ya hapa na pale nilichukua namba ya Masudi na kushika njia kurudi nyumbani huku nikiangaza macho huku na kule kwa matumaini ya kumuona Helena ,hadi nawasili sikuwa nimebahatika kumuona kabisa nilihuzunika sana.


Nikakumbuka namba ya Masudi nikaamua kumpigia muda huohuo na bahati nzuri simu yake ilikuwa hewani.


"Halo nani"


sauti niliyoitambua wazi kuwa ni ya Masudi ilisikika,nikacheka kwa furaha baada ya kuisikia sauti nyembamba ya Masudi,achana na mwili jumba jamaa alikuwa na sauti nyembamba kweli kweli ingawaje si kama ya mwanamke.


"Aloyce hapa"


"Aloyce gani Mtavangu au Maliki"


"Aloyce maliki kaka"


"Daah we mwana wewe hivi upo kweli!"


"Nipo kaka hivi nipo Kihanga saizi"


"Ebwana eeh usiniambie"


"Kweli Masudi muulize bimkubwa nilikuja kwenu na muda huu ndo nimerudi"


"Aisee nipo Mafinga ila hadi jioni nitakuwa huko kaka si utanipoza mafuta ya pikpiki?"


"We njoo tena nakutumia sasa hivi elfu ishirini ya mafuta"


"Mambo si ndo hayo sasaaa ila usimwambie mtu yeyote kama nitakuja huko"


"Usijali Masudi fanya uje"


"Poa hebu chachusha simu yangu kwa namba sifuri saba saba sita...saba nne moja..tano nneee tano"


"Dakika sifuri Masudi"


Nilimjibu na kukata simu,nikafanya muamala kwa ajili ya masudi kisha nikaingia ndani kutazama taarifa ya habari,ingawaje akili yangu haikutulia kwa kumuwaza Helena,ama kweli nilikuwa nimepatikana.


Hatimaye jioni ilinikuta nikiwa naelekea nyumbani kwa Kina Masudi ilikuwa saa moja kasoro tu hivi Masudi aliponijulisha kuwa alikwa amefika.


Baada ya kufika na kweli nilimkuta,alikuwa amebadilika kwelikweli,alikuwa pande la mtu ama kweli alifaa sana kuwa baunsa huko miji mikubwa ambako kila kukicha matajiri na watu maarufu wanahitaji walinzi binafsi.


Baada ya salamu za hapa na pale nikaamua kumweleza ukweli juu ya Helena ambaye alikuwa ni nduguye kwani wote walitoka ukoo wa Mtavangu,alicheka sana na kuniambia nisiwe na wasiwasi.


Akaitwaa simu na kutuma ujumbe,baada ya dakika chache akatabasam na kuniambia twende sasa,akavalia koti kubwa na kikoi kilichomziba kabisa sura yake,ingawaje mwendo wake bado ulimsaliti kwani ilikuwa ni rahisi kumtambua ila hakujali alikuwa anajiamini kwelikweli.


Kitu kilichonishangaza ni pale alipochukua waya unaotumika kama breki kwenye pikipiki na kuusundika kwenye mfuko wa suruali yake ya jeans bluu iliyopauka,sikumuuliza tukatoka taratibu na kushika njia inayoelekea kilabuni.


Dakika tano tu tangu tutoke mtu mwingine alijitokeza nyuma yetu,Masudi akasimama ila mimi sikusimama hadi aliponiita,ile kugeuka mapigo ya moyo yakapamba moto baada ya kubaini ya kuwa alikuwa ni Helena..!

ITAENDELEA....
 
BINAMU YANGU-03

ROBIN MIHO

0776741545


Nikapiga hatua kuwasogele pale walipokuwa wamesimama,huku bado mapigo ya moyo yakinienda mbio ajabu.

"Helena dogo huyu anaitwa Aloyce anatokea Morogoro ni wa ukoo wa chifu" akanitambulisha Masudi.

"Huyu ni mdogo wangu anakaa nyumba ya pili toka nyumbani" akasita kidogo na kuendelea.

"Helena naomba umsikilize rafiki yangu mara moja,Aloyce utanikuta kilabuni"

Masudi hakungoja majibu zaidi Masudi akashika njia kuelekea kilabuni,nikajikuta nakosa cha kuongea na hofu ikinitawala moyoni mwangu lakini nikajikaza kisabuni.


"Unaelekea wapi Helena?"


"Naenda kilabuni mara moja kuchukua mboga"


"Anha sawa nadhani hautojali tukisogea pembeni tutete angalau dakika chache"

niliongea huku nikisogea kwenye kijinjia kilichokuwa katikati ya shamba la mahindi,Helena naye alijivuta vuta kwa mashaka kunifuata.


"Samahani Heleni naomba nikuulize"


"Uliza Aloyce"


"Nakumbuka uliniambia utaenda kuchukua mafunzo ya ufundi cherehani,je! Utakwenda lini?"


"Mmmh kwakweli bado sina uhakika sana huenda ikawa mwezi ujao"


"Ooh sawa je kwa sasa unafanya shughuli gani au bado unapumzika?".


"Nilikuwa ninafundisha shule moja inaitwa Marian Hills Mafinga,lakini ilipigwa mnada japokuwa hadi sasa bado haijauzwa,imefungwa"


"Kwanini sasa ikafungwa?"


"Mnunuzi aliyeshinda mnada ule alisema hivi "mimi nanunua haya majengo na sio wanafunzi na walimu,atakayebaki atalisha mifugo na bata na simlipi" ilikuwa ni balaa"


"Kwahiyo na weww ukaondoka sio?"


"Ndio nani abaki kutawaza mabata sasa"


Tukajikuta tukiangua kicheko,nilibaini Helena licha ya upole wake alikuwa ni mcheshi kwelikweli.



"Sasa Helena binafsi ninataka nikuambie kitu kimoja muhimu sana"


"Kitu gani Aloyce?"


"Kiukweli sitoongea mengi ila nitakuambia moja kwa moja ya kwamba tangu nikuone ile jana nimejikuta nikikupenda sana,natamani uwe mke wangu wa ndoa tuzae tulee watoto mamaangu"


"Mmmh jamani" aliongea kwa kubabaika huku akisugua sugua viganja vya mikono yake.


"Namaanisha Helena tafadhali usiniangushe katika hili"


"Mmh kwa kweli sina cha kukujibu kwa sasa"


"Usijali nakuachia namba yangu mara baada ya kutafakari tafadhali usisite kunifahamisha"

Niliongea huku nikiichukua simu yake ndogo ya batani,nikaandika namba yangu kisha nikamtaka anitumie sms,baada ya hapo tukaagana.


Nikamwacha atangulie kwa zaidi ya dakika mbili kisha nami nikaahika njia kuelekea kilabuni,sikupenda kuonekana nimeanza vurugu na watoto wa watu kwani waliniheshinu na kunichukulia kama kijana mwenye nidhamu sana.


Nilifika kilabuni na kukuta kuna zogo,binti mmoja alikuwa akitandikwa na Masudi akitumia ule waya wa breki ya pikpiki,nikashikwa na butwaa hadi Maaudi aliponishika mkono na kuniambia tuondoke.



Sijawahi kuona vitendo kama hivi vya binti mtu mzima kama yule kushushiwa kichapo namna ile,ikabidi nimuulize Masudi chanzo cha yale yote,akaniambia yule binti ndiye aliyeeneza habari kuwa ule ujauzito wa mtoto wa chifu ulikuwa wake,kwani mtoto wa chifu aligoma kumtaja mhusika.


Baada ya mazungumzo machache nikaagana na Masudi kwa ahadi ya kuonana kesho yake,yeye alienda kulala kijiji cha pili kwa ajili ya usalama wake.


Tayari ilishatimu saa tatu usiku,nikakaza mwendo kurudi nyumbani ambapo nilikula na kuingia chumbani kulala.


Nikaamua kumtumia ujumbe wa kumtakia usiku mwema huku nikimjulisha ya kwamba kesho nitaenda Mafinga kumfuata baba pamoja na Babu.


Vilevile akaniambia kama nipo tayari atanipa jibu langu lakini angependa kuniambia laivu.


Akanielekeza kwenda karibu na kwao ambapo mita kadhaa kulikuwa na nyumba isiyokaliwa na watu,nikakurupuka kitandani na kujiandaa kisha nikatoka.


Niliwasili katika gofu lile na kumkuta akiwa ameketi katika uwalaza,alikuwa amependeza sana kwa kuvalia vazi la kihindi lenye suruali na shati refu karibia kuyafikia magoti likifatiwa na sweta zito jeusi,nikamsogelea na kuketi pembeni yake.


"Umekula Aloyce?"


"Yeah nimekula Helena sijui wewe?"


"Mimi pia nimekula,je umewahi kula Sungura?"


"Mmh sungura hapana sijawahi kula"


Helena akageuka upande wa pili na kutoa kontena dogo,akalifungua na kutwaa kipande cha nyama iliyokaangwa na kuchanganywa vizuri na viungo,akanitazama kwa chati kisha akaelekeza kipande kile mdomoni kwangu,bila ajizi nikakipokea na kuanza kukitafuna
.

"Mmh ni tamu sana" nikasema mara baada ya kumaliza kutafuna.


"Mmh kwelI?"


"Yeah ni tamu sana,amepika nani?"


"Mimi" Helena alijibu kwa maringo huku akiwa amejawa na tabasanu pana.


Nikapitisha mkono wangu begani kwake na kumwambia..


"Natamani uwe wangu unipikie vinono kama hivi"


"Mmmh kweli? Je utakuwa tayari kuja kujitambulisha kwetu?"


"Yeah hata kesho nakuja maadam umeridhia mamaangu" niliongea huku nikiwa nimemkazia macho usoni,Helena hakujibu kitu akainama akiitazama ardhi iliyomulikwa kwa mbalamwezi za usiku ule pasi na kuzungumza kitu.


Nikatumia nafasi ile kujisogeza jirani yake, nikamuinua kichwa chake nikasogeza uso wangu bila ajizi naye alinipokea tukajikuta tukibadilishana mate.


Hisia za mwili zilipanda vilivyo mkono wangu ukianza kutalii katika kifua cha Helena,naye akazidi kulegea na kujigesha kifuani kabla hajaushika mkono wangu kuzuia kuendelea kwa zoezi lile.



"Aloyce je! Unanipenda?"


"Nakupenda tangu siku ya kwanza kukuona na nitakupenda milele"


"Aloyce nikuambie kitu?"


"Yes niambie mpenzi"



"Mimi ni bikra"


Nikamtazama kwa tuo,kwa msaada wa mbalamwezi niliweza kuuona uso mzuri uliovutia sana wa binti huyu nisiamini nilichokisikia.


"Helena ya kweli hayo?"


"Yeah ni kweli huniamini"


"Aah nakuamini mamaa ila nashangaa pia,binti mrembo kama wewe umewaepukaje wakware!?"


"Ha ha ha kujiheshimu tu mpenzi"


Baada ya jibu hilo nikamuomba twende tukalale kwetu,mwanzo aligoma kata kata lakini nilimbembeleza na kumuahidi kumsindikiza kurudi,mwisho akakubali na kuniomba nitangulie yeye anakwenda kuweka mambo sawa kwao.


Kidume nikaondoka huku nikijisifu kimoyomoyo nilijiona mwenye bahati isiyopimika kwa kunpata kigori yule,nikawasili nyumbani na kumsubiri Helena kwa hamu kwelikweli.



Hatimaye ujumbe uliingia nao ulitoka kwa Helena kunijulisha ya kuwa alikuwa pembeni ya nyumba yetu,nikatoka na hakika nilishukuru kweli kweli kupewa chumba cha uwanj,nikamfuata na kuingia nae chumbani.


Kilichoendelea ni siri yangu lakini kwa kukujuza tu ni kwamba alilia sana muda wote nilihangaika kumziba mdomo hadi mwisho wa shughuli ile nililazimika kubadili mashuka kwani damu kiasi ilichafua mandhari ya shuka lile.


Mnamo saa saba kasoro nilitoka pamoja na Helena nikamsindikiza hadi jirani kabisa na kwao,tukaagana kwa ahadi ya kuonana kesho yake.


Naweza kukiri ya kwamba huenda hii ikawa ni siku niliyofurahi sana katika maisha yangu,nilitabasamu kama mwendawazimu hadi nilipopitiwa na usingizi mzito.



Siku iliyofuata ilikuwa ni nzuri nilikuwa mwenye furaha muda wote na baada ya kumfuata baba na babu Mafinga hospitali saa saba mchana ilinikuta nikiwa naongea mawili matatu na wazee wangu.


Simu ya Helena ndiyo iliyoninyanyua na kusogea pembeni ili niweze kuzungumza nae kwa uhuru,kilichonishitua ni sauti isiyo na furaha ikinitaka tuonane,tukakubaliana kuonana mtaa wa pili kwenye uwanja wa mpira wa miguu wa kanisa.



Nikatoka na kushika njia kuelekea uwanjani huku nikiwa na mawazo mengi nikijaribu kufikiria kilichomsibu mpenzi wangu bila mafanikio.


Niliwaaili uwanjani na kumkuta Helena akiwa amekwishafika nikamfuata chini ya mti wa mlingoti alipokuwa ameketi,nilibaini ya kwamba hakuwa mwenye furaha na alionekana kama mtu aliyetoka kulia muda si mrefu.


"Mambo mpenzi?"


Nikamsalimu,hakujibu aliishia kunitazama tu huku machozi yakianza kumlenga,nikaingia kazi ya kumbembeleza na kumtaka anijulishe kilichomsibu.


"Aloyce" aliniita huku akijifuta machozi.


"Naam mamaangu"


"Mama yako bi Magdalena ni mtoto wa nani?"


"Mtoto wa mzee Mwendamseke"nilimjibu nisipate mantiki ya swali lake.


"Mwendamseke nani?"


Nikagutuka na kusikia baridi likinitembea mgongoni baada ya kubaini kuwa mama yangu bi Magralena alikuwa ni dada wa mamamdogo wa mama yake Helena.


Nikamtupia macho Helena na kukwepesha uso wangu kwa aibu,kwanini mambo haya sikuyaona tangu mapema? Nikajiuliza huku nikijihisi hatia.


"Kwahiyo mimi ni binamu yako kabisa Aloyce"


"BINAMU YANGU" nikatamka huku nikijilaza katika majanj,hakika nilihitaji kulala,nilikuwa nimechoka kwelikwelj,aibu gani hii......

USIKOSE SEHEMU YA NNE
 
BINAMU YANGU-04

ROBIN MIHO

0776741545




"Najuta sana kukutana na wewe,nimejitunza hadi hapa halafu usichana wangu anautoa mtu ambaye hata hawezi kuwa mume wangu najuta sana" aliongea Helena akionekana mwenye majuto mengi rohoni mwake.

"Helena,hili ni jambo la bahati mbaya,mimi sijaishi hapa kijijini naanzaje kumfahamu kila mtu?" Nikaongea huku nikijiinua na kukaa kitako.

"Aloyce unafikiria nini? Je upo tayari kuniacha na kunisahau?" Helena aliuliza.

Nikamtazama kwa makini na kubaini ya kwamba alikuwa akimaanisha kile alichokuwa anauliza na alihitaji kupara jibu.

"Ndio nitakuacha,naanzaje kumuoa binamu yangu? Na unafahamu wazi jinsi hili suala linavyokemewa vikali na wazee wa ukoo?" Nilimjibu pasi na kukipima nilichoongea.

"Sawa Aloyce mimi ninakwenda zangu sasa" Helena akainuka na kupiga hatua kuondoka eneo lile,baada ya hatua tano hivi akasimama na kunigeukia,alikuwa analia!..

Alisimama kwa sekunde kadhaa na kugeuka kuendelea na safari yake,nilimtazama pasi na kufanya jambo lolote,ni matone ya maji yakiliangukia shati langu ndiyo yaliyonigutusha.

Lahaulaa! Nilikuwa ninalia! Niliusikia uchungu mwingi ukiutafuna moyo wangu,moyo wangu ulikataa kata kata kuukubali ukweli ule mchungu.

Hatimaye nikajiinua na kushika njia kuelekea nyumbani,niliwasili na moja kwa moja nikapitiliza chumbani kulala,lakini wapi usingizi ulikataa kata kata.

Kila sekunde niliyojaribu kumuondoa Helena kichwani mwangu ndivyo alivyozidi kujikita akilini mwangu,nikajiuliza sana je nitaweza kuishi bila Helena?..majibu yalikuwa ni wazi kuwa sitaweza abadani,hadi saa kumi na mbili jioni sikuwa nimeambulia lepe la usingizi kabisa.

Nikaamua kutoka na kwenda kwa shangazi,nyumba ya pili tu toka pale nikamkuta shangazi akimuogesha mwanae pekee,hakuwa ameolewa akiwa na umri wa makamo ya chini ya miaka 32 tu hivi.

Sikutaka kumficha kitu,kwani alikuwa ni mtu pekee ambaye ningeweza kumuuliza kuhusiana na suala lile,naye alinijulisha kuwa ni kweli Helena alikuwa ni binamu yangu hivyo kama nilikuwa na mawazo ya kuwa naye ni bora nikaachana nayo tu.

Nikiwa naendelea kuzungumza na shangazi simu ilianza kuita,alikuwa ni Masudi,nikatoka nje na kuipokea.

"Haloo Masu"

"Kimetokea nini na uko wapi?" Sauti ya Masudi ikionesha kupaniki ilisikika.

"Nipo nyumbani kaka kuna nini"

"Helena, Helena hali yake mbaya njoo nyumbani na usafiri sasa hivi tumuwahishe hospitali haraka sana" aliongea kwa msisitizo sana na kukata simu.

Nikakimbilia ndani kujiandaa na dakika tano tu nilikuwa nje ya nyumba ya kina Masudi,Masudi alitoka na kuzama garini huku akinielekeza kwenda katika nyumba ya kina Helena.

Nikasogeza gari na mara moja Helena aliletwa akiwa hajitambui,nilichanganyikiwa sana kumuona katika hali kama ile,Helena alikuwa amekunywa sumu!

Niliendesha gari kwa kasi kuelekea katika zahanati ya kijiji na nusu saa baadaye tulikuwa tumeshawasilj,Helena aliingizwa zahanati na madaktari kuanza kuhangaika kuokoa maisha yake.

Masudi,mama yake Helena pamoja na mimi tulibaki tukisubiria nje,muda wote Masudi alikuwa akinitazama kwa jicho la hasira sana,huku mara chache Mama Helena akinitupia jicho la lawama.

Mwisho nilishindwa kuvumilia nikamvuta Masudi nje na kumuuliza kilichotokea,Masudi akaniambia ya kwamba Helena alikunywa sumu ya kuulia wadudu katika mahindi na kabla hajapoteza fahamu alikuwa akilitaja jina langu huku akilia.

Moyo wangu ukaingia ubaridi,nikajikuta nikikaa upenuni mwa zahanati huku nikijishika kichwa changu,niliumia sana nikabaini ya kwamba isingewezekana kumwacha Helena kwa wakati huo,nilikuwa nikimpenda kuliko kitu chochote na huenda ikahatarisha uhai wake zaidi.

Nikajikuta nikiapa ya kuwa endapo atapona sitokuwa tayari kuhatarisha uhai wake tena na wala sitokuwa tayari kuruhusu kuukatili moyo wangu kiasi hiki.

Masudi alinijulisha ya kwamba yeye alifahamu hilo na alijua kuwa nami nilifahanu uhusiano wa kibinamu uliopo baina yetu,akaomba radhi kwa kuniambia ya kwamba yeye anaamini ya kwamba ubinamu sio kikwazo na hiyo ndiyo imani yake ndio maana hakusita kunisaidia juu ya Helena.

Baada ya mazungumzo marefu Masudi aliaga ya kwamba anarudi nyumbani kujiandaa kwani kesho yake alfajiri anaondoka kwenda kibaruani Mafinga.

Hadi kufikia saa sita usiku Helena alikuwa ameamka tayari ingawaje bado hali yake haikuwa nzuri sana lakini ilikuwa ni nafuu zaidi,sikutaka anione nikaagana na mama yake kwa ahadi ya kwenda asubuhi.

Baada ya siku tatu Helena aliruhusiwa kutoka,niliitumia siku hiyo kwenda naye Mafinga ambapo nilimfanyia manunuzi ya nguo na vikorokoro vingine,niliitumia siku hiyo kumuomba radhi na kila mmoja aliahidi kuwa hatoweza kumwacha mwenzie kwani tulipendana sana.

Baada ya kurudi kijijini kuanzia siku hiyo hatuficha kitu na habari zikasambaa kwa kasi kuhusiana na uhusiano ule.

Nakumbuka zilikuwa zimesalia siku tatu kabla ya safari ya kurudi Morogoro,nilipokea simu kutoka kwa mtu aliyejitambulisha kama mjomba yake Helena,alijitambulisha kama Juakali Mtavangu.

Akanieleza kuhusiana na tetesi za kuwa na mahusiano na binamu yangu na kuniambia kama ni kweli akasisitiza na kunionya ya kwamba ananipa wiki moja tu mahusiano hayo yawe yamekufa vinginevyo nisidhubutu kumtafuta tena.

Baada ya simu ile kukatika nikaipuuza na kuendelea na masuala mengine kwani sikuwa na wazo la kumwacha Helena kwanza niliamini sitoweza.

Hatimaye niliagana na Helena kwa ahadi ya kuja kumchukua siku za usoni,ilikuwa ni siku ya huzuni sana hatimaye nayo ikapita na safari ikawadia.

Tuliingia Morogoro saa kumi na moja jioni,saa mbili usiku ilinikuta nikiwa nyumbani kwangu Mbuyuni.

**********************

Kwa vile likizo yangu kazini ilikuwa imekwisha kesho yake ilinikuta nikiwa ofisininikijumuika na wafanyakazi wenzangu.

" Aloyce! Aloyce! Aloyce!"

Niligutuka na kuangaza macho huku na huko,ofisi hii ilikuwa na wafanyakazi watatu tu na wote walikuwa bize na kompyuta zao,nikachukulia labda huenda nilikuwa nimesinzia tu.

"Aloyce! Aloyce! Aloyce!" Sauti niliyoibaini wazi kuwa ni ya Helena niliisikia tena,nikaangaza macho na kukuta bado kila mtu yupo bize na kazi.

"Alfred" nikamuita mfanyakazi mwenzangu aliyekuwa ameketi meza ya pembeni yangu.

"Yeah Aloyce" aliitikia huku akisitisha alichokuwa akikifanya.


"Umesikia mtu yeyote akiniita?"


"Hapana Aloyce hapana"


"Aaah samahani bwana labda ni mawazo tu Alfred"


Alfred alicheka na kuendelea na kazi,nikaitwaa simu yangu na kumpigia Helena,hakuwa hewani!


"Aloyce nakufaaa" sauti ya Helena ilisikika safari hii kwa nguvu zaidi,nikashituka na kusimama kwa kasi kiasi kwamba wenzangu wakageuka kunitazama kwa mshangao.


"Alfred ina maana hamsikii chochote hapa" nikauliza huku nikijifuta kijasho chembamba kilichokuwa kikinitoka.


"Hapana kaka kwani vipi mwenzetu"


"Alooooyce" sauti ya Helena ilisikika tena,nikaanza kuhaha huku na huko nisielewe nilichokuwa nikikitafuta,nikatoka ofisini kwa kasi lakini kabla sijaufikia mlango mkubwa wa kutokea ofisini,Alfred akiongozana na wafanyakazi wengine wawili walinidaka kunizuia.

"Unaenda wapi Aloyce muda wa kazu bado" Stephano moja kati ya wafanyakazi wenzangu aliniuliza huku wakiwa wamenishika mikono.


"Niacheni niacheni nawaambia" nilifoka.


"Mfungeni kamba ni malaria imempanda kichwani huyu" Alfred aliongea huku wakiniangusha na kunikandamiza sakafuni.


"Niacheni Alfred niacheni nitaua nitaua mtu niacheni" nilifurukuta kujinasua bila mafanikio.


"Huyu kachanganyikiwa kawa chizi huyu" Salum aliongea huku akivua tai na kuanza kunifunga mikono.


"Mimi sio chizi! mimi sio chizi!" nililalalama kwa kelele lakini hakuna aliyenielewa...


JE! ALOYCE AMEPATWA NA NINI? TUKUTANE SEHEMU YA TANO.
 
BINAMU YANGU-05 (FINAL EPISODE)

ROBIN MIHO

0776741545


Nilibebwa msobemsobe hadi kwenye gari ya Alfred na kuwahishwa hospitali,muda wote sauti ya Helena iliendelea kuniita akidai anakufa.


Hali hii ilinipelekea kuwehuka kabisa,baada ya vipimo vya hospitali ilionekana ya kwamba nilikuwa ni mzima kabisa,ikabidi wazazi wangu wajulishwe juu ya yaliyonisibu.


Baba na mama walifika na kunikuta nikiwa nimefungwa kamba mikononi na miguuni na kushikizwa kwa mikanda kitandani.


Mara baada ya kumuona mama yangu nikapiga kelele kumtaka mama anifungulie.


""mama nifungulie mimi sio chizi..mama nifungulieee mimi mzimaa" nilipiga kelele kwa hasira.


Mama alibaki akinitazama huku akilengwa lengwa machozi,sekunde chache baadaye mama alianza kulia,hawakukaa sana wakatoka kwenda kuonana na daktari.


Baada ya muda walirudi wakiwa wameongozana na daktari,baba akanifuata na kunifungua kamba nikaketi kitako,kisha baba akaniuliza kinachonisibu,kabla sijamjibu nikasikia sauti ya Helena akiniita.


Safari hii sauti ilitokea mlangonj,nikageuka kutazama mlangoni na kumuona Helena akiwa katika muonekano wa ajabu,alikuwa kavalia gauni kubwa jeupe,nywele zake zilikuwa ni chafu na ngozi yake ilijaa ukurutu,kucha zilikuwa ni ndefu na mkono wake wa kulia akishika kisu kikubwa akiwa kajawa na tabasamu.


Ghafla tabasamu likamyeyuka akainua kisu na kuanza kunijia kwa kasi,nikazunguka mgongoni kwa baba na kutoka mbio huku nikipiga kelele za kuomba msaada.


Mbio hizo zilinifikisha hadi round about ya Msamvu,nikasimama huku nikitweta nikatazama huku na huko,watu walikuwa wakinikodolea macho ya mshangao,nikajitazama nilivyochafuka vumbi,nilikuwa pekupeku.

Nikaita bodaboda anipeleke nyumbani kwangu Mbuyuni,dakika kumi zilinikuta nikiwa nyumbani kwangu nikinlipa bodaboda ujira wake.


Nikazama ndani kwa mashaka,sikuwa na simu!,nikajimwagia maji na kwenda kwa jirani yangu Mathius aliyekuwa na duka kubwa la rejareja pembeni tu ya nyumba yake,nikaazima simu na kuwapigia wazee wangu kuwa nipo nyumbani nikawaomba waje haraka,nikabaki palepale dukani nikipiga stori mbili tatu na Mati nilikuwa naogopa kukaa ndani peke yangu.


Baada ya dakika kadhaa gari ya baba ilipaki,nikajiinua na kwenda kuwalaki kwa huzuni,tukaongozana ndani.


Sikuwa na cha kuwaficha,nikawaeleza kila kitu kuanzia kuonana na Helena hadi maneno ya mzee Juakali,mjomba wa Helena.

Baada ya kunisikiliza kwa makini,wote tulibaki kimya tukitafakari,hatimaye baba akavunja ukimya.


"Jiandae twende MUfindi" akizungumza kwa amri.


"Saizi?" Nikauliza huku nikiitupia macho saa ya ukutani,ilikuwa saa kumi na dakika kumi na tano alasiri.


"Ndio sasa hivi"

Sikuwa na cha kusema,nikatwaa nguo chache tukatoka hadi Uhuru ambapo walijiandaa,saa kumi na dakika arobaini tulikuwa tunaiacha Morogoro,garini tukiwa watu watatu,mimi,mama na baba aliyekuwa dereva.


Saa mbili usiku tulikuwa Ilula,baba akaomba nimpokee kwani alijisikia uchovu,nikampokea na safari ikaendelea.


Dakika kumi na ushee kituko cha ajabu kilitokea,miguu miwili iliyoonekana kuanzia unyayoni hadi magotini ilikatiza barabarani ikivuka kutoka upande wa kulia kuelekea wa kushoto na kutokomea vichakani.


Nilishituka na kupunguza mwendo,nikawatupia macho wazee,baba alikuwa ameshasinzia vivo hivyo kwa mama.


Nikawaacha na kuendelea na safari huku nikiwa na wasiwasi,baada ya dakika kadhaa nilirudi hali ya kawaida,nikachochea gari.


Nikiwa katika mwendo wa wastani kph90 nikiimaliza Ruaha chini,nilimuona Helena akiwa kavalia mavazi yale yale niliyomuona nayo Hispitali amesimama katikati ya barabara akinitazama kwa huzuni.


Machozi ya mekundu yalianza kumchuruzika,nami nikakaza mikono na kuchochea gari nikiwa hatua tano tu kumfikia moyo wangu ulisita kabisa,ni kweli nilimpenda sana Helena.


Nikapiga kelele huku nikimkwepa "Helena piiish..." Sikunaliza kauli yangu,kishindo kikubwa kilisikika.


Gari ikauvaa ukingo wa barabara na kurukia korongo,ilibiringika mara tano na kujipigiza kwenye gema,gari haikutamanika,nikatoka garini kwa taaba,mguu wangu wa kulia ulikuwa umevunjika,jicho la kushoto halikuwepo!


Nikajaribu Kuwatazama wazazi wangu,hawakuwepo,sauti ya mtu akicheka tokea nyuma yangu ilinigutusha,nikageuka na kukutana uso kwa uso na Helena akiwa anatafuna kipande cha nyama mbichi.


Miguuni pake walilala wazazi wangu wakiwa hawana uhai,miili yao haikutamanika wala kutambulika ilikuwa na majeraha kila mahali ilitisha sana.


"Aloyce" sauti nzito ya kiume ilisikika ikitokea nyuma ya Helena,niliitambua sauti ile,ni sauti ya mzee Juakali,mjomba wake Helena.


Tokea kizani nyuma ya Helena aliibuka mzee Juakali akiwa kashikilia shoka,akalishusha kwa kasi na kujikita shingoni kwa Helena,nilimuona Helena akitapatapa kupigania uhai na kutulia tuli,mauti yalishamchukua!


"Aloyce una kazi nzuri,elimu nzuri,maisha mazuri na wazazi wema kama hawa" akanyooshea kidole miili ya wazazi wangu.


"Lakini kwa ujinga wako wa kutokujua ama kwa dhahiri ukachagua kulala na binamu yaki,damu yako,umetutia aibu na laana tutawatazama vipi mababu zetu huko kuzimu?" Akapiga hatua mbili kunifuata akasita,akarudi kulinyofoa shoka mwilini mwa Helena.


Akanigeukia na kuendelea
"Lakini tamaa yako ya kuzini na binamu yako imekufanya ukose vyote,umkose kila kitu ukiwemo uhai wako,gharama za dhambi hii ni damu ya wazazi wako,damu ya Helena na damu yako wewe"


Akapiga hatua taratibu kunifuata huku akiwa amelishikilia shoka lake barabara kwa mkono wa kulia,kuona vile nikajaribu kukimbia lakini mguu wangu wa kulia ukanisaliti,nikajikuta napiga mweleka bila kupenda.


Akanifikia pale nilipokuwa nimeangukia huku nikitweta kwa maumivu na kupiga kelele za kuomba radhi,akanitazama kwa sekunde chache,akainua shoka na kulishusha kwa kasi kichwani pangu..!


"Mama nakufaaaaa" nikapige kite huku nikikurupuka usingizini,jasho lilikuwa linanitoka na mapigo ya moyo yakinienda mbio.


Ilikuwa ni saa kumi na moja na robo alfahiri ni jana tu nilikuwa nimetoka Mafinga na leo ilikuwa ni siku ya mwisho ya likizo yangu nikitakiwa kuripoti kazini kesho yake.


"Hii ni ndoto mbaya sana,kama kutembea na binamu yangu malipo yake ndio haya hapana kwa kweli,potelea mbali sitaki tena,kwanza Juakali alinipa wiki moja na leo ndio kwanza siku ta kwanza basi na jana ndio mwanzo na mwisho kuwasiliana na Helena" nikaongea.

"Helena mwenyewe kwanza sio mzuri" nikajisemea kwa woga.


Nikaitwaa simu yangu na kutoa laini niliyoitumia kuwasiliana na Helena nikaivunja vunja kisha nikaingia maliwatoni.

*******MWISHO*******


HAPA NDIPO MWISHO WA RIWAYA YETU FUPI YA "BINAMU YANGU" KUNA MAMBI MENGI MAZURI YANAFUATIA HUSUSANI KWA WAPENZI WA RIWAYA FUPI ZA KUSISIMUA.

JE! KUNA MAFUNZO GANI UMEJIFUNZA KUPITIA RIWAYA HII?
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom