BC:Magazeti ya Udaku Yanajenga au kubomoa Jamii Ya Kitanzania??

TandaleOne

JF-Expert Member
Sep 4, 2010
1,644
709
Mjadala kuhusu mchango wa magazeti ya “Udaku” katika kujenga au kubomoa jamii una historia ndefu sana. Ni mjadala ambao ulikuwepo,upo na utaendelea kuwepo labda mpaka hapo itakapotokea kwamba maisha na watu watapotea katika sura ya ulimwengu.

Binadamu anabakia kuwa kiumbe mdadisi anayependa kupata habari,kujua kinachoendelea na pia hata kujua alichokifanya jirani yake jana usiku kama sio alichokifanya au anachokifanya mkuu wa nchi awapo mapumzikoni.

Nchini Tanzania, baada ya mapinduzi ya habari na mawasiliano,yaani baada ya kuvuka kile kipindi ambacho kulikuwa na magazeti matatu na kituo kimoja cha redio, paliibuka magazeti ambayo baadaye tumekuja kuyaita “magazeti ya udaku”. Hapo ndipo nasi tulipoingia rasmi kwenye mjadala wa; Je magazeti haya yana mchango gani katika jamii? Yanajenga au yanabomoa?

Hivi karibuni tulipata fursa adimu ya kufanya mahojiano na Abdallah Mrisho Salawi (pichani) Meneja Mkuu wa kampuni inayoongoza kwa uchapishaji wa magazeti ya “udaku” nchini Tanzania ya Global Publishers.Pamoja na mambo kadha wa kadha kumhusu yeye binafsi, Abdallah Mrisho anajaribu kueleza kuhusu kazi zao kama wanahabari na mchango wao au ubomoaji wao wa jamii.Hiyo itatokana na unavyoona wewe hasa baada ya kusoma alichotuambia Abdallah Mrisho.Pia anatoa ushauri muhimu kwa jamii hususani vijana kuhusiana na majanga kama umasikini,ukosefu wa ajira,ukimwi nk.Fuatana nasi katika mahojiano yafuatayo;


BC: Unaweza kutuambia historia ya maisha yako kwa kifupi? Ulizaliwa wapi,ukasomea wapi nk


AM: Nilizaliwa February 24, 1968, Bukene Tabora, nikiwa mtoto wa nne, kati ya watoto 9 wa Mzee Salawi. Katika familia yetu tulizaliwa jumla ya watoto 10, tupo hai 8, wavulana 5, wasichana 3. Wawili walishatangulia mbele ya haki.(Mungu awarehemu).

Elimu yangu ya msingi niliipata Bukene Primary School, kisha Ngerengere Secondary School ambayo inamilimilikiwa na Jeshi la Wanannchi wa Tanzania (JWTZ) kikosi cha anga, ambacho ndicho kinadili na ufundishaji wa marubani wa ndege za kivita nchini tanzania. Nilipata Stashahada yangu ya Business & Sales Letter Writing kutoka Chuo cha International Correspondence Schools cha Glasgow, UK mwaka 1993.


BC: Ilikuwa vipi na lini ulipoamua kuingia kwenye masuala ya habari?


AM: Kilichoniingiza kwenye media naweza kusema ni passion na niliingia kupitia mgongo wa picha. Nilianza kupenda kupiga picha tangu nikiwa shuleni ambako nilikuwa napiga picha wanafunzi wenzangu.Baadaye hata nilipoanza kazi niliendelea kupiga picha mitaani, kwenye harusi na function mbalimbali za kijamii.Huko ndiko nikajikuta pia napiga picha za habari ambazo ndizo zilizonikutanisha na GLOBAL PUBLISHERS LTD ambayo wakati huo ilikuwa ikijulikana kama SAFEGUARD TANZANIA LTD ikiwa ina magazeti mawili, Uwazi na Kiu na baadae Ijumaa.

Pamoja na kuwa hivi sasa ni Kiongozi wa kampuni, naendelea na upigaji picha kwani ndiyo fani yangu na nimeendelea kujifunza kila wakati na hata kusoma On Line sanaa mbalimbali za upigaji picha (Art of Photography). Chuo cha New York Institute of Photography (www.nyip.com) kimenipa maarifa mengi ya fani hii. Baadhi ya kazi zangu unaweza kuziona hapa:www.mrisho.faithweb.com. Pia nimejifunza na kusomea vitu vingi vya Information Technology (IT), Ghaphics na Printing.


BC: Kabla ya hapo uliwahi kufanya kazi zingine mbali na uandishi na masuala ya habari kwa ujumla?Ilikuwa ni kazi gani?


AM: Kabla na baada ya kuingia kwenye media nikiwa kama mpiga picha na mwandishi wa habari za entertainment, nilikuwa nafanyakazi katika kampuni nyingine. Nilianza kufanyakazi na Car & General Trading yenye ofisi zake pale Azikiwe Street karibu na Posta mpya nikiwa upande wa kiwandani kule Chang’ombe Industrial Area ambako nilikuwa Salesman. Jamaa walikuwa wana dili na utengenezaji na uuzaji wa matairi ya magari.

Hapo nilifanya kazi kwa miaka kama 5, (1990-95), then nikahamia kampuni ya K. J. Motors mwaka huo wa 95 mwishoni kama sikosei, enzi hizo kampuni hii ikiwa inaongoza nchini kwa uuzaji wa magari aina ya Isuzu, Honda na pikipiki aina ya Honda Excel na 110 trail. Niliajiriwa kama Administration Officer.


BC: Ni mwandishi gani wa habari, vitabu au makala nchini Tanzania anayekuvutia zaidi? Kwanini?


AM: Naweza kuonekana namfagilia bosi wangu, lakini nasema ukweli tu kwamba mwandishi wa vitabu anayenivutia ni Shigongo. Sababu kubwa ni jinsi ambavyo anaweza kuandika kila siku hadithi na zikapendwa na wasomaji wake. Hebu fikiria, Global ina jumla ya magazeti sita ambayo yanatoka kuanzia Jumatatu hadi Jumamosi na kila gazeti lina hadithi ya ukurasa mmoja.

Katika hadithi hizo, kila moja inajitegemea isipokuwa magazeti mawili ambayo hadhiti zake zinaendelea kutoka toleo moja hadi jingine. Lakini kikubwa zaidi ni jinsi anavyoweza kuandika mwendelezo wa hadhithi zake ambao unawavutia sana wasomaji wake.Huwa najiuliza points anapata wapi nashindwa kupata jibu. Naona ana kipaji cha kipekee ambacho si watu wote waweza kuwanacho. Amekuwa akiandika hadithi hizo karibu miaka kumi sasa na hajawahi kurudia stori.

Wengine wanafikia hatua ya kudai kuwa anatafsiri kutoka novel za kiingereza. Hana sababu ya kufanya hivyo.Shigongo ana kipaji cha kipekee cha kuandika hadithi, nafikiri comments za wasomaji wake wa kwenye mtandao zinajieleza, wanaguswa sana na hadithi zake! Mwenyewe hutuambia kuwa kuandika hadithi haoni kama ni kazi ngumu bali ni kama burudani, anapoandika huwa ana enjoy sana!

Kwa upande wa waandishi wa habari, naweza kusema navutiwa sana na Absolom Kibanda, mwandishi na mhariri mkuu wa gazeti la Tanzania Daima. Nampenda jamaa kwa sababu ana aina fulani ya uandishi wa habari ambao unatakiwa nchini, ujasiri usiokuwa na woga. Scoop ya kifo cha Balali nafikiri ni ushahidi tosha wa ujasiri wake!

BC: Ni jambo gani unalipenda zaidi kuhusu maisha yako kama kiongozi wa kampuni ya media na mwandishi wa makala? Lipi usilolipenda?


AM: Napenda ninapoona kampuni yangu inafanya jambo ambalo linainufaisha jamii na kubadilisha maisha ya mtu. Pia napenda pale ninapoandika makala zangu (You are what you eat) ambazo wasomaji zinawasaidia kuokoa maisha yao kwa kwa njia moja ama nyingine na kufikia hatu ya kunipigia simu na kuthamini kile nilichokiandika. Hali kadhalika kwa upande wa habari za entertainment, napenda kuandika kuhusu habari nikiwa wa kwanza kuiandika na kuihabarisha jamii.

Nikiwa kiongozi wa kampuni ya habari, sipendi kuona mtu yoyote anaonewa. Pale ninapoletewa malalamiko na msomaji akilalamika kuonewa kwa kuandikwa vitu ambavyo hakuvifanya huwa nakosa amani ndani ya nafsi yangu.Siku zote tunajaribu kusimamia uwazi na ukweli, sipendi kumuonea mtu kwa kitu cha uongo.


BC: Hivi sasa wewe ni meneja katika kampuni ambayo karibuni magazeti yote yanaandika habari ambazo zinazoitwa za “udaku”. Kwa maoni yako nini mchango wa magazeti ya “udaku” katika kuijenga au kuibomoa jamii?


AM: Mchango wa magazeti haya, ambayo sasa ‘yanaitwa magazeti pendwa’ kwa jamii ni mkubwa sana katika kuijenga zaidi kuliko kuibomoa. Japokuwa jamii hukasirika pale inapokosolewa kwa kwenda kinyume na maadili yetu na hiyo ni kawaida kwa binadamu yoyote, kwani siku zote ukweli huuma.

Lakini kupitia magazeti haya watu wameweza kupata haki zao walizokuwa wamedhulumiwa. Kupitia magazeti haya watu wamepona magonjwa ambayo yangeweza kuondoa uhai wao.Kupitia magazeti haya watoto wa masikini wengi wamesoma na wengine wanaendelea kusoma kwa kulipiwa ada na kampuni.Kupitia magazeti haya watu wengi wamepewa misaada ambayo imeweza kubadili maisha yao, achilia mbali familia za wafanyakazi na wauzaji wa magazeti haya walioko nchi nzima wanavyoweza kumudu maisha yao ya kila siku kwa kutegemea uuzaji wa magazeti hayo.


BC: Kama sikosei, changamoto moja kubwa ambayo lazima mnakabiliana nayo kila mara(kama sio kila siku) ni lawama mbalimbali kwamba magazeti ya udaku yanapotosha jamii hususani vijana na watoto na kwa maana hiyo kuchangia katika kuporomoka kwa maadili katika jamii. Je unakubaliana na lawama hizi? Kama hukubaliani unadhani lawama kama hizi zinatokana na nini?


AM: Hatukubaliani na lawama hizo.Kama nilivyojibu hapo juu, jamii wakati mwingine hukasirika pale inapokosolewa hata kwa jambo ambalo kweli imelifanya. Magazeti yetu siyo ya kulaumiwa, wanaopaswa kulaumiwa katika kupotosha vijana na watoto ni hao wanaofanya mambo yanayokwenda kinyume na jamii hadharani, kosa letu lisiwe kukemea kwa kuandika ukweli na kila mtu akajua.

Siku zote tunapoandika habari ya kashfa au ya ngono iliyofanywa na mwanajamii, hususan wale ambao wanaaminika kuwa ‘kioo cha jamii’, lengo letu huwa ni kukemea tabia hiyo ili isiendelee na kuonekana kama kitu cha kawaida kwa vijana na watoto.

Na hili limesaidia sana kubadili tabia za watu wengi, hasa hao ‘kioo cha jamii’ ambao zamani walikuwa wanaweza kufanya ufuska wa aina yoyote hadharani bila woga. Kadri siku zinavyokwenda ni wachache sana wanaodiriki kufanya ufuska hadharani kwani wengi wao wanaogopa kuumbuka.

Inaendelea hapa;
MAGAZETI YA UDAKU:YANAJENGA AU KUBOMOA JAMII? - BongoCelebrity
 
...magazeti ya aina hii yapo mahsusi kudumaza au kutojenga uwezo wa watanzania kufikiria mambvo ya msingi kwa maisha yao na taifa lao maana habari za humo ni kigogo X kafumaniwa na mke wa mtu.......X na X wakutwa laivu wakila denda.......n.k. hata serikali inajua hilo ndio maana hutamsikia Mkuchika akiyafungia au kyakemea hata kama wataandika the same story ambayo Mwanahalisi au Raia Mwema au Kulikoni wataandika. mbaya zaidi ni magazeti yanayopendwa na teens ambao naamini kamwe hawatakuwa na muda wa kusoma investigative au consructive news!!
 
...magazeti ya aina hii yapo mahsusi kudumaza au kutojenga uwezo wa watanzania kufikiria mambvo ya msingi kwa maisha yao na taifa lao maana habari za humo ni kigogo X kafumaniwa na mke wa mtu.......X na X wakutwa laivu wakila denda.......n.k. hata serikali inajua hilo ndio maana hutamsikia Mkuchika akiyafungia au kyakemea hata kama wataandika the same story ambayo Mwanahalisi au Raia Mwema au Kulikoni wataandika. mbaya zaidi ni magazeti yanayopendwa na teens ambao naamini kamwe hawatakuwa na muda wa kusoma investigative au consructive news!!

Naomba kuuliza,hivi haya magazeti hayapo katika nchi zilizoendelea????
 
kuna mtu pale GP anaitwa Issa Mnali na Richard Bukosi hawa jamaa wadaku sana wasikuone mahali wanakuvizia wakupige picha yaani wanaingilia privacy za watu sana sipendi aina hii ya uandishi wa kidaku
 
kuna mtu pale GP anaitwa Issa Mnali na Richard Bukosi hawa jamaa wadaku sana wasikuone mahali wanakuvizia wakupige picha yaani wanaingilia privacy za watu sana sipendi aina hii ya uandishi wa kidaku

Ila nasikia kuna wengine wanakubali na wanalipwa for that.
 
Back
Top Bottom