Askofu Niwemugizi: Nitaendelea Kuhoji Mambo ya Muhimu ya Nchi ikiwemo Katiba sitanyamaza

Mwanahabari Huru

JF-Expert Member
Mar 9, 2015
14,243
34,898
nemugiza.jpg

Bado nitaendelea kuizungumzia Katiba na Mambo mengine yenye maslai kwa nchi yangu kwa sababu inagusa maisha yangu na Kanisa ninalotumikia, lakini pia inayagusa maisha ya raia wenzangu wote.

=====

NIANZE kwa kujitambulisha kuwa mimi Severine Niwemugizi ni raia wa Tanzania, pia ni Askofu Mkatoliki wa Jimbo la Rulenge-Ngara.

Lakini pia niongeze kusema kuwa haya ninayoandika ni maoni yangu binafsi, hayawakilishi msimamo wa Kanisa Katoliki.

Septemba 20 mwaka huu, nilialikwa na Asasi za Kiraia kushiriki kama raia Mtanzania kwenye mazungumzo ya kitaifa ya kufufua mchakato wa Katiba.

Bahati mbaya asubuhi ya siku hiyo nikaombwa kufungua mazungumzo na baadaye kufunga. Kwa nia nzuri nikasema ni muhimu kwa nchi yetu ikapata Katiba nzuri na madhubuti ambayo naamini ndiyo dira muhimu kwa uhai na maendeleo ya taifa letu.

Nilisema kwa maoni yangu, naamini Katiba ni kipaumbele cha wananchi. Hii ni kwa sababu ya kile nilichokishuhudia kwenye mchakato wa Katiba miaka mitatu iliyopita.

Nilishuhudia namna watu walivyojaa hamasa, walivyojitokeza kutoa maoni yao, walivyoufuatilia mchakato wenyewe hadi ilipotolewa rasimu ya Katiba Pandekezwa.

Lakini pia kiasi cha rasilimali kilichotumika katika mchakato huo! Ninaamini Rais mstaafu Kikwete aliamini pamoja na umma wa Watanzania wengi kuwa Katiba ilikuwa kipaumbele, ndiyo maana fedha nyingi ilitengwa kwa ajili ya mchakato huo wa Katiba.

Kwa kusema hivyo nilieleweka vibaya kwa wengine. Kwanza kwamba nilionekana kusema hayo kwa niaba ya Kanisa Katoliki au ya Baraza la Maaskofu Katoliki.

Ukweli ni kuwa kwenye mazungumzo yangu hayo ya Septemba 20, nilianza kwa kusema wazi kuwa sikutumwa na TEC kuzungumza pale.

Nilizungumza kama raia mwingine yeyote wa Tanzania anavyoweza kutoa maoni yake. Tatizo ni kwa baadhi ya watu kushindwa kutofautisha maoni ya mtu binafsi na msimamo wa taasisi aliyo sehemu yake.

Bado nitaendelea kuizungumzia Katiba kwa sababu inagusa maisha yangu na Kanisa pia ninalotumikia, lakini pia inayagusa maisha ya raia wenzangu wote.

Kwa vyovyote naheshimu tofauti zetu za kuwaza na kuona mambo, kwani ndivyo ilivyompendeza Mungu kutuumba hatufanani tangu sura hadi kuwaza. Nilifurahi nilipopingwa, nikajua kuwa lengo limefanikiwa kuchokoza ili tuanze tena kuzungumzia mchakato wa Katiba.

Bado siogopi kukoromewa na sauti nzito, nikijua kuwa hata Yesu alikoromewa na wakuu! Naamini hatimaye kitu kizuri kitazaliwa baada ya michango ya mawazo kwa lengo la kujenga.

Mimi siamini kuwa Katiba mpya ilikuwa kipaumbele wakati ule tu na sasa sio. Kwa hiyo kwa kweli, si kwamba tunavumbua gurudumu jipya, bali ni kulifanya lile lililokwishaanza kuzunguka liendelee.

Ndiyo maana pia ilani ya uchaguzi ya CCM ikabeba ajenda hiyo kama jambo la kukamilisha katika muda wa miaka mitano ijayo.

Leo napenda tu kujieleza kiasi ninavyofahamu Katiba na umuhimu wake kwa taifa au nchi yoyote, bila kujali lini Tanzania itaipata Katiba nzuri wanayoitaka wananchi. Mimi naamini Watanzania wengi wanaitaka hiyo Katiba sasa.

Lakini yawezekana kabisa kuwa wale wenye jukumu la kuhakikisha Katiba hiyo inapatikana, wana majukumu mengi wanayoona inafaa yashughulikiwe haraka zaidi kwanza kabla ya Katiba. Tuwape muda ila tuwaeleze bila woga kuwa Katiba nzuri ni hitaji kubwa la Watanzania walio wengi.

Mimi naamini kabisa kuwa Rais wetu anayo moyoni ajenda ya Katiba mpya. Tusisahau kuwa naye ni binadamu. Bila shaka ana anachokiwazia, huenda.

Tulishafundishwa na Bwana Yesu kuwa “mti mwema huzaa matunda mazuri na mti mwovu huzaa matunda mabaya” (Mt. 7:17).

Huduma zote iwe ni kuhakikishiwa chakula, matibabu, ulinzi wa uhai, utawala wa sheria, chochote kile kizuri lazima viratibiwe kwa mujibu wa sheria nzuri zilizotokana na Katiba nzuri.

Hata kama si daima Katiba ndiyo mwarobaini wa kila jambo, lakini kwa kiasi kikubwa unaweza kusema Katiba ni kila kitu kwa taifa.

Yale mapungufu makubwa katika kuiendesha nchi ikiwa ni pamoja na ufisadi, wizi na matumizi mabaya ya rasilimali za nchi, matumizi mabaya ya madaraka, utumishi wa umma usio na uadilifu, utendaji usiozingatia utawala bora na karaha nyingi tulizoshuhudia zikikabiliwa na utawala wa awamu ya tano ni matunda ya sheria mama isiyokidhi haja za wakati wa sasa.

Hayo ndiyo yaliyozaa kilio cha Watanzania kutaka Katiba mpya enzi za utawala wa awamu ya nne.

Kwa uelewa wangu mdogo, Katiba ndiyo mwongozo mkuu wenye sheria na kanuni za msingi zinazoongoza nchi, vyama, mashirika au taasisi. Nchi zote zenye demokrasia huwa na Katiba zinazoongoza nchi.

Sheria au kanuni kwenye katiba hueleza namna raia wa taifa fulani wanavyohusiana, wanavyopaswa kuenenda, inakuwaje raia akivunja sheria, viongozi wa taifa ni akina nani na wanapatikanaje, nchi inatawalikaje.

Sheria hizi au kanuni hizo zinakuwa muhimu hivyo kiasi viongozi wakuu wanaapa kuheshimu na kuilinda katiba pale wanapokabidhiwa madaraka.

Isipokuwa hivyo, nchi inaweza kuingia gizani au katika vurugu kubwa! Sielewi mtu akisema Katiba nzuri si muhimu sasa.

Kwa uelewa wangu mdogo zipo aina nyingi za Katiba, lakini aina kuu ni nne; Katiba iliyoandikwa au Katiba isiyoandikwa; Katiba inayonyumbulika au isiyonyumbulika au ngumu.

Katiba iliyoandikwa sheria zake zimekusanywa katika hati au kitabu kimoja. Mfano Tanzania tunayo Katiba iliyoandikwa. Katiba isiyoandikwa ni kinyume cha iliyoandikwa.

Sheria zake hazikuwekwa katika kitabu au hati moja mfano Uingereza haina katiba iliyoandikwa. Mambo mengi yanafahamika kwa mapokeo. Inapobidi pokeo fulani libadilishwe, hapo Bunge hupaswa kulitungia sheria.

Kwa mfano wote wanajua kuwa mtu asiye Mwanglikana hawezi kuwa Malkia au Mfalme wa Uingereza. Haikuandikwa popote. Ikibidi hilo libadilike lazima sheria itungwe.

Katiba inayonyumbulika ni ile ambayo sheria zake au kanuni zinazoongoza nchi zinaweza kudadilishwa kwa urahisi hitaji linapojitokeza. Idadi kadhaa ya wabunge iliyoainishwa inatosha kufanya badiliko katika katiba.

Katiba isiyonyumbulika au ngumu ni ile ambayo sheria zake zinazoongoza nchi haziwezi kubadilishwa au kurekebishwa kirahisi.

Ili yafanyike mabadiliko ya msingi katika Katiba lazima mfano theluthi mbili au ziadi za wabunge waidhinishe kwa kura, lakini pia raia wapige kura ya maoni juu yake.

Ni tumaini yangu mimi kuona Katiba ya Tanzania inabaki kuwa iliyoandikwa na isiyonyumbulika, ili kuzuia urekebishaji kirahisi wa mambo ya msingi kwa masilahi ya watu fulani au vyama vya siasa, bila ridhaa ya wananchi waliotaka jambo likae walivyoliidhinisha kwa kura ya maoni.

Mara nyingi wanasiasa husingizia kuwakilisha wananchi kufanya mabadiliko kwenye Katiba lakini kumbe ni matakwa yao tu binafsi. Bila shaka zipo faida na hasara za aina zote mbili za Katiba ni juu ya raia kupima kinachofaa zaidi.

Kwa uelewa wangu mdogo Katiba ndiyo sheria kuu ya nchi. Hakuna sheria nyingine iipitayo Katiba. Sheria nyingine zote zinapaswa zitokane au ziendane na Katiba.

Katiba ndiyo inabeba malengo makuu ya taifa; ndiyo inaainisha wazi taratibu zitakiwazo kufuatwa ili mtu atambulike kuwa ni raia wa nchi; ndiyo inatamka na kulinda haki na wajibu za raia wa nchi; ndiyo inatamka au kuainisha aina ya mfumo wa siasa unaofuatwa na nchi; inaweka taratibu za namna ya kuwapata viongozi wa nchi na kuainisha madaraka yao na mipaka ya madaraka yao.

Katiba ndiyo chimbuko la utawala wa sheria. Katiba ndiyo huiwajibisha Serikali, ikiweka wazi kuwa Serikali inawajibika kwa watu. Katiba inabainisha haki za raia na kuelekeza zikivunjwa anawezaje raia kuzidai au kutaka zilindwe na zisichezewe.

Kwa maoni yangu mimi Katiba ni moja ya vipaumbele kwa taifa lolote kutokana na umuhimu wake, taifa linalotaka kuongozwa inavyoeleweka kwa mwananchi.

Najua hata uhuru wangu wa kuabudu usipolindwa na Katiba ya nchi, hali yangu kiroho itakuwa mbaya.

Uhuru huo usipolindwa napaswa kuishi kama mtu asiyemjua Mungu wala kumtii huyo anayenifunza kutii mamlaka zilizopo (Rum 13:1-7; 1 Pet 2:13-17).

Kwa mwendo huo nchi haitatawalika au kukalika kwa amani na utulivu kama Watanzania tunavyotamani na kuimba kila siku, tutapaswa kuishi kwa lijamu na hatamu. Nawaomba tuendelee kusali ili Mungu atupe hekima na busara, amani ya kweli na nia njema ya kuijenga nchi na kuleta mabadiliko ya kweli chanya.

Chanzo: Mtanzania
 
Afadhar Baba Askofu komaa na katiba mpya, hakika katiba ya jaji Warioba ingekamilika hawa WABUNGE malofa na wapumbav hawa wasinge chezea Kodi za walala hoi kama saiz wanavyochezea pesa holela na upande wa pili wakiona ufahar kuchezea Kodi zetu wao wakila viyoyoz tu! Nyambafu
 
Asante baba askofu.
Naomba uwatie Moyo maaskofu wenzako na mapadri, wajue kwamba, wasipoyasemea haya, wanakuwa wanasaliti kiapo chao cha kuwatumikia wanyonge waluo wengi.
 
nikikumbuka kibao alichokatwa waziri mkuu mstaafu, halafu namwona mtu fulani akilamba madaraka kwa kupongezwa fulani hivi, huwa nakuwa mpole na mambo ya katiba mpya sitaki kuyajadili kabisa. we acha watawale tu kwani mi ni nani?
 
Ya Kaisari mwachie Kaisari na ya Mungu mwache Mungu. Haipendezi baba askofu au sheikh akawa anashughulika na mambo ya kaisari. Tutaipeleka pabaya nchi yetu. Katiba mpya au iliyopo hazihusiki na ibada yo yote ile.
 
Mwanahabari huru wa CHADEMA
Awe chadema, cuf, ccm au independent kama analeta ujumbe ambao hata wasio na vyama wanaupenda asonge mbele. Nchi ni zaidi ya vyama na matabaka. Vyama vitakufa, matabaka yatasambaratika , dini zitaisha mvuto na kusepa lakini nchi itabaki na watu wake watakuwepo ni watanzania ingawa hatujui kabla ya ili jina nchi hii iliitwaje. Nyika, bara, au?
 
View attachment 650932
Bado nitaendelea kuizungumzia Katiba na Mambo mengine yenye maslai kwa nchi yangu kwa sababu inagusa maisha yangu na Kanisa ninalotumikia, lakini pia inayagusa maisha ya raia wenzangu wote


Basi mimi nitakunyamazisha kwa kukuzaba kibao na kelbu moja ya nguvu na usipoenda chini nakumaliza na mtama, halafu ukamuonyeshe babako!
 
View attachment 650932
Bado nitaendelea kuizungumzia Katiba na Mambo mengine yenye maslai kwa nchi yangu kwa sababu inagusa maisha yangu na Kanisa ninalotumikia, lakini pia inayagusa maisha ya raia wenzangu wote
Hawa ndio viongozi wanaohijika katika Tanzania ya sasa..

Nampa pongezi zote baba Askofu kwa kuweza kubaki na msimamo wako uleule hata kama wanatia shaka uraia wako.
 
Katiba ni muhimu sana ili mihimili iwe Huru, Sio Mtu kununua Bombadier bila Bunge kupitisha

Maoni ya Wamarekani wengi, wanasema watamchagua tena Rais Donald Trup

Wamarekani wanasema pamoja na vituko vyake, Trump ameboresha uchumi na ajira zimeongezeka

When you have something in the pocket, no matter what

African people, watch out,...Mnamchagua tena Rais kwa mafanikio yapi?
 
Ya Kaisari mwachie Kaisari na ya Mungu mwache Mungu. Haipendezi baba askofu au sheikh akawa anashughulika na mambo ya kaisari. Tutaipeleka pabaya nchi yetu. Katiba mpya au iliyopo hazihusiki na ibada yo yote ile.
Ww jamaa bado hujabalehe kiakili,katba ndyo sheria mama,ndyo muongozo Mkuu wa nchi na watu wake pamoja na rasilimali zote..., we need a constitution amendment ili kuweka mambo sawa
Ninauhakika kama pangekuwepo na kipengele chenye kuwabana wabunge mataka taka wasingejiuzulu!
 
26 Reactions
Reply
Back
Top Bottom