Baada Ya Seacliff Kuungua: Yafukuza Wafanyakazi 200...!!

Steve Dii

JF-Expert Member
Jun 25, 2007
6,402
1,254
Balaa la wafanyakazi wa SeaCliff baada ya balaa la moto:

Hoteli iliyoungua Dar yafukuza wafanyakazi 200

Na Kizitto Noya

LICHA ya kuahidi mbele ya Makamu wa Rais Dk Ali Mohamed Shein kwamba hakuna mfanyakazi atakayeachishwa kazi kutokana na ajali ya moto ulioteketeza sehemu kubwa ya hoteli ya Kitalii ya SeaCliff, sasa imefahamika kuwa, zaidi ya wafanyakazi 200 wa hoteli hiyo wameachishwa kazi.


Habari zilizolifikia gazeti hili jana zilieleza kuwa wafanyakazi hao wameachishwa kazi na kulipwa mafao ya kati ya Sh 130,000 na 200,000 fedha ambayo wote wamegoma kuipokea wakidai kuwa ni kidogo mno ikilinganishwa na muda waliofanyakazi hotelini hapo.


Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Majumbani na Mahotelini (Chodau), tawi la SeaCliff, Peter Sarakani alilithibitishia gazeti hili juu ya tukio hilo lakini hakutaka kulizungumzia kwa kina kwa maelezo kuwa linashughulikiwa na Chodau ngazi ya mkoa.


�Tukiwasiliana Jumatatu naweza kusema chochote kwani ndio siku ambayo Chodau Mkoa ilikubaliana na wafanyakazi hao kufika SeaCliff kwa suala hilo,� alisema.


Alisema uongozi wa Chodau uliwazuia wafanyakazi hao kuchukua mafao yao hadi hapo mazungumzo baina yake na uongozi wa Seacliff yatakapokamilika.


Baadhi ya wafanyakazi waliliambia gazeti hili juzi kuwa, wamegoma kuchukua mafao yao kwa agizo la Chodau mkoa, kutokana na malalamiko kuwa hayatoshi.


Walisema baada ya hoteli hiyo kuungua moto mwezi Septemba mwaka huu, uongozi wa hoteli umeshindwa kutekeleza ahadi iliyowapa mbele ya makamu wa rais kwamba hautamfukuza hata mfanyakazi mmoja kutokana na tukio hilo bali wote wataendelea na kazi.


�Baada ya hapo walitulipa mshahara wa Mwezi Oktoba na tulipoenda kuchukua mshahara wa Mwezi Novemba wakatupa barua za kutuachisha kazi na mafao ambayo hayatoshi kwa chochote,� alisema mmoja wa wafanyakazi hao ambaye hakutaka kutajwa jina lake gazetini.


Meneja Mkuu wa hoteli hiyo, Keven Stander aliulaumu uongozi wa Chodau akisema kuwa ndio uliosababisha mgomo wa wafanyakazi hao kuchukua mafao yao.


Alisema uongozi wa SeaCliff haujakiuka sheria katika kuwapa mafao hayo wafanyakazi hao kwani ulifanya hivyo baada ya kuwasiliana na wizara ya Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana.


"Hatujakiuka sheria yoyote ya kazi kwani tulipanga kuwalipa mafao yao baada ya kuwasiliana na wizara," alisema Stander.


Alisema pamoja na mafao hayo, Seacliff imeendelea kutekeleza ahadi yake ya kutowafukuza kazi wafanyakazi hao kwa kuwatafutia kazi katika hoteli zingine za jijini la Dar es Salaam.


Alieleza kuwa tangu hoteli hiyo iwaachishe kazi wafanyakazi hao imefanikiwa kuwapatia ajira mpya wafanyakazi 60 ambao wanafanyakazi katika hoteli za Kilimanjaro na Movenpick.


Septemba 22 mwaka huu sehemu kubwa ya hoteli ya SeaCliff ya jijini Dar es Salaam iliungua moto na kusababisha hasara ya zaidi ya Sh33bilioni.


Moto huo ulianzia sehemu ya jikoni, ulizimwa kwa msaada wa taasisi mbalimbali za zima moto ikiwamo kikosa kikosi chenyewe cha zimamoto.

Source link: Mwananchi.

SteveD.
 
Back
Top Bottom