Bajeti kuu mbadala yapendekeza mfumo mpya wa uchumi Tanzania

CHADEMA

JF-Expert Member
Apr 13, 2013
488
2,468
MAONI YA KAMBI RASMI YA UPINZANI BUNGENI KUHUSU HALI YA UCHUMI WA TAIFA, MPANGO WA MAENDELEO WA TAIFA NA MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI YA SERIKALI KWA MWAKA WA FEDHA 2019/2020
Inatolewa chini ya Kanuni ya 99(9) ya Kanuni za Kudumu za Bunge, Toleo la Januari, 2016
UTANGULIZI
Mheshimiwa Spika, hii ni bajeti ya nne ya Serikali hii ya awamu ya tano ambapo imebaki bajeti moja tu ya mwaka wa fedha 2020/2021 kabla Serikali hii haijamaliza muda wake wa kuwa madarakani. Hata hivyo, pamoja na kwamba imebaki takriban miaka miwili Serikali hii imalize mhula wake wa miaka mitano madarakani, utekelezaji wa bajeti zilizotangulia umekuwa ni wa kusuasua jambo ambalo limeathiri sana sekta nyingi za uzalishaji na hivyo kupunguza kasi ya ukuaji wa uchumi na maendeleo ya watu.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa mara zote Kambi Rasmi ya Upinzani imekuwa ikiishauri Serikali hii juu ya masuala mbalimbali ya kiuchumi, kisiasa na kijamii kwa ajili ya ustawi wa wananchi na mustakabali mwema wa taifa letu; na kwa kuwa mara nyingi Serikali imekuwa ikiubeza ushauri huo na kufanya mambo kwa sifa au kwa kiburi cha madaraka bila kuzingatia ushauri wa Bunge; safari hii Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni itajikita zaidi katika kutoa misimamo ya kisera katika sekta za kiuchumi, kijamii na kisiasa ili watanzania wajue, Serikali itakayoundwa na CHADEMA itafanya nini katika sekta hizo ikiwa CHADEMA itapewa ridhaa ya kuongoza dola.

MAPENDEKEZO YA MFUMO MPYA WA UCHUMI KWA TANZANIA
UCHUMI WA SOKO JAMII (SOCIAL MARKET ECONOMY)
Mheshimiwa Spika, baada kipindi kirefu cha takriban miongo mitano cha mapambano ya Tanzania kujinasua katika lindi la umasikini na kushindwa kufikia lengo hilo; Kambi Rasmi ya Upinzani imegundua kwamba lipo tatizo la msingi katika mfumo wetu wa uchumi. Kwanza mfumo wetu wa uchumi umepitwa na wakati na hauendani na mahitaji ya dunia ya sasa; lakini pili ni uchumi uliohodhiwa na Serikali jambo ambalo limeua nguvu ya soko katika kuamua mustakabali wa uchumi. Mfumo wa Uchumi wetu usipofanyiwa marekebisho makubwa; Tanzania itaendelea kuwa maskini milele yote.
Mheshimiwa Spika, uchumi weti umeendelea kwa duni na madeni makubwa, lakini jambo la msingi zaidi ni kwamba; hali hii inazidi kuwaathiri Watanzania. Ukweli huu haupingiki: Mwaka 2017 zaidi ya watanzania milioni 12 waliishi katika umaskini uliokithiri (Benki ya Dunia 2017). Takriban asilimia 28 ya Watanzania walikuwa chini ya Mstari wa Umaskini wa Mahitaji ya Msingi (NBS 2017, uk.52). Mamilioni ya watu hawakuwa na maji wala umeme (Kessy/Mahali 2017). Ukosefu wa ajira umekuwa mkubwa sana kwa kipindi chote cha miaka iliyopita (ILO 2018). Takwimu zinaonyesha kwamba kiwango cha chini cha mahitaji ya kumwezesha mtu kuishi bado hakijafikiwa; na pia maendeleo ya kiuchumi bado hayajapatikana.
Mheshimiwa Spika, Mwalimu Nyerere tayari alishatoa moni yake juu ya viashiria vya umasikini katika miaka ya 1960, akisisitiza kwamba; Watanzania sasa wanajua kwamba umasikini wetu, ujinga wetu, na maradhi yetu hayawezi kukwepeka kama sehemu ya maisha ya binadamu (Nyerere 1973, uk.110). Kwa kukubaliana na hoja ya Mwalimu Nyerere, Kambi Rasmi ya Upinzani kupitia CHADEMA inaamini kwamba, kwa namna ile ile, umaskini wa leo umesababishwa na watu. Unaweza ukahusishwa na mfumo mbovu wa uendeshaji wa uchumi na uwepo wa sera mbovu za uchumi. Kwa miongo kadhaa sasa, watawala wamekuwa wakitumia mfumo huo mbovu wa uchumi kuwakandamiza Watanzania. Mfumo wa uchumi umelenga kulipa madeni, lakini hautengenezi fursa za maendeleo ya kiuchumi kwa watu. Jambo hili halikubaliki!!!
Mheshimiwa Spika, Ili kukabiliana na hali tete ya uchumi wa nchi yetu, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni kupitia CHADEMA inahimiza uwepo wa mfumo imara wa uchumi unaofanya kazi vizuri. Ili kuwasaidia Watanzania kuondokana na vikwazo vya kijamii vya maisha duni, kuboresha maisha ya mamilioni ya watu na kuiendeleza nchi kwa ujumla wake. Kambi ya Upinzani kupitia CHADEMA inakusudia kutatua changamoto hizo kwa kuanzisha mfumo wa maendeleo ya kiuchumi kwa Watanzania wote. Kwahiyo, CHADEMA inapendekeza kuanzishwa kwa Mfumo wa Uchumi wa Soko Jamii nchiniaTanzania mfumo ambao umefanikiwa kuziimarisha na kuziendeleza nchi mbalimbali duniani, na wakati huohuo, kuwaondoa wananchi wa nchi hizo kwenye umaskini na kuwapatia fursa za ajira zenye uhakika.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni kupitia CHADEMA inaungana na mawazo ya Mwalimu Nyerere katika kuamini kwamba; maendeleo halisi yanaweza tu kutokea kwa kuondoa umaskini nchi nzima. Katika mfumo wa uchumi unaopendekezwa, jitihada zote za kiuchumi zitaelekezwa kwenye kuanzisha utajiri na hivyo kuushinda umasikini ambao ni adui wa maendeleo.
Mheshimiwa Spika, Uchumi wa Soko Jamii, ni Mfumo wa Uchumi unaolenga kuleta maendeleo shirikishi na endelevu kwa kila mtu. Unatokana na mfumo wa Ubepari, unaojulikana pia kama uchumi wa soko, ambao unalenga kuanzisha soko huru la kiushindani. Changamoto za mfumo wa uchumi wa soko zinaweza kuchukuliwa na mfumo wa uchumi wa kijamaa. Uchumi wa Soko jamii unalenga kukidhi kiwango cha chini cha ustawi wa kiuchumi kwa kila mwananchi.
Mheshimiwa Spika, Kimsingi mfumo huu unaleta pamoja faida za ubepari na ujamaa na unaondoa kabisa hasara zake. Hii inaanzisha mfumo mpya wa uchumi ambao unatekelezeka, unakubalika na unaolenga ustawi wa watu. Ili kuimarisha uchumi wa nchi, kila kikwazo kwa maendeleo ya uchumi kinaondolewa. Hata hivyo, kila hatua lazima ichukuliwe kwa kuzingatia ushirikishwaji, uendelevu na kujali utu. Jambo hili hatimaye, litampatia kila Mtanzania fursa za uhakika za kustawi kiuchumi na kuboresha maisha yake.
Mheshimiwa Spika, Dhana ya Uchumi wa Soko Jamii imejengwa katika misingi ya mshikamano na imani kwamba, ngazi ya chini kabisa katika jamii mahalia inao uwezo wa kushughulikia masuala yanayoihusu. Kwa upande mwingine, mshikamano unakuza shauku ya umoja katika Taifa. Kutokana na hali hii, viongozi wa kisiasa, waajiri na waajiriwa husimama pamoja kumtetea kila mmoja na kwa sababu hiyo, husababisha maendeleo ya kiuchumi kuwa kwa ajili ya kila mmoja. Halikadhalika, hali ya ngazi ya chini kabisa katika jamii kuwa na uwezo wa kushughulikia masuala yake yenyewe, ni chachu ya kumjengea uwezo kila mtu kushiriki katika maendeleo ya uchumi. Humpa kila mtu, vikundi vidogovidogo na taasisi zilizogatuliwa wajibu wa kushughulikia mambo yanayowahusu, na kupatiwa msaada tu pale inapobidi.
Mheshimiwa Spika, Misingi mingine ya Mfumo wa Soko Jamii ni soko huru lenye mfumo huru wa upangaji wa bei, na pia mfumo wa udhibiti ili kuzuia baadhi ya watu au taasisi kuhodhi mwenendo wa soko. Zaidi ya hayo, Uchumi wa Soko Jamii unatoa uhuru kwa kila mtu kumiliki mali binafsi. Serikali huusaidia mfumo huu kwa kutoa huduma za jamii, ikiwa ni pamoja na mazingira ya uhakika na shirikishi ya hifadhi ya jamii. Misingi na tabia nyingine za Uchumi wa Soko Jamii zipo katika mfumo imara wa kisheria ili kuhakikisha kwamba uchumi unakuwa imara na thabiti kisheria.

Kwa Nini Tunapendekeza Mfumo waUchumi Wa Soko Jamii?
Mheshimiwa Spika, Mfumo wa Uchumi wa Tanzania umepitia mabadiliko kadhaa kwa kipindi chote cha miaka iliyopita. Ulitoka katika uchumi wa soko wa kikoloni, ukaenda kwenye uchumi wa kijamaa na baadaye ukarudi tena kwenye uchumi wa soko. Licha ya juhudi za kufanya maboresho, hakuna mfumo hata mmoja ambao umefanikiwa kuondoa umaskini na kutengeneza fursa sawa za kiuchumi.
Mheshimiwa Spika, Mfumo wa kiuchumi wa kibepari umethibitika kuwa sio mzuri kwa maendeleo ya nchi kwa kuwa umeshindwa kuziba pengo katika ya matajiri na masikini. Hivyo haukuweza kuliunganisha Taifa katika ukuaji wa uchumi.Uchumi wa Soko Jamii unaziba pengo hilo kwa kutoa fursa za kiuchumi kwa kila mmoja, na wakati huohuo unatoa hifadhi ya jamii katika nyanja za ajira, huduma za afya, elimu na huduma nyingine za jamii.
Mheshimiwa Spika, Mfumo wa pili ambao ni wa kijamaa, uliondoa kabisa ushindani katika soko la Tanzania. Kupitia mfumo huu, viwanda vya Tanzania vilikufa kutokana na kukosa mazingira mazuri ya kukua. Uchumi wa Soko Jamii unalinda ushindani wa nchi kwa kujiepusha na vikwazo wa kiuchumi visivyo vya lazima vinavyoweza kuathiri ushindani.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni kupitia CHADEMA inaunga mkono uanzishwaji wa Uchumi wa Soko Jamii kutokana na kwamba mfumo huo unatekelezeka. Mfumo huu umechukua baadhi ya mambo mazuri kutoka katika mifumo yote miwili ya ya kiuchumi kutoka katika ujamaa na ubepari na miwili ya kibepari na kijamaa na kuyaunganisha pamoja katika mfumo wa mmoja wa uchumi uliosukwa vizuri. Matokeo ya jambo hili ni kwamba; Tanzania inakwenda kushuhudia maendeleo ya kiuchumi yaliyo imara na shirikishi.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni kupitia
CHADEMA inaamini kwamba mfumo huu ndio suluhisho pekee kwa Taifa kusonga mbele kiuchumi. Uchumi wa Soko Jamii unatoa uhakika kwamba, Tanzania inaweza kuwa na ushindani kimataifa na wakati huohuo kuwa na uwezo wa kulinda maslahi ya wananchi wake. Fursa kama hizo, huwawezesha watu kutumia uwezo wao wa kufanya kazi au biashara na hivyo kujikwamua kutoka kwenye lindi la umaskini. Ni katika kujitegemea kwa namna hiyo kwa mtu mmoja mmoja, ambapo Tanzania inaweza kujinasua na utegemezi wa kisiasa na kifedha kutoka kwa wafadhili wake. Kutokana na hali hiyo, Watanzania wataweza kutengeneza Sera na kuzitekeleza kwa ajili ya kukidhi malengo ya kuiendeleza nchi yao.
Mheshimiwa Spika, Historia ya mafanikio ya uanzishwaji wa Uchumi wa Soko Jamii, imeelezwa katika mawanda mapana ya uchumi wa kimataifa. Kwa jinsi hiyo, mfumo huu umeonyesha mafanikio makubwa katika maendeleo ya kiuchumi katika nchi mbalimbali zikiwemo Sweden, Finland na Ujerumani.
Mheshimiwa Spika, CHADEMA inaunga mkono mfumo wa uchumi wa soko Jamii kama hatua ya kurekebisha uchumi wa nchi, kutokana na Serikali kuendelea kushindwa kuleta maendeleo ya kiuchumi.
Mheshimiwa Spika, maelezo ya kina kuhusu historia ya mfumo wetu wa Uchumi na sababu zilizopelekea CHADEMA kubuni sera ya uchumi inayopendekeza kuwa na Mfumo huu mpya wa Uchumi yapo katika kitabu cha Sera ya Uchumi ya CHADEMA kitakachozinduliwa mapema baada ya Mkutano huu wa Bunge, ili kuwa kuwapa watanzania uelewa juu ya mageuzi makubwa ya uchumi tunayokwenda kufanya katika Taifa hili ikiwa tutapewa ridhaa na watanzania ya kuendesha Serikali.

MWENENDO WA HALI YA UCHUMI NCHINI
Ukuaji wa Uchumi Usiopunguza Umasikini
Mheshimiwa Spika, Ni jambo lisilobishaniwa tena kuhusu kuongezeka kwa ukali wa maisha, kwa kila Mtanzania. Kwa muda mrefu, Serikali ya CCM imekua ikitumia kigezo cha ukuaji uchumi kupotosha kuhusu hali halisi ya uchumi wa taifa letu. Serikali ya awamu ya tano inatumia dhana ya ukuaji wa uchumi kwa asilimia 7 kama hoja ya kukaririsha Watanzania waamini kwamba hali ya uchumi ni shwari na kwamba kiwango chetu cha ukuaji uchumi ni kikubwa ukilinganisha na nchi washindani wetu hususani Kenya ambayo uchumi wake unakua kwa asilimia 6.
Mheshimiwa Spika, Kwanza, ni vyema tukafafanua kwamba uchumi wa
Kenya ni zaidi ya dola 65 billioni, hivyo unapokua kwa asilimia 6 ni sawa na ongezeko la dola 4 bilioni , wakati uchumi wa Tanzania wa dola 45 billion, unapokua kwa asilimia 7 ni sawa na ongezeko la dola 3 bilioni. Hii ni tafsiri muhimu sana kujulikana kwa Watanzania kwamba kwa mwaka uchumi wa Kenya unaongezeka kwa kiasi kikubwa kuliko uchumi wetu badala ya kuwadanganya na takwimu za asilimia bila kuzingatia ukubwa wa uchumi wa kila nchi.

Mheshimiwa Spika, ni vema ikaeleweka pia kwamba ukuaji huu wa uchumi kwa asilimia 7 haukuanza leo baada ya Serikali ya awamu ya tano kuingia madarakani. Ukuaji huu umekuwepo kwa zaidi ya muongo mmoja sasa, kwa maana tangu awamu ya tatu (rejea hotuba ya bajeti ya 2005/06), chini ya Benjamini Mkapa, uchumi ulikua kwa kiwango hicho cha asilimia 7, na ifahamike tu kwamba mwaka 2011, Ukuaji huo ulifikia asilimia 7.9.
Mheshimiwa Spika, Ni vema ikafahamika kwamba changamoto tuliyonayo kama taifa kuhusu uchumi sio ukuaji pekee, bali kilicho muhimu zaidi ni namna ya kufanya ukuaji huo utafsiri maisha ya Watanzania. Ilitegemewa tangu kuingia awamu ya nne na sasa ya tano, kazi kubwa ingekuwa kuhakikisha ukuaji wa uchumi unapunguza umasikini, badala yake imekua kinyume chake kwani awamu ya nne ilishindwa kupunguza idadi ya masikini, na mbaya zaidi awamu hii ya tano inafanya vibaya zaidi kuliko awamu ya nne katika mkakati wa kupunguza umasikini kama inavyojipambanua kwenye ripoti mbalimbali za kiuchumi za kimataifa na kitaifa sanjari na hali halisi wanayopitia wananchi kwasasa.
Mheshimiwa Spika, Bado Uchumi wetu kwa kiasi kikubwa unakuzwa na sekta zilezile, za Utalii, Madini, Huduma ya fedha, Mawasiliano, ambazo kwa hakika zinabeba watu wachache na ndio sababu ya uchumi kuendelea kukua bila kupuguza umasikini. Kwa zaidi ya muongo mmoja, Taasisi maarufu nchini inayohusika na tafiti za kiuchumi ijulikanayo kama Research on Poverty Alleviation(REPOA) imebainisha wazi kwamba ili kupunguza umasikini ni sharti kukuza sekta ya kilimo katika dhana pana(mazao, uvuvi na ufugaji) kwa asilimia 8 mpaka 10, na kwamba tukikuza Kilimo kwa kiasi hicho kwa miaka mitatu 3 mfululizo tutakata umasikini kwa asilimia 50.
Mheshimiwa Spika, Ni bahati mbaya kwamba tangu awamu ya tatu mpaka awamu ya nne kilimo kiliendelea kukua chini ya asilimia 4 na mbaya zaidi, katika mwaka wa kwanza wa serikali ya wamu ya tano inayojinasibu kama serikali ya masikini, kilimo kimekua kwa asilimia 1.7 kiwango ambacho ni hafifu kupata kutokea tangu enzi za Utawala Serikali ya awamu ya Tatu na ya Nne.
Mheshimiwa Spika, ukuaji huu mdogo wa sekta za kilimo mifugo na uvuvi, ambazo ndizo tunazitegemea kuondoa umasikini umesababishwa na utekelezaji duni wa bajeti za maendeleo katika sekta hizo. Kwa mfano tathmini ndogo ya utekelezaji wa bajeti ya maendeleo kwa miaka miwili ya mwanzo ya utawala wa Serikali ya awamu ya tano ilikuwa ni kama ifuatavyo:-
Wizara ya Kilimo:-
Katika mwaka wa fedha 2016/17, Wizara ya Kilimo iliidhinishwa fedha za maendeleo kiasi cha shilingi bilioni 100.527 lakini hadi Machi, 2017 zilitolewa shilingi bilioni 2.252 sawa na asilimia 2.22 ya fedha iliyoidhinishwa na Bunge. Hii ina maana kwamba takribani asilimia 98 ya bajeti hiyo haikutekelezwa.
Katika mwaka wa fedha 2017/18; wizara hii iliidhinishiwa na Bunge fedha za maendeleo jumla ya shilingi bilioni 150.253 (150,253,000,000/-) lakini hadi kufikia mwezi Machi, 2018; ni shilingi bilioni 16.5 tu (16,520,540,444/-) zilikuwa zimetolewa ikiwa ni sawa na asilimia 11 tu ya fedha za maendeleo zilizokuwa zimeidhinishwa. Hii ina maana kwamba asilimia 89 ya bajeti ya maendeleo katika sekta ya kilimo haikutekelezwa.

Wizara ya Mifugo na Uvuvi:
Kwa mwaka wa fedha 2016/17 Wizara iliidhinishiwa fedha za maendeleo kiasi cha shilingi bilioni 4 lakini zilizotolewa ni shilingi milioni 130 tu sawa na asilimia 3.25 ya bajeti ya maendeleo iliyoidhinishwa. Hii ina maana kwamba takribani asilimia 97 ya bajeti hiyo haikutekelezwa.
kwa mwaka wa fedha 2017/18 Wizara hii iliidhinishiwa na Bunge jumla ya shilingi bilioni 4 (4,000,000,000/=) kama fedha za kutekeleza miradi ya maendeleo katika sekta ya mifugo na uvuvi; lakini hadi kufikia mwezi machi, 2018 hakuna hata shilingi moja ambayo ilikuwa imepokelewa kutoka hazina kwa ajili ya miradi ya maendeleo katika sekta hizo. Hii ina maana pia kwamba asilimia 100 ya bajeti ya maendeleo katika sekta za mifugo na uvuvi ilikuwa ni hewa!

Mheshimiwa Spika, Ndio sababu Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni tunapenda Watanzania watambue kuwa Serikali hii inayojinasibu kuwa mtetezi wa wanyonge ambao wengi wao ni wakulima, wafugaji na wavuvi kimsingi inawahadaa. Kuhusu ruzuku ya pembejeo za kilimo hali ni mbaya zaidi ukilinganisha na wakati wa Serikali ya awamu ya nne. Kwa mfano katika bajeti ya kwanza ya kilimo katika utawala huu wa awamu ya tano ya mwaka wa fedha 2016/17; ruzuku ya mbolea ilikuwa shilingi billioni10; na katika Bajeti ya pili katika mwaka wa fedha 2017/18 Serikali Ilipanga kutumia shilingi billion 15 kama ruzuku ya pembejeo ukilinganisha na shilingi billion 78 ya mwaka wa mwisho wa Serikali ya awamu ya nne 2015/16. Hili ni anguko la wastani wa shilinigi bilioni 65.5 katika ruzuku ya pembejeo za kilimo na kwa mwaka 2018/19, hali ni mbaya zaidi kwa kuwa hata fedha ya ruzuku ya mbolea haikutajwa kwenye randama ya Wizara ya Kilimo.
Mheshimiwa Spika, Ni vema ikaeleweka kwamba moja ya tatizo kubwa katika sekta ya kilimo Tanzania ni matumizi duni ya pembejeo bora, kwani imesisitizwa kwenye ripoti mbalimbali za tafiti za uchumi na kilimo. Kwa mujibu wa Ripoti ya Umasikini na Maendeleo ya Binadamu 2014 (Poverty and Human Development 2014). Mathalani matumizi ya Mbolea Tanzania ilikuwa ni 9kg kwa ekari 1 wakati nchi zenye chumi ndogo kama Malawi, wakulima wamewezeshwa kiasi cha kutumia 29kg kwa ekari1 na nchi zilizopiga hatua zaidi kwa kilimo kama China, ekari 1 wanatumia zaidi ya 260kg.
Mheshimiwa Spika, Kama tathimini hii ya matumizi ya 9kg kwa ekari1 Tanzania ni utafiti; wakati ambapo serikali ya awamu ya nne walau ilikuwa ikitenga fedha kiasi cha kuonekana kwenye ruzuku ya mbolea, Watanzania na hususan wakulima wanapaswa kujiuliza leo, ambapo Serikali inatenga shilingi bilioni 10 kutoka shilingi bilioni 78 hali itakuwaje?.
Mheshimiwa Spika, Ni vigumu kwa Serikali ya Tanzania kufanya mapinduzi makubwa kiuchumi yenye kupunguza umasikini bila kukuza kilimo katika dhana pana (mazao,ufugaji na uvuvi). Kwa mujibu wa Ripoti ya USAID ya 2014, asilimia 70% ya Watanzania wanategemea Kilimo, na kati yao asilimia 75% ni wanawake. Hivyo masikini wakubwa Tanzania ni wanawake ambao ni asilimia 75% ya watu wote wanaotegemea kilimo, hivyo mwenendo wa sasa ambapo Bajeti ya Miradi ya kilimo inatekelezwa kwa asilimia 2 3 ni rekodi mbaya ambayo haijapata kutokea tangu Uhai wa Taifa hili na ni ishara tosha kwamba Serikali hii haina mpango na masikini watanzania, na tabia ya Mhe Rais kujinasibu kuwa ni Rais wa wanyonge (masikini) ni dhihaka kwa watanzania masikini.
Mheshimiwa Spika, sekta pana ya kilimo, ndiyo inayobeba maskini na wanyonge wengi wa nchi yetu. Umaskini ni laana na siyo sifa. Kujinasibu kama kiongozi wa wanyonge na masikini wakati tunatembeza misafara ya magari takriban 50 ya gharama kubwa yakiambatana na helikopta ni vitu visivyoshabihiana. Sekta pana ya kilimo inagusa lishe na afya za watu wetu, inagusa uwezo wao wa kuhudumia familia katika huduma mbalimbali za kijamii na hata makazi. Kutowekeza vya kutosha katika sekta hizi ni ushuhuda tosha kuwa huruma ya watawala dhidi ya masikini na wanyonge ni sawa na machozi ya mamba.
Mheshimiwa Spika, dhana mpya inayojengwa kwa kasi ya kutenga fedha nyingi kwa kinachoitwa miradi mikubwa ya kimkakati kwa gharama (at the expense of) ya wakulima, wafugaji na wavuvi wetu, hakika ni dhana itakayochelewesha maendeleo ya watu wetu bila sababu za msingi. Mataifa makini duniani, hujikita kwanza kwenye sekta zinazogusa maisha ya wengi kisha hizo sekta nyingine hukua automatically wananchi wanapokuwa na uwezo mzuri kiafya, kielimu, kimazingira na hivyo kiuchumi.
Mheshimiwa Spika, ni jambo la kusikitisha na kutia huruma unapoona Taifa zima linakaririshwa kuabudu miradi isiyozidi mitano ya miundombinu kwa gharama ya ubora wa elimu ya watoto wetu tunayoiita ya bure; maji kwa Taifa zima ikiwa ni kilio cha wengi na ukuaji wa huduma za afya ukiwa wa kasi ndogo kulinganisha na wingi wa watu wetu na mtawanyiko wao!


Mkwamo wa Uchumi na Ongezeko la Ukata Nchini
Mheshimiwa Spika, imekuwa changamoto kubwa hata miongoni mwa wachumi kuhusu hali ya uchumi nchini hasa inapoonekana biashara nyingi zinafungwa kwa kushindwa kujiendesha, kusinyaa kwa uwekezaji mkubwa; kudorora kwa FDI (Foreign Direct investments) kuyumba kwa biashara katika sekta ya nyumba(real estate); makampuni kwa ujumla wake yanazidi kupunguza wafanyakazi, kuporomoka kwa thamani ya hisa katika soko la mitaji (stock market); ukata kwenye uchumi (decline in liquidity) nk, lakini bado serikali inatangaza uchumi kuwa ni imara.
Mheshimiwa Spika, Ipo haja ya kuchunguza uhalisia wa takwimu zetu kuepuka kujenga uchumi hewa kwa takwimu za kupika. Ndio sababu IMF ilitoa angalizo kwa mwaka wa fedha 2018/19 kwamba; mwenendo mbovu wa sera za kibajeti na kutokutabirika kwa utawala huu kutasababisha kuzorota kwa uchumi.
Mheshimiwa Spika, katika tathmini ya saba ya hali ya uchumi wa Tanzania iliyotolewa na Shirika la Fedha Duniani (IMF) tarehe (11/01/2018) takribab mwaka mmoja na nusu uliopita; ni kwamba hali ya uchumi wa Tanzania imekuwa ikipanda na kushuka na kwamba matazamio ya mwenendo huo yanaonyesha mashaka.Tathmini hiyo IMF imetaja baadhi ya maeneo ambayo Tanzania imefanya vizuri kiuchumi. Imesema kiwango cha ukuaji wa uchumi kimeendelea kupanda taratibu; upandaji wa bei za bidhaa muhimu umekuwa wa wastani; akiba ya fedha za kigeni imekuwa nzuri, na utekelezaji wa Mpango wa Sera ya Misaada (PSI) kwa miezi ya Julai hadi Septemba 2017 umekuwa wa kuridhisha, na takwimu za maendeleo ya kujamii inaridhisha, ingawa utekelezaji wa maboresho ya sera yanakwenda polepole.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, IMF imetaja maeneo mengi ambayo kiuchumi Tanzania imefanya vibaya katika kipindi hiki kama ifuatavyo:-
Ukusanyaji wa kodi umepungua,
Mikopo toka mabenki imeendelea kuwa changamoto kutokana na madeni yasiyorejeshwa au yasiyolipika,
Katika siku za usoni uchumi wa Tanzania uko katika hatari ya kuporomoka kutokana na Serikali kushindwa kutekeleza bajeti ya maendeleo, mazingira hasi ya uwekezaji na biashara, na wasiwasi unaotokana na watawala kutofuata sheria na taratibu katika utendaji,
Umasikini na ukosefu wa ajira umezidi kuongezeka nchini,
Kuna uwiano mbovu wa utekelezaji wa miradi ya miundombinu,
Kuna mazingira yasiyoridhisha ya kufanya biashara na uwekezaji nchini,

Mheshimiwa Spika, Shirika la Fedha Duniani (IMF) linahitimisha kwa kuitaka Serikali ya Tanzania kutekeleza yafuatayo ili uchumi wa nchi usididimie mbele ya safari.

Sera za uchumi mpana ni lazima zihuishwe na kuratibiwa kwa ukaribu
Utekelezaji wa bajeti ya maendeleo lazima uongezewe kiwango na kasi.
Sera za fedha na usimamizi wa fedha lazima zihuishwe na maendeleo ya kibajeti.
Ni lazima kukuza zaidi uchumi, kupunguza umasikini na kukuza ajira.
Mazingira ya biashara lazima yaboreshwe ili kuvutia sekta binafsi kuwekeza nchini kama mpango wa maendeleo unavyotamka,
Utekelezaji wa bajeti lazima uwekewe umakini mkubwa zaidi,
Ukusanyaji wa kodi za ndani uongezwe kwa kutumia sera nzuri za kodi na uboreshaji wa utendaji,
Urejeshaji wa kodi ya VAT kwa wafanyabishara na wawekezaji wanaohusika lazima utekelezwe vizuri na haraka kwa mujibu wa taratibu,
Malimbikizo ya mikopo iliyotolewa na mabenki uwekewe mkakati ili mikopo irejeshwe kuwezesha ufanisi wa mabenki ziweze kutoa mikopo kwa wafanyabiashara na wajasiriamali.

Mheshimiwa Spika, Pamoja na maangalizo hayo ya IMF, taarifa za BOT zinaonesha wazi kwamba kushuka huko kwa ujazo wa fedha kwenye uchumi kunatokana na kushuka kwa kiwango cha mikopo kutoka Benki za biashara kwa sekta binafsi, na hivyo kuyumba kwa sekta binafsi ambayo kimsingi ndio injini ya uchumi.Na ndio sababu Benk Kuu ya Tanzania, kama msimamizi wa sera ya fedha, ikachukua hatua mbili kama namna ya kutafuta ufumbuzi wa ukata wa fedha kwenye uchumi(liquidity tightness). Hatua ya kwanza ni ile ya tangazo la kupunguza riba(credit discount) kwa mikopo ya Bank kuu kwenda bank za biashara kutoka riba ya asilimia 16% mpaka riba ya silimia 12%. Ikafuatiwa na tangazo la Benki Kuu la kupunguza dhamana za Benki za biashara zinazowekwa benki kuu kutoka asilimia 10% mpaka asilimia 8%
Mheshimiwa Spika, Hatua zote hizo zilichukuliwa kwa lengo la kukabili ukata kwenye uchumi kwa kuhakikisha sekta binafsi zinapata mikopo na kuchangamsha biashara kwenye uchumi na hivyo kukabili ukata mkali unaokabili uchumi kwasasa. Hata hivyo, pamoja na juhudi zote hizo za Benki Kuu kwa kutumia sera ya fedha(Monetary Policy), bado ukata umebaki kuwa tatizo kwenye uchumi ikiwa ni kielelezo kwamba mzizi wa tatizo la uchumi kwa sasa chimbuko lake sio sera ya fedha( monetary policy)bali sera ya bajeti na mazingira ya biashara kwa ujumla (Fiscal Policy&Business environment).
Mheshimiwa Spika, Tatizo la uchumi kwasasa sio benki kukosa fedha kukopesha sekta binafsi, tatizo ni Serikali imeshindwa kujenga mazingira rafiki kwa biashara na wawekezaji kwa ujumla. Wafanyabiashara na wawekezaji wa ndani na nje kwa ujumla wanakabiliwa na mazingira magumu kibiashara ndio sababu kiwango cha mikopo isiyolipika(Non Performing loans-NPL) kimezidi kuongezeka kwa kiasi ambacho hakijawahi kutokea kwa zaidi ya miongo miwili.Kwa mujibu wa ripoti ya BoT, kiwango cha mikopo isiyolipika kimefikia zaidi ya asilimia 10 ambapo wastani ni asilimia 5
Mheshimiwa Spika, Hii ni ishara mbaya sana kwa sekta binafsi ambayo ndio inapaswa kuwa injini ya uchumi katika uchumi wa soko. Sio kwamba wafanya biashara hawa wanapenda kushindwa kulipa mikopo hiyo bali mazingira ya biashara ni mabovu na hivyo kusababisha wafanyabiashara kuogopa kukopa kwa ajili ya biashara na pia mabenki kuongeza urasimu wa kutoa mikopo kwa hofu ya mikopo isiyolipika kutokana na mazingira mabovu ya kibiashara ambayo msingi wake ni sera duni za kodi na utawala unaoendesha nchi kwa amri za Rais Presidential decrees, kuliko kufuata sheria. Na ndio maana hata ripoti ya mwaka 2017 kuhusu urahisi wa kufanya biashara (EASY OF DOING BUINESS) inayotolewa na Bank ya Dunia, Tanzania bado iko nyuma ya Kenya, Uganda na Rwanda ambao ndio washindani wetu kibiashara.

HALI YA SIASA NA MAHUSIANO YAKE KATIKA MAENDELEO YA KIUCHUMI, KISIASA NA KIJAMII KATIKA TAIFA
Mheshimiwa Spika, kama nilivyoeleza hapo awali, hii ni bajeti ya nne ya Serikali hii ya awamu ya tano. Ni dhahiri kwamba miaka mitatu ya utekelezaji wa bajeti zilizopita, ni muda unaotosha kutoa tathmini ya mwendendo wa uongozi wa nchi na matokeo yake katika maendeleo ya kiuchumi, kisiasa na hata kijamii pia.
Mheshimiwa Spika, baada ya kufanya tathmini ya mwenendo wa uongozi wa nchi katika miaka mitatu iliyopita; nathubutu kusema kwamba, Taifa linapita kwenye kipindi kigumu cha uongozi, usioheshimu Katiba, Sheria, Taratibu na wala tamaduni zetu kama Watanzania. Tunapita kwenye kipindi kigumu cha uongozi usioamini katika nguvu ya taasisi za dola. Tunapita kwenye kipindi cha uongozi usioamini katika Uhuru wa mihimili mingine kwa maana ya Bunge na Mahakama. Tunapita kwenye kipindi kigumu cha utawala usioamini katika kazi zilizofanywa na Serikali zilizotangulia kwa mfano mchakato wa katiba mpya, uwekezaji kwenye sekta ya gesi, ujenzi wa bandari ya Bagamoyo, ujenzi wa kituo cha uwekezaji Kurasini nk.
Mheshimiwa Spika, tunapita katika kipindi ambacho vilevile; Serikali hii ya awamu ya tano imeamua kuuwa kabisa dhana ya ugatuzi wa madaraka kwa Serikali za mitaa na kujilimbikizia madaraka kwa kuzinyanganya halmashauri vyanzo vyake vya mapato. Kwa kifupi, ni aina ya uongozi ambao mtu mmoja anajilimbikizia madaraka na kutaka kila kitu afanye mwenyewe na kuziacha taasisi njia panda bila kujua zifanye nini. Aina hii ya uongozi Waingereza wanauita POPULIST LEADERSHIP.
Mheshimiwa Spika, tabia ya Utawala wa namna hii umechambuliwa vizuri katika Makala ya Mwandishi na Mkurugenzi wa kituo cha Utafiti cha Chuo Kikuu cha Central Europe, Dr Milkoz Harasz kwenye Jarida maarufu duniani la Washington Post la Disemba 28, 2016, ambapo kwa kifupi naomba ninukuu maneno yake kuhusu tabia za populist leaders kwa faida ya Bunge lako na watanzania;
Mheshimiwa Spika, Mwandishi na Mtafiti Milkoz Harasz, anasema:- Populists govern by swapping issues as opposed to resolving them. They dont mind being hated.Their two basic postures of defending and triumphing are impossible to perform without picking enemies.Populist can turn into peace nicks or imperialist depending on what they think could yield good spin that boost their support. Hypocrisy is in the genes of populists, in many countries they betray expectations of selfless strongman and have lead to civic awekeny..
Mheshimiwa Spika, Kwa tafsiri isiyo rasmi, Dr Miltoz anasema Kiongozi mpenda sifa na mwenye kujikweza hutawala kwa kufunika matatizo ya msingi badala ya kuyatafutia ufumbuzi, watawala hawa hawaoni shida kuchukiwa.Dhamira zao mbili za kulinda utawala wao na kuwashinda wapinzani wao wanaamini hazitafanikiwa, bila kutengeneza maadui. Watawala wapenda sifa na wenye kijikweza huweza ama kuwa wahubiri wa Amani ya uongo ama wakawa mabeberu madikteta kutegemea wanachodhani kinaweza kulinda matakwa yao.Unafiki ndio asili yao, hata hivyo katika nchi nyingi watawala wa namna hii hudhihirisha utawala wenye maslahi binafsi, na mwishowe wananchi huwaelewa, huzinduka na kuasi
Mheshimiwa Spika, Tabia hizo za viongozi wapenda sifa mara nyingi hutumia muda na akili nyingi kuzuia au kukabiliana na wakosoaji ndani na nje ya vyama vyao na kuwaita wapinga maendeleo na kwamba si wazalendo. Wanaposhindwa kukidhi matarajio waliyoyajenga kwa Umma, hugeuka na kutumia mbinu za kikatili kwa mkono wa dola kutawala,na mara nyingi hukanyaga demokrasia na kuvunja katiba. Hali hii tayari imeshatokea hapa kwetu Tanzania ambapo tunashuhudia utawala huu ukikanyaga Katiba na misingi yake sambamba na kuminya demokrasia kwa kisingizio cha kuleta maendeleo.
Mheshimiwa Spika, Tawala za namna hii hutumia muda mwingi kutaka umma uamini kwamba demokasia ni kikwazo cha Maendeleo na kwamba Udikteta unaweza kuleta maendeleo (kitu ambacho hakijawahi kuonekana kwenye tafiti yoyote kuhusu maendeleo). Ni vema viongozi wetu wakaelewa na kuamini kama pengine kuna tawala wanazochukulia mfano katika kuliongoza taifa letu, watambue zina historia tofauti na Taifa letu. Baadhi ya mataifa watawala wake waliingia madarakani kwa njia za mapinduzi na au umwagaji damu, na sio sanduku la kura kwa hiyo ni lazima kuwa makini sana kabla ya kuiga mienendo na tabia za watawala wa namna hiyo katika kuliongoza taifa letu.
Mheshimiwa Spika, Kwa hali ilivyo sasa; ni dhahiri kwamba utawala wetu una sifa na mwenendo anaozungumzia Dr Milkoz Sarasz. Kwa sababu hiyo ni lazima tusimame imara kama taifa kupinga Taifa hili zuri kupelekwa kusikojulikana ambako Demokrasia inaelekezwa kuzimu, biashara zinapukutika, ukata unazidi na Watanzania wanazidi kuzama kwenye lindi la umasikini na hofu dhidi ya utawala wao inazidi kuongezeka.
Mheshimiwa Spika, Haya ni maisha ambayo Watanzania hawakutarajia, na hii ndio changamoto kuu kwa Bunge hili lenye dhamana ya mwisho kuhusu mustakabali wa Taifa hili kikatiba. (Parliament is the supreme organ of the state; and so it has to stand on its feet).

SERIKALI KUINGILIA BIASHARA YA KOROSHO NA KUTOTEKELEZA MIRADI YA LANGO LA MAENDELEO LA MTWARA (MTWARA DEVELOPMENT CORRIDOR)
Kuingilia Biashara ya Korosho
Mheshimiwa Spika, Kwa mujibu wa takwimu za Randama ya Wizara ya Kilimo kwa mwaka wa fedha 2018/19; mwenendo wa uzalishaji wa zao la korosho kwa miaka mitatu kuanzia msimu wa mwaka 2015/16 hadi msimu wa 2018/19 umekuwa unapanda ambapo mwaka 2015/16 uzalishaji ulikuwa tani 155,416; 2016/17 tani 265,238 na 2017/18 uzalishaji ulifikia tani 311,899. Aidha, matarajiokwa mwaka 2018/19 yalikuwa ni kuzalisha tani 350,000.
Mheshimiwa Spika, takwimu hizo zinaonesha kwamba, wakulima wadogo wadogo takribani 280,000 wanaendesha maisha yao na familia zao kutegemea zao la Korosho kwa kulima kati ya heka moja hadi mbili na kufanya eneo linalolimwa zao hilo kufikia heka 400,000. Na kwa sasa eneo hilo litakuwa limeongezeka kutokana na mwamko wa wananchi kulima zao hilo.
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa sheria ya korosho(Cashewnut Industry Act (Cap, 203), inasema kuwa asilimia 65 ya kodi ya mauzo nje yarudishwe kwa wakulima kupitia bodi ya korosho (CBT) na Serikali ibakie na asilimia 35. Mgawo wa hizo asilimia 65 wa export levy, matumizi yake makubwa ni ununuzi wa Pembejeo za kilimo cha Korosho na kuendeleza utafiti kwenye zao la Korosho.
Mheshimiwa Spika, katika hali ambayo mpaka sasa haieleweki; Serikali ilivunja bodi ya Korosho; na kutaifisha ile asilimia 65 ya kodi ya mauzo ya korosho nje; na pia kuingilia biashara ya korosho kwa kuwazuia wanunuzi binafsi kununua korosho. Matokeo yake ni kwamba hakuna mauzo ya korosho nje ya nchi yaliyofanyika mpaka sasa; Serikali ilichofanya ni kununua korosho kwa wananchi tena kwa mkopo kwa ahadi ya shilingi 3,300 kwa kilo lakini wakati wa kulipa bei hiyo ikapungua kwa madai kwamba korosho hazina ubora.
Mheshimiwa Spika,uamuzi wa Serikali kununua Korosho toka kwa wakulima badala ya kuhusisha makampuni binafsi umeligharimu taifa letu kwa kukosa fedha za kigeni, mfano kwa mwaka wa fedha 2017/18 fedha za kigeni zilizotokana na korosho zilikuwa ni dola za kimarekani milioni 965, kwa mwaka huu 2018/19 unaoishia hadi sasa ni Zero. Kodi ya mauzo nje (export levy) kwa mwaka 2017/18 ilikuwa ni dola za kimarekani milioni 200; kwa mwaka 2018/19 hakuna chochote
Mheshimiwa Spika,kitendo cha kuvunja Bodi ya Korosho chombo ambacho kiliundwa kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge bila kuleta Bungeni muswada wa sheria wa kuifuta sheria hiyo mosi ni ukiukwaji wa katiba, pili ni dharau kwa Bunge; lakini mbaya zaidi ni hujuma kwa wakulima wa zao la korosho ambao mpaka sasa haijulikani zao lao linaratibiwa na chombo gani. Kwa maneno mengine zao la korosho ni kama vile halina mwenyewe na wakulima wa korosho wamekuwa kama kondoo wasio na mchungaji.
Mheshimiwa Spika, kutokana na mchanganyiko huo wa mambo kumekuwa pia na sintofahamu ya biashara ya korosho katika msimu huu ambapo wakulima wengi wameshindwa kupata fedha kulingana na mauzo ya korosho zao. Jambo la ajabu ni kwamba korosho ambazo zilikuwa zimechukuliwa na Serikali na kwa maana kwamba kilichokuwa kikisubiriwa ni wananchi kulipwa fedha zao zimeanza kurejeshwa kwa wenyewe kwa madai kuwa hazina ubora unaostahili. Na pia wakulima wenye korosho nyingi kukataliwa kulipwa kwa kigezo cha uhakiki wa mashamba.
Mheshimiwa Spika, ni ajabu kwamba; kwa mara ya kwanza katika historia ya Tanzania tunakwenda kuhakiki shamba la mkulima kisa tu ana mazoo mengi. Kambi Rasmi ya Upinzani inaamini kuwa uzalishaji mkubwa ni neema kwa nchi kwa kuwa wingi wa korosho ndani ya nchi maana yake ni kupata fedha za kigeni kwa wingi tutakapouza nje na hivyo kukuza uchumi wetu. Inashangaza sana kwa Serikali hii kuzuia watu wa Msumbiji kuwauzia wananchi wetu korosho wakati koroho hiyo ingeuzwa nje kwa jina la Tanzania na fedha za kigeni tungepata sisi.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa lengo la nchi ni kuwa na Tanzania ya viwanda, ni muda mwafaka sasa kuhakikisha viwanda vinakuwa na uhakika wa malighafi, na malighafi itapatikana ndani au nje ya mipaka ya nchi yetu.
Mheshimiwa Spika, Uchumi wa Viwanda kwa nchi hii utafikiwa tu, pale bei za mazao ya kilimo zitakapokuwa nzuri na hivyo kumfanya mkulima kuongeza uzalishaji kwa kutumia teknolojia bora na ya kisasa. Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaamini kwamba, mustakabali wa kilimo cha kisasa, endelevu na cha kibiashara upo katika soko la mazao ya bidhaa za kilimo, ambapo wakulima na wanunuzi wataendesha shughuli zao za kibiashara katika mazingira yanayotabirika, na kwamba wakulima wanaweza kupata bei nzuri kwa mazao yao. Hivyo ndivyo Sera ya Chadema ya Kilimo inavyosema katika sura 9.3; na hivyo ndiyo Kambi Rasmi ya Upinzani inawaahidi wananchi kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo ikiwa kitapata ridhaa ya kuongoza Serikali.

Utekelezaji Duni wa Miradi ya Lango la Maendeleo la Ukanda wa Mtwara (Mtwara Development Corridor)

Mheshimiwa Spika, Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano umeanisha miradi kadha ya kielelezo kwa Lango la Maendeleo la Ukanda wa Mtwara. Miradi hiyo ni pamoja na Mradi wa makaa ya mawe na chuma (Mchuchuma na Liganga); Mradi wa ujenzi wa mtambo wa gesi(Liquefied Natural Gas Plant); Mradi wa Upanuzi wa Bandari ya Mtwara; Mtwara Petrochemical Special Economic Zone; Mradi wa Ujenzi wa kiwanda cha Mbolea; Ujenzi wa Reli ya kisasa kati ya Mtwara-Liganga-Mchuchuma na Mwisho ni Mradi wa Maendeleo ya Kilimo katika Ukanda wa Kusini ; yaani Southern Agricultural Growth Corridor of Tanzania - SAGCOT.
Mheshimiwa Spika, miradi yote hiyo ambayo ingefungua uchumi wa kusini, ilitakiwa ikamilike ndani ya miaka mitano lakini mpaka sasa hakuna mradi hata mmoja uliokamilika kwa asilimia 100. Hata hivyo, mradi wa upanuzi wa Bandari ya Mtwara ambayo tayari ulikwishaonesha mwelekeo mzuri; nao utakuwa hauna tija sana kwa kuwa bandari hiyo inategemea sana kuhudumia shehena ya korosho ambayo kwa sasa imeshuka sana ukilinganisha na miaka mingine kutokana na Serikali kuingilia biashara hiyo.
Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2016/ 2017 bandari ya Mtwara ilihudumia shehena ya korosho tani 216,000 na mapato yatokanayo na kuhudumia shehena hiyo yalikuwa ni Sh Bilioni 20.266 sawa na asilimia 74 ya mapato mwaka huo ya Sh Bilioni 27.549. Mapato yatokanayo na kuhudumia shehena ya korosho yamekuwa yakiongezeka kwa wastani wa asilimia 20 kwa mwaka. Ongezeko hilo la mapato lilichangiwa na ongezeko la shehena ya korosho inayozalishwa katika mikoa ya kusini mwa Tanzania.
Mheshimiwa Spika, kutokana na hali ya kutegemeana kati ya usafirishaji wa shehena ya korosho kwenda nje ya nchi na maendeleo na ufanisi wa bandari ya Mtwara, kitendo chochote kitakachoweka kikwazo katika uzalishaji na usafirishaji wa zao la korosho kitaathiri pia utendaji wa bandari.
Mheshimiwa Spika, bandari ya Mtwara itakuwa kichocheo kikubwa cha uchumi kama upanuzi wake utaenda sambamba na uimarishaji wa kilimo cha korosho, ufuta, mihogo, samaki na hivyo kuwa lango kuu kwa usafirishaji wa bidhaa kwenda nje. Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, ina mtazamo kwamba; kitendo cha Serikali kutotekeleza Miradi ya Maendeleo ya Ukanda wa Mtwara; sambamba na kuingilia biashara ya korosho ambayo ilikuwa ni chanzo kikubwa cha mapato cha Badari ya Mtwara; hakina maana nyingine zaidi ya kuuwa na kudidimza uchumi wa mikoa ya kusini na kuzifanya hali za maisha ya wananchi wa kusindi kuendela kuwa mbaya zaidi siku hadi siku.


DENI LA TAIFANA ATHARI ZAKE UCHUMI WA TANZANIA
Mheshimiwa Spika, mserereko wa kupaa wa deni la taifa kila mwaka ni tishio na kiashiria kikubwa cha kuporomoka kwa uchumi wa nchi yetu. Pamoja na ukweli kwamba Wizara ya fdha ndiyo yenye wajibu wa kusimamia deni la taifa; kwa maana ya kudhibiti ukopaji usio na tija pamoja na kulipa deni hilo; Wizara ya fedha inaonekana kushindwa kutekeleza wajibu huo kwa ufanisi; kwa kuwa deni hili limeendelea kuwa kubwa kila mwaka jambo ambalo limekuwa na athari kubwa katika bajeti ya Serikali na hivyo kuathiri uchumi wetu na maisha ya wananchi kwa jumla.
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) ya mwaka 2017/18; ni kwamba hadi kufikia tarehe 30 Juni, 2018, deni la Serikali lilikuwa limefikia Shilingi trilioni 50.926. Kati ya fedha hizo, shilingi trilioni 14.732 zilikuwa ni deni la ndani na shilingi trilioni 36.194 zilikuwa ni deni la nje.
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa ripoti hiyo, deni la Serikali limeongezeka kwa shilingi trilioni 4.845 sawa na asilimia 10.5 ikilinganishwa na deni la Shilingi trilioni 46.081 lililoripotiwa tarehe 30 Juni, 2017.
Mheshimiwa Spika, Deni linaendelela kukua kila mwaka kutokana na:-
kuwepo kwa nakisi ya mapato ya serikali dhidi ya matumizi. Na jambo hili tumelipigia kelele miaka mingi; Serikali imekuwa ikiweka makisio makubwa ya makusanyo ya mapato namatokeo yake hushindwa kukusanya mapato hayo. Aidha, imekuwa ikipanga matumizi makubwa kuliko mapato inayokusanya Kwa mfano; katika mwaka wa fedha 2016/17 Serikali ilipanga kukusanya kiasi cha shilingi trilioni 29.54 lakini iliweza kukusanya mapato kutoka vyanzo vyote yaliyofikia shilingi trilioni 20.7 sawa na asilimia 70.1 ya lengo. Hii ina maana kwamba, asilimia takriban 30 iliyobaki (sawa na shilingi trilioni 8.83) ilikuwa ni nakisi ya bajeti husika na kwa maana hiyo kiasi hicho inabidi kikopwe ili kukidhi matumizi ya bajeti husika. Aidha, katika mwaka wa fedha 2017/18 Serikali ilipanga kukusanya jumla ya shilingi trilioni 31.71 lakini iliweza kukusanya kiasi cha shilingi trilioni 21.89 sawa na asilimia 69 ya lengo. Hii ina maana kwamba, asilimia 31 iliyobaki (sawa na shilingi trilioni 9.82) inabidi kikopwe ili kukidhi matumizi ya bajeti husika.
Aidha, deni limeendelea kukua kila mwaka kutokana na ubadilishwaji wa hati fungani,
ukopaji kwa ajili ya shughuli za maendele na
hasara katika kubadilisha fedha za kigeni ikisababishwa na kushuka kwa thamani ya shilingi dhidi ya fedha nyingine za kigeni ambazo ni imara.
Jedwali Na. 1 linaonyesha mwenendo wa ukuaji wa deni kwa miaka mitatu iliyopita:-


Jedwali Na. 1. Mwenendo wa Ukuaji wa Deni la Serikali kwa miaka mitatu iliyopita

2015/16
2016/17
2017/18


Shilingi bilioni

Jumla ya Deni
41,039
46,081
50,927

Deni la Nje
29,846
32,746
36,194

Deni la Ndani
11,193
13,335
14,732.45

Chanzo: CAG 2017/18 (uk. 138)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia mwenendo huo wa ukuaji wa deni, utaona kwamba Serikali hii ya awamu ya tano inayojigamba kwamba haikopi nje, na kwamba inatumia fedha zake za ndani kuendesha miradi yake ya maendeleo, ilikuta deni la taifa likiwa shilingi trilioni 41.039 ilipoingia madarakani; ikaongeza deni hilo kwa shilingi trilioni 5 hadi kufikia shilingi trilioni 46.081 kwa mwaka wake wa kwanza tu madarakani. Aidha, katika mwaka wake wa pili madarakani, Serikali hii imeliongeza deni kwa shilingi kwa takribani shilingi trilioni 5 nyingine hadi kufikia shilingi trilioni 50.927.
Mheshimiwa Spika, deni la shilingi trilioni 50 .9 ambayo ni karibu sawa na trilioni 51 ni asilimia 40.6ya Pato la Taifa ambalo kwa sasa ni shilingi trilioni 125.6 . Kiwango hiki cha deni ni kikubwa mno na kina mwelekeo wa kuiweka nchi rehani kwa kuwa kinakaribia kufikia nusu ya pato letu.
Mheshimwiwa Spika, Sababu za kuongezeka kwa Deni la Serikali kwa kiasi kikubwa kunasababishwa na mikopo halisi (mikopo halisi hapa inajumuisha mapokezi ya fedha za mikopo, ulipaji wa mtaji, malipo ya riba za dhamana za Serikali za muda mfupi na misamaha ya madeni).
Mheshimiwa Spika, Kwa miaka mitatu iliyopita, sababu hii imekuwa ikichangia ukuaji wa deni kwa zaidi ya asilimia 70, ambapo mwaka 2016/17 ilikuwa juu zaidi na kufikia asilimia 88. Uchambuzi wa Ofisi ya Ukaguzi ulibainisha kuwa, kushuka kwa thamani ya sarafu/fedha ya Tanzania kumechangia ongezeko la deni la taifa kwa asilimia 20 kwa mwaka 2017/18 (hili ni ongezeko kubwa ikilinganishwa na asilimia 9 ya mwaka 2016/17).
Mheshimiwa Spika,kwa mujibu wa CAG, kushuka kwa thamani ya sarafu ya Tanzania kunaathiri vibaya ongezeko la deni, na uchumi pia hivyo wito unatolewa kwa watunga sera kubuni mikakati itakayopunguza athari hizo.
Mheshimiwa Spika, kuhusu malimbikizo ya riba, CAG alibaini kwamba Malimbikizo hayo yanatokana na nchi tano (Iraq, India, Romania, Angola na Iran) za kundi lisilo la wanachama wa Paris, ambazo hazijatoa misamaha ya madeni kwa Tanzania kulingana na makubaliano.

F1. Deni la Ndani
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani imeona ni muhimu kuzungumzia deni la ndani kwa kuwa kitendo cha Serikali kukopa ndani kinawaathiri sana wananchi hasa wajasiriamali kushindwa kupata mikopo kwenye mabenki na taasisi za fedha za ndani. Kwa mujibu wa Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ya mwaka 2017/18; hadi kufikia tarehe 30 Juni, 2018 deni la ndani lilifikia shilingi trilioni 14.732. Hili ni ongezeko la shilingi trilioni 1.396 sawa na asilimia 10 kutoka shilingi trilioni 13.335 kwa kipindi kama hicho mwaka 2017.

Mheshimiwa Spika, deni hilo linatokana na Serikali kukopa fedha katika soko la ndani kwa ajili ya kusaidia bajeti na kwa ajili ya kulipia dhamana za Serikali zilizoiva kwa kipindi cha mwaka 2017/18. CAG anasema kwamba; Ijapokuwa deni la ndani haliathiriwi na kushuka kwa thamani ya shilingi lakini linakuwa; na linaathiri ukopeshaji kwa sekta binafsi, na ni mzigo kwa serikali kwa siku zijazo.

Mheshimiwa Spika, Uchambuzi wa CAG unaonesha kuwa, jumla ya Shilingi trilioni 5.704 zilizokopwa kwenye mabenki na taasisi za fedha za ndani hazikuweza kulipa deni na riba za mwaka husika zilizofikia shilingi trilioni 6.152 Hivyo, serikali ilitumia Shilingi billion 448.75 toka vyanzo vingine vya mapato ili kuhudumia deni la ndani. Kwa sabu hiyo CAG anasema deni la ndani halikuchangia miradi ya maendeleo. Kiwango cha kuhudumia deni la ndani kilifikia asilimia 108 ya fedha zilizopatikana toka mikopo ya ndani.

Mheshimiwa Spika, kutokana na mwenendo huo wa Serikali kukopa ndani kwa kiwango kikubwa na kushindwa kulipa fedha hizo, Kambi Rasmi ya Upinzani ina mtazamo kwamba jambo hilo lisipotafutiwa ufumbuzi wa mapema, kuna hatari ya uchumi wetu kuendelea kuporomoka na kusababisha hali ngumu zaidi ya maisha kuliko ilivyo sasa. Kwa sababu hiyo, ni rai ya Kambi Rasmi ya Upinzani kwamba; Waziri wa Fedha na timu yake ambao ndio watunga sera za fedha kuvaa viatu vyao sawasawa maana inaonekana vinawapwaya.

Mheshimiwa Spika,ni aibu kwetu sisi wabunge kuimba wimbo uleule kila mwaka wa bajeti kuhusu madeni ya Serikali, lakini ni aibu zaidi kwa Serikali kubanana na wananchi kwenye mabenki na taasisi za fedha za ndani, kukopa fedha ajili ya kulipa madeni yake ya ndani!!

F2. Deni la Nje
Mheshimiwa Spika,ni Serikali hii hii ya awamu ya tano iliyoingia madarakani kwa tambo kwamba haina haja na fedha za wahisani na kwamba ina uwezo wa kujiendesha na kugharamia miradi ya maendeleo kwa kutumia fedha za ndani. Imefikia hatua Serikali inawaita watu wanaoikosoa na kuielekeza mambo mazuri ya kufanya, kuwa ni vibaraka wanaotumika na mabeberu ikimaanisha mataifa ya nje.
Mheshimiwa Spika, hayo mabeberu ambayo Serikali imeamua kuyaita hivyo, yanaidai Serikali hii jumla ya shilingi trilioni 36.194. Kwa mujibu wa CAG, deni hilo ni sawa na asilimia 71 ya deni lote la Serikali. Deni hili liliongezeka kwashilingi trilioni 3.448 ambazo ni sawa na ongezeko la asilimia 10.5 kutoka shilingi trilioni 32.745 za mwaka 2016/17. Kwa mujibu wa CAG, taasisi za Kimataifa ndio wakopeshaji wakubwa zaidi wakiwa na asilimia 58 zikifuatiwa na nchi marafiki asilimia 11.

F3. Usimamizi Dhaifu wa Deni la Taifa
Mheshimiwa Spika, suala la kuendelea kupaa kwa deni la taifa kunasababishwa pia na usimamizi dhaifu wa deni hilo kupitia kitengo cha usimamizi wa deni la taifa. Kwa mfano, ukaguzi wa CAG ulibaini mapungufu yafuatayo katika usimamizi wa deni la taifa.
Upotoshwaji wa mapokezi ya mikopo kutokana na mapungufu ya Udhibiti wa Ndani katika kurekodi na kutaarifu,
Kuchelewesha kulipa madeni ya Benki Kuu, Shilingi bilioni 212.7;
Kutokuwapo kwa uwiano wa taarifa za mfumo wa malipo (Epicor) na mfumo wa kutunza taarifa za deni la taifa (Common Wealth Secretariat-Debt Record Management System (CSDRMS));
Kushindwa kutambua madeni yatokanayo na malimbikizo ya michango ya pensheni;
Mheshimiwa Spika, licha ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kuonyesha madhaifu ya kitengo cha usimamizi wa deni la Taifa kwa miaka mingi, na licha ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni kutoa rai kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kufanya ukaguzi maalum (Special Audit) katika kitengo cha deni la Taifa (Fungu 22) ili tuweze kujua mikopo tunayoichukua kila mwaka inatumika kufanyia nini, na kama miradi iliyotekelezwa kutokana na mikopo hiyo ni ya kipaumbele au la kwa mujibu wa mpango wa Taifa wa Maendeleo; na licha ya kuitaka Serikali kutenganisha deni halisi la Taifa na matumizi mengineyo yanayohusu Mfuko Mkuu wa Hazina ili kuziba mianya ya ubadhirifu au matumizi mabaya ya fedha za umma kwa kisingizio cha Deni la Taifa; na licha ya kuionya Serikali kuacha kukopa mikopo mikubwa yenye masharti ya kibiashara, ambayo hatimaye inaliingiza taifa kwenye mzigo wa madeni; na licha ya kuitaka Serikali kuleta pendekezo la mkopo Bungeni kabla haijakopa pamoja na orodha ya miradi itakayotekelezwa kwa kutumia mkopo huo ili Bunge liidhinishe; Serikali hii ya awamu ya tano imepuuza mapendekezo yote hayo na badala yake imeendelea kukopa mikopo yenye mashari ya kibaishara jambo ambalo limeongeza kiwango cha deni kwa hali ya juu sana. Athari za jambo hili ni kwamba fedha nyingi karibia nusu ya Pato la Taifa, zitatumika kulipa madeni na kuwaacha wananchi wakiwa hawana huduma muhimu za jamii na pia kuacha miradi mingi ya maendeleo bila kutekelezwa.
Mheshimiwa Spika, CAG anasema; kwa kuwa mapendekezo ya kurekebisha mfumo wa usimamizi wa deni la taifa ni ya muda mrefu; na kuwa kuwa Serikali haikutekeleza mapendekezo hayo licha ya kukumbushwa kila wakati; hii inaashiria kuwa, serikali imekuwa na umakini hafifu katika utekelezaji wa mapendekezo ya Ukaguzi. Na kwa sababu hiyo; Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaipa changamoto Serikali hii ya awamu ya tano, na kuitaka kulieleza Bunge hili; inatoa wapi mamlaka ya kimaadili (moral authority) ya kusema inapiga vita rushwa na ufisadi; na kwamba inataka kujenga uchumi wa kati kupitia mapinduzi ya viwanda, ikiwa imeshindwa kudhibiti madeni na upotevu wa fedha za umma kwa uzembe na udhaifu mkubwa wa Wizara ya Fedha ambayo kwa kila kigezo, imeshindwa kutumia mamlaka yake ya kisheria kusimamia na kutekeleza sera ya fedha.

UKUSANYAJI DUNI WA MAPATO UNAVYOATHIRI UTEKELEZAJI WA BAJETI YA SERIKALI
Mheshimiwa Spika, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imeonyesha udhaifu na uwezo mdogo wa kukusanya mapato jambo ambalo limeathri sana utekelezaji wa Bajeti za Serikali kwa miaka ya hivi karibuni na hivyo kurudisha nyuma maendeleo ya uchumi na watu. Kwa mujibu wa ripoti ya CAG ya mwaka 2017/18; Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ilikusanya jumla ya shilingi trilioni 15.386 ikiwa ni pungufu ya shilingi trilioni 1.929 ya lengo la kukusanya shilingi trilioni 17.315. Upungufu huo ni sawa na asmilimia 11 ya lengo.

Mheshimiwa Spika, taarifa ya CAG inaonyesha pia kwamba; kwa ujumla, idara zote tatu za mapato zilishindwa kufikia malengo kwa mwaka wa fedha 2017/18. Taarifa hiyo inaonesha kwamba Idara ya walipa kodi wakubwa ilikusanya asilimia 41 ya makusanyo yote ambayo ndiyo sehemu kubwa kuliko idara zote; ikifuatiwa na Idara ya Forodha yenye asilimia 40 na idara ya kodi za ndani yenye asilimia 19 ambayo ndiyo ya mwisho kwa mwaka wa fedha 2017/2018, makusanyo haya hayahusishi vocha ya misamaha ya kodi kutoka Hazina.

Mheshimiwa Spika, Kutokana na mchanganuo huo, ni dhahiri kuwa mchango wa makusanyo kutoka Idara ya Mapato ya Ndani umekuwa nyuma ikilinganishwa na idara nyingine. Aidha, taarifa hiyo inaonesha kuwa mwelekeo wa makusanyo ya mapato kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita kwa wastani, ulikuwa chini ya makadirio yaliyoidhinishwa, isipokuwa kwa mwaka wa fedha 2015/16 wakati wa Serikali ya awamu ya nne ndipo makusanyo halisi yalikuwa juu ya makadirio kwa asilimia 0.13.

Mheshimiwa Spika, Taarifa ya CAG inaeleza kuwa ufanisi katika ukusanyaji mapato kwa mwaka wa fedha 2017/18 haukuwa mzuri kwani uwiano wa kodi dhidi ya pato la ndani la taifa ulipungua (kodi kwa pato la taifa) mpaka kufikia asilimia 12.8 ikilinganishwa na asilimia 13.2 kwa mwaka 2016/17. Kwa sababu hiyo, Mamlaka ilishindwa kutimiza lengo na mkakati wa kufikia uwiano wa asilimia 19.9 wa kodi dhidi ya pato la ndani la taifa, lengo ambalo Mamlaka ilijiwekea kulifikia katika mwaka 2018.

Mheshimiwa Spika, hakuna fedheha na aibu mbaya kama kujiwekea lengo na kushindwa kulifikia. Kitendo hicho kikitokea, kinadhihirisha uwezo mdogo wa kufikiri, kupanga na kutekeleza. Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni haioni mantiki ya Serikali hii kutafuta umaarufu uchwara (cheap popularity) kwa wananchi kwa kuwaaminisha kuwa ina uwezo mkubwa wa kukusanya mapato wakati tofauti kati ya tambo hizo na uhalisia wenyewe ni sawa na tofauti ya umbali kati ya Mbingu na Ardhi.

Mheshimiwa Spika, uwezo mdogo wa TRA kukusanya kodi unafahamika pia kimataifa. Ripoti ya CAG inasema kwamba; Mchanganuo linganifu wa ufanisi wa kodi kwa nchi za Afrika Mashariki unaonesha kwamba, Tanzania ilishika nafasi ya mwisho katika ukusanyaji mapato kwa mwaka wa fedha 2017/18. Kambi Rasmi ya Upinzani inaionya Serikali kuacha kujitapa kuwa ina uwezo mkubwa wa kukusanya mapato wakati tafiti zimeonyesha kuwa ina uwezo mdogo na badala yake ijielekeze kutekeleza mapendekezo ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni tuliyoyatoa siku nyingi.

Mheshimiwa Spika, mapendekezo hayo ni pamoja na kuongeza wigo wa vyanzo vya kodi, kudhibiti mianya ya upotevu wa kodi na kuwapa motisha walipa kodi, ili kuongeza ulipaji kodi kwa hiari.

Mheshimiwa Spika, hatua alizochukua za kuwabadili mara kadhaa Makamishna Wakuu wa TRA, kutokana na madhaifu mengi katika Mamlaka hiyo; pamoja na kwamba kunampatia Rais sifa kwamba Serikali yake inafanya kazi; lakini mifumo mibovu ya kitaasisi isipobadilishwa, hata akija malaika atashindwa kufanya kazi kwa ufanisi. Kubadilisha watendaji wakati mifumo ni ile ile iliyoshindwa toka awali; ni sawa na kuweka davai mpya kwenye kiriba kikuukuu au kuwa muumini mpya katika dini ya zamani. Hakuna kitakachobadilika zaidi ya kuleta madhara zaidi!!!. Kwa sababu hiyo, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaitaka Serikali kwenda mbali zaidi na kubadili mfumo mzima wa utendaji wa Mamlaka ya Mapato Tanzania ili kuleta mageuzi makubwa katika ukusanyaji wa mapato nchini.



MFUMO WA KODI SI RAFIKI KWA WALIPA KODI JAMBO AMBALO LINAPUNGUZA MAPATO YA SERIKALI
Mheshimiwa Spika, mfumo wa kodi umekuwa ukilalamikiwa sana kwa miaka mingi na jamii ya wafanyabiashara ambao ndio walipa kodi wakubwa. Hoja zao ni kwamba, mfumo wetu wa kodi si shirikishi wala si rafiki jambo ambalo limesababisha wafanyabiashara kukwepa kodi na hivyo kupunguza wigo wa walipa kodi na mapato ya Serikali.
Mheshimiwa Spika, Tanzania ikiwa ni moja wapo ya nchi zinazoendelea, inajitahidi sana kurekebisha mfumo wa kodi ili kuweza kuongeza makusanyo ya mapato na kupunguza utegemezi wa misaada ya kibajeti kutoka kwa wahisani. Kambi Rasmi ya Upinzani inatoa pendekezo hili kutokana na kuendelea kupungua kwa makusanyo ya kodi licha ya Serikali hii ya awamu ya tano kutumia mbinu nyingi za kukusanya mapato ikiwa ni pamoja na kuanzisha Kikosi cha Maalum (Special Task Force) cha kukusanya kodi.
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Taarifa ya IMF ya Februari, 2019, uwiano wa kodi kwa pato la taifa (Tax to GDP ratio) kwa sasa; ni takriban 12.8% kwa mwaka 2017/18 ambao ni uwiano wa chini kwa nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara zenye wastani wa 15.1% mwaka 2018. Kiwango hiki cha Tanzania cha 12.8% kinaifanya Tanzania kuwa na safari ndefu sana ya kufikia lengo la uwiano wa 25% uliowekwa kwenye Mkataba wa Sarafu ya Pamoja wa nchi za Jumuiya ya Afrika ya Mashariki.

Jedwali: TAX/ GDP ratio,
Nchi
2013/14
2014/15
2015/16
2016/17
2017/18

Tanzania
12.5%
11.6%
12.9%
13.2%
12.8%

Kenya
19.1%
18.7%
18.8%
19.3%
18.5%

Rwanda
14.5%
15.1%
16.1%
15.2%
18.8%

Uganda
11.3%
12.3%
12.8%
14%
14.2%

Burundi
13.6%
13.7%
13%
13.4%
13%

Kutoka Policy Furum- Tanzania Tax Justice Coalition Position Statement on the 2019/20 National Budget

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Miaka Mitano ni kuwa juhudi zilikuwa zinafaywa ili mapato ya kodi yaongezeke kutoka shilingi trilioni 15.11 mwaka wa fedha 2016/17 hadi shilingi trilioni 25.592 ifikapo mwaka wa fedha 2020/21, ambayo ni sawa na kuongeza uwiano wa Kodi kwa Pato la Taifa kuwa 15.9% kwa mwaka 2020 kutoka uwiano wa 13% uliokuwepo kwa mwaka 2014/15.
Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo Mpango unaeleza wazi kuwa ili kufikia hapo mfumo wa kodi unatakiwa kuwa wazi na haki kwa wadau wote; hivyo ni muhimu kueleza mapungufu hayo yote kwa uwazi. Sasa hivi mfumo wetu wa kodi usio wa haki unatumika kuwanyamazisha wafanyabiashara na kuwa kama ni bakora kwa wafanyabiashara badala ya kusaidia katika kukuza uchumi wetu.
Mheshimiwa Spika, ili kuthibitisa udhaifu wa mfumo wetu wa kodi; na jinsi unavyoliingizia taifa hasara kubwa; Taarifa ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali ya mwaka 2017/18 inaonesha kuwa; Mamlaka ya Mapato ina kesi zilizo katika Bodi ya Rufaa za Kodi, Baraza la Rufaa za Kodi na Mahakama ya Rufaa kwa muda mrefu zenye jumla ya kodi ya Shilingi trilioni 382.6 ambapo, kiasi cha Shilingi trilioni 382 (asilimia 99.84) kimekwama katika Bodi ya Rufaa za Kodi, Shilingi bilioni 65.995 (asilimia 0.02) kimekwama katika Baraza la Rufaa za Kodi, na kiasi kilichobaki cha Shilingi bilioni 548.31 (asilimia 0.14) kinasubiri maamuzi katika Mahakama ya Rufaa Tanzania.
Mheshimiwa Spika,kwa mujibu wa taarifa hiyo ya CAG, ongezeko hili kubwa la kesi za kodi limetokana na uelewa zaidi wa walipakodi na jamii kwa ujumla kuhusu uwepo wa mamlaka za rufaa za kodi na mabadiliko ya taratibu za Bodi ya Rufaa za Kodi ya mwaka 2018 ambazo zimerahisisha namna ya kushughulikia mapingamizi ya kodi. Aidha, kati ya jumla ya kesi za kodi zilizopo katika Bodi ya Rufaa ya Kodi ya shilingi trilioni 382, kuna kesi nne zenye jumla ya kodi ya shilingi trilioni 374.7 sawa na asilimia 98.08 zinahusu kampuni ya uchimbaji madini ya ACACIA. Ikilinganishwa na mwaka wa fedha (2016/17), mapato yaliyokwama katika Mamlaka za Rufaa za Kodi yameongezeka kwa Shilingi trilioni 378.2 (sawa na asilimia 85) kutoka kesi 709 zenye kodi yenye thamani ya Shilingi trilioni 4.4 kwa mwaka 2016/17 hadi kufikia kesi 817 zenye kodi yenye thamani ya Shilingi trilioni 382.6 kwa mwaka 2017/18. Uchambuzi wa Mkaguzi unaonesha kuwa mapato yaliyokwama katika Mamlaka za Rufaa za Kodi ni asilimia
1,206 ya bajeti ya mwaka 2017/2018 na ni asilimia 317.9 ya pato la ndani la Taifa (GDP) kwa mwaka 2017/2018, kiwango ambacho ni unthinkable - hakifikiriki na wala hakikubaliki.
Mheshimiwa Spika, kuongezeka kwa mashauri au kesi za kupinga kodi ni ushahidi wa wazi kuwa mfumo wetu wa kodi sio wa haki wala wa wazi na pia hauwashirikishi walipa kodi jambo ambalo linawalazimu walipa kodi wafungue mashauri kupinga jinsi wanavyolipishwa kodi kwa viwango vya juu isivyo halali.


MGAWANYO USIO WA UWIANO WA FEDHA KATIKA WIZARA
MBALIMBALI UNAVYOATHIRI UTEKELEZAJI WA BAJETI ZA WIZARA HUSIKA

Mheshimiwa Spika, kulingana na kanuni na utaratibu tuliojiwekea, Wizara ya Fedha ina jukumu la kugawa fedha kwa wizara nyingine zote kwa uwiano ulio sawa kwa kuzingatia ukomo wa bajeti uliopangwa kwa mwaka wa fedha husika. Kwa msingi huo, ukomo wa bajeti uliopangwa kwa mwaka wa fedha 2019/20 ni asilimiai 1.9
Mheshimiwa Spika, kinyume cha utaratibu huo, Wizara ya Fedha imevunja rekodi kwa kukiuka masharti ya ukomo wa bajeti uliowekwa, na kujipendelea kwa kujitengea fedha zaidi ya ukomo huo kwa mwaka wa fedha 2019/2020. Ushahidi wa kujipendelea unatokana na ukweli kwamba; katika mwaka wa fedha 2018/19, fungu 21- Hazina; lilitengewa shilingi bilioni 531 kwa ajili ya matumizi ya kawaida; lakini katika mwaka 2019/2020 wamejitengea shilingi trilioni moja (1) na bilioni 302 sawa na ongezeko la asilimia 245 ambazo ni sawa na shilingi bilioni 771. Kwa upande wa fedha za maendeleo mwaka 2018/19 fungu 21 lilitengewa shilingi bilioni 12.6 lakini mwaka 2019/2020 limetengewa shilingi bilioni 806 ikiwa ni ongezeko la shilingi bilioni 793.4 sawa na asilimia 6,700 nje ya ukomo wa asilimia 1.9 . Halikadhalika fungu 50 - Wizara ya Fedha bajeti yake imeongezeka kwa zaidi ya asilimia 15 tofauti na ukomo uliowekwa wa asilimia 1.9.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, inaitaka Serikali kupitia Waziri wa Fedha, kulieleza Bunge hili; uthubutu wa kukiuka masharti ya ukomo wa bajeti unatokana na ubeberu wa wizara hii dhidi ya wizara nyingine au ni kwa ajili ya maslahi ya watu binafsi ndani ya wizara. Tunauliza swali hili kwa kuwa ni jambo la ajabu sana kurundika fedha nyingi namna hiyo kwenye wizara ambayo haizalishi wala haiajiri sehemu kubwa ya watanzania ambao kimsingi ndio wazalishaji wakubwa wanaochangia maendeleo ya uchumi wetu. Serikali hii inayojinasibu kuwa ni Serikali ya wanyonge wanyonge ambao ni wakulima, wavuvi na wafufaji na wafanya biashara ndogondogo; imekataa kuongeza bajeti kwa wizara zinazowagusa moja kwa moja wanyonge hao na kujipendelea yenyewe kwa kujitengea zaidi ya ukomo uliowekwa.

USIMAMIZI MBOVU WA SERA YA FEDHA NI KIASHIRIA CHA KUPOROMOKA KWA UCHUMI WA NCHI
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Instrument ya Mgawanyo wa kazi za Wizara mbalimbali, Wizara ya fedha pamoja na mambo mengine, ina mamlaka na wajibu wa kusimamia sera ya fedha kikamilifu. Hata hivyo, wizara hii imeonyesha udhaifu mkubwa sana wa kutotekeleza madaraka yake ya kisheria kutimiza wajibu huo.
Mheshimiwa Spika, suala la vitambulisho vya wajasiriamali lilitakiwa, kwa mujibu wa sheria, kuratibiwa na kutekelezwa kwa asilimia 100 na Wizara ya Fedha. Kinyume na uhalisia huo, Taifa limebaki kwenye mshangao mkubwa kuona suala hilo likishughulikiwa na vyombo vingine ambavyo havina mamlaka ya kisheria kuhusu masuala ya fedha.
Mheshimiwa Spika, jambo hili limeleta mkanganyiko mkubwa na mgongano wa majukumu miongoni mwa Wizara ya Fedha na Ofisi ya Rais - TAMISEMI. Mpaka sasa Wizara ya Fedha haijatoa tamko au mwongozo wowote, wa namna ya kuendesha zoezi hilo. Matokeo yake kila Mkuu wa Wilaya na Mkuu wa Mkoa anajitengenezea mwongozo wake. Ni Tanzania pekee ambapo Serikali haina mfumo mmoja makini wa utendaji; isipokuwa kila mtu anafanya analojisikia na kwa namna atakavyo ilhali Serikali ni moja. Huku ni kuwachanganya wananchi!!!!
Mheshimiwa Spika, pamoja na vitambulisho vya wajasiriamali kutofuata utaratibu, zoezi hilo limekwenda kunyanganya vyanzo vya mapato vya halmashauri na kuziacha zikiwa muflisi. Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaitaka Serikali kutoa maelezo, ni kwa nini Ofisi ya Rais TAMISEMI inaingilia majukumu ya Wizara ya Fedha? Au ni kwa sababu Wizara ya Fedha ni dhaifu na imeshindwa kutunga na kusimamia utekelezaji wa Sera ya Fedha? Na kama jibu ni ndiyo; kwanini Wizara hiyo isifutwe na badala yake majukumu yake yatekelezwe na kitengo kitakachoanzishwa ndani ya Ofisi ya Rais- TAMISEMI kwa ajili hiyo?


SERIKALI INAKIUKA SHERIA YA BAJETI KWA KUBADILI MATUMIZI YA FEDHA TOFAUTI NA BAJETI ILIYOIDHINISHWA NA BUNGE
Mheshimiwa Spika, Kwa mujibu wa Sheria ya Bajeti ya mwaka 2015 kifungu cha 31, 34(2)(3) na (4); 41(1); 43 na fasili zake zote ni kwamba; Serikali haitakuwa na mamlaka ya kubadili kwa namna yoyote ile bajeti iliyopitishwa na Bunge, bila kuleta mabadiliko hayo Bungeni kwa ajili ya kupata idhini ya Bunge.
Mheshimiwa Spika, kinyume na utaratibu huo wa kisheria; Serikali kupitia Wizara ya Fedha imekuwa ikifanya mabadiliko kwenye bajeti iliyopitishwa na Bunge kimyakimya, bila kuomba ridhaa ya Bunge, jambo ambalo Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inalitafsiri kuwa ni dharau kwa Bunge Bunge ambalo, kwa mujibu wa ibara ya 63(2) ya Katiba ndio chombo kikuu katika Jamhuri ya Muungano chenye madaraka ya kuismimia Serikali katika utendaji wake wa kazi.
Mheshimiwa Spika, mpaka kufikia mwezi machi 2019, Wizara ya Fedha ilikuwa imeshatoa mgawanyo wa matumizi ya kawaida kwa wizara na idara zinazojitegemea, mikoa na halmashauri, kiasi cha shilingibilioni 355.815 zaidi ya bajeti iliyokuwa imepitishwa na Bunge ya shilingi trilioni 20.468 na kufanya jumla ya fedha iliyotolewa kuwa shilingi trilioni 20.824.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaitaka Serikali kutoa malezo kiburi na uthubutu wa kukiuka sheria ya bajeti kwa makusudi vimetoka wapi? Na ni lini tabia hii itakoma? Kitendo cha Serikali kuweka sheria pembeni na kufanya itakavyo kuhusu masuala ya fedha; kikiachwa hivi hivi bila kukomeshwa kitafungua mianya ya ubadhirifu na wizi wa fedha za umma, na matokeo yake ni nchi kuendelea kuogelea kwenye lindi la umasikini licha ya rasilimali nyingi tulizo nazo.
Mheshimiwa Spika, imefika mahali inabidi Bunge lichukue hatua dhidi ya dharau za namna hii. Kwa sababu hiyo; Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inashauri na kupendekeza kwaba, Bunge hili litoe karipio na onyo kali kwa Serikali kwa vitendo vya ukiukaji wa sheria ya bajeti na sheria ya fedha; lakini mbaya zaidi kwa kulidharau bunge kwa kufanya mabadiliko ya bajeti iliyopitishwa na bunge bila kuomba ridhaa ya bunge.

KITENGO CHA KUDHIBITI FEDHA HARAMU KUSHINDWA KUTEKELEZA WAJIBU WAKE
Mheshimiwa Spika, wizara ya fedha ina kitengo cha kudhibiti fedha haramu. Hata hivyo, jukumu hilo kwa sasa linaonekana likifanywa na Mwendesha Mashtaka Mkuu wa Serikali (DPP) jambo ambaolo linadhihirisha uzoefu wa wizara ya fedha kukwepa na kuyakimbia majukumu yake kama ilivyokimbia jukumu la kuratibu vitambulisho vya wajasiriamali.
Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya udhaifu wa kitengo cha kudhibiti fedha haramu, kumekuwa na malalamiko mengi sana kwa wafanyabiashara kubambikiwa kesi za utakatishaji fedha na uhujumu uchumi; kwa kuwa jukumu hilo linafanywa na watu wasiojua sheria za fedha. Kwa sababu hiyo, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaitaka Serikali kutoa maelezo mbele ya Bunge hili; kwamba mamala ya DPP kuingilia shughuli za Financial Inteligence Unit ameyatoa kwenye sheria ipi ya fedha? Kambi Rasmi ya Upinzani inauliza swali hili kwa kuwa inaeleweka kwamba kazi ya DPP ni kumkamata na kumpeleka mahakamani mtuhumiwa aliyebainika na Kitengo hicho kuhusu masuala ya utakatishaji fedha na uhujumu uchumi, na sio kazi ya DPP kuwabaini watu hao kwa kuwa hana taaluma ya mifumo ya fedha.


UTEKELEZAJI DUNI WA BAJETI ZA MAENDELEO KATIKA WIZARA MBALIMBALI HAUNA AFYA KWA MAENDELEO YA UCHUMI NA USTAWI WA WANANCHI
Mheshimiwa Spika, Kwa muda mrefu sasa Serikali kupitia Wizara ya Fedha imekuwa ama ikichelewa kupeleka fedha kwenye wizara na idara mbalimbali za Serikali au kutoa fedha pungufu na katika mazingira mengine kutokutoa fedha kabisa kama ambayo zimeidhinishwa na Bunge. Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni imekuwa ikiitaka Serikali kuandaa makisio yake ya mwaka, yanayoshabihiana na makusanyo ya mapato!!Kwa kufanya hivyo, inatarajiwa kwamba shughuli zilizopangwa zitatekelezwa kama zilivyopangwa.
Mheshimiwa Spika, Hali hii inaondoa umuhimu wa Bunge kukaa kwa gharma kubwa kupitisha bajeti ya Serikali ambayo haitekelezwi ipasavyo. Tofauti na awamu za utawala wa CCM zilizotangulia, Serikali hii ya awamu ya tano ambayo imekuwa ikijigamba kwamba imefanikiwa kukusanya mapato Kwa kiwango cha hali ya juu kuzidi makisio iliyoyaweka kila mwezi, lakini ukweli ni kuwa imekuwa na hali mbaya zaidi katika utekelezaji wa bajeti na hasa bajeti ya maendeleo kuliko awamu zilizopita.
Mheshimiwa Spika, katika kuonesha ukweli huo, zifuatazo ni baadhi ya wizara na fedha za maendeleo zilizotolewa hadi Mwezi Machi, 2019 kulinganisha na fedha zilizokuwa zimeidhinishwa na Bunge hili tukufu:

Wizara ya Maliasili na Utalii
Mheshimiwa Spika, fedha ya maendeleo iliyotengwa kwa ajili ya Wizara ya Maliasili na Utalii ilikuwa kwa mwaka wa fedha 2018/19 ni shilingi bilioni 29.978. Hata hivyo, fedha iliyotolewa hadi kufikia mwezi Februari, 2019 ilikuwa shilingi bilioni 10.551 sawa na asilmia 35 ya bajeti ya maendeleo. Hii ina maana kwamba asilimia 65 ya fedha za maendeleo katika wizara hii hazikutolewa.

Wizara ya Ardhi
Mheshimiwa Spika, Katika mwaka wa fedha 2018/2019 Wizara ya ilitengewa jumla ya shilingi bilioni 30.537 ikiwa ni fedha za maendeleo; lakini hadi kufikia Februari, 2019 fedha iliyokuwa imetolewa ni shilingi bilioni 16.858 sawa na asilimia 55 ya bajeti ya maendeleo. Kwa maana hiyo, asilimia 45 ya bajeti hiyo haikutekelezwa.

Tume ya Ardhi
Mheshimiwa Spika,kwa mwaka 2018/19 Tume ya Ardhi ilitengewa shilingi bilioni 5 kwa ajili ya kugharamia miradi ya maendeleo; lakini hadi kufikia Januari, 2019 hakuna hata senti moja iliyokuwa imetolewa na hazina. Pamoja na Serikali kujigamba kwamba; tengeo la 2018/19 liliongezeka kwa asilimia 234 ikilinganishwa la lile la shilingi bilioni 2.115 la mwaka 2017/18; lakini kama fedha hazikutolewa kabisa ongezeko hilo lina maana gani?

Wizara ya Mifugo na Uvuvi
Mheshimiwa Spika, fedha za miradi ya maendeleo zilizotolewa katika Sekta ya mifugo hadi kufikia Aprili, 2019 ni shilingi bilioni 2.173 sawa na asilimia 43. Aidha, fedha za maendeleo zilizotolewa katika idara ya uvuvi kwa kipindi hicho zilikuwa bilioni 4.012 sawa na asilimia 56.3 ya bajeti iliyopangwa. Hivyo, kwa wastani, utekelezaji wa bajeti ya maendeleo kwa sekta zote mbili, ulikuwa chini ya asilimia 50.

Wizara ya Maji
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2018/19 Wizara ya Maji ilitengewa shilingi bilioni 673.214 kwa ajili ya kugharamia miradi ya maendeleo; lakini hadi kufikia mwezi februari, 2019, ni shilingi bilioni 100.068 sawa na asilimia 14.5 tu ndizo zilizokuwa zimetolewa na hazina.

Mheshimiwa Spika, hii ina maana kwamba asilimia takriba asilimia 85 ya bajeti ya miradi ya maji hakikutekelezwa. Na pia takwimu zinaonesha kuwa fedha za maendeleo zinazotolewa katika wizara hii zimekuwa na mserereko wa kupungua kila mwaka. Huu ni ushahidi tosha kwamba, maji sio kipaumbele kwa Serikali yah ii ya CCM.

Wizara ya Elimu
Mheshimiwa Spika, kati ya miradi ya maendeleo 41 yenye thamani ya shilingi 929,969,402,000/= miradi 24 yenye thamani ya shilingi 100,894,000,000/- haikupatiwa hata senti moja kwa ajili ya utekelezaji wa miradi katika mwaka wa fedha 2018/19.

Wizara ya Kilimo
Mheshimiwa Spika, Wizara ya Kilimo fungu 43 ilitengewa shilingi bilioni 98.119 ikiwa ni fedha za kugharamia miradi ya maendeleo; lakini fedha zilizotolewa hadi kufikia Machi, 2019, zilikuwa shilingi bilioni 41.222 sawa na asilimia 42 ya bajeti ya maendeleo iliyotengwa.
Mheshimiwa Spika, bajeti ya Wizara inayoajiri takriban asilimia 75 ya watanzania; haikutekelezwa kwa asilimia 58. Kwa hiyo, hizi tambo za Serikali kwamba inawajali wanyonge wakati haipeleki fedha kwenye sekta zinazotoa ajira kwa wanyonge hao; ni chukizo hata kwa Mwenyezi Mungu; maana huo ni uongo na ni unafiki!! Na msema uongo si mpenzi wa Mungu!!

Wizara ya Viwanda na Biashara
Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2018/19, Wizara ya Viwanda na Biashara ilitengewa shilingi bilioni 90.5 ikiwa ni fedha za maendeleo. Hata hivyo fedha zilizopokelewa kutoka hazina hadi kufikia Machi, 2019 ni shilingi bilioni 6.477 sawa na asilimia 6.5 tu ya bajeti ya maendeleo.
Aidha, Idara ya Biashara na Uwekezaji Fungu 60 ilikuwa imetengewa shilingi bilioni 7 kwa ajili ya maendeleo; lakini hadi Machi, 2019 hakuna hata shilingi moja iliyokuwa imepokelewa. Hii ina maana kwamba bajeti ya maendeleo katika idara hii haikutekelezwa kabisa.
Mheshimiwa Spika,ni bahati mbaya sana kwamba Serikali hii ya awamu ya tano inatekeleza uchumi wa viwanda kwa kupeleka asilimia 6 ya fedha za maendeleo kwenye Wizara ya Viwanda; na pia bila aibu haipeleki chochote kwenye Idara ya biashara na uwekezaji.
Mheshimiwa Spika, ipo methali isemayo, akutukanaye hakuchagulii tusi; kitendo cha Serikali hii kutotekeleza bajeti ya maendeleo katika Wizara ya Viwanda na Biashara na wakati huohuo ikijivika mabango kuwa kuwa inajenga uchumi wa viwanda ni matusi kwa watanzania kwamba wao ni wajinga, na hawaelewi nini maana ya uchumi wa viwanda ndio maana Serikali haiogopi kuendelea kuwandanganya watanzania.

Wizara ya Madini
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2018/2019 Wizara iliidhinishiwa jumla ya shilingi Bilioni 19.620 kw ajili ya miradi ya maendeleo. Hata hivyo, fedha iliyopokelewa kutoka hazina hadi kufikia February, 2019 ilikuwa ni shilingi shilingi milioni 100 tu, sawa na asilimia 0.5% ya bajeti yote ya fedha zilizotengwa kwa ajili ya shughuli za maendeleo. Kwa uwekezaji duni namna hiyo; tutaendelea kulalamika kuwa tunaibiwa madini lakini tatizo sio wizi bali ni uwekezaji usio na tija. Huwezi kuvuna usikopanda!!!
Mheshimiwa Spika,kwa kifupi, ukitafuta wastani utakuta kwamba bajeti ya maendeleo imetekelezwa chini ya asilimia 50 jambo ambalo ni kikwazo katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Kwa vyovyote vile utekelezaji huu duni unatokana na mipango duni inayoandaliwa na wizara ya fedha kuanzia kwenye kupanga makisio ya bajeti, ukusanyaji wa mapato na ugawanyaji wa fedha kwa kuzingatia vipaumbele vya taifa katika bajeti ya mwaka wa fedha husika.
Mheshimiwa Spika, Wizara ya Fedha haiwezi kukwepa lawama kwa uzembe na udhaifu huo. Kwa mantiki hiyo, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inamtaka Waziri wa Fedha alieleza Bunge hili kuna nini kinamkwamisha katika kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi? Je, ni ukosefu wa rasilimaliwatu wenye ujuzi wa masuala ya mipango; Je ni Seriali imefilisika; au ni mashinikizo kutoka juu; au viatu vya mtangulizi wake vinampwaya.


AKAUNTI YA PAMOJA YA FEDHA KATIKA MASUALA YA MUUNGANO
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa ibara ya 133 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 ni kwamba; Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itatunza akaunti maalum itakayoitwa Akaunti ya Pamoja na ambayo itakuwa ni sehemu ya Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano, ambamo kutawekwa fedha yote itakayochangwa na Serikali mbili kwa kiasi kitakachoamuliwa na Tume ya Pamoja ya Fedha kwa mujibu wa Sheria itakayotungwa na Bunge, kwa madhumuni yay a shughuli za Jamhuri ya Muungano kwa Mambo ya Muungano. Aidha, ibara ya 134 (1) na (2) inasema kuwa kutakuwa na Tume ya Pamoja ya Fedha yenye wajumbe wasiozidi saba ambao watateuliwa na Rais, ambayo pamoja na mambo mengine, itakuwa na majukumu ya kuchambua mapato na matumizi yanayotokana na, au yanayohusu utekelezaji wa mambo ya Muungano na kutoa mapendekezo kwa Serikali mbili kuhusu mchango na mgawo wa kila mojawapo ya Serikali hizo. Aidha, tume hiyo itakuwa na jukumu la kuchunguza wakati wote mfumo wa shughuli za fedha wa Jamhuri ya Muungano na pia uhusiano katika mambo ya kifedha kati ya Serikali mbili.
Mheshimiwa Spika, ibara ya 114 ya Katiba ya Zanzibar inasema kwamba; Fedha zote ambazo ni sehemu ya mchagno wa Muungano na ambazo Serikali ya Mapinzudi Zanzibar inawajibika kulipa, zitakuwa ni gharama itakayotoka Mfuko Mkuu wa Hazina. Aidha, ibara ya 115 ya Katiba ya Zanzibar inasema kwamba; Hakuna fedha itayotumiwa katika Sehemu hii hadi:
Tume ya Pamoja ya Fedha inayohusu mambo ya Muungano kama ilivyoanzishwa na Katiba ya Muungano imechambua mapato na matumizi ya shughuli za Muungano na kutoa mapendekezo yake kwa vyombo vinavyohusika juu ya mgawanyo wa matumizi hayo; na
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuyakubali mapendekezo hayo na mgawanyo wake.
Mheshimiwa Spika, pamoja na Serikali zote mbili kutambua uwepo wa Akaunti ya Pamoja na utaratibu wa namna ya kuchangia; upo mkanganyiko kwenye uwiano wa mgawo wa fedha kwenye akaunti hiyo. Katiba zote mbili ziko kimya kuhusu uwiano wa mgawo wa fedha za Akaunti ya Pamoja kwa Serikali zote mbili kwa mambo ya muungano, jambo ambalo linatoa shaka kwamba pengine kuna Serikali mojawapo na hasa ya Zanzibar haipati mgawo wake kama inavyostahili.
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa taarifa zilizopo ndani ya Serikali zote mbili washirika wa Muungano ni kwamba, tangu mwaka 1977 Serikali ya Muungano haijawahi kutoa fedha yoyote kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kama mgawo wake kutoka kwenye Akaunti ya Pamoja kuhusu mambo ya Muungano kama Katiba ya Jamhuri ya Muungano na ya Zanzibar zinavyoelekeza.

Mheshimiwa Spika, hivi karibuni Serikali ilitoa uwiano wa nafasi za Zazibar na Tanzania Bara katika utumishi wa umma katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa ni 28:72 kwa maana kwamba katika nafasi 100 za ajira katika utumishi wa umma; nafasi 28 zitakuwa za Zanzibar na nafasi 72 zitakuwa za Tanzania Bara. Kwa kuwa hakuna mahali pengine ambapo uwiano wa fursa, rasilimali na mambo mengine ya Muungano umetajwa; Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaamini kwamba uwiano huo wa 28:72 ndio uwiano rasmi wa mgawanyo wa fursa, rasilimali na mambo mengine ya Muungano. Kwa sababu hiyo; uwiano wa makusanyo yote ya fedha za kodi pamoja na mikopo na misaada kutoka nje ambayo ni mambo ya Muungano, sharti yagawanywe kwa uwiano huo.

Mheshimiwa Spika, kwa muktadha huo, kama fedha za kodi au za mikopo na biashara ya nchi za nje ndizo zinajenga SGR na STIEGLERs GORGE, na ikiwa miradi hiyo haimo kwenye mambo ya muungano, maana yake ni kwamba ilitakiwa kwanza fedha hizo zigawanywe kwa uwiano wa 28:72 ili Zanzibar ipate haki yake, na Tanzania Bara ibaki na asilimia yake 72 kwa ajili ya kutekeleza miradi yake ambayo siyo mambo ya Muungano.

Mheshimiwa Spika, kama tangu mwaka 1977, Zanzibar haijwahi kupewa mgawo wake wa fedha za Akaunti ya Pamoja zinazotokana na mambo ya Muungano; maana yake ni kwamba; Mgawo wa fedha za Zanzibar umekuwa ukitumika kutekeleza miradi ya maendeleo ya Tanzania Bara, ambayo haimo katika mambo ya Muungano kwa miaka 42 kinyume na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kinyume na Katiba ya Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa fedha zinazopatikana kupitia mikopo na misaada ya kibajeti kwa Jamhuri ya Muungano ni miongoni mwa mambo ya Muungano; na kwa kuwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imekuwa ikipokea fedha zitokanazo na mikopo na misaada ya kibajeti kwa ajili ya kuziba nakisi ya bajeti; na kwa kuwa kwa mujibu wa ibara za 133 na 134 za Katiba ya SMT, fedha za namna hiyo zinatakiwa kuwekwa kwenye akaunti ya Pamoja; ili zigawiwe kwa Serikali zote mbili kwa ajili ya utekelezaji wa mambo ya Muungano kupitia Tume ya Pamoja ya Fedha; na kwa kuwa tangu mwaka 1977, Zanzibar haijawahi kupata mgawo wake wa fedha kutoka kwenye Akaunti ya Pamoja ya Fedha, na kwa kuwa kwa miaka 42 iliyopita hakuna mradi wowote wa kielelezo ambao ni miongoni mwa mambo ya Muungano uliowahi kutekelezwa Zanziabar; na kwa kuwa deni la Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania linaihusu pia Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar; na kwa kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar haiwezi kukopa nje peke yake; Hivyo, basi; Kambi Rasmi ya Upinzani inashauri na kupendekeza kwamba; Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iipatie Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar mgawo wake wa fedha kwenye Akaunti ya Pamoja ambayo kwa sasa inakadiriwa kuwa takriban shilingi trilioni 50 ikiwa ni malimbikizo ya tangu mwaka 1977.

UWIANO HASI KATI YA MAUZO YA NJE NA MAUNUNUZI YA BIDHAA NA HUDUMA KUTOKA NJE YA NCHI
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa taarifa ya kila mwezi ya mapitio ya Uchumi, inayotolewa na Benki Kuu ya Tanzania, toleo la April, 2019 ni kwamba; kwa kipindi kinachoishia Machi, 2019 Tanzania ilikuwa na nakisi katika biashara ya nje ya dola za Kimarekani milioni 654.8 Kwa kipindi cha hiki cha 2019 nakisi ya akaunti ya mauzo nje ya nchi inaonesha dolla za kimarekani milioni 2,526.8 kulinganisha na dolla za Kimarekani milioni 2,049.3 kwa kipindi cha Machi, 2018. Hii inatokana na kuagiza nje zaidi kuliko tunavyouza bidhaa na huduma nje.
Mheshimiwa Spika, taarifa hiyo inaonesha kuwa; kwa kipindi kinachoishia Machi, 2019, mauzo nje ya nchi yaliongezeka kuwa dolla ya kimarekani milioni 8,544.5 kwa kulinganisha na dolla za Kimarekani milioni 8,488.2 kipindi kama hicho mwaka 2018. Ongezeko hilo lilitokana na mauzo ya bidhaa zisizo asilia zilizokuwa kwa asilimia 78 ya bidhaa zilizouzwa nje na asilimia 40.7 ya mauzo yote nje ya nchi. Mauzo haya yalikuwa ni dhahabu ambayo ni takriban nusu ya bidhaa zisizo za asili kwenye mauzo nje ya nchi.
Mheshimiwa Spika,kwa upande wa manunuzi nje ya nchi, kwa huduma na bidhaa takwimu zinaonesha kuwa hadi Mwezi Machi, 2019 tulitumia bidhaa na huduma zenye thamani ya Dola za Kimarekani milioni 10,550.4 kulinganisha na Dola za Kimarekani milioni 9,916.1 kwa kipindi kilichoishia Machi, 2018. Ongezeko hilo, likichangiwa kwa kiwango kikubwa uagizaji wa mafuta kwa kasi. Aidha uagizaji wa bidhaa za vyakula ulishuka kutokana na mavuno mazuri kwa kipindi cha msimu wa 2017/18.
Mheshimiwa Spika, Wizara ya fedha ndiye mpangaji mkubwa wa uchumi wetu, mvurugano wa kushindwa kuuza nje bidhaa asilia ambazo ni bidhaa za kilimo kama Kahawa, Korosho, Pamba n.k ni kutokana na ukweli kwamba Serikali iliingilia kwa makusudi/ ilihujumu mfumo wa ndani wa ununuzi wa mazao hayo na hivyo kupelekea kukatisha tama wazalishaji wakubwa wa mazao hayo. Hivyo kupelekea kushuka sana kwa mauzo yetu bidhaa za asilia nje ya nchi. Aidha, kwa kuwa Wizara ya fedha imeshindwa kurekebisha mfumo mzima wa uzalishaji hasa kwa kutumia gesi asilia na hivyo kuendelea kutoa mwanya kwa nchi kuendelea kujikita katika matumizi makubwa ya mafuta na hivyo kuendelea kutoa fedha zetu kidogo za kigeni kwenda nje.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kutoa maelezo mbele ya Bunge hili, kuhusu hatua iliyofikia ya uzalishaji wa gesi asilia huko mtwara gesi ambayo kwa kiasi kikubwa ingepunguza manunuzi ya mafuta kutoka nje jambo ambalo limesababisha kuwe na uwiano hasi kati ya mauzo yetu na maununuzi yetu nje ya nchi.

KUPOROMOKA KWA THAMANI YA SHILINGI NA ATHARI ZAKE KATIK UCHUMI
Mheshimiwa Spika, mwenendo wa thamani ya shilingi katika nchi ni moja wapo ya kiashiria kuwa uchumi wa Nchi uko imara au unaelekea kusikojulikana. Thamani ya shilingi yetu inapimwa katika ulinganisho waDola ya Kimarekani, na sarafu nyingine za mataifa ambapo tunafanyia manunuzi.
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa hotuba ya Waziri wa fedha kuhusu hali ya Uchumi wa Taifa iliyosomwa tarehe 13 Juni, 2019, ni kwamba; thamani ya shilingi imeendelea kuwa imara ambapo katika kipindi kinachoishia Aprili 2019 dola moja ya Marekani ilibadilishwa kwa wastani wa shilingi 2,300.9 ikilinganishwa na shilingi 2,270.3 katika kipindi kama hicho mwaka 2018. Kambi Rasmi ya Upinzani inauliza uimara wa shilingi katika takwimu hizo zilizotolewa na Serikali unatokea wapi? Mserereko huu wa shilingi hadi kufikia hapo ulipo ni wa kwanza katika historia ya Tanzania toka tupate uhuru wetu. Hii ni ishara mbaya sana katika uchumi wetu, na jambo hili ndilo limepelekea kwa mara ya kwanza bidhaa ya petrol zimepanda kwa bei ambayo haijawahi kutokea katika nchi yetu. Lita moja ya petrol kuwa shilingi 2,415/- wakati dizeli lita moja ni shilingi 2,385/-, hiyo ni kwa Jiji la Dodoma lakini kwa mkoa wa Kigoma ni shilingi 2,509/- kwa petrol kutoka shilingi 2,349/- mwezi uliopita.
Mheshimiwa Spika, naomba kunukuu kauli ya Makamu wa Rais wa Ghana, Dr. Mahamudu Bawumia wakati akitoa muhadhara wa uchumi alisema kuwa; uchumi unaendeshwa kwa misingi yake na uchumi hauendeshwi kwa propaganda, na kama propaganda zitaendesha uchumi ni dhahiri kuwa mwenendo wa thamani ya fedha exchange rate itaiumbua Serikali hiyo. Hivyo basi, kitendo cha kutokusema ukweli katika suala hili la thamani ya shilingi dhidi ya dola litaleta aibu kubwa sana kwa nchi yetu.
WAKALA WA NDEGE ZA SERIKALI
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa hotuba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, wakati akiwasilisha Bungeni makadirio ya mapato na matumizi ya fedha ya Ofisi hiyo kwa mwaka wa fedha 2019/2020 ni kwamba; Wakala wa Ndege za Serikali uliokuwa chini ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano; umehamishiwa Ofisi ya Rais, Ikulu tangu tarehe 23 Aprili, 2019 kwa Tangazo la Serikali Namba 252.

Mheshimiwa Spika, miongoni mwa majukumu ya Wakala huyo ni pamoja na:-
Kusimamia mikataba ya ukodishwaji wa ndege kwa kampuni ya ndege ya Taifa(ATCL);
Kufanya matengenezo na ununuzi wa vipuri vya ndege za Serikali ikiwa ni pamoja na Ndege zote mpya zilizonunuliwa na Serikali ya awamu ya tano;
Kufanya ukarabati wa karakana ya ndege za Serikali;
Kulipia gharama za bima za ndege;
Kugharamia uendeshaji wa ofisi na kulipia gharama za mafuta ya ndege.
Mheshimiwa Spika, sababu kubwa ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni kusema kwamba, kitendo cha kuhamisha wakala wa ndege za Serikali kutoka Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Masiliano kwenda Ofisi ya Rais Ikulu kuna dalili za kukwepa uwajibikaji katika matumizi ya fedha za umma, ni kutokana na gharama kubwa itakayotumika kuhudumia ndege hizo kama iliyoanishwa katika majukumu ya Wakala huyo katika kipengele ( i v) lakini zaidi sana gharama hizo hazitakaguliwa kutokana na kuhamishiwa katika fungu 20 Ikulu; fungu ambalo huwa halikaguliwi na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali.
Mheshimiwa Spika, sote tunafahamu vilevile kwamba ndege hizi za Serikali zilinunuliwa kishabiki bila kufuata utaratibu wa sheria ya manunuzi ya umma; na manunuzi yakafanyika bila kushindanisha makampuni ya kutengeneza na kuuza ndege, mambo yanayoashiria kwa viwango vyote, mazingira ya rushwa na ufisadi kutokana na kukosekana kwa uwazi katika matumizi ya fedha za umma.
Mheshimiwa Spika, Serikali inajua kwamba ingekuja kuumbuka kama Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali angekuja kufanya ukaguzi wa mchakato wa manunuzi ya ndege za Serikali. Kutokana na hofu hiyo, imeamua kuhamishia wakala wa ndege za Serikali kwenye Ofisi ya Rais Ikulu ili kumfunga mikono CAG wa kutohoji chochote kuhusu mosi, mchakato wa manunuzi ya ndege hizo, lakini pili gharama zitakazoendelea kutumika kuhudumia ndege hizo. Katika mazingira kama hayo, hakuna lugha nyingine ya kutumia zaidi ya kusema kwamba Ikulu imetumika kukwepa uwajibikaji wa matumizi ya fedha za umma na kwa maana hiyo imetumika kama kichaka cha kuficha ufisadi na matumizi mabaya ya fedha za umma.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani ilikuwa na matumaini kwamba; pengine TAKURURU ingetekeleza wajibu wa kuchunguza mwenendo wa matumizi ya fedha za umma katika eneo hili baada ya CAG kufungwa mikono; lakini matumaini hayo yamekufa kwa kuwa TAKUKURU iko chini ya Rais, na kwa sababu hiyo haiko huru kumchunguza Rais. Na hii ndiyo hoja kuu ambayo Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni imekuwa ikiipigia kelele siku zote; kwamba tujenge taasisi imara na huru zitakazotimiza wajibu wao kwa mujibu wa sheria bila kutegemea maelekezo ya mtu au kikundi cha watu wenye nia ya kutimiza maslahi yao binafsi.


MAPATO YA SERIKALI YANAPUNGUA KUTOKANA NA UKOSEFU WA SERA MADHUBUTI YA MAPATO
Mheshimiwa Spika, Kwa uelewa wa Kawaida, dhana ya Bajeti inahusu mchakato wa mapato na matumizi. Lakini kwa bahati mbaya, na kwa kiasi kikubwa Bunge lako Tukufu limejikita sana katika mijadala ya matumizi sana kuliko mapato ya Serikali. Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inapendekeza kwamba, kabla ya kuanza kupanga matumizi ni muhimu kuwa na sera madhubuti ya mapato ambayo itatoa uhalisia wa mapato yaliyopo na baadaye Bunge lako tukufu lijielekeze katika upande mwingine wa matumizi kulingana na mapato ambayo serikali inakusudia kupata.

Mheshimiwa Spika, Kwa miaka yote, Bunge limekuwa likipanga matumizi ya miradi ya maendeleo na matumizi ya kawaida bila ya kuwa limejiridhisha na vyanzo vya mapato vilivyopo na madhara yake ni kwamba, miradi mingi hushindwa kutekelezewa na hivyo Bunge kuonekana kama halitimizi wajibu wake wa kuisimamia Serikali. Haitoshi kwa wizara kuonesha tu kwamba mradi utajengwa kwa fedha za ndani, bila kufahamu fedha hizo za ndani zinatokana na vyanzo vipi vya mapato. Kwa Bunge kukosa fursa ya kujadili vyanzo vya mapato ya Serikali kwa ukamilifu wake kunapelekea Bunge lako tukufu kushindwa kuishauri Serikali juu ya vyanzo vya mapato; lakini pia Seikali inashindwa kuliambia Bunge kwa niaba ya wananchi sababu za kushindwa kukusanya mapato kutokana na vyanzo hivyo kwa kila Wizara.
Mheshimiwa Spika, Serikali kwa nyakati tofauti imekuwa ikifanya makadirio ya mapato kwa mazoea tu, na hivyo kujikuta kila mwaka ikishindwa kufikia hata 50% ya kukusanya mapato kutokana na Serikali kuliomba Bunge kupitisha mapato ambayo hayakufanyiwa utafiti wa kina. Mifano inayodhihirisha hoja hiyo ni kama ifuatavyo:
a). Kodi ya Mishahara - PAYE
Mwaka wa fedha 2017/18 Bunge lilipitisha kodi ya PAYE kwa watumishi wa Serikali ya shilingi 181,869,223,132.00 lakini kiasi halisi kilichokusanywa ni shilingi 75,999,360,973.00 ikiwa ni sawa na 41.7% ya makadirio
PAYE kutoka watumishi walioajiriwa kwenye mashirika, makadirio yalikuwa ni shilingi 68,507,964,093.00 lakini kiasi halisi kilichokusanywa ni shilingi 27,166,781,015.00 ikiwa ni sawa na 39.6% ya makadirio
PAYE kutoka kwa watumishi kwenye sekta binafsi makadirio yalikuwa ni shilingi 652,793,348,248.00 lakini fedha halisi zilizokusanywa ni shilingi 290,484,480,441.00 ikiwa ni sawa 44.5% ya makadirio
b). Individuals Presumptive Tax
Bunge lilipitisha kiasi cha shilingi 168,348,861,855.00 lakini kiasi halisi kilichokusanywa ni shilingi 55,835,601,417.00 ikiwa ni sawa na 33% ya makadirio
c). Payroll/Skills Development Levy
Bunge lilipitisha jumla ya shilingi 138,580,288,635.00 lakini makusanyo halisi yakawa ni shilingi 55,862,033,937.00 ikiwa ni sawa na 40% ya makadirio
d). Ushuru wa bidhaa (Excise duty)
Bunge lilipitisha makadirio ya shilingi 1,091,358,252,595.00 lakini makusanyo halisi yakawa shilingi 359,115,221,579.00 sawa na 32.9% ya makadirio
Mheshimiwa Spika, kwa mifano hiyo michache, Bunge lako tukufu linaweza kuona ni kwa kiwango gani Bunge linapitisha bajeti isiyokuwa na uhalisia wa vyanzo vya mapato. Hii kwa maneno mengine, ni sawa na kusema kwamba, Serikali huwa inafanya makadirio hewa ya vyanzo vya mapato. Tukiangalia kwa mfano makadirio ya kodi inayotokana na wafanyakazi dhidi ya kiwango kinachopatikana, utagundua kwamba; Serikali haina takwimu sahihi za watumishi wake; na ndio sababu ya takwimu za kodi ya mishahara kutofautiana kwa mbali kutoka kwenye makadirio. Kambi Rasmi ya Upinzani inapendekeza kwamba, ni muda mwafaka kwa Bunge lako Tukufu kujiondoa katika aibu hii ya kupitisha bajeti hewa na kwamba kuanzia sasa Bunge lako tukufu lianze kupitia na kujadili uhalisia wa vyanzo vyetu vya mapato ili kuliwezesha kupanga matumizi yanayolingana na makadirio sahihi ya mapato tarajiwa . Aidha, ni muhimu Serikali ikaandaa Sera mahususi itakayoratibu ukusanyaji wa mapato.

VYANZO VYA MAPATO AMBAVYO HAIVITILIWI MKAZO NA SERIKALI
UVUVI
Mheshimiwa Spika, mara nyingi Kambi Rasmi ya Upinzani tumejitahidi kutoa ufafanuzi wa kina ni jinsi gani Sekta ya uvuvi na hasa ile ya uvuvi wa bahari kuu (deep sea fishing) kuwa nchi yetu hatujaitumia vizuri katika kukusanya mapato. Haya ni baadhi ya yale tuliyoshauri, Katika kuhakikisha kuwa Sekta Uvuvi inaleta mabadiliko ya kiuchumi kwa nchi na wananchi kwa ujumla, ni kuwa bandari za Mtwara, Dar es Salaam,Tanga na Zanzibar zitenge maeneo ya bandari za samaki (Fish Ports and Fish Processing plants) ili meli zote za uvuvi wa bahari kuu zilazimike kununua mahitaji yao yote ya mafuta, maji, chumvi na vyakula wanapo kuja kukaguliwa kwa ajili ya kukusanya mapato. Aidha, njia hii itakuza uchumi wa mtu mmoja mmoja kwa maana ya kuwepo kwa kile kinachoitwa forward and backward linkage Kwa uamuzi huu wa kuweka mazingira wezeshi tu ni dhahiri mapato yangeongezeka mara dufu zaidi ya yale yanayokusanywa hivi sasa.

SEKTA YA MIFUGO
Mheshimiwa Spika, sekta hii imekuwa ikichukuliwa kwa uzito mdogo na imekuwa haipewi heshma inayostahiki. Ni matumaini ya Wafugaji,baada ya kuwa na wizara maalum,hali ya wafugaji ikabadilika kwa kuwa na madawa,majosho na maeneo maalum ya malisho ya mifugo yao.
Mheshimiwa Spika,kama ilivyo kwa mazo ya baharini na kwenye maziwa,mifigo inaweza kuwa kichecheo kikubwa cha mapato ya haraka kama ushirikiano wa wafugaji na serikali utaimarishwa zaidi ili kutumia masoko kama ya SAUDI ARABIA ambao kwa wastani huagizia ma milioni ya mbuzi,kondoo na nyama kutoka nchi mbali duniani kwa matumizi yao,ibada ya Hijja na Umra. Uganda imepewa order ya mbuzi 100000 kwa mwaka. Na sisi tunaweza kutumia fursa ya masoko haya kama tutawapa hudma stahili wafugaji wetu
REAL ESTATE REGULATORY AUTHORITY
Mheshimiwa Spika, Vile vile, Kambi ya Upinzani hapo awali tulipendekeza kuanzishwa kwa Real Estate Regulatory Authority- ili kila mwenye nyumba ya kupangisha atambuliwe na kulipa kodi inavyostahili, jambo ambalo kwa sasa halifanyiki na badala yake wale wasiokuwa na hela ndio wanaosumbuliwa mno kulipa kodi ya majengo. Lengo la kutoa pendekezo hilo ni kuhakikisha Sekta ya Nyumba inatoa mapato ya kutosha kwa Serikali na kuzuia mianya ya ukwepaji kodi inayofanywa na wenye nyumba.
KODI DHANIWA - PRESUMPTIVE TAX
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni ilipendekeza mwaka 2011/12 kwamba ushauri wa Mradi wa kuboresha mfumo wa kodi (Tax Modernization Project) ambao ulishauri kwamba ipo haja kwa Presumptive Tax anayotozwa kwa mfanyabiashara ndogondogo kabla hajaanza kufanya biashara ifutwe kabisa. Na tunarudia tena kuwa kodi hii badala ya kushamirisha biashara kwa kuingiza wafanyabiashara kwenye mfumo rasmi wa kodi inawafanya watu kuendelea kutokuwa kwenye mfumo rasmi wa kodi. Lakini ni wazi kuwa kufutwa kwa kodi hiyo itakuwa ni kichocheo kikubwa cha kuongeza wigo wa kodi. Hii inaweza kuwa hasara katika kipindi cha muda mfupi lakini itakuwa ni chanzo kikubwa sana cha mapato katika kipindi cha muda mrefu.

T. UWAJIBIKAJI MDOGO WA SERIKALI KATIKA UTEKELEZAJI WA MPANGO WA TAIFA WA MAENDELEO
167. Mheshimiwa Spika, Serikali ndiyo yenye wajibu wa kwanza katika kusimamia utekelezaji wa Mipango ya Maendeleo nchini. Hata hivyo, Serikali imekuwa na tabia ya kukwepa kutimiza wajibu huo kikamilifu.
168. Mheshimiwa Spika, misingi ya uwajibikaji katika kutekeleza Mpango wa Maendeleo ipo kikatiba na kisheria. Mathalani, Ibara ya 63(3)(c) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya 1977 inalipa Bunge mamlaka ya kujadili na kuidhinisha Mpango wowote wa muda mrefu au wa muda mfupi unaokusudiwa kutekelezwa katika Jamhuri ya Muungano, na kutunga sheria ya kusimamia utekelezaji wa mpango huo. Lakini, kwa miaka yote, Serikali imekuwa ikigoma kuleta miswada ya sheria ili bunge litekeleze madaraka yake kwa mujibu wa ibara ya 63(3)(c) ya katiba kutunga sheria ya kusimamia mipango inayoidhinishwa na Bunge.
169. Mheshimiwa Spika, jambo hili tumelipiga kelele sana, lakini Serikali hii ya CCM imeamua kuweka pamba masikioni. Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inatafsiri mgomo huo wa Serikali kuleta miswada ya sheria ya kusimamia utekelezaji wa mipango ya maendeleo kama kukwepa kuwajibika, lakini mbaya zaidi ni kwamba Serikali inavunja katiba kwa makusudi. Hii ni kwa sababu hitaji la kutunga sheria ya kusimamia mipango inayoidhinishwa na Bunge ni takwa la kikatiba na sio hiari. Kutotekeleza takwa hilo, ni kuvunja Katiba.
170. Mheshimiwa Spika, uthibitisho mwingine kuwa Serikali inakwepa kuwajibika katika kuisimamia kikamilifu mipango ya maendeleo ni kitendo chake cha kuifanyia marekebisho sheria ya bajeti ambayo inatoa mwongozo wa uwajibikaji wa kifedha/kibajeti (financial accountability) katika kutekeleza miradi ya maendeleo. Serikali ilileta mapendekezo ya kuvifanyia marekebisho vifungu vya 41, 53, 56, 57 na 63 vya sheria ya bajeti ya 2017 kwa kuondoa wajibu wa Serikali wa kuwasilisha kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali na Bungeni ripoti ya matumizi ya fedha kwa kila robo mwaka ya mzunguko wa bajeti (yaani kila baada ya miezi mitatu) ambapo sasa ripoti hiyo itakuwa ya nusu mwaka wa mzunguko wa bajeti (yaani kila baada ya miezi sita).
171. Mheshimiwa Spika, athari za marekebisho hayo ya sheria ya bajeti ni kudumaza ufuatiliaji thabiti (tight follow-up) wa utekelezaji wa bajeti ya Serikali; na jambo hilo linaweza kupelekea utekelezaji mbovu wa bajeti kutokana na matumizi yasiyofaa au hata ubadhirifu wa fedha za umma. Nasema hivi kwa sababu ikiwa ripoti ya matumizi ya Serikali itatolewa kwa kila nusu mwaka wa utekelezaji wa bajeti, maana yake ni kwamba, ripoti hiyo itatoka wakati mchakato wa maandalizi ya mpango wa maendeleo na bajeti ya mwaka wa fedha unaofuata ukiwa umeshaanza. Kwa hiyo, ripoti hiyo inakuwa haisaidii katika kufanya tathmini ya utekelezaji wa bajeti katika mwaka wa fedha unaoendelea (current financial year) ili hatimaye kuweza kufanya makisio na maoteo ya bajeti inayofuata.
172. Mheshimiwa Spika, ili mapendekezo haya ya Mpango wa Maendeleo yawe na tija, Kambi Rasmi ya Upinzani inashauri na kupendekeza kwamba; Serikali ilete muswada wa marekebisho ya sheria ya bajeti ili kurejesha vile vifungu vilivyokuwa vinaelekeza ripoti za matumizi ya fedha ziwe zinaletwa kila baada ya miezi mitatu (robo mwaka). Kwa kufanya hivyo, kwanza kutakuwa na ufuatiliaji madhubuti wa matumizi ya Serikali, lakini pia ripoti za robo mwaka, zitawezesha kufanya tathmini ya mwenendo wa utekelezaji wa bajeti na hivyo kuisadia Serikali kujipanga vizuri zaidi kwa bajeti zinazofuata.

MKANGANYIKO WA TAKWIMU ZA PATO LA TAIFA
173. Mheshimiwa Spika, kiashiria kikuu cha ukuaji wa Uchumi ni mwenendo wa ukuaji wa Pato la Taifa. Hataa hivyo, takwimu za Pato la Taifa zinazotolewa na Serikali, zimekuwa zikitofautiana jambo ambalo linatia mashaka juu ya usahihi wa Pato halisi la Taifa. Kwa mfano, Taarifa ya Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa mwaka 2019/20 iliyotolewa Mwezi Oktoba 2018, katika ukurasa wa 4 aya ya 2.2.3.1 inasema kuwa, Pato la Taifa lilikuwa shilingi milioni 125,624,406 mwaka 2017 ikilinganishwa na shilingi milioni 111,537,022 mwaka 2016.

174. Mheshimiwa Spika, Aidha, ukiangalia Taarifa ya Mapendekezo ya Serikali ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa mwaka 2019/20 iliyoletwa kwenye kamati ya Bajeti Machi 2019 katika ukurasa wa 6 aya ya 2.2.2.2 inasema kuwa; katika kipindi cha Januari hadi Septemba 2018, Pato halisi la Taifa lilifikia shilingi trilioni 84.46 kutoka shilingi trilioni 79.19 katika kipindi kama hicho mwaka 2017 sawa na ongezeko la asilimia 6.7 ikilinganishwa na kiwango cha ukuani wa asilimia 6.2 mwaka 2017.

175. Mheshimiwa Spika, Sambamba na hilo ukisoma Taarifa ya Hali ya Uchumi wa Taifa iliyowasilishwa hapa Bungeni tarehe 13 Juni, 2019, katika ukurasa wa 7 aya ya 14 anasema kuwa, Pato la taifa kwa bei za mwaka husika lilikuwa shilingi trilioni 129.4 mwaka 2018 ikilinganishwa na shilingi trilioni 118.7 mwaka 2017.

176. Mheshimiwa Spika, Kutokana na takwimu za Pato la Taifa kutofautiana; Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaitaka Serikali kutoa takiwimu sahihi za Pato la Taifa ili kuwe na uelewa wa pamoja kuhusu pato hilo; lakini pili kutoa fursa kwa waheshimiwa Wabunge kujadili hali ya uchumi wa taifa kwa kutumia takwimu sahihi.

UWEKEZAJI KATIKA RASILIMALI WATU KWA MAENDELEO ENDELEVU (INVESTING ON HUMAN CAPITAL FOR SUSTAINABLE DEVELEOPMENT)

177. Mheshimiwa Spika, ni nadharia na uzoefu wa kawaida kwamba; taifa lolote linalotaka kujitegemea na kujinasua kwenye dimbwi la utegemezi na umasikini linajitahidi sana kuwajengea watu wake uwezo wa ki-elimu, ki-ufundi na maarifa ili kuweza kukabiliana changamoto mabalimbali na hivyo kuweza kuyamudu mazingira yao. Kwa sababu hiyo; taifa la namna hiyo, huwekeza sana katika elimu ili kuandaa wataalamu (rasilimali watu) wa kutosha wenye weledi wa kuendesha sekta mbalimbali za uchumi.

178. Mheshimiwa Spika, ni kwa sababu hiii, Serikali ya awamu ya kwanza ilikuja na sera ya Elimu ya Msingi kwa Wote - Universal Primary Education na kujikita sana kwenye elimu ya kujitegemea ambayo iliwapatia wengi maarifa ya kujiajiri na kuendesha maisha yao. Hata elimu ya juu iligharamiwa kwa asilimia 100 na Serikali.
179. Mheshimiwa Spika, Licha ya nchi yetu kuwa bado kwenye dimbwi la umasikini; na licha ya kuwa bado nchi inakabiliwa na upungufu mkubwa sana wa rasilimali watu, Serikali hii ya awamu ya tano imechagua kuwekeza katika vitu badala ya watu. Ni kweli tunahitaji maendeleo ya vitu kama tunavyoona Serikali ikijenga reli ya kisasa, viwanja vya ndege, kununua ndege, ujenzi wa mabarabara nk. lakini nachelea kusema kwamba vitu hivyo vinaweza kudumu kwa muda mfupi mno kama hatutawajengea watu wetu uwezo wa kuvifanya wenyewe na kuviendesha. Kambi Rasmi ya Upinzani ingefurahi kuona makandarasi wa kujenga reli ya kisasa; na hata mabarabara yetu wakiwa ni watanzania wenzetu. Lakini tathmini fupi inaonyesha kuwa miradi mikubwa ya maendeleo hapa nchini iko mikononi mwa makandarasi wageni. Watu wetu wanaambulia kazi za kuchimba mitaro, kubeba mizigo na kufanya kazi zile ambazo hazihitaji ujuzi na matokeo yake hata ujira wao ni ule wa mboga tu.

180. Mheshimiwa Spika, Katika ulimwengu wa utandawazi, ufunguo wa mafanikio ya kiuchumi unategemea sana uwezo wa nchi kupata na kutumia ujuzi/maarifa kwa ufanisi na kwa faida katika sekta za kipaumbele na ambazo zinaweza kukua. Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kufanya uwekezaji mkubwa katika rasilimali watu, kwa kuwa watu wenye ujuzi ndio msingi mkuu wa kuwepo kwa mfumo wa viwanda unaochochea ukuaji wa uchumi. Uwekezaji katika vitu na katika taasisi ni vikamilisho muhimu vya rasilimali watu; kwani rasilimali (vitu) haitatumiwa vizuri, iwapo itakosa ujuzi wa kiufundi na kiuongozi.
 
MIRADI YA SERIKALI ISIYOKUWA NA MPANGO MKAKATI WA KIBIASHARA
181. Mheshimiwa Spika, Serikali ya awamu ya tano inatekeleza miradi ambayo sisi tunaona ipo kisiasa zaidi na hakuna mkakati wala mpango wa kibiashara ambao umewekwa wazi na Serikali hadi sasa.Naomba kutoa ufafanuzi na uchambuzi kwenye miradi mitatu yaani Mradi wa Reli ya Standard Gauge (SGR), Ujenzi wa Mradi wa Kuzalisha Umeme- MW 2,100 maarufu kama Stieglers Gorge na Kufufua Shirika la Ndege (ATCL) ambao Serikali imejikita kwenye mradi wa ununuzi wa Ndege;
Mradi wa Reli ya Standard Gauge
182. Mheshimiwa Spika, Mradi wa Reli ya Kisasa kutoka Dar es-Salaam hadi Mwanza ambao unatarajiwa kugharimu Trilioni 17.6 na unatarajiwa kukamilika 2021, ambapo kwa sasa umeanza kutekelezwa kuanzia Dar-es-Salaam- Morogoro KM 205 na Morogoro Makutupora KM 422 hauna mkakati endelevu wa kufungamanisha sekta za kiuchumi na mradi huo. Hakuna anayeweza kubisha au kupinga kuwa kama nchi tunahitaji reli ya kisasa kwa ajili ya kurahisisha shughuli mbalimbali za maendeleo. Hata hivyo, Serikali imejikita kwenye ujenzi wa miundombinu ya reli pekee na sio kufanya uchambuzi wa mradi mzima kuanzia utaratibu wa kuwa na mabehewa ya kisasa, mfumo wa uendeshaji ikiwemo kutoa mafunzo kwa madereva wataoendesha treni hizo, mafunzo kwa watoa huduma, mafunzo kwa watakaokuwa wanafanya shughuli za ukarabati wa miundombinu ya SGR. Aidha, Serikali haijaweka wazi na wala haina mpango wa kuendesha mradi wa SGR kibiashara zaidi ya kupiga porojo za Miundombinu pekee jambo ambalo linaonyesha kuwa tunaweza kuwa na mradi utakaolitia Taifa hasara. Taarifa zinaonyesha kuwa SGR inajengwa kwa mikopo ya masharti ya kibiashara ambapo Taifa litalazimika kuanza kulipa madeni ya mradi huu kabla haujakamilika.
Mradi wa Kufua Umeme wa Maji katika Bonde la Mto Rufiji - Stieglers Gorge Hydro Power Project
183. Mheshimiwa Spika, Mradi huu unategemewa kuzalisha MW 2100 kwa kutumia maji (Hydro Power Plant) katika Bonde la Mto Rufiji. Mpaka kukamilika kwa mradi kwa utafiti wa NORCONSULT wa mwaka 2006 mradi ulikisiwa kugharimu kiasi cha Tshs. Trillion 4 (Dola bilioni 2) Hata hivyo, kutokana na ukosefu wa mpango madhubuti wa utekelezaji, kuna mashaka kama mradi huo utafikia malengo yaliyokusudiwa. Hii ni kwa sababu tayari ipo mifano ya miradi iliyojengwa kwa kutumia fedha nyingi na faida zake hazionekani. Kwa mfano, Itakumbukwa kuwa Serikali ilitumia takribani trilioni 1.2 kujenga bomba la gesi kutoka Mtwara hadi Dar-es-Salaam. Taarifa zinaonyesha kuwa kwa sasa Bomba la gesi hutumika kwa 6% pekee, kama Serikali itaweza kulifanya Bomba kutumika kwa 25% linawez kuzalisha MW 2000 takribani sawa na mradi wa Trilioni 7 wa Stiglers Gorge. Bomba likitumika kwa 100% litaweza kuzalisha MW 10,000. Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kulieleza Bunge; Ni sababu zipi zinazoifanya serikali kutoendelea kuwekeza kwenye umeme wa gesi ambao miundombinu ipo tayari na kukimbilia kwenye mradi wa Stieglers Gorge ambao unagharimu Taifa trilioni 7? Aidha, Kambi Rasmi ya Upinzani inaendelea kusisitiza kwamba haioni tija katika mradi huo zaidi ya kuliingiza taifa kwenye mzigo wa madeni kutokana na Serikali kukopa fedha za kuutekeleza mradi huo.
Kufufua Shirika la Ndege
Mheshimiwa Spika, Serikali imekua ikinunua Ndege kwa ajili ya kulifufua Shirika la Ndege la ATCL. Hata hivyo, Mfumo wa Manunuzi ya Ndege haujawekwa wazi hata baada ya Kambi kuhoji kwa miaka miwili mfululizo na kibaya zaidi sasa wakala wa ndege umehamishwa kutoka wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano na kwenda Ikulu kwa makusudi ili kukwepa ukaguzi wa hesabu kutoka kwa CAG. Ikumbukwe kwamba; ATCL inategemea ruzuku ya Serikali na kwa sababu hiyo, ni lazima hesabu zake zikaguliwe na CAG. Hivyo ukwepaji wa ukaguzi wa hesabu uliofanywa kimkakati kwa kuhamishia masuala ya ndege Ikulu kuna kila dalili ya hila mbaya ya kuficha ubadhirifu na matumizi mabaya ya fedha za umma.
Mheshimiwa Spika, Ili Ndege iweze kuwa na faida ni lazima itumie muda mwingi kusafiri na sio kuwa kukaa kwenye Viwanja vya Ndege. Kwa sasa nchini kuna Viwanja vine pekee ambavyo vina taa kwa ajili ya ndege kutua na kuruka usiku. Kwa hiyo ndege za Serikali haziwezi kutengeneza faida. Pili, Hakuna mkakati wowote wa kibiashara wa kimataifa kwenye uboreshaji wa Shirika la Ndege. Hakuna mkakati wowote wa kuwa na Ndege za mizigo hasa mbogamboga na maua kwa ajili ya kusafirisha kwenda nje ya nchi. Mapungufu yote haya yanadhihirisha kukurupuka kwa Serikali bila kuanzisha miradi ya kisiasa bila kuwa na mipango mkakati ya utekelezaji wa miradi hiyo. Ni Tanzania pekee ambapo miradi inabuniwa halafu mpango wa utekelezaji ndio unafuata. Kwa hali hiyo, hatuwezi kusonga mbele.
VIPAUMBELE VYA BAJETI MBADALA
Mheshimiwa Spika, Bajeti mbadala ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni itakua na vipaumbele katika sekta zafuatazo;
Elimu
Kilimo, Mifugo na Uvuvi (agrarian revolution)
Viwanda katika mnyororo wa thamani wa Kilimo (Agro- Processing Industries
Afya na Maji
Utawala Bora (Good Governance)

Mheshimiwa Spika, pamoja na vipaumbele hivyo; naomba kuweka msisitizo kidogo katika Utawala Bora kwa kuwa Serikali hii imepuuza kabisa dhana ya utawala Bora jambo ambalo limeleta athari kubwa sana katika uchumi na hata mahusiano yetu kitaifa na kimataifa.
Mheshimiwa Spika, uchumi imara ni matokeo ya utawala bora. Ujenzi wa uchumi imara ni matokeo ya moja kwa moja na utawala bora katika nchi. Ukuaji wa uchumi ni lazima uende sambamba na utawala bora. Lakini katika nchi nchi yetu kumekuwa na mambo yanayoifanya nchi yetu isiwe mahala salama kwa ajili ya uwekezaji. Matukio yafuatayo yanaathiri uwekezaji pamoja na utekelezaji wa Bajeti;

Kukwama kwa mchakato wa Katiba Mpya
Tishio la Watu wasiojulikana kuteka, kutesa, kujeruhi na kuwauwa wananchi
Kuminywa kwa Vyombo vya Habari na uhuru wa kupata na kupokea habari kwa kutumia Sheria ya Huduma za Habari pamoja na Makosa ya Mtandao.
Kuminya demokrasia kwa kukataza mikutano ya hadhara ya vyama vya siasa na kutunga sheria kandamizi za kudhibiti siasa na demokrasia.
Kuweka kando utawala wa sheria na badala yake kuongoza nchi kwa utashi wa mtu mmoja.
Kuweka kando mifumo ya kitaasisi katika utendaji na badala yake kutegemea maelekezo ya mtu mmoja.
MAPENDEKEZO YA MPANGO WA KUFUNGAMANISHA KILIMO NA MAENDELEO YA VIWANDA (AGRO ECONOMY)

Mheshimiwa Spika, Sekta ya kilimo inachangia ajira kwa asilimia 70, pato la taifa kwa asilimia 28.2 lakini ukuaji wake unakuwa kidogo sana kwa wastani wa asilimia 5.2 na hivyo kuwa na mchango mdogo sana katika sekta ya viwanda. Kambi Rasmi ya Upinzani italenga kufanya yafuatayo ili kufungamanisha kilimo na uchumi wa viwanda:-

Kuondoa kodi kwenye uwekezaji katika sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi.Hii ni pamoja na kuondoa kodi kwenye viwanda vinavyotengeneza na kukarabati mashine, zana na pembejeo za kilimo, uvuvi na mifugo.
Uwepo wa umeme wa uhakika ili kuendesha shughuli za uzalishaji viwandani. Hivyo, itawekeza ipasavyo katika umeme wa gesi asilia.
Kushirikisha sekta binafsi kupitia mpango wa (PPP) ambapo serikali itawekeza kwenye mitaji ya uwekezaji kwa asilimia 40 na sekta binafsi itashirikishwa kwa asilimia 60.
Kuongeza idadi ya ajira kwa vijana kupitia sekta ya kilimo na viwanda.
Kuongeza pato la mwananchi mmoja mmoja na pia Serikali itapanua wigo wa kodi.
Kusisimua sekta ya usafirishaji na mauzo nje ya nchi.

BAJETI YA SERIAKALI IMEONGEZA MZIGO KWA WANANCHI

Mheshimiwa Spika, serikali katika mwaka wa fedha 2019/20 inapendekeza kufanya marekebisho katika baadhi ya sheria ili kubadilisha viwango vya kodi, baadhi ya sheria hizo ni shaeria ya kodi ya ongezeko la thamani, Sura 148, sheria ya kodi ya mapato, sura 332, sheria ya ushuru wa bidhaa, sura 147, sheria ya usalama barabarani, sura 168, sheria ya forodha ya jumuiya ya Afrika ya mashariki ya mwaka 2004 n.k.
Mheshimiwa Spika, katika marekebisho ya sheria hiyo kuna sheria ya forodha ya Jumuiya ya Afrika ya Mashariki ya mwaka 2004 ambayo pamoja na mambo mengine inapndisha kodi katika vifaa vya ujenzi (mabati na nondo). Kutokana na hali hiyo, bei ya bidhaa na vifaa mbalimbali vinavyotumika kwa ajili ya ujenzi zitaendelea kupanda na hivyo kuathiri azma ya serikali ya ujenzi wa makazi bora na ya kudumu. Mara kadhaa Serikali hii hii imekuwa ikisisitiza kupunguza kodi kwenye vifaa vya ujenzi ili watanzania waweze kujenga nyumba bora; lakini cha ajabu Serikali hiyohiyo, imekuwa na ndimi mbili katika jambo hilo. Kwa mfano, Mei 6, 2014 aliyekuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi alishauri kupunguzwa au kuondolewa kwa kodi katika vifaa vya ujenzi ili watanzania wengi waweze kujenga nyumba bora. Aidha, September 5 2018, akiwa mjini Mwanza kushuhudia utiaji saini wa mikataba minne ya ujenzi wa meli kubwa ya abiria na mizigo ya Serikali, chelezo na ukarabati wa meli za MV Butiama na MV Victoria, Rais John Magufuli alizungumza mambo mengi na kutoa maelekezo kwa watendaji wa Serikali. Miongoni mwa maelekezo aliyoyatoa ni pamoja na kuwaagiza Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano na Waziri wa Fedha na Mipango, kukutana haraka ili kumaliza kilio cha kodi kwenye vifaa vya ujenzi.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inashangaa kuona Waziri wa Fedha akikaidi agizo la Rais la kupunguza kodi kwenye vifaa vya ujenzi na badala yake kupandisha kodi hiyo. Kambi Rasmi ya Upinzani inaamini kuwa punguzo la vifaa vya ujenzi hasa mabati, cement, vifaa vya mabomba ya plastiki na nondo ni hatua mojawapo ya kuelekea kwenye Tanzania ya makazi bora. Kuwa na makazi bora ni mkakati wa kuwa na ongezeko la kodi la uhakika la kodi ya majengo Property tax.

Mheshimiwa Spika, kuhusu punguzo la ushuru wa forodha kutoka 100% hadi 35% kwa mwaka kwenye sukari ya matumizi ya kawaida inayoagizwa kutoka nje ya nchi kwa vibali maalum kwa lengo la kuziba pengo la uzalishaji. Kambi rasmi ya upinzani inaona hatua hii sio kama inaleta tija kwa viwanda vya ndani bali italeta balaa kubwa kwa wakulima wa miwa, kwani sukari nyingi itaingizwa na sukari inayozalishwa ndani itashindwa kuwa na ushindani na hivyo viwanda vitashindwa/vitaacha kununua miwa ya wakulima.

ZA. BAJETI YA SERIKALI IMEJIKITA KWENYE MAENDELEO YA VITU NA SIO MAENDELEO YA WATU
Mheshimiwa Spika, uchambuzi uliofanywa na Kambi Rasmi ya Upinzani kuhusu mgawanyo wa fedha za maendeleo umebaini kwamba; bajeti imejikita kwenye maendeleo ya vitu na sio maendeleo ya watu. Kwa mfano; katika bajeti ya shilingi trilioni 33.104; fedha za maendeleo ni shilingi trilioni 12.25 sawa na asilimia 37 ya bajeti yote. Hata hivyo, mchanganuo wa bajeti ya maendeleo unajumuisha fedha za ndani kiasi cha shilingi trilioni 9.74na fedha za nje kiasi cha shilingi trilioni 2.51.
Mheshimiwa Spika, mgawo wa fedha hizo ni kama ifuatavyo:-
shilingi trilioni 2.48 sawa na asilimia 20.245 ya bajeti yote ya maendeleo ni kwa ajili ya Mradi wa Ujenzi wa Reli kwa kiwango cha Kimataifa (SGR)
shilingi trilioni 1.44 sawa na asiliia 11.755 ya bajeti yote ya maendeleo ni kwa ajili ya Mradi wa Kufua Umeme katika mto rufiji 9( Stiegler’s Gorge Hydoro Power Project) na
shilingi bilioni 500 sawa na asilimia 4.081 ya bajeti yote ya maendeleo ni kwa ajili ya kumalizia malipo kwa ajili ya ununuzi wa Ndege za Serikali.
Mheshimiwa Spika,miradi hiyo mitatu imechukua shilingi trilioni 4.42 ambayo ni sawa na asilimia 36.081 ya fedha zote za maendeleo. Hii miradi ipo kwenye wizara mbili tu, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano pamoja na wizara ya Nishati. Pamoja na miradi hiyo michache kuchukua sehemu kubwa ya bajeti ya maendeleo; bado miradi hiyo haina faida za moja kwa moja katika uchumi wan chi yetu na wake. Hii inatokana na ukweli kwamba malighafi inayotumika kujenga SGR (Chuma na cement) karibu zote zinatoka nje ya nchi na hivyo fedha zinaondoka katika mzunguko wa ndani na kupelekwa nje kwa ajili ya ununuzi wa malighafi hizo. Aidha, ajira zinazozalishwa haziingizi chochote kwenye bajeti yetu kamakdoi ya mshahara (PAYE) kwa kuwa wengi walioajiriwa katika mradi huo ni vibarua (casual laborers) ambao hawapo kwenye mfumo wa kodi. Kwa maneno mengine, hii ni miradi ambayo inanyonya uchumi wetu kwa kutoa fedha ndani na kuzipeleka nje; lakini pili haina multiplier effect katika kuchechemua sekta nyingine za kiuchumi kama vile biashara na ajira.
Mheshimiwa Spika,Kutokana na bajeti hii kuweka kipaumbele katika maendeleo ya vitu badala ya maendeleo ya watu; sekta nyingine zinazogusa maisha ya watu moja kwa moja zimepata mgawo mdogo sana wa fedha za maendeleo jambo linaloashiria kwamba Serikali hii haina mpango na maendeleo na ustawi wa watu. Hata hivyo, miradi na sekta ambazo Serikali inasema ndiyo vipaumbele vyake, nayo imepata mgawo mdogo jambo ambalo linaleta mkanganyiko kuhusu vipaumbele vya Serikali. Mgawo wa fedha kwenye sekta hizo ni kama ifuatavyo:-
Wizara ya Viwanda na Biashara ambayo ndiyo kipaumbele cha kwanza katika bajeti ya Serikali, imetengewa shilingi bilioni 51.5 sawa na asilimia 0.42 ya bajeti nzima ya maendeleo.
Wizara ya Kilimoimetengewa shilingi bilioni 134.577 sawa na asilimia 1.098 ya bajeti ya yote maendeleo.
Wizara ya Elimu imepewa shilingi bilioni 863 ambayo ni sawa na asilimia 7.045 ya bajeti nzima ya maendeleo;
Afya imepewa shilingi bilioni 544.137 sawa na asilimia 4.44 ya bajeti yote ya maendeleo;
Maji yamepewa shilingi bilioni 610.5 sawa na asilimia 4.98 ya fedha zote za maendeleo.
Mheshimiwa Spika, kwa mwenendo huo wa mgawo wa fedha za maendeleo, ni dhahiri shahiri kwamba Serikali hii inayojinasibu kuwa ni ya wanyonge; haipendi wanyonge hao waishi kwa neema kwa kupata huduma bora za kijamii kama vile afya, elimu, maji safi na salama, au kuwekeza katika kilimo chao kinachowapatia ajira na chakula; isipokuwa inawekeza katika vitu ambayo hao wanyonge hawatakuwa na uwezo wa kuvitumia pia.
ZB. BAJETI YA SERIKALI IMEWASAHAU WATUMISHI WA UMMA AMBAO NI WALIPA KODI WA UHAKIKA
Mheshimiwa Spika,bajeti ya Serikali imewasahau kabisa watumishi wa umma ambao toka Serikali hii ya awamu ya tano iingie madarakani hawajawahi kupata nyongeza ya mishahara ya kila mwaka (annual increment) licha ya madai mengine wanayoidai Serikali ikiwa ni pamoja na fedha za likizo; kupandishwa madaraja; malimbikizo ya mishahara na stahili nyingine za kikanuni.
Mheshimiwa Spika, Ikumbukwe kwamba watumishi wa umma ndio walipa kodi wa uhakika kupitia kodi ya mshahara (PAYE) hivyo kutowapandishia mishahara si tu kunafanya maisha yao yaendelee kuwa magumu lakini pia Serikali inapoteza mapato kupitia kodi hiyo. Kwa mujibu wa Kitabu cha Mapato (Revenue Book Volume I) cha mwaka wa fedha 2019/2020 katika ukurasa wa 19 kinaonyesha kwa mwaka wa fedha 2018/19 kodi iliyokuwa imeidhinishwa kukusanywa kutoka kwa wafanyakazi ilikuwa ni shilingi bilioni 998.511 na kwa mwaka wa fedha 2019/20 kodi inayotarajiwa kukusanywa ni shilingi trilioni 1. 065ikiwa ni ongezeko la shilingi bilioni 67.181
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani haioni nia njema ya Serikali kwa watumishi wake kwa kuwa kuna kila dalili za kuwaonea watumishi hao. Dalili ya kwanza ilikuwa ni mkakati wa kuwapunja watumishi mafao yao ya kustaafu kwa kubadili kwa hila kikokotoo cha mafao hayo bila hata kuwashirikisha. Dalili ya pili ni kitendo cha Serikali kufuta fao la kujitoa katika mifuko ya hifadhi ya jamii jambo ambalo linawabana watumishi hasa wale wanaocha kazi kabala ya kufikisha miaka 60; na dalili ya tatu ni kitendo cha Serikali kukopa sana kwenye mifuko ya hifadhi ya jamii na kuchelewa kurejesha fedha hizo kiasi kwamba wastaafu wanakosa kulipwa mafao yao kwa wakati kutokana na mifuko hiyo kukosa fedha.
Mheshimiwa Spika,Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaitaka Serikali kuwapandishia watumishi mishahara katika bajeti hii kwa kuwa ni stahili zao za kisheria na pia kulipa madeni yote ya watumishi ikiwa ni pamoja na madai yao ya fedha za likizo, uhamisho, malimbikizo ya mishahara na stahili nyingine za kikakuni. Aidha, ulipaji wa madeni hayo uende sambamba na kuwapandisha madaraja watumishi wenye sifa za kupandishwa madaraja sambamba na kuwalipa mishahara yao mipya kwa wakati.

ZC. MPANGO WA PILI WA MAENDELEO WA MIAKA MITANO DHIDI YA MIRADI YA MAENDELEO YA KILA MWAKA
Mheshimiwa Spika, mpango wa maendeleo wa miaka mitano ndiyo dira inayotuongoza katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo inayotakiwa kutekelezwa na serikali kwa kipindi cha kuanzia bajeti ya mwaka 2016/17 hadi 2020/21. Mpango huo umetoa mwelekeo ambavyo miradi yote ya maendeleo kwa kipindi hicho itakavyopatiwa fedha za maendeleo na kwa kiwango gani Serikali inatakiwa na Sekta binafsi zinatakiwa kuchangia. Mpango wa maendeleo wa miaka mitano ulihitaji jumla ya shilingi za kitanzania trilioni 107 na kati ya fedha hizo Serikali serikali ilitakiwa kuchangia kiasi cha shilingi trilioni 59(fedha za ndani, mikopo na misaada), ambazo zinatakiwa kila mwaka Serikali itenge kwenye bajeti yake wastani wa shilingi trilioni 11.8 na sekta binafsi ilitakiwa kuchangia shilingi trilioni 48 kwa wastani wa shilingi trilion 9.6 kila mwaka.
Mheshimiwa Spika, kuna miradi ambayo tayari fedha zilikwisha tumika kuanzia kwenye awamu ya kwanza ya mpango wa maendeleo wa miaka mitano FYDP I na pia miradi hiyo imewekwa kama miradi ya kielelezo inayohusu kanda za maendeleo(Flagship projects associated with Development Corridors) na kupitishwa na Bunge hili Tukufu ni pamoja na Undelezaji wa Ujenzi wa Bandari Mpya ya Bagamoyo, Uanzishwaji wa SEZ Bagamoyo, Kigoma,Ruvuma na Mtwara, Uanzishwaji wa Kurasini Trade Logistics Centre, Uanzishwaji wa Dodoma Trade and Logistics Centre.
Mheshimiwa Spika, tukumbuke kwamba Mpango huu wa pili ya miaka mitano (FYDP II) ulipitishwa na Bunge na hivyo ni sheria au ndio mwongozo wetu katika uwekezaji, kwa muktadha huo Kambi Rasmi ya Upinzani inaamini kuwa mabadiliko ya chochote katika nyaraka hiyo ni lazima Bunge lishirikishwe na likubali kuidhinisha mabadiliko hayo. Kambi Rasmi ya Upinzani inasema hayo kutokana na ukweli kwamba Bunge limekuwa kama punching bag kutokana na kutoletewa mikataba ya miradi mikubwa ya maendeleo na hivyo Bunge linapitisha Mpango wa Maendeleo lakini Serikali inabadi Mpango huo bila kuomba kibali cha Bunge. Kwa mfano; Ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo umekuwepo kwenye mpango wa maendeleo wa miaka mitano awamu ya kwanza na kuendelea hadi katika Mpango wa Pili wa Maendeleo, lakini kwa sasa Serikali imegoma kuutekeleza licha ya suala hilo kuwa kwenye Mpango. Kambi Rasmi ya Upinzani ina mtazamo kwamba kitendo cha Serikali kugoma kutekeleza baadhi ya miradi iliyopitishwa na Bunge katika Mpango wa Taifa wa Maendeleo. Kwanza ni dharau kwa bunge; lakini pili ni ishara kuwa Serikali hii haiko makini katika kupanga mipango yake.
Mheshimiwa Spika, jambo jingine la ajabu ni Serikali kuweka kando masharti ya utekekelezaji wa Mpango wenyewe masharti ambayo Serikali ndiyo iliyoyaweka. Kwa mfano; mpango umeeleza vizuri kuwa miradi yote ambayo ni ya kibiasahara itekelezwe na sekta binafsi lakini commercially viable projects should be left to the private sector, unless there is strong justification for doing otherwise. Pamoja na takwa hilo la Mpango, Serikali inatekeleza miradi yote mikubwa bila kuishirikisha sekta binafsi.Miradi hiyo ni pamoja na ujenzi wa SGR, Ujenzi wa kiwanda cha LNG, Liganga Mchuchuma Industrial Park, Mtwara Petrochemical Special Economic Zone na Bagamoyo Special Economic Zone.

Jedwali Na. 1: Sura ya Bajeti mbadala kwa Mwaka Wa Fedha 2019/20
MAELEZO
MAPATO (TZS)

JUMLA YA MAPATO YA KODI
18% of GDP

23,292,000,000,000.00


MAPATO YASIYO YA KODI 2% YA GDP
2,588,000,000,000.00


MAPATO YA HALMASHAURI 1.5% YA GDP
1,941,000,000,000.00


MISAADA YA KIBAJETI TOKA NJE- Capital Grnts from Forign Government (Bilateral) + Capital Grants from International Organization (Multilateral)
1,210,143,710,000.00


JUMLA YA MAPATO

29,031,143,710,000.00


MATUMIZI


MATUMIZI YA KAWAIDA



Deni la Taifa
7,004,480,000,000.00


Mishahara ni 23% ya bajeti mbadala
6,677,163,053,300.00


Matumizi mengineyo
2,054,244,000,000.00


JUMLA YA MATUMIZI YA KAWAIDA
15,735,887,053,300.00


MATUMIZI YA MAENDELEO



Fedha za ndani + Nje
13,295,256,656,700.00






JUMLA YA FEDHA ZA MATUMIZI

29,031,143,710,000.00


































ULINGANISHO NA BAJETI YA SERIKALI


Mheshimiwa Spika, katika bajeti yetu mbadala; badala ya kulipa deni la taifa la shilingi trilioni 10 kama ambavyo bajeti ya serikali inaonesha, Sisi tutalipa kiasi cha shilingi trillion 7. Hii ni kutokana na ukweli kwamba katika biashara yoyote kuna nafasi ya majadiliano, hivyo tutafanya majadiliano ya kulipa kiasi hicho.
Mheshimiwa Spika, bajeti mbadala haiwezi kulipa mishahara kwa kiwango cha shilingi kama Serikali inavyolipa kutokana na ukweli kwamba Serikali inalipa mishahara hiyo bila ya kuwa na uhakika inao watumishi wangapi. Jambo hilo linasababisha fedha nyingi kulipwa kiholela. Tumefikia uamuzi huo kutokana na makusanyo halisi ya kodi ya Mshahara (PAYE) kuwa ndogo sana kulingana na makisio ambayo yanakuwa yamewekwa na Serikali. Kwa muktadha huo mishahara itakayolipwa na Bajeti Mbadala ni trilioni 6.7 ambayo ni sawa na 23% ya bajeti yetu. Mikopo ya kibiashara kutoka nje yenye thamani ya shilingi 3,889,935,853,000.00 hatutaichukua na hivyo kuifanya bajeti Mbadala kuwa na nakisi ya 4.288% tu
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Serikali sura ya bajeti inaonesha nakisi ni asilimia 2.3 ya pato la taifa sawa na shilingi trilioni 2.976, lakini ukiangalia fedha zote kutokana nje (yaani mikopo na misaada ya kibajeti) ambazo kimsingi ndiyo nakisi yenyewe; nitakriban shilingi trilioni 10 ambayo ni takriban asilimia 30 ya bajeti yote. Hivyo nakisi halisi ya bajeti ni asilimia 30 kwa kizio cha jumla ya bajeti yote. Kambi Rasmi ya Upinzani inaionya Seriali kuacha kukokotoa nakisi ya bajeti kwa pato la taifa ambapo nakisi huonekana kuwa ndogo wakati kimsingi bajeti yetu ni tegemezi kwa asilimia 30.
ZD. MAENEO YA KIPAUMBELE KATIKA BAJETI MBADALA
Mheshimiwa Spika, Bajeti mbadala ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni itakua na vipaumbele katika sekta zafuatazo;



Jedwali Na. 2 : Mgawanyo wa Fedha katika Sekta za Kipaumbele
Na.
Sekta
Kiasi (Tshs.)
Asilimia (%)


Elimu
4,354,671,556,500.00
15


Kilimo
5,806,228,742,000.00
20


Viwanda
4,354,671,556,500.00
15


Maji
2,903,114,371,000.00
10


Afya
2,903,114,371,000.00
10


Mengineyo
8,709,343,113,000.00
30


JUMLA
29,031,143,710,000.00
100



ZE. HITIMISHO

Mheshimiwa Spika, naomba kumalizia hotuba yangukwa kusema kwamba kusuasua kwa uchumi wetu kumetokana na kutokuwa na mfumo wa uchumi unaoeleweka. Serikali hii ya awamu ya tano, haijui inafuata mfumo gani wa uchumi. Nimeeleza kwa kirefu hapo awali jinsi ambavyo mfumo wetu wa uchumi umepitwa na wakati na jinsi ambavyo hauendani na mahitaji ya dunia ya sasa; Aidha, nimeeleza madhara ya uchumi kuhodhiwa na Serikali jambo ambalo limeua nguvu ya soko katika kuamua mustakabali wa uchumi. Kutokana na madhaifu hayo ya mfumo wetu wa uchumi, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeniimependekeza mfumo wetu wa uchumi kufanyiwa marekebisho makubwa ikiwa ni pamoja na kupendekeza mfumo mpya wa uchumi ujulikanao kama Mfumo wa Uchumi wa Soko Jamii (Social Market Economy) Mfumo ambao ni wa kisasa kabisa duniani; ili Taifa liweze kujinasua na matatizo ya kiuchumi ambayo yamelifanya taifa hili kuwa masikini kwa miongo yote mitano toka tupate uhuru.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani imeeleza pia kwamba ukuaji wa uchumi na ustawi wa watu ni matokeo ya utawala bora. Hivyo, ujenzi wa uchumi imara ni lazima uende sambamba na utawala bora. Kama kuna tishio la usalama kwa maana ya watu kutekwa na kuteswa wakiwemo wafanya biashara wakubwa; kama kuna ukandamizaji wa demokrasia na haki za binadamu; kama hakuna uhuru wa habari; kama hatuna mahusiano mazuri ya kidiplomasia na Jumuiya ya Kimataifa n.k tusitegemee uwekezaji wa maana katika nchi yetu.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani imeonyesha pia namna bajeti hii ya nne ya Serikali ya awamu ya tano ilivyojikita kwenye maendeleo ya vitu badala ya maendeleo ya watu. Takriban asilimia 40 ya fedha za maendeleo zimetumika kugharamia miradi mitatu tu iliyopo katika Wizara mbili; yani wizara Nishati na Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano. Miradi hiyo ni SGR, Stieglers Gorge, na Ufufuaji wa Shirika la ndege. Jambo hili limesababisha fedha za maendeleo katika sekta nyingine zinazoguza moja kwa moja maisha ya wananchi kama vile afya, kilimo, elimu maji,mifugo na uvuvi kupungua sana.
Mheshimiwa Spika,naomba nimalizie kwa kusema kwamba; hili taifa ni letu sote Hakuna Mtanzania mwenye sifa za utanzania zaidi ya mwingine wote ni watanzania. Kwa hiyo, kitendo cha watawala kuona kwamba wao ni bora zaidi na kutuita sisi wenye mawazo mbadala kwamba si wazalendo na kwamba tunapinga maendeleo ni kauli za kibaguzi na hazilijengi taifa bali zinalipasua. Serikali iwe inapokea changamoto na mawazo mbadala kutoka upinzani na kuyafanyia kazi.
Mwisho kabisa Mheshimiwa Spika, Serikali iache kufanya propaganda katika mambo ya msingi hasa katika bajeti ya Serikali. Tumeeleza kwa kirefu jinsi Serikali inavyowahadaa wananchi kwa kuweka makisio makubwa ya ukusanyaji wa mapato ambayo inajua kabisa kuwa haiwezi kukusanya na hivyo kuwapa wananchi matumaini hewa! Kwa kuwa Serikali hii ya awamu ya tano ilikuwa bingwa sana kukabiliana na vitu hewa kuanzia wafanyakazi hewa na madai hewa ya watumishi; ijisafishe na yenywe kwa kuacha kupanga bajeti hewa kwa maendeleo ya taifa hili.
Mheshimiwa Spika,baada ya kusema hayo, naomba kuwasilisha.


David Ernest Silinde (Mb)
KNY:WAZIRI KIVULI WA FEDHA NA MIPANGO
NA MSEMAJI MKUU WAKAMBI RASMI YA UPINZANI BUNGENI,
KATIKA WIZARA YA FEDHA NA MIPANGO
17 Juni, 2019
 
Inawezekana kuna hoja kuntu, mtupe executive summary. Walau PG.Tatu.
 
nina swali dogo, tangu lini CHADEMA kimeanza kuwa chama cha kijamaa mpaka kupendekeza uchumi wa soko jamii( social market economy)? tunajua, nchi za kijamaa kama china ndio muundo huo wa soko katika uchumi lakini kwa nchi za kipebari ni "free market econony".
 
MIRADI YA SERIKALI ISIYOKUWA NA MPANGO MKAKATI WA KIBIASHARA
181. Mheshimiwa Spika, Serikali ya awamu ya tano inatekeleza miradi ambayo sisi tunaona ipo kisiasa zaidi na hakuna mkakati wala mpango wa kibiashara ambao umewekwa wazi na Serikali hadi sasa.Naomba kutoa ufafanuzi na uchambuzi kwenye miradi mitatu yaani Mradi wa Reli ya Standard Gauge (SGR), Ujenzi wa Mradi wa Kuzalisha Umeme- MW 2,100 maarufu kama Stieglers Gorge na Kufufua Shirika la Ndege (ATCL) ambao Serikali imejikita kwenye mradi wa ununuzi wa Ndege;
Mradi wa Reli ya Standard Gauge
182. Mheshimiwa Spika, Mradi wa Reli ya Kisasa kutoka Dar es-Salaam hadi Mwanza ambao unatarajiwa kugharimu Trilioni 17.6 na unatarajiwa kukamilika 2021, ambapo kwa sasa umeanza kutekelezwa kuanzia Dar-es-Salaam- Morogoro KM 205 na Morogoro Makutupora KM 422 hauna mkakati endelevu wa kufungamanisha sekta za kiuchumi na mradi huo. Hakuna anayeweza kubisha au kupinga kuwa kama nchi tunahitaji reli ya kisasa kwa ajili ya kurahisisha shughuli mbalimbali za maendeleo. Hata hivyo, Serikali imejikita kwenye ujenzi wa miundombinu ya reli pekee na sio kufanya uchambuzi wa mradi mzima kuanzia utaratibu wa kuwa na mabehewa ya kisasa, mfumo wa uendeshaji ikiwemo kutoa mafunzo kwa madereva wataoendesha treni hizo, mafunzo kwa watoa huduma, mafunzo kwa watakaokuwa wanafanya shughuli za ukarabati wa miundombinu ya SGR. Aidha, Serikali haijaweka wazi na wala haina mpango wa kuendesha mradi wa SGR kibiashara zaidi ya kupiga porojo za Miundombinu pekee jambo ambalo linaonyesha kuwa tunaweza kuwa na mradi utakaolitia Taifa hasara. Taarifa zinaonyesha kuwa SGR inajengwa kwa mikopo ya masharti ya kibiashara ambapo Taifa litalazimika kuanza kulipa madeni ya mradi huu kabla haujakamilika.
Mradi wa Kufua Umeme wa Maji katika Bonde la Mto Rufiji - Stieglers Gorge Hydro Power Project
183. Mheshimiwa Spika, Mradi huu unategemewa kuzalisha MW 2100 kwa kutumia maji (Hydro Power Plant) katika Bonde la Mto Rufiji. Mpaka kukamilika kwa mradi kwa utafiti wa NORCONSULT wa mwaka 2006 mradi ulikisiwa kugharimu kiasi cha Tshs. Trillion 4 (Dola bilioni 2) Hata hivyo, kutokana na ukosefu wa mpango madhubuti wa utekelezaji, kuna mashaka kama mradi huo utafikia malengo yaliyokusudiwa. Hii ni kwa sababu tayari ipo mifano ya miradi iliyojengwa kwa kutumia fedha nyingi na faida zake hazionekani. Kwa mfano, Itakumbukwa kuwa Serikali ilitumia takribani trilioni 1.2 kujenga bomba la gesi kutoka Mtwara hadi Dar-es-Salaam. Taarifa zinaonyesha kuwa kwa sasa Bomba la gesi hutumika kwa 6% pekee, kama Serikali itaweza kulifanya Bomba kutumika kwa 25% linawez kuzalisha MW 2000 takribani sawa na mradi wa Trilioni 7 wa Stiglers Gorge. Bomba likitumika kwa 100% litaweza kuzalisha MW 10,000. Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kulieleza Bunge; Ni sababu zipi zinazoifanya serikali kutoendelea kuwekeza kwenye umeme wa gesi ambao miundombinu ipo tayari na kukimbilia kwenye mradi wa Stieglers Gorge ambao unagharimu Taifa trilioni 7? Aidha, Kambi Rasmi ya Upinzani inaendelea kusisitiza kwamba haioni tija katika mradi huo zaidi ya kuliingiza taifa kwenye mzigo wa madeni kutokana na Serikali kukopa fedha za kuutekeleza mradi huo.
Kufufua Shirika la Ndege
Mheshimiwa Spika, Serikali imekua ikinunua Ndege kwa ajili ya kulifufua Shirika la Ndege la ATCL. Hata hivyo, Mfumo wa Manunuzi ya Ndege haujawekwa wazi hata baada ya Kambi kuhoji kwa miaka miwili mfululizo na kibaya zaidi sasa wakala wa ndege umehamishwa kutoka wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano na kwenda Ikulu kwa makusudi ili kukwepa ukaguzi wa hesabu kutoka kwa CAG. Ikumbukwe kwamba; ATCL inategemea ruzuku ya Serikali na kwa sababu hiyo, ni lazima hesabu zake zikaguliwe na CAG. Hivyo ukwepaji wa ukaguzi wa hesabu uliofanywa kimkakati kwa kuhamishia masuala ya ndege Ikulu kuna kila dalili ya hila mbaya ya kuficha ubadhirifu na matumizi mabaya ya fedha za umma.
Mheshimiwa Spika, Ili Ndege iweze kuwa na faida ni lazima itumie muda mwingi kusafiri na sio kuwa kukaa kwenye Viwanja vya Ndege. Kwa sasa nchini kuna Viwanja vine pekee ambavyo vina taa kwa ajili ya ndege kutua na kuruka usiku. Kwa hiyo ndege za Serikali haziwezi kutengeneza faida. Pili, Hakuna mkakati wowote wa kibiashara wa kimataifa kwenye uboreshaji wa Shirika la Ndege. Hakuna mkakati wowote wa kuwa na Ndege za mizigo hasa mbogamboga na maua kwa ajili ya kusafirisha kwenda nje ya nchi. Mapungufu yote haya yanadhihirisha kukurupuka kwa Serikali bila kuanzisha miradi ya kisiasa bila kuwa na mipango mkakati ya utekelezaji wa miradi hiyo. Ni Tanzania pekee ambapo miradi inabuniwa halafu mpango wa utekelezaji ndio unafuata. Kwa hali hiyo, hatuwezi kusonga mbele.
VIPAUMBELE VYA BAJETI MBADALA
Mheshimiwa Spika, Bajeti mbadala ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni itakua na vipaumbele katika sekta zafuatazo;
Elimu
Kilimo, Mifugo na Uvuvi (agrarian revolution)
Viwanda katika mnyororo wa thamani wa Kilimo (Agro- Processing Industries
Afya na Maji
Utawala Bora (Good Governance)

Mheshimiwa Spika, pamoja na vipaumbele hivyo; naomba kuweka msisitizo kidogo katika Utawala Bora kwa kuwa Serikali hii imepuuza kabisa dhana ya utawala Bora jambo ambalo limeleta athari kubwa sana katika uchumi na hata mahusiano yetu kitaifa na kimataifa.
Mheshimiwa Spika, uchumi imara ni matokeo ya utawala bora. Ujenzi wa uchumi imara ni matokeo ya moja kwa moja na utawala bora katika nchi. Ukuaji wa uchumi ni lazima uende sambamba na utawala bora. Lakini katika nchi nchi yetu kumekuwa na mambo yanayoifanya nchi yetu isiwe mahala salama kwa ajili ya uwekezaji. Matukio yafuatayo yanaathiri uwekezaji pamoja na utekelezaji wa Bajeti;

Kukwama kwa mchakato wa Katiba Mpya
Tishio la Watu wasiojulikana kuteka, kutesa, kujeruhi na kuwauwa wananchi
Kuminywa kwa Vyombo vya Habari na uhuru wa kupata na kupokea habari kwa kutumia Sheria ya Huduma za Habari pamoja na Makosa ya Mtandao.
Kuminya demokrasia kwa kukataza mikutano ya hadhara ya vyama vya siasa na kutunga sheria kandamizi za kudhibiti siasa na demokrasia.
Kuweka kando utawala wa sheria na badala yake kuongoza nchi kwa utashi wa mtu mmoja.
Kuweka kando mifumo ya kitaasisi katika utendaji na badala yake kutegemea maelekezo ya mtu mmoja.
MAPENDEKEZO YA MPANGO WA KUFUNGAMANISHA KILIMO NA MAENDELEO YA VIWANDA (AGRO ECONOMY)

Mheshimiwa Spika, Sekta ya kilimo inachangia ajira kwa asilimia 70, pato la taifa kwa asilimia 28.2 lakini ukuaji wake unakuwa kidogo sana kwa wastani wa asilimia 5.2 na hivyo kuwa na mchango mdogo sana katika sekta ya viwanda. Kambi Rasmi ya Upinzani italenga kufanya yafuatayo ili kufungamanisha kilimo na uchumi wa viwanda:-

Kuondoa kodi kwenye uwekezaji katika sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi.Hii ni pamoja na kuondoa kodi kwenye viwanda vinavyotengeneza na kukarabati mashine, zana na pembejeo za kilimo, uvuvi na mifugo.
Uwepo wa umeme wa uhakika ili kuendesha shughuli za uzalishaji viwandani. Hivyo, itawekeza ipasavyo katika umeme wa gesi asilia.
Kushirikisha sekta binafsi kupitia mpango wa (PPP) ambapo serikali itawekeza kwenye mitaji ya uwekezaji kwa asilimia 40 na sekta binafsi itashirikishwa kwa asilimia 60.
Kuongeza idadi ya ajira kwa vijana kupitia sekta ya kilimo na viwanda.
Kuongeza pato la mwananchi mmoja mmoja na pia Serikali itapanua wigo wa kodi.
Kusisimua sekta ya usafirishaji na mauzo nje ya nchi.

BAJETI YA SERIAKALI IMEONGEZA MZIGO KWA WANANCHI

Mheshimiwa Spika, serikali katika mwaka wa fedha 2019/20 inapendekeza kufanya marekebisho katika baadhi ya sheria ili kubadilisha viwango vya kodi, baadhi ya sheria hizo ni shaeria ya kodi ya ongezeko la thamani, Sura 148, sheria ya kodi ya mapato, sura 332, sheria ya ushuru wa bidhaa, sura 147, sheria ya usalama barabarani, sura 168, sheria ya forodha ya jumuiya ya Afrika ya mashariki ya mwaka 2004 n.k.
Mheshimiwa Spika, katika marekebisho ya sheria hiyo kuna sheria ya forodha ya Jumuiya ya Afrika ya Mashariki ya mwaka 2004 ambayo pamoja na mambo mengine inapndisha kodi katika vifaa vya ujenzi (mabati na nondo). Kutokana na hali hiyo, bei ya bidhaa na vifaa mbalimbali vinavyotumika kwa ajili ya ujenzi zitaendelea kupanda na hivyo kuathiri azma ya serikali ya ujenzi wa makazi bora na ya kudumu. Mara kadhaa Serikali hii hii imekuwa ikisisitiza kupunguza kodi kwenye vifaa vya ujenzi ili watanzania waweze kujenga nyumba bora; lakini cha ajabu Serikali hiyohiyo, imekuwa na ndimi mbili katika jambo hilo. Kwa mfano, Mei 6, 2014 aliyekuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi alishauri kupunguzwa au kuondolewa kwa kodi katika vifaa vya ujenzi ili watanzania wengi waweze kujenga nyumba bora. Aidha, September 5 2018, akiwa mjini Mwanza kushuhudia utiaji saini wa mikataba minne ya ujenzi wa meli kubwa ya abiria na mizigo ya Serikali, chelezo na ukarabati wa meli za MV Butiama na MV Victoria, Rais John Magufuli alizungumza mambo mengi na kutoa maelekezo kwa watendaji wa Serikali. Miongoni mwa maelekezo aliyoyatoa ni pamoja na kuwaagiza Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano na Waziri wa Fedha na Mipango, kukutana haraka ili kumaliza kilio cha kodi kwenye vifaa vya ujenzi.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inashangaa kuona Waziri wa Fedha akikaidi agizo la Rais la kupunguza kodi kwenye vifaa vya ujenzi na badala yake kupandisha kodi hiyo. Kambi Rasmi ya Upinzani inaamini kuwa punguzo la vifaa vya ujenzi hasa mabati, cement, vifaa vya mabomba ya plastiki na nondo ni hatua mojawapo ya kuelekea kwenye Tanzania ya makazi bora. Kuwa na makazi bora ni mkakati wa kuwa na ongezeko la kodi la uhakika la kodi ya majengo Property tax.

Mheshimiwa Spika, kuhusu punguzo la ushuru wa forodha kutoka 100% hadi 35% kwa mwaka kwenye sukari ya matumizi ya kawaida inayoagizwa kutoka nje ya nchi kwa vibali maalum kwa lengo la kuziba pengo la uzalishaji. Kambi rasmi ya upinzani inaona hatua hii sio kama inaleta tija kwa viwanda vya ndani bali italeta balaa kubwa kwa wakulima wa miwa, kwani sukari nyingi itaingizwa na sukari inayozalishwa ndani itashindwa kuwa na ushindani na hivyo viwanda vitashindwa/vitaacha kununua miwa ya wakulima.

ZA. BAJETI YA SERIKALI IMEJIKITA KWENYE MAENDELEO YA VITU NA SIO MAENDELEO YA WATU
Mheshimiwa Spika, uchambuzi uliofanywa na Kambi Rasmi ya Upinzani kuhusu mgawanyo wa fedha za maendeleo umebaini kwamba; bajeti imejikita kwenye maendeleo ya vitu na sio maendeleo ya watu. Kwa mfano; katika bajeti ya shilingi trilioni 33.104; fedha za maendeleo ni shilingi trilioni 12.25 sawa na asilimia 37 ya bajeti yote. Hata hivyo, mchanganuo wa bajeti ya maendeleo unajumuisha fedha za ndani kiasi cha shilingi trilioni 9.74na fedha za nje kiasi cha shilingi trilioni 2.51.
Mheshimiwa Spika, mgawo wa fedha hizo ni kama ifuatavyo:-
shilingi trilioni 2.48 sawa na asilimia 20.245 ya bajeti yote ya maendeleo ni kwa ajili ya Mradi wa Ujenzi wa Reli kwa kiwango cha Kimataifa (SGR)
shilingi trilioni 1.44 sawa na asiliia 11.755 ya bajeti yote ya maendeleo ni kwa ajili ya Mradi wa Kufua Umeme katika mto rufiji 9( Stiegler’s Gorge Hydoro Power Project) na
shilingi bilioni 500 sawa na asilimia 4.081 ya bajeti yote ya maendeleo ni kwa ajili ya kumalizia malipo kwa ajili ya ununuzi wa Ndege za Serikali.
Mheshimiwa Spika,miradi hiyo mitatu imechukua shilingi trilioni 4.42 ambayo ni sawa na asilimia 36.081 ya fedha zote za maendeleo. Hii miradi ipo kwenye wizara mbili tu, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano pamoja na wizara ya Nishati. Pamoja na miradi hiyo michache kuchukua sehemu kubwa ya bajeti ya maendeleo; bado miradi hiyo haina faida za moja kwa moja katika uchumi wan chi yetu na wake. Hii inatokana na ukweli kwamba malighafi inayotumika kujenga SGR (Chuma na cement) karibu zote zinatoka nje ya nchi na hivyo fedha zinaondoka katika mzunguko wa ndani na kupelekwa nje kwa ajili ya ununuzi wa malighafi hizo. Aidha, ajira zinazozalishwa haziingizi chochote kwenye bajeti yetu kamakdoi ya mshahara (PAYE) kwa kuwa wengi walioajiriwa katika mradi huo ni vibarua (casual laborers) ambao hawapo kwenye mfumo wa kodi. Kwa maneno mengine, hii ni miradi ambayo inanyonya uchumi wetu kwa kutoa fedha ndani na kuzipeleka nje; lakini pili haina multiplier effect katika kuchechemua sekta nyingine za kiuchumi kama vile biashara na ajira.
Mheshimiwa Spika,Kutokana na bajeti hii kuweka kipaumbele katika maendeleo ya vitu badala ya maendeleo ya watu; sekta nyingine zinazogusa maisha ya watu moja kwa moja zimepata mgawo mdogo sana wa fedha za maendeleo jambo linaloashiria kwamba Serikali hii haina mpango na maendeleo na ustawi wa watu. Hata hivyo, miradi na sekta ambazo Serikali inasema ndiyo vipaumbele vyake, nayo imepata mgawo mdogo jambo ambalo linaleta mkanganyiko kuhusu vipaumbele vya Serikali. Mgawo wa fedha kwenye sekta hizo ni kama ifuatavyo:-
Wizara ya Viwanda na Biashara ambayo ndiyo kipaumbele cha kwanza katika bajeti ya Serikali, imetengewa shilingi bilioni 51.5 sawa na asilimia 0.42 ya bajeti nzima ya maendeleo.
Wizara ya Kilimoimetengewa shilingi bilioni 134.577 sawa na asilimia 1.098 ya bajeti ya yote maendeleo.
Wizara ya Elimu imepewa shilingi bilioni 863 ambayo ni sawa na asilimia 7.045 ya bajeti nzima ya maendeleo;
Afya imepewa shilingi bilioni 544.137 sawa na asilimia 4.44 ya bajeti yote ya maendeleo;
Maji yamepewa shilingi bilioni 610.5 sawa na asilimia 4.98 ya fedha zote za maendeleo.
Mheshimiwa Spika, kwa mwenendo huo wa mgawo wa fedha za maendeleo, ni dhahiri shahiri kwamba Serikali hii inayojinasibu kuwa ni ya wanyonge; haipendi wanyonge hao waishi kwa neema kwa kupata huduma bora za kijamii kama vile afya, elimu, maji safi na salama, au kuwekeza katika kilimo chao kinachowapatia ajira na chakula; isipokuwa inawekeza katika vitu ambayo hao wanyonge hawatakuwa na uwezo wa kuvitumia pia.
ZB. BAJETI YA SERIKALI IMEWASAHAU WATUMISHI WA UMMA AMBAO NI WALIPA KODI WA UHAKIKA
Mheshimiwa Spika,bajeti ya Serikali imewasahau kabisa watumishi wa umma ambao toka Serikali hii ya awamu ya tano iingie madarakani hawajawahi kupata nyongeza ya mishahara ya kila mwaka (annual increment) licha ya madai mengine wanayoidai Serikali ikiwa ni pamoja na fedha za likizo; kupandishwa madaraja; malimbikizo ya mishahara na stahili nyingine za kikanuni.
Mheshimiwa Spika, Ikumbukwe kwamba watumishi wa umma ndio walipa kodi wa uhakika kupitia kodi ya mshahara (PAYE) hivyo kutowapandishia mishahara si tu kunafanya maisha yao yaendelee kuwa magumu lakini pia Serikali inapoteza mapato kupitia kodi hiyo. Kwa mujibu wa Kitabu cha Mapato (Revenue Book Volume I) cha mwaka wa fedha 2019/2020 katika ukurasa wa 19 kinaonyesha kwa mwaka wa fedha 2018/19 kodi iliyokuwa imeidhinishwa kukusanywa kutoka kwa wafanyakazi ilikuwa ni shilingi bilioni 998.511 na kwa mwaka wa fedha 2019/20 kodi inayotarajiwa kukusanywa ni shilingi trilioni 1. 065ikiwa ni ongezeko la shilingi bilioni 67.181
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani haioni nia njema ya Serikali kwa watumishi wake kwa kuwa kuna kila dalili za kuwaonea watumishi hao. Dalili ya kwanza ilikuwa ni mkakati wa kuwapunja watumishi mafao yao ya kustaafu kwa kubadili kwa hila kikokotoo cha mafao hayo bila hata kuwashirikisha. Dalili ya pili ni kitendo cha Serikali kufuta fao la kujitoa katika mifuko ya hifadhi ya jamii jambo ambalo linawabana watumishi hasa wale wanaocha kazi kabala ya kufikisha miaka 60; na dalili ya tatu ni kitendo cha Serikali kukopa sana kwenye mifuko ya hifadhi ya jamii na kuchelewa kurejesha fedha hizo kiasi kwamba wastaafu wanakosa kulipwa mafao yao kwa wakati kutokana na mifuko hiyo kukosa fedha.
Mheshimiwa Spika,Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaitaka Serikali kuwapandishia watumishi mishahara katika bajeti hii kwa kuwa ni stahili zao za kisheria na pia kulipa madeni yote ya watumishi ikiwa ni pamoja na madai yao ya fedha za likizo, uhamisho, malimbikizo ya mishahara na stahili nyingine za kikakuni. Aidha, ulipaji wa madeni hayo uende sambamba na kuwapandisha madaraja watumishi wenye sifa za kupandishwa madaraja sambamba na kuwalipa mishahara yao mipya kwa wakati.

ZC. MPANGO WA PILI WA MAENDELEO WA MIAKA MITANO DHIDI YA MIRADI YA MAENDELEO YA KILA MWAKA
Mheshimiwa Spika, mpango wa maendeleo wa miaka mitano ndiyo dira inayotuongoza katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo inayotakiwa kutekelezwa na serikali kwa kipindi cha kuanzia bajeti ya mwaka 2016/17 hadi 2020/21. Mpango huo umetoa mwelekeo ambavyo miradi yote ya maendeleo kwa kipindi hicho itakavyopatiwa fedha za maendeleo na kwa kiwango gani Serikali inatakiwa na Sekta binafsi zinatakiwa kuchangia. Mpango wa maendeleo wa miaka mitano ulihitaji jumla ya shilingi za kitanzania trilioni 107 na kati ya fedha hizo Serikali serikali ilitakiwa kuchangia kiasi cha shilingi trilioni 59(fedha za ndani, mikopo na misaada), ambazo zinatakiwa kila mwaka Serikali itenge kwenye bajeti yake wastani wa shilingi trilioni 11.8 na sekta binafsi ilitakiwa kuchangia shilingi trilioni 48 kwa wastani wa shilingi trilion 9.6 kila mwaka.
Mheshimiwa Spika, kuna miradi ambayo tayari fedha zilikwisha tumika kuanzia kwenye awamu ya kwanza ya mpango wa maendeleo wa miaka mitano FYDP I na pia miradi hiyo imewekwa kama miradi ya kielelezo inayohusu kanda za maendeleo(Flagship projects associated with Development Corridors) na kupitishwa na Bunge hili Tukufu ni pamoja na Undelezaji wa Ujenzi wa Bandari Mpya ya Bagamoyo, Uanzishwaji wa SEZ Bagamoyo, Kigoma,Ruvuma na Mtwara, Uanzishwaji wa Kurasini Trade Logistics Centre, Uanzishwaji wa Dodoma Trade and Logistics Centre.
Mheshimiwa Spika, tukumbuke kwamba Mpango huu wa pili ya miaka mitano (FYDP II) ulipitishwa na Bunge na hivyo ni sheria au ndio mwongozo wetu katika uwekezaji, kwa muktadha huo Kambi Rasmi ya Upinzani inaamini kuwa mabadiliko ya chochote katika nyaraka hiyo ni lazima Bunge lishirikishwe na likubali kuidhinisha mabadiliko hayo. Kambi Rasmi ya Upinzani inasema hayo kutokana na ukweli kwamba Bunge limekuwa kama punching bag kutokana na kutoletewa mikataba ya miradi mikubwa ya maendeleo na hivyo Bunge linapitisha Mpango wa Maendeleo lakini Serikali inabadi Mpango huo bila kuomba kibali cha Bunge. Kwa mfano; Ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo umekuwepo kwenye mpango wa maendeleo wa miaka mitano awamu ya kwanza na kuendelea hadi katika Mpango wa Pili wa Maendeleo, lakini kwa sasa Serikali imegoma kuutekeleza licha ya suala hilo kuwa kwenye Mpango. Kambi Rasmi ya Upinzani ina mtazamo kwamba kitendo cha Serikali kugoma kutekeleza baadhi ya miradi iliyopitishwa na Bunge katika Mpango wa Taifa wa Maendeleo. Kwanza ni dharau kwa bunge; lakini pili ni ishara kuwa Serikali hii haiko makini katika kupanga mipango yake.
Mheshimiwa Spika, jambo jingine la ajabu ni Serikali kuweka kando masharti ya utekekelezaji wa Mpango wenyewe masharti ambayo Serikali ndiyo iliyoyaweka. Kwa mfano; mpango umeeleza vizuri kuwa miradi yote ambayo ni ya kibiasahara itekelezwe na sekta binafsi lakini commercially viable projects should be left to the private sector, unless there is strong justification for doing otherwise. Pamoja na takwa hilo la Mpango, Serikali inatekeleza miradi yote mikubwa bila kuishirikisha sekta binafsi.Miradi hiyo ni pamoja na ujenzi wa SGR, Ujenzi wa kiwanda cha LNG, Liganga Mchuchuma Industrial Park, Mtwara Petrochemical Special Economic Zone na Bagamoyo Special Economic Zone.

Jedwali Na. 1: Sura ya Bajeti mbadala kwa Mwaka Wa Fedha 2019/20
MAELEZO
MAPATO (TZS)

JUMLA YA MAPATO YA KODI
18% of GDP

23,292,000,000,000.00


MAPATO YASIYO YA KODI 2% YA GDP
2,588,000,000,000.00


MAPATO YA HALMASHAURI 1.5% YA GDP
1,941,000,000,000.00


MISAADA YA KIBAJETI TOKA NJE- Capital Grnts from Forign Government (Bilateral) + Capital Grants from International Organization (Multilateral)
1,210,143,710,000.00


JUMLA YA MAPATO

29,031,143,710,000.00


MATUMIZI


MATUMIZI YA KAWAIDA



Deni la Taifa
7,004,480,000,000.00


Mishahara ni 23% ya bajeti mbadala
6,677,163,053,300.00


Matumizi mengineyo
2,054,244,000,000.00


JUMLA YA MATUMIZI YA KAWAIDA
15,735,887,053,300.00


MATUMIZI YA MAENDELEO



Fedha za ndani + Nje
13,295,256,656,700.00






JUMLA YA FEDHA ZA MATUMIZI

29,031,143,710,000.00


































ULINGANISHO NA BAJETI YA SERIKALI


Mheshimiwa Spika, katika bajeti yetu mbadala; badala ya kulipa deni la taifa la shilingi trilioni 10 kama ambavyo bajeti ya serikali inaonesha, Sisi tutalipa kiasi cha shilingi trillion 7. Hii ni kutokana na ukweli kwamba katika biashara yoyote kuna nafasi ya majadiliano, hivyo tutafanya majadiliano ya kulipa kiasi hicho.
Mheshimiwa Spika, bajeti mbadala haiwezi kulipa mishahara kwa kiwango cha shilingi kama Serikali inavyolipa kutokana na ukweli kwamba Serikali inalipa mishahara hiyo bila ya kuwa na uhakika inao watumishi wangapi. Jambo hilo linasababisha fedha nyingi kulipwa kiholela. Tumefikia uamuzi huo kutokana na makusanyo halisi ya kodi ya Mshahara (PAYE) kuwa ndogo sana kulingana na makisio ambayo yanakuwa yamewekwa na Serikali. Kwa muktadha huo mishahara itakayolipwa na Bajeti Mbadala ni trilioni 6.7 ambayo ni sawa na 23% ya bajeti yetu. Mikopo ya kibiashara kutoka nje yenye thamani ya shilingi 3,889,935,853,000.00 hatutaichukua na hivyo kuifanya bajeti Mbadala kuwa na nakisi ya 4.288% tu
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Serikali sura ya bajeti inaonesha nakisi ni asilimia 2.3 ya pato la taifa sawa na shilingi trilioni 2.976, lakini ukiangalia fedha zote kutokana nje (yaani mikopo na misaada ya kibajeti) ambazo kimsingi ndiyo nakisi yenyewe; nitakriban shilingi trilioni 10 ambayo ni takriban asilimia 30 ya bajeti yote. Hivyo nakisi halisi ya bajeti ni asilimia 30 kwa kizio cha jumla ya bajeti yote. Kambi Rasmi ya Upinzani inaionya Seriali kuacha kukokotoa nakisi ya bajeti kwa pato la taifa ambapo nakisi huonekana kuwa ndogo wakati kimsingi bajeti yetu ni tegemezi kwa asilimia 30.
ZD. MAENEO YA KIPAUMBELE KATIKA BAJETI MBADALA
Mheshimiwa Spika, Bajeti mbadala ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni itakua na vipaumbele katika sekta zafuatazo;



Jedwali Na. 2 : Mgawanyo wa Fedha katika Sekta za Kipaumbele
Na.
Sekta
Kiasi (Tshs.)
Asilimia (%)


Elimu
4,354,671,556,500.00
15


Kilimo
5,806,228,742,000.00
20


Viwanda
4,354,671,556,500.00
15


Maji
2,903,114,371,000.00
10


Afya
2,903,114,371,000.00
10


Mengineyo
8,709,343,113,000.00
30


JUMLA
29,031,143,710,000.00
100



ZE. HITIMISHO

Mheshimiwa Spika, naomba kumalizia hotuba yangukwa kusema kwamba kusuasua kwa uchumi wetu kumetokana na kutokuwa na mfumo wa uchumi unaoeleweka. Serikali hii ya awamu ya tano, haijui inafuata mfumo gani wa uchumi. Nimeeleza kwa kirefu hapo awali jinsi ambavyo mfumo wetu wa uchumi umepitwa na wakati na jinsi ambavyo hauendani na mahitaji ya dunia ya sasa; Aidha, nimeeleza madhara ya uchumi kuhodhiwa na Serikali jambo ambalo limeua nguvu ya soko katika kuamua mustakabali wa uchumi. Kutokana na madhaifu hayo ya mfumo wetu wa uchumi, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeniimependekeza mfumo wetu wa uchumi kufanyiwa marekebisho makubwa ikiwa ni pamoja na kupendekeza mfumo mpya wa uchumi ujulikanao kama Mfumo wa Uchumi wa Soko Jamii (Social Market Economy) Mfumo ambao ni wa kisasa kabisa duniani; ili Taifa liweze kujinasua na matatizo ya kiuchumi ambayo yamelifanya taifa hili kuwa masikini kwa miongo yote mitano toka tupate uhuru.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani imeeleza pia kwamba ukuaji wa uchumi na ustawi wa watu ni matokeo ya utawala bora. Hivyo, ujenzi wa uchumi imara ni lazima uende sambamba na utawala bora. Kama kuna tishio la usalama kwa maana ya watu kutekwa na kuteswa wakiwemo wafanya biashara wakubwa; kama kuna ukandamizaji wa demokrasia na haki za binadamu; kama hakuna uhuru wa habari; kama hatuna mahusiano mazuri ya kidiplomasia na Jumuiya ya Kimataifa n.k tusitegemee uwekezaji wa maana katika nchi yetu.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani imeonyesha pia namna bajeti hii ya nne ya Serikali ya awamu ya tano ilivyojikita kwenye maendeleo ya vitu badala ya maendeleo ya watu. Takriban asilimia 40 ya fedha za maendeleo zimetumika kugharamia miradi mitatu tu iliyopo katika Wizara mbili; yani wizara Nishati na Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano. Miradi hiyo ni SGR, Stieglers Gorge, na Ufufuaji wa Shirika la ndege. Jambo hili limesababisha fedha za maendeleo katika sekta nyingine zinazoguza moja kwa moja maisha ya wananchi kama vile afya, kilimo, elimu maji,mifugo na uvuvi kupungua sana.
Mheshimiwa Spika,naomba nimalizie kwa kusema kwamba; hili taifa ni letu sote Hakuna Mtanzania mwenye sifa za utanzania zaidi ya mwingine wote ni watanzania. Kwa hiyo, kitendo cha watawala kuona kwamba wao ni bora zaidi na kutuita sisi wenye mawazo mbadala kwamba si wazalendo na kwamba tunapinga maendeleo ni kauli za kibaguzi na hazilijengi taifa bali zinalipasua. Serikali iwe inapokea changamoto na mawazo mbadala kutoka upinzani na kuyafanyia kazi.
Mwisho kabisa Mheshimiwa Spika, Serikali iache kufanya propaganda katika mambo ya msingi hasa katika bajeti ya Serikali. Tumeeleza kwa kirefu jinsi Serikali inavyowahadaa wananchi kwa kuweka makisio makubwa ya ukusanyaji wa mapato ambayo inajua kabisa kuwa haiwezi kukusanya na hivyo kuwapa wananchi matumaini hewa! Kwa kuwa Serikali hii ya awamu ya tano ilikuwa bingwa sana kukabiliana na vitu hewa kuanzia wafanyakazi hewa na madai hewa ya watumishi; ijisafishe na yenywe kwa kuacha kupanga bajeti hewa kwa maendeleo ya taifa hili.
Mheshimiwa Spika,baada ya kusema hayo, naomba kuwasilisha.


David Ernest Silinde (Mb)
KNY:WAZIRI KIVULI WA FEDHA NA MIPANGO
NA MSEMAJI MKUU WAKAMBI RASMI YA UPINZANI BUNGENI,
KATIKA WIZARA YA FEDHA NA MIPANGO
17 Juni, 2019
Chadema bajeti ni namba na si porojo.Nini maoni yenu kwenye vyanzo vipya (mbadala) vya mapato?nini vipaumbele mbadala kwenye matumizi ya maendeleo?Porojo,vijembe na kejeli haviwezi kuwa maoni mbadala.Kwa kifupi mmechemka.
 
MIRADI YA SERIKALI ISIYOKUWA NA MPANGO MKAKATI WA KIBIASHARA
181. Mheshimiwa Spika, Serikali ya awamu ya tano inatekeleza miradi ambayo sisi tunaona ipo kisiasa zaidi na hakuna mkakati wala mpango wa kibiashara ambao umewekwa wazi na Serikali hadi sasa.Naomba kutoa ufafanuzi na uchambuzi kwenye miradi mitatu yaani Mradi wa Reli ya Standard Gauge (SGR), Ujenzi wa Mradi wa Kuzalisha Umeme- MW 2,100 maarufu kama Stieglers Gorge na Kufufua Shirika la Ndege (ATCL) ambao Serikali imejikita kwenye mradi wa ununuzi wa Ndege;
Mradi wa Reli ya Standard Gauge
182. Mheshimiwa Spika, Mradi wa Reli ya Kisasa kutoka Dar es-Salaam hadi Mwanza ambao unatarajiwa kugharimu Trilioni 17.6 na unatarajiwa kukamilika 2021, ambapo kwa sasa umeanza kutekelezwa kuanzia Dar-es-Salaam- Morogoro KM 205 na Morogoro Makutupora KM 422 hauna mkakati endelevu wa kufungamanisha sekta za kiuchumi na mradi huo. Hakuna anayeweza kubisha au kupinga kuwa kama nchi tunahitaji reli ya kisasa kwa ajili ya kurahisisha shughuli mbalimbali za maendeleo. Hata hivyo, Serikali imejikita kwenye ujenzi wa miundombinu ya reli pekee na sio kufanya uchambuzi wa mradi mzima kuanzia utaratibu wa kuwa na mabehewa ya kisasa, mfumo wa uendeshaji ikiwemo kutoa mafunzo kwa madereva wataoendesha treni hizo, mafunzo kwa watoa huduma, mafunzo kwa watakaokuwa wanafanya shughuli za ukarabati wa miundombinu ya SGR. Aidha, Serikali haijaweka wazi na wala haina mpango wa kuendesha mradi wa SGR kibiashara zaidi ya kupiga porojo za Miundombinu pekee jambo ambalo linaonyesha kuwa tunaweza kuwa na mradi utakaolitia Taifa hasara. Taarifa zinaonyesha kuwa SGR inajengwa kwa mikopo ya masharti ya kibiashara ambapo Taifa litalazimika kuanza kulipa madeni ya mradi huu kabla haujakamilika.
Mradi wa Kufua Umeme wa Maji katika Bonde la Mto Rufiji - Stieglers Gorge Hydro Power Project
183. Mheshimiwa Spika, Mradi huu unategemewa kuzalisha MW 2100 kwa kutumia maji (Hydro Power Plant) katika Bonde la Mto Rufiji. Mpaka kukamilika kwa mradi kwa utafiti wa NORCONSULT wa mwaka 2006 mradi ulikisiwa kugharimu kiasi cha Tshs. Trillion 4 (Dola bilioni 2) Hata hivyo, kutokana na ukosefu wa mpango madhubuti wa utekelezaji, kuna mashaka kama mradi huo utafikia malengo yaliyokusudiwa. Hii ni kwa sababu tayari ipo mifano ya miradi iliyojengwa kwa kutumia fedha nyingi na faida zake hazionekani. Kwa mfano, Itakumbukwa kuwa Serikali ilitumia takribani trilioni 1.2 kujenga bomba la gesi kutoka Mtwara hadi Dar-es-Salaam. Taarifa zinaonyesha kuwa kwa sasa Bomba la gesi hutumika kwa 6% pekee, kama Serikali itaweza kulifanya Bomba kutumika kwa 25% linawez kuzalisha MW 2000 takribani sawa na mradi wa Trilioni 7 wa Stiglers Gorge. Bomba likitumika kwa 100% litaweza kuzalisha MW 10,000. Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kulieleza Bunge; Ni sababu zipi zinazoifanya serikali kutoendelea kuwekeza kwenye umeme wa gesi ambao miundombinu ipo tayari na kukimbilia kwenye mradi wa Stieglers Gorge ambao unagharimu Taifa trilioni 7? Aidha, Kambi Rasmi ya Upinzani inaendelea kusisitiza kwamba haioni tija katika mradi huo zaidi ya kuliingiza taifa kwenye mzigo wa madeni kutokana na Serikali kukopa fedha za kuutekeleza mradi huo.
Kufufua Shirika la Ndege
Mheshimiwa Spika, Serikali imekua ikinunua Ndege kwa ajili ya kulifufua Shirika la Ndege la ATCL. Hata hivyo, Mfumo wa Manunuzi ya Ndege haujawekwa wazi hata baada ya Kambi kuhoji kwa miaka miwili mfululizo na kibaya zaidi sasa wakala wa ndege umehamishwa kutoka wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano na kwenda Ikulu kwa makusudi ili kukwepa ukaguzi wa hesabu kutoka kwa CAG. Ikumbukwe kwamba; ATCL inategemea ruzuku ya Serikali na kwa sababu hiyo, ni lazima hesabu zake zikaguliwe na CAG. Hivyo ukwepaji wa ukaguzi wa hesabu uliofanywa kimkakati kwa kuhamishia masuala ya ndege Ikulu kuna kila dalili ya hila mbaya ya kuficha ubadhirifu na matumizi mabaya ya fedha za umma.
Mheshimiwa Spika, Ili Ndege iweze kuwa na faida ni lazima itumie muda mwingi kusafiri na sio kuwa kukaa kwenye Viwanja vya Ndege. Kwa sasa nchini kuna Viwanja vine pekee ambavyo vina taa kwa ajili ya ndege kutua na kuruka usiku. Kwa hiyo ndege za Serikali haziwezi kutengeneza faida. Pili, Hakuna mkakati wowote wa kibiashara wa kimataifa kwenye uboreshaji wa Shirika la Ndege. Hakuna mkakati wowote wa kuwa na Ndege za mizigo hasa mbogamboga na maua kwa ajili ya kusafirisha kwenda nje ya nchi. Mapungufu yote haya yanadhihirisha kukurupuka kwa Serikali bila kuanzisha miradi ya kisiasa bila kuwa na mipango mkakati ya utekelezaji wa miradi hiyo. Ni Tanzania pekee ambapo miradi inabuniwa halafu mpango wa utekelezaji ndio unafuata. Kwa hali hiyo, hatuwezi kusonga mbele.
VIPAUMBELE VYA BAJETI MBADALA
Mheshimiwa Spika, Bajeti mbadala ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni itakua na vipaumbele katika sekta zafuatazo;
Elimu
Kilimo, Mifugo na Uvuvi (agrarian revolution)
Viwanda katika mnyororo wa thamani wa Kilimo (Agro- Processing Industries
Afya na Maji
Utawala Bora (Good Governance)

Mheshimiwa Spika, pamoja na vipaumbele hivyo; naomba kuweka msisitizo kidogo katika Utawala Bora kwa kuwa Serikali hii imepuuza kabisa dhana ya utawala Bora jambo ambalo limeleta athari kubwa sana katika uchumi na hata mahusiano yetu kitaifa na kimataifa.
Mheshimiwa Spika, uchumi imara ni matokeo ya utawala bora. Ujenzi wa uchumi imara ni matokeo ya moja kwa moja na utawala bora katika nchi. Ukuaji wa uchumi ni lazima uende sambamba na utawala bora. Lakini katika nchi nchi yetu kumekuwa na mambo yanayoifanya nchi yetu isiwe mahala salama kwa ajili ya uwekezaji. Matukio yafuatayo yanaathiri uwekezaji pamoja na utekelezaji wa Bajeti;

Kukwama kwa mchakato wa Katiba Mpya
Tishio la Watu wasiojulikana kuteka, kutesa, kujeruhi na kuwauwa wananchi
Kuminywa kwa Vyombo vya Habari na uhuru wa kupata na kupokea habari kwa kutumia Sheria ya Huduma za Habari pamoja na Makosa ya Mtandao.
Kuminya demokrasia kwa kukataza mikutano ya hadhara ya vyama vya siasa na kutunga sheria kandamizi za kudhibiti siasa na demokrasia.
Kuweka kando utawala wa sheria na badala yake kuongoza nchi kwa utashi wa mtu mmoja.
Kuweka kando mifumo ya kitaasisi katika utendaji na badala yake kutegemea maelekezo ya mtu mmoja.
MAPENDEKEZO YA MPANGO WA KUFUNGAMANISHA KILIMO NA MAENDELEO YA VIWANDA (AGRO ECONOMY)

Mheshimiwa Spika, Sekta ya kilimo inachangia ajira kwa asilimia 70, pato la taifa kwa asilimia 28.2 lakini ukuaji wake unakuwa kidogo sana kwa wastani wa asilimia 5.2 na hivyo kuwa na mchango mdogo sana katika sekta ya viwanda. Kambi Rasmi ya Upinzani italenga kufanya yafuatayo ili kufungamanisha kilimo na uchumi wa viwanda:-

Kuondoa kodi kwenye uwekezaji katika sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi.Hii ni pamoja na kuondoa kodi kwenye viwanda vinavyotengeneza na kukarabati mashine, zana na pembejeo za kilimo, uvuvi na mifugo.
Uwepo wa umeme wa uhakika ili kuendesha shughuli za uzalishaji viwandani. Hivyo, itawekeza ipasavyo katika umeme wa gesi asilia.
Kushirikisha sekta binafsi kupitia mpango wa (PPP) ambapo serikali itawekeza kwenye mitaji ya uwekezaji kwa asilimia 40 na sekta binafsi itashirikishwa kwa asilimia 60.
Kuongeza idadi ya ajira kwa vijana kupitia sekta ya kilimo na viwanda.
Kuongeza pato la mwananchi mmoja mmoja na pia Serikali itapanua wigo wa kodi.
Kusisimua sekta ya usafirishaji na mauzo nje ya nchi.

BAJETI YA SERIAKALI IMEONGEZA MZIGO KWA WANANCHI

Mheshimiwa Spika, serikali katika mwaka wa fedha 2019/20 inapendekeza kufanya marekebisho katika baadhi ya sheria ili kubadilisha viwango vya kodi, baadhi ya sheria hizo ni shaeria ya kodi ya ongezeko la thamani, Sura 148, sheria ya kodi ya mapato, sura 332, sheria ya ushuru wa bidhaa, sura 147, sheria ya usalama barabarani, sura 168, sheria ya forodha ya jumuiya ya Afrika ya mashariki ya mwaka 2004 n.k.
Mheshimiwa Spika, katika marekebisho ya sheria hiyo kuna sheria ya forodha ya Jumuiya ya Afrika ya Mashariki ya mwaka 2004 ambayo pamoja na mambo mengine inapndisha kodi katika vifaa vya ujenzi (mabati na nondo). Kutokana na hali hiyo, bei ya bidhaa na vifaa mbalimbali vinavyotumika kwa ajili ya ujenzi zitaendelea kupanda na hivyo kuathiri azma ya serikali ya ujenzi wa makazi bora na ya kudumu. Mara kadhaa Serikali hii hii imekuwa ikisisitiza kupunguza kodi kwenye vifaa vya ujenzi ili watanzania waweze kujenga nyumba bora; lakini cha ajabu Serikali hiyohiyo, imekuwa na ndimi mbili katika jambo hilo. Kwa mfano, Mei 6, 2014 aliyekuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi alishauri kupunguzwa au kuondolewa kwa kodi katika vifaa vya ujenzi ili watanzania wengi waweze kujenga nyumba bora. Aidha, September 5 2018, akiwa mjini Mwanza kushuhudia utiaji saini wa mikataba minne ya ujenzi wa meli kubwa ya abiria na mizigo ya Serikali, chelezo na ukarabati wa meli za MV Butiama na MV Victoria, Rais John Magufuli alizungumza mambo mengi na kutoa maelekezo kwa watendaji wa Serikali. Miongoni mwa maelekezo aliyoyatoa ni pamoja na kuwaagiza Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano na Waziri wa Fedha na Mipango, kukutana haraka ili kumaliza kilio cha kodi kwenye vifaa vya ujenzi.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inashangaa kuona Waziri wa Fedha akikaidi agizo la Rais la kupunguza kodi kwenye vifaa vya ujenzi na badala yake kupandisha kodi hiyo. Kambi Rasmi ya Upinzani inaamini kuwa punguzo la vifaa vya ujenzi hasa mabati, cement, vifaa vya mabomba ya plastiki na nondo ni hatua mojawapo ya kuelekea kwenye Tanzania ya makazi bora. Kuwa na makazi bora ni mkakati wa kuwa na ongezeko la kodi la uhakika la kodi ya majengo Property tax.

Mheshimiwa Spika, kuhusu punguzo la ushuru wa forodha kutoka 100% hadi 35% kwa mwaka kwenye sukari ya matumizi ya kawaida inayoagizwa kutoka nje ya nchi kwa vibali maalum kwa lengo la kuziba pengo la uzalishaji. Kambi rasmi ya upinzani inaona hatua hii sio kama inaleta tija kwa viwanda vya ndani bali italeta balaa kubwa kwa wakulima wa miwa, kwani sukari nyingi itaingizwa na sukari inayozalishwa ndani itashindwa kuwa na ushindani na hivyo viwanda vitashindwa/vitaacha kununua miwa ya wakulima.

ZA. BAJETI YA SERIKALI IMEJIKITA KWENYE MAENDELEO YA VITU NA SIO MAENDELEO YA WATU
Mheshimiwa Spika, uchambuzi uliofanywa na Kambi Rasmi ya Upinzani kuhusu mgawanyo wa fedha za maendeleo umebaini kwamba; bajeti imejikita kwenye maendeleo ya vitu na sio maendeleo ya watu. Kwa mfano; katika bajeti ya shilingi trilioni 33.104; fedha za maendeleo ni shilingi trilioni 12.25 sawa na asilimia 37 ya bajeti yote. Hata hivyo, mchanganuo wa bajeti ya maendeleo unajumuisha fedha za ndani kiasi cha shilingi trilioni 9.74na fedha za nje kiasi cha shilingi trilioni 2.51.
Mheshimiwa Spika, mgawo wa fedha hizo ni kama ifuatavyo:-
shilingi trilioni 2.48 sawa na asilimia 20.245 ya bajeti yote ya maendeleo ni kwa ajili ya Mradi wa Ujenzi wa Reli kwa kiwango cha Kimataifa (SGR)
shilingi trilioni 1.44 sawa na asiliia 11.755 ya bajeti yote ya maendeleo ni kwa ajili ya Mradi wa Kufua Umeme katika mto rufiji 9( Stiegler’s Gorge Hydoro Power Project) na
shilingi bilioni 500 sawa na asilimia 4.081 ya bajeti yote ya maendeleo ni kwa ajili ya kumalizia malipo kwa ajili ya ununuzi wa Ndege za Serikali.
Mheshimiwa Spika,miradi hiyo mitatu imechukua shilingi trilioni 4.42 ambayo ni sawa na asilimia 36.081 ya fedha zote za maendeleo. Hii miradi ipo kwenye wizara mbili tu, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano pamoja na wizara ya Nishati. Pamoja na miradi hiyo michache kuchukua sehemu kubwa ya bajeti ya maendeleo; bado miradi hiyo haina faida za moja kwa moja katika uchumi wan chi yetu na wake. Hii inatokana na ukweli kwamba malighafi inayotumika kujenga SGR (Chuma na cement) karibu zote zinatoka nje ya nchi na hivyo fedha zinaondoka katika mzunguko wa ndani na kupelekwa nje kwa ajili ya ununuzi wa malighafi hizo. Aidha, ajira zinazozalishwa haziingizi chochote kwenye bajeti yetu kamakdoi ya mshahara (PAYE) kwa kuwa wengi walioajiriwa katika mradi huo ni vibarua (casual laborers) ambao hawapo kwenye mfumo wa kodi. Kwa maneno mengine, hii ni miradi ambayo inanyonya uchumi wetu kwa kutoa fedha ndani na kuzipeleka nje; lakini pili haina multiplier effect katika kuchechemua sekta nyingine za kiuchumi kama vile biashara na ajira.
Mheshimiwa Spika,Kutokana na bajeti hii kuweka kipaumbele katika maendeleo ya vitu badala ya maendeleo ya watu; sekta nyingine zinazogusa maisha ya watu moja kwa moja zimepata mgawo mdogo sana wa fedha za maendeleo jambo linaloashiria kwamba Serikali hii haina mpango na maendeleo na ustawi wa watu. Hata hivyo, miradi na sekta ambazo Serikali inasema ndiyo vipaumbele vyake, nayo imepata mgawo mdogo jambo ambalo linaleta mkanganyiko kuhusu vipaumbele vya Serikali. Mgawo wa fedha kwenye sekta hizo ni kama ifuatavyo:-
Wizara ya Viwanda na Biashara ambayo ndiyo kipaumbele cha kwanza katika bajeti ya Serikali, imetengewa shilingi bilioni 51.5 sawa na asilimia 0.42 ya bajeti nzima ya maendeleo.
Wizara ya Kilimoimetengewa shilingi bilioni 134.577 sawa na asilimia 1.098 ya bajeti ya yote maendeleo.
Wizara ya Elimu imepewa shilingi bilioni 863 ambayo ni sawa na asilimia 7.045 ya bajeti nzima ya maendeleo;
Afya imepewa shilingi bilioni 544.137 sawa na asilimia 4.44 ya bajeti yote ya maendeleo;
Maji yamepewa shilingi bilioni 610.5 sawa na asilimia 4.98 ya fedha zote za maendeleo.
Mheshimiwa Spika, kwa mwenendo huo wa mgawo wa fedha za maendeleo, ni dhahiri shahiri kwamba Serikali hii inayojinasibu kuwa ni ya wanyonge; haipendi wanyonge hao waishi kwa neema kwa kupata huduma bora za kijamii kama vile afya, elimu, maji safi na salama, au kuwekeza katika kilimo chao kinachowapatia ajira na chakula; isipokuwa inawekeza katika vitu ambayo hao wanyonge hawatakuwa na uwezo wa kuvitumia pia.
ZB. BAJETI YA SERIKALI IMEWASAHAU WATUMISHI WA UMMA AMBAO NI WALIPA KODI WA UHAKIKA
Mheshimiwa Spika,bajeti ya Serikali imewasahau kabisa watumishi wa umma ambao toka Serikali hii ya awamu ya tano iingie madarakani hawajawahi kupata nyongeza ya mishahara ya kila mwaka (annual increment) licha ya madai mengine wanayoidai Serikali ikiwa ni pamoja na fedha za likizo; kupandishwa madaraja; malimbikizo ya mishahara na stahili nyingine za kikanuni.
Mheshimiwa Spika, Ikumbukwe kwamba watumishi wa umma ndio walipa kodi wa uhakika kupitia kodi ya mshahara (PAYE) hivyo kutowapandishia mishahara si tu kunafanya maisha yao yaendelee kuwa magumu lakini pia Serikali inapoteza mapato kupitia kodi hiyo. Kwa mujibu wa Kitabu cha Mapato (Revenue Book Volume I) cha mwaka wa fedha 2019/2020 katika ukurasa wa 19 kinaonyesha kwa mwaka wa fedha 2018/19 kodi iliyokuwa imeidhinishwa kukusanywa kutoka kwa wafanyakazi ilikuwa ni shilingi bilioni 998.511 na kwa mwaka wa fedha 2019/20 kodi inayotarajiwa kukusanywa ni shilingi trilioni 1. 065ikiwa ni ongezeko la shilingi bilioni 67.181
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani haioni nia njema ya Serikali kwa watumishi wake kwa kuwa kuna kila dalili za kuwaonea watumishi hao. Dalili ya kwanza ilikuwa ni mkakati wa kuwapunja watumishi mafao yao ya kustaafu kwa kubadili kwa hila kikokotoo cha mafao hayo bila hata kuwashirikisha. Dalili ya pili ni kitendo cha Serikali kufuta fao la kujitoa katika mifuko ya hifadhi ya jamii jambo ambalo linawabana watumishi hasa wale wanaocha kazi kabala ya kufikisha miaka 60; na dalili ya tatu ni kitendo cha Serikali kukopa sana kwenye mifuko ya hifadhi ya jamii na kuchelewa kurejesha fedha hizo kiasi kwamba wastaafu wanakosa kulipwa mafao yao kwa wakati kutokana na mifuko hiyo kukosa fedha.
Mheshimiwa Spika,Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaitaka Serikali kuwapandishia watumishi mishahara katika bajeti hii kwa kuwa ni stahili zao za kisheria na pia kulipa madeni yote ya watumishi ikiwa ni pamoja na madai yao ya fedha za likizo, uhamisho, malimbikizo ya mishahara na stahili nyingine za kikakuni. Aidha, ulipaji wa madeni hayo uende sambamba na kuwapandisha madaraja watumishi wenye sifa za kupandishwa madaraja sambamba na kuwalipa mishahara yao mipya kwa wakati.

ZC. MPANGO WA PILI WA MAENDELEO WA MIAKA MITANO DHIDI YA MIRADI YA MAENDELEO YA KILA MWAKA
Mheshimiwa Spika, mpango wa maendeleo wa miaka mitano ndiyo dira inayotuongoza katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo inayotakiwa kutekelezwa na serikali kwa kipindi cha kuanzia bajeti ya mwaka 2016/17 hadi 2020/21. Mpango huo umetoa mwelekeo ambavyo miradi yote ya maendeleo kwa kipindi hicho itakavyopatiwa fedha za maendeleo na kwa kiwango gani Serikali inatakiwa na Sekta binafsi zinatakiwa kuchangia. Mpango wa maendeleo wa miaka mitano ulihitaji jumla ya shilingi za kitanzania trilioni 107 na kati ya fedha hizo Serikali serikali ilitakiwa kuchangia kiasi cha shilingi trilioni 59(fedha za ndani, mikopo na misaada), ambazo zinatakiwa kila mwaka Serikali itenge kwenye bajeti yake wastani wa shilingi trilioni 11.8 na sekta binafsi ilitakiwa kuchangia shilingi trilioni 48 kwa wastani wa shilingi trilion 9.6 kila mwaka.
Mheshimiwa Spika, kuna miradi ambayo tayari fedha zilikwisha tumika kuanzia kwenye awamu ya kwanza ya mpango wa maendeleo wa miaka mitano FYDP I na pia miradi hiyo imewekwa kama miradi ya kielelezo inayohusu kanda za maendeleo(Flagship projects associated with Development Corridors) na kupitishwa na Bunge hili Tukufu ni pamoja na Undelezaji wa Ujenzi wa Bandari Mpya ya Bagamoyo, Uanzishwaji wa SEZ Bagamoyo, Kigoma,Ruvuma na Mtwara, Uanzishwaji wa Kurasini Trade Logistics Centre, Uanzishwaji wa Dodoma Trade and Logistics Centre.
Mheshimiwa Spika, tukumbuke kwamba Mpango huu wa pili ya miaka mitano (FYDP II) ulipitishwa na Bunge na hivyo ni sheria au ndio mwongozo wetu katika uwekezaji, kwa muktadha huo Kambi Rasmi ya Upinzani inaamini kuwa mabadiliko ya chochote katika nyaraka hiyo ni lazima Bunge lishirikishwe na likubali kuidhinisha mabadiliko hayo. Kambi Rasmi ya Upinzani inasema hayo kutokana na ukweli kwamba Bunge limekuwa kama punching bag kutokana na kutoletewa mikataba ya miradi mikubwa ya maendeleo na hivyo Bunge linapitisha Mpango wa Maendeleo lakini Serikali inabadi Mpango huo bila kuomba kibali cha Bunge. Kwa mfano; Ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo umekuwepo kwenye mpango wa maendeleo wa miaka mitano awamu ya kwanza na kuendelea hadi katika Mpango wa Pili wa Maendeleo, lakini kwa sasa Serikali imegoma kuutekeleza licha ya suala hilo kuwa kwenye Mpango. Kambi Rasmi ya Upinzani ina mtazamo kwamba kitendo cha Serikali kugoma kutekeleza baadhi ya miradi iliyopitishwa na Bunge katika Mpango wa Taifa wa Maendeleo. Kwanza ni dharau kwa bunge; lakini pili ni ishara kuwa Serikali hii haiko makini katika kupanga mipango yake.
Mheshimiwa Spika, jambo jingine la ajabu ni Serikali kuweka kando masharti ya utekekelezaji wa Mpango wenyewe masharti ambayo Serikali ndiyo iliyoyaweka. Kwa mfano; mpango umeeleza vizuri kuwa miradi yote ambayo ni ya kibiasahara itekelezwe na sekta binafsi lakini commercially viable projects should be left to the private sector, unless there is strong justification for doing otherwise. Pamoja na takwa hilo la Mpango, Serikali inatekeleza miradi yote mikubwa bila kuishirikisha sekta binafsi.Miradi hiyo ni pamoja na ujenzi wa SGR, Ujenzi wa kiwanda cha LNG, Liganga Mchuchuma Industrial Park, Mtwara Petrochemical Special Economic Zone na Bagamoyo Special Economic Zone.

Jedwali Na. 1: Sura ya Bajeti mbadala kwa Mwaka Wa Fedha 2019/20
MAELEZO
MAPATO (TZS)

JUMLA YA MAPATO YA KODI
18% of GDP

23,292,000,000,000.00


MAPATO YASIYO YA KODI 2% YA GDP
2,588,000,000,000.00


MAPATO YA HALMASHAURI 1.5% YA GDP
1,941,000,000,000.00


MISAADA YA KIBAJETI TOKA NJE- Capital Grnts from Forign Government (Bilateral) + Capital Grants from International Organization (Multilateral)
1,210,143,710,000.00


JUMLA YA MAPATO

29,031,143,710,000.00


MATUMIZI


MATUMIZI YA KAWAIDA



Deni la Taifa
7,004,480,000,000.00


Mishahara ni 23% ya bajeti mbadala
6,677,163,053,300.00


Matumizi mengineyo
2,054,244,000,000.00


JUMLA YA MATUMIZI YA KAWAIDA
15,735,887,053,300.00


MATUMIZI YA MAENDELEO



Fedha za ndani + Nje
13,295,256,656,700.00






JUMLA YA FEDHA ZA MATUMIZI

29,031,143,710,000.00


































ULINGANISHO NA BAJETI YA SERIKALI


Mheshimiwa Spika, katika bajeti yetu mbadala; badala ya kulipa deni la taifa la shilingi trilioni 10 kama ambavyo bajeti ya serikali inaonesha, Sisi tutalipa kiasi cha shilingi trillion 7. Hii ni kutokana na ukweli kwamba katika biashara yoyote kuna nafasi ya majadiliano, hivyo tutafanya majadiliano ya kulipa kiasi hicho.
Mheshimiwa Spika, bajeti mbadala haiwezi kulipa mishahara kwa kiwango cha shilingi kama Serikali inavyolipa kutokana na ukweli kwamba Serikali inalipa mishahara hiyo bila ya kuwa na uhakika inao watumishi wangapi. Jambo hilo linasababisha fedha nyingi kulipwa kiholela. Tumefikia uamuzi huo kutokana na makusanyo halisi ya kodi ya Mshahara (PAYE) kuwa ndogo sana kulingana na makisio ambayo yanakuwa yamewekwa na Serikali. Kwa muktadha huo mishahara itakayolipwa na Bajeti Mbadala ni trilioni 6.7 ambayo ni sawa na 23% ya bajeti yetu. Mikopo ya kibiashara kutoka nje yenye thamani ya shilingi 3,889,935,853,000.00 hatutaichukua na hivyo kuifanya bajeti Mbadala kuwa na nakisi ya 4.288% tu
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Serikali sura ya bajeti inaonesha nakisi ni asilimia 2.3 ya pato la taifa sawa na shilingi trilioni 2.976, lakini ukiangalia fedha zote kutokana nje (yaani mikopo na misaada ya kibajeti) ambazo kimsingi ndiyo nakisi yenyewe; nitakriban shilingi trilioni 10 ambayo ni takriban asilimia 30 ya bajeti yote. Hivyo nakisi halisi ya bajeti ni asilimia 30 kwa kizio cha jumla ya bajeti yote. Kambi Rasmi ya Upinzani inaionya Seriali kuacha kukokotoa nakisi ya bajeti kwa pato la taifa ambapo nakisi huonekana kuwa ndogo wakati kimsingi bajeti yetu ni tegemezi kwa asilimia 30.
ZD. MAENEO YA KIPAUMBELE KATIKA BAJETI MBADALA
Mheshimiwa Spika, Bajeti mbadala ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni itakua na vipaumbele katika sekta zafuatazo;



Jedwali Na. 2 : Mgawanyo wa Fedha katika Sekta za Kipaumbele
Na.
Sekta
Kiasi (Tshs.)
Asilimia (%)


Elimu
4,354,671,556,500.00
15


Kilimo
5,806,228,742,000.00
20


Viwanda
4,354,671,556,500.00
15


Maji
2,903,114,371,000.00
10


Afya
2,903,114,371,000.00
10


Mengineyo
8,709,343,113,000.00
30


JUMLA
29,031,143,710,000.00
100



ZE. HITIMISHO

Mheshimiwa Spika, naomba kumalizia hotuba yangukwa kusema kwamba kusuasua kwa uchumi wetu kumetokana na kutokuwa na mfumo wa uchumi unaoeleweka. Serikali hii ya awamu ya tano, haijui inafuata mfumo gani wa uchumi. Nimeeleza kwa kirefu hapo awali jinsi ambavyo mfumo wetu wa uchumi umepitwa na wakati na jinsi ambavyo hauendani na mahitaji ya dunia ya sasa; Aidha, nimeeleza madhara ya uchumi kuhodhiwa na Serikali jambo ambalo limeua nguvu ya soko katika kuamua mustakabali wa uchumi. Kutokana na madhaifu hayo ya mfumo wetu wa uchumi, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeniimependekeza mfumo wetu wa uchumi kufanyiwa marekebisho makubwa ikiwa ni pamoja na kupendekeza mfumo mpya wa uchumi ujulikanao kama Mfumo wa Uchumi wa Soko Jamii (Social Market Economy) Mfumo ambao ni wa kisasa kabisa duniani; ili Taifa liweze kujinasua na matatizo ya kiuchumi ambayo yamelifanya taifa hili kuwa masikini kwa miongo yote mitano toka tupate uhuru.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani imeeleza pia kwamba ukuaji wa uchumi na ustawi wa watu ni matokeo ya utawala bora. Hivyo, ujenzi wa uchumi imara ni lazima uende sambamba na utawala bora. Kama kuna tishio la usalama kwa maana ya watu kutekwa na kuteswa wakiwemo wafanya biashara wakubwa; kama kuna ukandamizaji wa demokrasia na haki za binadamu; kama hakuna uhuru wa habari; kama hatuna mahusiano mazuri ya kidiplomasia na Jumuiya ya Kimataifa n.k tusitegemee uwekezaji wa maana katika nchi yetu.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani imeonyesha pia namna bajeti hii ya nne ya Serikali ya awamu ya tano ilivyojikita kwenye maendeleo ya vitu badala ya maendeleo ya watu. Takriban asilimia 40 ya fedha za maendeleo zimetumika kugharamia miradi mitatu tu iliyopo katika Wizara mbili; yani wizara Nishati na Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano. Miradi hiyo ni SGR, Stieglers Gorge, na Ufufuaji wa Shirika la ndege. Jambo hili limesababisha fedha za maendeleo katika sekta nyingine zinazoguza moja kwa moja maisha ya wananchi kama vile afya, kilimo, elimu maji,mifugo na uvuvi kupungua sana.
Mheshimiwa Spika,naomba nimalizie kwa kusema kwamba; hili taifa ni letu sote Hakuna Mtanzania mwenye sifa za utanzania zaidi ya mwingine wote ni watanzania. Kwa hiyo, kitendo cha watawala kuona kwamba wao ni bora zaidi na kutuita sisi wenye mawazo mbadala kwamba si wazalendo na kwamba tunapinga maendeleo ni kauli za kibaguzi na hazilijengi taifa bali zinalipasua. Serikali iwe inapokea changamoto na mawazo mbadala kutoka upinzani na kuyafanyia kazi.
Mwisho kabisa Mheshimiwa Spika, Serikali iache kufanya propaganda katika mambo ya msingi hasa katika bajeti ya Serikali. Tumeeleza kwa kirefu jinsi Serikali inavyowahadaa wananchi kwa kuweka makisio makubwa ya ukusanyaji wa mapato ambayo inajua kabisa kuwa haiwezi kukusanya na hivyo kuwapa wananchi matumaini hewa! Kwa kuwa Serikali hii ya awamu ya tano ilikuwa bingwa sana kukabiliana na vitu hewa kuanzia wafanyakazi hewa na madai hewa ya watumishi; ijisafishe na yenywe kwa kuacha kupanga bajeti hewa kwa maendeleo ya taifa hili.
Mheshimiwa Spika,baada ya kusema hayo, naomba kuwasilisha.


David Ernest Silinde (Mb)
KNY:WAZIRI KIVULI WA FEDHA NA MIPANGO
NA MSEMAJI MKUU WAKAMBI RASMI YA UPINZANI BUNGENI,
KATIKA WIZARA YA FEDHA NA MIPANGO
17 Juni, 2019
Nahitaji cilp maana kusoma nasinzia
 
Back
Top Bottom