The Genius
JF-Expert Member
- May 29, 2018
- 820
- 2,070
Sherehe ya mwisho ya bibi Susana Benjamin Mmary imefanyika nyumbani kwake huko Old Moshi Kidia, baada ya BWANA kumuita akiwa na umri wa miaka 131. Ni bahati mbaya kwamba taasisi zinazotunza rekodi za dunia haziangalii sana Afrika, lakini kabla hajafariki alipaswa kuwa ndiye mwanadamu mwenye umri mkubwa zaidi (the oldest living person).
_
Dunia inamtambua Kane Tanaka wa Japan kuwa mwanadamu mwenye umri mkubwa aliye hai kwa sasa (The Oldest Living person). Kane alitimiza miaka 117 tarehe 05 January mwaka huu.
Lakini Susana alitimiza miaka 131 March 23 mwaka huu. Rekodi ya kuzaliwa kwake ilipatikana katika kitabu cha kumbukumbu ya kanisa kilichoachwa na wamisionari wa kwanza wa Kijerumani waliokuja kueneza injili Kaskazini mwa Tanganyika na kujenga kituo cha kwanza cha misioni ya Kidia mwaka 1884.
Katika picha waliobeba maua ni wajukuu zake Susana ambao nao wana wajukuu na wengine wana vitukuu. Mtoto wa pili wa Susana alifariki mwaka 1999 akiwa na umri wa miaka 82 (angekua hai leo angekua na miaka 103). Mjukuu wake mkubwa ana mika 78.
Jambo la kumtukuza Mungu ni kwamba pamoja na umri wake mkubwa bado alikuwa na uwezo wa kusikia, kuona na kuzungumza. Pia akili yake ilikuwa timamu hata katika uzee wake aliweza kukumbuka na kusimulia baadhi ya matukio ya zamani. Alikuwa bibi mcheshi na mwenye tabasamu wakati wote.
Old Moshi imepoteza mtu muhimu sana katika historia. Dunia imempoteza mwanadamu mwenye umri mkubwa zaidi, na Kanisa limempoteza mmoja wa wakristo wa mwanzo kabisa nchini. BWANA alitoa na BWANA ametwaa jina lake lihimidiwe.
Malisa GJ
UKWELI KUHUSU UMRI WAKE
Kutokana na habari ya bibi Susana Benjamin Mmary, kuna watu wameuliza kuhusu taarifa za tarehe za kuzaliwa kwake zimepatikana wapi kutokana na ukweli kwamba wazee wengi wa zamani hawakujua miaka waliyozaliwa bali walitunza rekodi kwa kumbukumbu za matukio makubwa yaliyotokea wakati huo. Kuhusu bibi Susana rekodi zote zipo wazi. Hii sio hadithi ya kubuni.
Wakati wamisionari wa Kianglikana kutoka Uingereza wa shirika la Church Missionary Society (CMS) wanafika Tanganyika mwaka 1848 waliweka kituo chao maeneo ya Kitimbirihu (Moshi). Baada ya Berlin Conference mwaka 1984/85 Tanganyika ilipewa Ujerumani na hivyo Waingereza wa CMS wakaondoka kwenda Kenya na kupeleka injili huko maana Kenya iligawanywa kwa Waingereza.
Kwa kuwa Tanganyika ilipewa Ujerumani wakaja wamisionari wa Kilutheri akina Emil Mueller, Franz Boohme na Dr.Bruno Gutman kutoka Ujerumani. Wakahamishia kituo hicho cha misioni kutoka Kitimbirihu kwenda kijiji cha Kidia mwaka 1885. Hii ni kwa sababu kijiografia Kidia ndio ilikua katikati ya eneo lote la Old Moshi kuanzia Mbokomu mpaka Sango. Na hata jina "kiidi- aa" maana yake ni hapa ni katikati.
Kituo hicho cha kwanza cha uinjilishaji eneo la Kaskazini mwa Tanganyika kikaanza kutoa huduma za kiroho, akina Dr.Gutman wakihubiri neno la Mungu na kubatiza watu. Waumini wa kwanza kubatizwa eneo hilo ni Tomaso Ringo na Samueli Tenga waliobatizwa tar 21 Februari mwaka 1892. Miaka miwili baadae 1894 bibi Susana nae akabatizwa akiwa na umri wa miaka mitano.
Majina ya Wakristo hao wa mwanzo kubatizwa yametunzwa kwenye nyaraka zilizoachwa na wamisionari hao. Nimejulishwa na familia ya akina Mmary kwamba mwaka jana (2019) kitukuu wa Dr.Gutman alifika Kidia na alimtembelea bibi Susana ambaye alibatizwa na babu yake. Bibi Susana alimhadithia mambo mengi ya nyakati hizo za kale wakati injili inafika Afrika.!
Malisa GJ