Athari za kukopesha Wateja Bidhaa

Miss Zomboko

JF-Expert Member
May 18, 2014
4,500
9,279

1. Kumpoteza mteja​

Kuna usemi usemao kumkopesha mteja ni kumfukuza. Nimesikia mara kadhaa wafanyabiashara wakisema tangu ni mkopeshe haji tena dukani kwangu, au tangu nimkopeshe anapita mbali tu. Mara nyingi mteja akishakopeshwa pesa au bidhaa haji tena kwenye biashara husika ili kukwepa kulipa deni.

Kuliko umpoteze mteja kwa kumkopesha ni bora umueleze ukweli kwa kutumia busara; ingawa hatofurahi kwa wakati ule lakini baada ya muda atakuelewa na ataendelea kuwa mteja wako.

2. Ugomvi au kuharibu mahusiano​

Kuna msemo usemao kukopa harusi kulipa matanga. Mara nyingi watu huja kwa uso mzuri uliojaa furaha na uaminifu wakati wa kukopa. Mara tu baada ya kukopa maisha ya shari na kusumbuana yanaweza kutokea hasa kwa wale wateja wasio waaminifu kulipa deni.

Kuna wafanyabiashara walioishia kugombana vibaya au hata kuvurugika kabisa kwa mahusiano yao na baadhi ya wateja wao kutokana na kuwakopesha bidhaa au pesa kutoka kwenye biashara zao.

Hivyo basi, kuliko uishie kugombana na wateja wako au watu wako muhimu, ni vyema ukaepuka suala hili la mikopo katika biashara yako.

3. Athari katika mzunguko wa pesa​

Pesa za biashara zinatakiwa kuzunguka na si kukaa eneo moja. Mtaji wa biashara unapokuwa bidhaa katika biashara, bidhaa hizo zinapaswa kuuzwa, baada ya bidhaa hizo kuuzwa tunatakiwa kupata mauzo ambayo hujumuisha sehemu ya mtaji na faida. Mtu anapokopa pesa au bidhaa kutoka kwenye biashara yako, moja kwa moja anavuruga mzunguko huu.

Hili husababisha matatizo kama vile kukosa pesa timilifu kwa ajili ya manunuzi au gharama nyingine. Tatizo hili limewasababishia wengine kuchukua pesa zao binafsi au zilizoko nje ya biashara ili kuzipa pengo lililotokana na mikopo ili biashara isiyumbe.

4. Kupoteza fedha na mali​

Kwa hakika hakuna hakikisho la asilimia mia moja kuwa pesa au bidhaa ulizomkopesha mteja zitalipwa. Ikizingatiwa kuwa watu wengi hukopeshana pesa na bidhaa kienyeji bila kufuata taratibu za kisheria zinazoweza kuwalinda baadaye iwapo mkopaji hatokuwa mwaminifu.

Hivyo basi, mikopo inaweza kukusababishia kupoteza fedha na mali ulizowakopesha wateja iwapo wateja hao hawatakuwa waaminifu kulipa, jambo ambalo linaweza kukuathiri pia kibiashara.

5. Kufilisika au kufa kwa biashara​

Hoja hii ni hitimisho tu la hoja zilizotangulia; ikiwa mikopo haitalipwa kwa wakati au haitolipwa kabisa, biashara yako inaweza kufilisika au kufa kabisa. Imeshuhudiwa wafanyabiashara wakiwa na mikopo wanayodai kutoka kwa wateja wao ambayo inazidi hata nusu ya mitaji yao; huku wakiwa hawana uhakika kama watalipwa pesa hizo au laa. Ni muhimu sana kulichukulia swala la mikopo kwa tahadhari kubwa lisije likasababisha biashara yako kufa.
 
mbona waha wanskopesha wanapitia bukubuku hazifi biashara zao, mkuu mfano unauza mashuka watu wakitaka uwakope upitie kidogo kidogo itakuwaje?
 
Hakuna mfanya biashara duniani ambaye anaweza fanya biashara bila kukopa au kukopesha.

Kufirisika au kufa biashara ni management ya mtu tu.
 
Hakuna mfanya biashara duniani ambaye anaweza fanya biashara bila kukopa au kukopesha.

Kufirisika au kufa biashara ni management ya mtu tu.
Vipi kuhusu mteja aliekopa kukukimbia Asije kununua bidhaa kwako Kwasababu ya Deni?
 
Back
Top Bottom