Asilimia 99 Vivimbe Vya Kinywa Sasa Vinatibiwa Muhimbili

diana chumbikino

JF-Expert Member
May 29, 2018
428
368
Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) imesema kwamba asilimia 99 ya wagonjwa wenye vivimbe vya kinywa (dental ehemngiomas) hivi sasa wanapatiwa huduma ya kibingwa ya tiba radiolojia (interventional radiology) badala ya kupelekwa nje ya nchi kwa ajili ya matibabu zaidi. A


Awali, wagonjwa wenye matatizo ya vivimbe vya kinywa walikuwa wanapewa rufaa ya kwenda kutibiwa nchini India, lakini hivi sasa wanatibiwa Muhimbili baada ya huduma hiyo kuanza kutolewa katika hospitali hiyo.Akizungumza na waandishi wa habari leo, Mkuu wa Idara ya Radiolojia, Dkt. Flora Lwakatare wa hospitali hiyo amesema wagonjwa ambao tayari wamepatiwa huduma hiyo wamekuwa wakipata matokeo mazuri katika tiba zao.

Dkt. Lwakatare amesema kuwa tiba hiyo inafanywa na wataalam wa Muhimbili akiwamo Daktari Bingwa wa Radiolojia, Dkt. Gerald Mpemba na Fundi Sanifu wa Radiolojia, Fabian Maha kwa kushirikiana na wenzao kutoka vyuo vikuu vya Yale, Indiana na Emory nchini Marekani wakiongozwa na Dkt. Frank Minja na Dkt. Troy Koch ambaye anatoka Chuo Kikuu cha Utah, Marekani.

“Tiba hii ni mwendelezo wa mafunzo yalioanza Novemba, mwaka jana. Huduma ambazo zimetolewa na zinazoendelea kutolewa ni utoaji wa sampuli kutoka kwenye vivimbe kutoka sehemu mbalimbali za mwili ambazo si rahisi kufikiwa bila kufanyika upasuaji mkubwa na kuzibua mirija ya nyongo (percutaneous biliary drainage),” amesema Dkt. Lwakatare.

Amesema huduma nyingine ni kuvyonya vivimbe vyenye maji au usaha (percutaneous drainage) na kuweka mirija kwenye figo ambazo mirija ya mkojo imeziba (nephrostomy tube placement).

Amesema tiba hiyo ina faida kubwa kwa kuwa inamuepusha mgonjwa kufanyiwa upasuaji mkubwa ambao ni hatarishi na kwamba mgonjwa anayepatiwa tiba radiolojia anaruhusiwa kurejea nyumbani siku hiyo hiyo na hivyo kupunguza gharama endapo angelazwa kwa ajili ya kuendelea na matibabu.

“Tumeweza kuokoa fedha za kuwatibia wagonjwa waliokuwa wanapata huduma hizi nje ya nchi hasa wale wenye vivimbe vya kinywa. Kwa sasa wagonjwa hawa tunawatibu kwa Tshs. 2 milioni kila mmoja katika hatua nne ili kukamilisha tiba yake na mgonjwa huyo endapo angepelekwa kutibiwa nje ya nchi matibabu yake yangegharimu Tsh. 96 milioni kwa mgomjwa mmoja katika hatua zote nne,” amesema Dkt. Lwakatare.

Pia, Dkt. Lwakatare aliwashukuru wataalam kutoka Marekani kwa kujitolea kuendesha mafunzo hayo pamoja na kuleta vifaa kwa ajili ya kutoa huduma hiyo.“Tunapenda kutoa shukrani zetu kwa serikali kwa uwekezaji mkubwa wa kununua vifaa tiba katika hospitali yetu jambo ambalo limewezesha kuimarisha huduma za kibingwa ikiwamo tiba radiolojia.

Katika hatua nyingine, Dkt. Troy Koch ambaye anatokea Chuo Kikuu cha Utah nchini Marekani amewashukuru wataalam wa Muhimbili kwa ushirikiano waliouonyesha tangu walipofika kwa ajili ya kutoa huduma ya kibingwa ya tiba radiolojia.Tiba radiolojia ni tiba maalum ambayo inahusisha vifaa vya radiolojia kama vile X-ray, fluoroscopy, CT-scan na ultrasound kutibu moja kwa moja au kuchukua sampuli kwa ajili ya uchunguzi.Huduma hiyo ikijumuisha mafunzo ilianza ilianza Februari 4, mwaka huu katika Hospitali ya Taifa Muhimbili-Mloganzila ambako kinamama wenye vivimbe kwenye matiti walitibiwa na kwamba mafunzo hayo pamoja na tiba yataendelea hadi Machi 9, mwaka huu.

Tangu kuanzishwa kwa huduma hiyo Novemba, mwaka 2017, wagonjwa 220 wamepatiwa huduma ya kibingwa ya tiba radiolojia wengi wao wakiwa wagonjwa wenye vivimbe vya kinywa. Katika kambi hii, wagonjwa 50 wanatarajiwa kupatiwa huduma hiyo.
 
Habari njema ila mara wanakupasua Goti wakati ulienda na Kivimbe chako.
 
Ni kweli vinatibika ila kalenda zao za nenda rudi ni kiboko na kila ukirudi unalipa haupati huduma zaidi ya kipigwa kalenda uje ulipe tena, natena, natena, yalinikuta mpaka nikajuta kuwafahamu. Kuwa madakitari wa kichaga hao moto wa kuotea mbali.
 
Back
Top Bottom