Awamu ya nne na kizazi cha www.com

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,792
287,994
Awamu ya nne na kizazi cha www.com

Ayoub Rioba Oktoba 31, 2007
Raia Mwema

KWANZA walianza kuzomea viongozi wa Serikali. Baadaye hata Rais Jakaya Kikwete alipoenda Shinyanga, kule Buzwagi, wakambebea mabango. Wakampa ujumbe.

Kipindi kile habari za mkataba wa shaka wa Buzwagi zilikuwa zimetawala katika vyombo vya habari. Wananchi wale wale waliompenda sana Jakaya Kikwete na kumpa kura zao kwa moyo mmoja miaka miwili iliyopita, sasa wanaibebea mabango Serikali yake. Wanawafurumsha mawaziri kwa maswali magumu.

Zipo kila dalili kwamba kuna tatizo mahala. Tena tatizo kubwa. Yaani ghafla tu wananchi wa Kagera wanaandaa maandamano ya haraka haraka wanaelekea kituo cha polisi wakimtafuta mtuhumiwa wa kuuza viungo vya binadamu ili wamshughulikie wao wenyewe!

Huko Singida nako wananchi wenye hasira wanaandaa maandamano ya haraka haraka, wanaelekea kituo cha polisi wakimtafuta mtuhumiwa aliyebaka mabinti wawili na kuwaua ili wamtie adabu wao wenyewe.

Wanaingia kituo cha polisi; kabla askari hawajajua nini kinaendelea, wananchi wanaingia mahabusu. Wanamchoropoa mtuhumiwa wao. Wanaanza kumkanyagakanyaga hadi anakata roho. Askari polisi wanafyatua risasi juu kutishia, lakini wananchi hawa wanaendelea na hukumu yao!

Wakati huo huo, wananchi wa vijijini wanapotembelewa na viongozi wa Serikali wanahoji maswali mazito. Matokeo yake baadhi ya viongozi wa Serikali au chama kinachotawala wanataharuki. Wanaanza kusakama wauliza maswali. Wanawatuma watu wao kuchunguza ni nani kawafundisha wauliza maswali wale.

Nani kawafundisha kuuliza maswali ya kiakili vile. Kana kwamba wananchi walitakiwa kubaki wajinga wajinga wasojua kuuliza mambo ya kiakili. Wasojua kuhoji. Leo wanahoji. Mtoto wa kidato cha kwanza anamhoji Waziri Mkuu swali zito. Waziri Mkuu anasita kusema. Anaahidi kulijibu akirejea safari nyingine. Hao ndio Watanzania wa Kikwete. Watanzania wa www.com.

Ukiwaahidi jambo wanaandika mahala. Siku ukiwatembelea wanakukumbusha. Ukiwadanganya wanakupa takwimu au ukweli mwingine kama walivyoupata kutoka vyanzo mbadala. Kuna intaneti. Kuna simu. Kuna blogu. Kuna njia nyingi.

Ukiwaambia uchumi unapaa wanakutazama. Wanacheka. Wanakusubiri. Ukifika wanakuuliza : Mwenzetu-ee, mbona hata hizo ndege zikipaa tunaziona. Huo uchumi unapaa kutokea uwanja gani? Unarukia anga ipi? Uchumi ukipaa si wananchi wanapaswa kujua kwa sababu wao ndo abiria? Au rubani na wafanyakazi wameamua kupaisha ndege bila abiria?

Kwa muda mrefu kumekuwapo na sauti zinazoeleza kutoridhishwa na namna baadhi ya mambo yanavyokwenda nchini. Kwa hakika tumeamua kupuuza sauti hizo. Tulimpuuza aliyepata kuwa Katibu Mkuu wa chama kinachotawala, Horace Kolimba aliyetaka turejee katika meza ya majadiliano kuhusu dira ya nchi.

Tulivyompuuza Kolimba akafariki dunia. Hatukujifunza. Leo tena zinaibuka sauti za akina Joseph Butiku. Tunawadhihaki. Jinsi ile ile tulivyomdhihaki Kolimba. Hakika dhihaka hii itakuja kututokea puani.

Tazama tu jinsi tunavyojadili mjadala ulioanzia bungeni kuhusu hoja binafsi ya Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe, ya utata wa mkataba wa Buzwagi. Ni dhahiri nchi sasa imeingia katika mgogoro unaofukuta kama volkano ya Oldoinyo Lengai.

Tayari kuna mpasuko wa wazi unaoanza kujidhihirisha katika mitazamo yetu ya mambo. Pamoja na ukweli kwamba hiyo ni sehemu ya kukomaa kwa demokrasia, upo ukweli dhahiri kwamba katika mjadala wa Buzwagi na watuhumiwa wa ufisadi, nchi imegawanyika makundi mawili makuu.

Kundi la kwanza ni la wale wanaoinuka kila uchao kutetea mambo yalivyo. Wao hoja zao ni kwamba kwanza nchi hii inanufaika sana na madini na rasilmali nyingine; kwamba ni wapinzani tu na wenye wivu wa kijinga wasiotaka kuona mafanikio ; kwamba uchumi wa Tanzania unafanya vizuri sana (japo ni ya nne katika orodha ya nchi maskini duniani) ; kwamba wapinzani hawana lolote wanaweweseka tu kwa kubwagwa vibaya katika uchaguzi wa 2005; n.k.

Hawa wanatetea maslahi binafsi ya kundi. Hawataki kuzungumzia maslahi ya Tanzania. Kwao wao wakifaidi kutokana na mikataba mibovu inayotia nchi hasara basi wanahitimisha kwamba nchi inanufaika.

Katika kundi hili mtu mmoja akinunuliwa nyumba Afrika ya Kusini pale katika jiji la Johannesburg, akasaini mkataba wa kijinga kama ile ya kina Lobengula na Chifu Mangungo, basi anahitimisha kwamba nchi nzima imenufaika. Anawauliza Watanzania : ‘Nyie vipofu kwa nini hamuoni nchi inavyoendelea?’

Kundi la pili linaangalia picha kubwa zaidi. Kundi hili linajadili masuala zaidi kuliko matukio tu. Linavuka mipaka ya awamu za utawala nchini ; mipaka ya kichama ; mipaka ya maslahi binafsi yapatikanayo katika kundi fulani ; n.k. Ni kundi lenye kuona mbali.

Linatazama mbele na kuona giza. Kundi hili linagundua kwamba kuna namna nchi hii inaporwa taratibu kutoka kwa Watanzania wanyonge walio wengi na kukabidhiwa kwa wasio na uchungu nayo.

Kwamba sasa hata pengo kati ya masikini na matajiri wa kukufuru linaongezeka. Na kuthibitisha uoga wa pengo hilo, wale wenye nacho kupindukia wakijenga nyumba zao wanaweka uzio mrefu kama jela. Wanaweka nyaya za umeme. Wanawaogopa walala hoi. Wengine wanaweka fedha zao Ulaya. Wananunua majumba huko. Wanajiwekea hazina katika mbingu ya Ulaya ambako si nondo wala TAKUKURU wanaweza kufika.

Hawajali ni mamilioni ya Watanzania wangapi wanaishi maisha ya kubangaiza. Maisha ya kuwaza mlo wa leo. Hawajali ni kina mama wangapi hufa wakati wa kujifungua kutokana na kukosa huduma muhimu.

Hawajali ni watoto wangapi hufa kabla ya kufikia miaka mitano kwa sababu tu hukosa huduma muhimu za afya na lishe. Hawajali kuna yatima wangapi katika nchi hii ambao wanajuta ni kwa nini walizaliwa!

Wiki ijayo nitajadili tatizo la msingi katika nchi zetu (za Afrika kwa ujumla) na kuonyesha kwamba hata mjadala wa sasa nchini unakazania zaidi matokeo ya tatizo na hauligusi tatizo lenyewe moja kwa moja.

Na madhali tunaendelea kuchangamkia kujadili matokeo basi wapo wanaofurahia ukweli kwamba hatujang’amua kiini cha tatizo letu. Kwa sababu siku tuking’amua kiini cha tatizo tutakasirika zaidi na mjadala utachukua sura mpya.
 
amezungumza mambo mazito sana...

worthless.gif
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom