Askofu aishangaa serikali kukumbatia mafisadi

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,790
288,007
Askofu aishangaa serikali kukumbatia mafisadi

na Mkolo Kimenya
Tanzania Daima~Sauti ya Watu

SERIKALI imetakiwa kuwachukulia hatua mafisadi waliochota zaidi ya sh bilioni 133 katika akaunti ya malipo ya madeni ya nje (EPA) katika Benki Kuu ya Tanzania (BoT) badala ya kuwalinda na kuwaacha wananchi wakiendelea kuteseka.
Hayo yalielezwa jana na Askofu Lusekelo Mwakafwila wa Kanisa la Morovian, Jimbo la Kusini Ushirika wa Tabata katika ibada ya Sikukuu ya Pasaka ambayo kitaifa ilifanyika kanisani hapo.

Akitolea mfano wa viongozi wanaoonekana kuendelea kulindwa ni wale waliofuja fedha za BoT na kusema kuwa wananchi bado wanahoji licha ya kurudisha mamilioni hayo bado haitoshi, kwani wanastahili pia kuchukuliwa hatua za kisheria.

Alisema anashangazwa na hatua ya mtu aliyeiba mamilioni ya wananchi walalahoi kurudisha fedha hizo huku viongozi wanaosimamia urudishaji huo kukataa kutaja majina ya mafisadi hao.

“Inashangaza na kutia uchungu kuona nchi inayumba kwa ajili ya baadhi ya watu kutaka kujinufaisha, hivi kuna haja gani kama mtu alishatuhumiwa kwamba kafuja mali ya nchi halafu wakati huohuo anachukua hatua ya kurudisha mali ile kimyakimya pasipo kutajwa majina, ili wananchi wapate kuwajua mafisadi hao…. sasa pesa inayorudishwa ilikopwa au? Vitu kama hivi ndivyo tunaita kulindana,” alisema.

Askofu huyo alisema hivi sasa suala la ufisadi haliisumbui serikali pekee, bali limeingia hadi katika nyumba za ibada na kutolea mfano wa kuibuka kwa wimbi la wachungaji matapeli ambao wamekuwa wakitumia madaraka yao vibaya na kuwarubuni waumini kwa lengo la kujinufaisha.

Alisema watu kama hao kamwe hawatamuona Mungu, kwani wamekuwa wakidhulumu mali za wananchi wanyonge wasiokuwa na hatia kwa ajili ya manufaa binafsi na familia zao.

Alisema ni vema viongozi wa Tanzania kutofuata tabia ya Pilato ambaye alishindwa kusema ukweli na akaacha Yesu akasulubiwa kwa lengo la kulinda madaraka kwa manufaa yake na viongozi wenzake huku akifahamu kuwa anachofanya ni dhambi kubwa.

“Na kama walikopa basi wanatakiwa kuzirejesha na riba kama wafanyavyo wakopaji wengine katika taasisi za fedha, ili waweze kuishi kwa amani kama alivyofanya Zakayo kwa Mungu wake baada ya kuona katenda dhambi.

“Hata Mungu katika maandiko yake matakatifu amekataza dhuluma sasa inapokuja dhana hii ya kutaka kujinufaisha kupitia migongo ya watu wengine inakuwa inakinzana…. hivi sasa inaonekana watu hawajali kabisa malipo ya mbinguni na kuangalia maisha ya duniani pekee,” alisema.

Alisema watu hao wanatakiwa kumrudia Mungu kwa kufanya ibada, ili kujinusuru na dhambi walizofanya za kuwaibia mamilioni ya fedha, kwani kwa kutofanya hivyo hawawezi kuishi maisha ya amani, furaha na upendo.

Askofu huyo ambaye alichukua muda mwingi kusisitizia hali ya amani, alisema bila kuwepo upendo baina ya viongozi iwe wa dini, serikalini hata katika familia ni dhahiri amani haiwezi kutawala ndani ya mioyo yao, hivyo kusababisha mtafaruku ambao mwisho wake ni kusambaratika kwa umoja uliopo.

“Ili nchi au kundi fulani liweze kusonga mbele ni lazima kuwepo amani bila hivyo hakuna kitakachoendelea,” alisema na kuongeza kuwa tumeshuhudia nchi jirani ya Kenya ilivyopoteza amani kwa kitu kidogo ambacho kingezungumzwa mapema kisingevunja umoja uliokuwepo na kusababisha vifo vya mamia ya watu wasio na hatia.

Askofu Mwakafwile aliwasifu na kuwashukuru aliyekuwa Katibu Mkuu wa AU, Koffi Anani, na Rais Jakaya Kikwete, kwa jitihada walizofanya kuhakikisha amani inarudi nchini Kenya.

“Ni jambo la kutia moyo na kufurahisha kuona wenzetu wamerudi katika hali ya amani na utulivu ambayo ilitoweka kwa tamaa ya madaraka ya watu wachache huku wahanga wakibaki kuwa wananchi wa hali ya chini,” alisema.

Hivi sasa kumekuwa na jitihada za kila aina kwa viongozi wa dini pindi wapatapo fursa ya kuzungumza na waumini wake kuhakikisha wanalipigia kelele suala la ufisadi ili kuhakikisha linakwisha kama si kutokomezwa kabisa, jitihada ambazo zinaelekea kuzaa matunda.

Fedha zilizoibwa BoT zilizokadiriwa kufikia sh bilioni 133, zilisababisha Rais Jakaya Kikwete kumfukuza kazi aliyekuwa gavana wa benki hiyo, Daudi Ballali, kwa manufaa ya umma huku wengine waliohusishwa na kashfa hiyo wakiendelea kuzirudisha.
 
It is apparent that our aid dependent budget will suffer greatly as a consequence of ufisadi and lack of transparency.Donor nations and aid agencies are following closely this saga through their embassies and intelligence disguised as expatriates.Watch the percentage of aid to Tanzania drop down dramatically in this budget.
 
Back
Top Bottom