Babu Seya kurudi uraiani kesho?

kilimasera

JF-Expert Member
Dec 2, 2009
3,068
266
HATIMAYE Mahakama ya Rufani nchini kesho inatarajia kutoa hukumu ya mwanamuziki mahiri wa muziki wa dansi nchini, Nguza Viking, maarufu kwa jina la ‘Babu Seya’ na wanawe watatu.

Watoto hao wa Babu Seya ni pamoja na Papii Kocha Nguza, Nguza Mbangu na Francis Nguza ambao wanatetewa na wakili wa kujitegemea Mabere Marando na Hamidu Mbwezeleni toka Zanzibar.

Hati ya kuitwa mahakamani iliyotolewa na Msajili wa Mahakama ya Rufani, Francis Mutungi, kwa Wakili Marando na uongozi wa Gereza la Ukonga, iliomba ruhusu warufani hao kufika mahakamani kusikiliza hukumu yao itakayotolewa na mahakama hiyo.

Akilithibithitishia gazeti hili, Marando, mmoja wa mawakili wakongwe nchini, alisema: “Ni kweli leo (jana) nimepokea hati ya wito (summons) toka Mahakama ya Rufani ikiniarifu mimi na wateja wangu tufike asubuhi katika mahakama hiyo ili tuweze kusikiliza hukumu itakayotolewa na majaji watatu ambao ndio walikuwa wakisikiliza rufaa yetu.

“Na ninakuhakikishia kwamba tayari wateja wangu (warufani) wameshapelekewa hati hiyo ya wito kule gerezani Ukonga na tumejiandaa kwenda kusikiliza na kuipokea kwa mikono miwili hukumu hiyo ambayo bila shaka inavuta hisia za watu wengi,” alisema Wakili Marando.

Januari 3, mwaka huu, jopo la majaji watatu wa Mahakama ya Rufani wakiongozwa na Jaji Nataria Kimaro, Salum Massati, na Mbarouk Mbarouk walisikiliza rufaa hiyo kwa siku moja.

Wakati wa utetezi wao, mawakili wa warufani hao, waliomba mahakama iwaachirie huru wanamuziki hao kwa madai kuwa hukumu iliyowatia hatiani, ilikuwa na dosari nyingi za kisheria.

Mawakili hao walidai kuwa kesi hiyo ilikuwa ya kupangwa na kwamba hawajawahi kuona hukumu ya hovyo ya ina hiyo tangu waanze kufanya kazi ya uwakili kwa zaidi ya miaka 30 sasa.

Mawakili hao waliwasilisha sababu nne za kupinga hukumu ya Mahakama Kuu iliyotolewa na Jaji mstaafu, Thomas Mihayo, na hukumu iliyotolewa na aliyekuwa Hakimu Mkuu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, Addy Lyamuya, ambao wote waliwatia hatiani washtakiwa kwa makosa ya kuwalawiti watoto wadogo, hivyo kuwafunga kifungo cha maisha jela.

Miongoni mwa sababu hizo ni kwamba jaji na hakimu huyo walikosea kisheria kutoa hukumu hiyo kwani sheria inaitaka mahakama kabla haijaanza kuchukua ushahidi wa mtoto ni lazima ijiridhishe kwamba mtoto huyo ana akili timamu na anaelewa maana ya kiapo na kisha irekodi hayo kwenye jarada la kesi lakini Hakimu Lyamuya hakufanya hivyo wala kuandika rekodi,” alidai Marando.

Marando akiwasilisha sababu hizo kwa kujiamini, alidai kuwa kwa makosa hayo ya kisheria, yaliyofanywa na hakimu Lyamuya na jaji huyo hadi wakafikia uamuzi wa kuwafunga kifungo cha maisha warufani, ni wazi kwamba walikuwa wanapingana na sheria za nchi na maamuzi yaliyotolewa na majaji wa mahakama za hapa nchini kwenye kesi mbalimbali, ambazo alizitumia kutetea hoja zake.

“Lakini majaji katika rufaa ya Mahakama Kuu hakuna ushahidi uliotolewa unaoonyesha warufani walibaka...hayo yalikuwa ni mawazo ya hakimu kwamba lazima Babu Seya na watoto wake waende gerezani,....narudia tena sijawahi kuona hakimu wa aina hii na hukumu ya aina hii ambayo hakimu aliamua kuweka maoni yake binafsi kwani kinachowatia hatiani washtakiwa katika kesi zote ni ushahidi na siyo maoni ya hakimu.

“Ni wajibu wa mahakama kutafakari ushahidi wa utetezi hata kama hauna uzito; sasa huyu Lyamuya katika hukumu yake amewataja mashahidi wa utetezi waliokuja kutoa ushahidi bila kueleza mashahidi kwa mapana walieleza nini!

“Kwa mkanganyiko huu uliofanywa na Hakimu Mkazi Mwandamizi, Lyamuya, siyo tu alikosea kisheria; nasema alifanya makusudi na alikuwa ameshaamua kuwapeleka jela warufani!” alidai Marando.

Alihoji sababu zilizosababisha upande wa mashtaka kuficha ripoti ya daktari aliyewafanyia uchunguzi watoto hao wanaodaiwa kubakwa na warufani na kushindwa kuleta mashahidi ambao ni wanamuziki wa bendi ya Achigo, mama wa Babu Seya na mke wa Babu Seya, kwa sababu waliona mashahidi hao wangewaumbua.

“Kesi hii ni ngumu kwetu sote na kama mahakama na sisi tunaona warufani walifanya haya makosa tuwalaani ila mimi Marando nasema nimejiridhisha hawajafanya hayo makosa.

“Hivi tujiulize kibaiolojia kweli inawezekana mtoto wa miaka sita abakwe na wanaume hawa (warufani) nyuma na mbele halafu aweze kutembea? Haingii akilini hata kidogo; nasema kesi hii ni ya kutunga kwani hata mwanamke mwenye umri wa utu uzima akifanyiwa unyama huu hawezi kutembea!” alidai Marando na kusababisha umati uliofurika kuendelea kuacha vinywa wazi kwa mshangao.

Akijibu hoja za mrufani, Wakili Mkuu wa Serikali, Justus Mulokozi, ambaye alitumia nusu saa kujibu hoja hizo alidai kuwa kitendo cha shahidi kushindwa kumtambua mshtakiwa mahakamani siyo sababu inayopelekea ushahidi wa shahidi huyo kuonekana hauna thamani.

Pia alidai mahakama ikiamini upande mmoja, hailazimiki kuangalia upande mwingine lakini hata hivyo hoja hiyo ilipingwa vikali na Marando ambaye alidai kuwa hoja hiyo haikupaswa kutolewa na wakili mwandamizi kama Mulokozi kwani hoja hiyo inatofautiana na sheria za nchi na kauli hiyo ya wakili wa serikali imedhihirisha sasa ni kweli Lyamuya aliegemea ushahidi wa upande wa mashtaka tu.

Januari 27, 2005, aliyekuwa Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Thomas Mihayo, ambaye kwa sasa amestaafu alitupilia mbali rufaa yao iliyokuwa ikipinga hukumu iliyotolewa na aliyekuwa Hakimu Mkuu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Addy Lyamuya, ambaye aliwatia hatiani kwa makosa yote waliyokuwa wameshtakiwa nayo Juni 25, 2004.

Waomba rufani hao wanakabiliwa na makosa kumi ya kubaka watoto wa kike wenye umri kati ya miaka sita na nane na makosa mengine 11 ya kulawiti watoto wa kike wenye umri huo na kwamba wanadaiwa kutenda makosa hayo kati ya Aprili na Oktoba, 2003 eneo la Sinza kwa Remmy, jijini Dar es salaam.

Aidha, katika kesi hiyo mwalimu wa shule ya msingi Mashujaa, Sigirinda Ligomboka, alishtakiwa kwa makosa mawili ya kumsaidia Babu Seya kutenda makosa ya kubaka na kulawiti kwa kuwaruhusu baadhi ya watoto hao kutoka madarasani.

Upande wa mashtaka ulileta mashahidi 24, ambao upande wa utetezi ulipinga vikali kutenda makosa hayo na uliita mashahidi nane. Katika hukumu yake Hakimu Lyamuya alitupilia mbali utetezi wa Babu Seya na wanawe na akawatia hatiani kwa makosa hayo na hivyo kuwafunga kifungo cha maisha jela.
 
hatimaye ndoto yangu niliyoota miezi kadhaa nyuma kuwa babu Seya, Papii kocha, Francis wanatumbuiza pale uwanja wa uhuru shamba la bibi baada ya kuachiwa huru inatimia.]
kweli sijui kwanini naamini hawa wanamuziki wanatakua huru, na kesho saa moja usiku watakua na ibada maalumu kumshukuru Mungu kwa kuachiwa kwao, kabla ya jumamosi kupiga show kubwa.
 
Mungu awasimamie waweze toka gerezani,na hila za muovu shetani zipate shindwa ktk jina la Mchajikobe.Amen
 
Naomba wajuzi wa sheria...watuambie kuna jamaa mmoja alisoma sheria ila si wakili....kuwa huwezi kufngwa maisha na kuachiwa huru...lazima itakuwa kifungo fulani hv..ila si huru kabisa!!!
 
Naomba wajuzi wa sheria...watuambie kuna jamaa mmoja alisoma sheria ila si wakili....kuwa huwezi kufngwa maisha na kuachiwa huru...lazima itakuwa kifungo fulani hv..ila si huru kabisa!!!
mimi sijasoma sheria , ila wapo watu waliwahi kuhukumiwa kifo na wakakata rufaa na wakashinda wakawa huru, huru kabisa....... kumbuka kunyongwa ndio hukumu kali kabisa hapa duniani lakini isio na maana.
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom