Baraza la madiwani kuamua hatima ya umeya Arusha

Analogia Malenga

JF-Expert Member
Feb 24, 2012
5,000
9,861
Arusha. Baraza la Madiwani wa Jiji la Arusha linatarajia kukutana hivi karibuni kuamua hatima ya nafasi ya meya wa jiji hilo, baada ya Calist Lazaro kujiuzulu nafasi hiyo na kujiunga na CCM.

Lazaro alijiunga CCM juzi na kupoteza nafasi zake za udiwani, umeya, uenyekiti wa mameya na madiwani wa Chadema na ujumbe wa kamati kuu ya chama hicho kikuu cha upinzani nchini.

Akizungumzia uamuzi huo jana, Kaimu Mkurugenzi wa Jiji la Arusha, Sifaeli Kulanga alisema baada ya Lazaro kujiuzulu, hatima ya nafasi ya meya itajulikana hivi karibuni kupitia kikao cha Baraza la Madiwani na maelekezo yatakayotolewa na mkurugenzi wa jiji.

Kufuatia uamuzi wa Lazaro, Halmashauri ya Jiji la Arusha imebaki na madiwani 33, kati yao 25 wakiwa wa Chadema na wanane CCM.
Katika Uchaguzi Mkuu wa 2015, CCM ilipata diwani mmoja wa kuchaguliwa katika jiji hilo lakini baadaye kwa nyakati tofauti madiwani saba walijiuzulu Chadema na kujiunga na chama hicho tawala ambako waligombea na kuchaguliwa tena.

Kulanga alisema kwa sasa nafasi ya meya inakaimiwa na Poul Matthysen, diwani wa Moshono (Chadema) ambaye pia ni naibu meya.
“Kwa kuwa meya aliondoka hapa ofisini kikazi, alimwachia kiti chake naibu meya ambaye hadi leo (jana) anatumia ofisi ya meya, ataendelea kukaimu lakini kujua nini kitatokea baadaye, itabidi tumsubiri mkurugenzi wa Jiji, Dk Hamis Madeni ambaye yupo safari ya kikazi,” alisema.

Kulanga ambaye pia ni mwanasheria wa Jiji alisema mkurugenzi wa jiji alikuwa kikazi Dar es Salaam na Meya Lazaro na hukohuko ambako alimkabidhi barua ya kujiuzulu kwake.

“Hatujui ameandika nini, tungojea barua zije na mkurugenzi atatoa taarifa rasmi na baadaye sheria zitapitiwa ili kutoa fursa kwa Baraza la Madiwani kukutana kufanya maamuzi kama watachagua mwingine,” alisema.

Diwani wa Kata ya Ngarenaro, Isaya Doita alisema kanuni zinawaruhusu kufanya uchaguzi wa kujaza nafasi hiyo, lakini pia inawezekana naibu meya akapandishwa na kuwa meya na nafasi yake kufanyiwa uchaguzi.

“Yote haya yatategemea mwongozo kutoka kwa mkurugenzi wa jiji utakavyopitishwa na madiwani,” alisema.

Kuhusu nafasi ya diwani, alisema sheria ipo wazi kwa sasa, kwamba miezi saba kabla ya kuvunjwa Baraza la Madiwani, hakuna nafasi ya kufanyika uchaguzi katika Kata ya Sokoni One ambako Lazaro amejiuzulu.

Uamuzi wa Lazaro umeibua maoni tofauti ya wananchi wa Arusha kuhusu sababu za uamuzi huo.

Mkazi wa Sombetini, Frednand Amath alisema kujiuzulu kwa Lazaro ni mwendelezo wa viongozi kutoka kambi ya upinzani kujiunga na CCM kutokana na mazingira ya kisiasa kutokuwa sawa na hivyo kuona aende upande ambao atakuwa na uhakika wa ushindi.

“Si jambo lililonishangaza kusikia Lazaro ameondoka Chadema kwa sababu ametathimini mambo mengi likiwamo la chama chake kutoshiriki uchaguzi wa mitaa mwaka huu na amehisi wanaweza wasishiriki uchaguzi mkuu mwakani na hivyo kukosa kuwahudumia wananchi wake,” alisema Amath.

Siah Augustine, mkazi wa Levolosi alisema inashangaza kuona kiongozi anaomba nafasi ya kuwatumikia wananchi kisha anajiuzulu na kuomba apewe nafasi hiyo hiyo bila vyombo vya kupambana na rushwa kuchunguza kwa kina sababu za msingi.

Alisema ni haki yake kikatiba lakini haiakisi utawala wa sheria na matumizi sahihi ya rasilimali kwani utaratibu wa viongozi kuhama vyama na kambi zao mara nyingi unafanyika wakati wa maandalizi ya chaguzi.

Hata hivyo, alisema haoni kama Chadema na kambi ya upinzani vitaathirika kwa viongozi wachache kuhama.


CHANZO: Mwananchi
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom