assadsyria3
JF-Expert Member
- Apr 9, 2013
- 6,904
- 4,050
Barazani kwa Ahmed Rajab | Ahmed Rajab | Toleo la 327 27 Nov 2013
Ni rahisi kubomoa Ikulu kuliko kuimarisha kwako
KAMA wiki tatu hivi zilizopita rafiki yangu mmoja ambaye ni mwanasiasa wa Kenya ingawa yeye mwenyewe huenda akakataa kuitwa mwanasiasa, aliniuliza swali lililonishangaza. Aliniuliza: Hivi huko kwenu hakuna chama chochote kingine cha siasa isipokuwa CCM?
Swali hilo, kama nilivyosema, lilinishangaza kwa sababu nilikuwa na hakika kwamba muulizaji alijuwa jawabu la swali lake. Yeye si mtu asiyeijuwa Tanzania na siasa zake. Hivyo, nikaamua kumjibu kwa kumuuliza yeye swali: Kwa nini waniuliza hivyo?
Kwa sababu, alinijibu, umeishika CCM. Umeiandama.
Nikamwambia kwamba CCM ni chama kinachostahili kuandamwa kwa sababu ya vituko vyake. Baadaye nikamsomea baadhi ya madhambi ya chama chicho.
Si kwamba nataka kumfurahisha lakini leo naona itanilazimu walau kidogo kukitupia macho Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na viongozi wake wa juu. Si dhamira yangu leo kukitupia macho CHADEMA kwa kuzichambua shutuma za udugu na udini zinazokikabili chama hicho.
Nikiangalia kwa juu juu naona kwamba shutuma za udini hazina mashiko makubwa lakini zile za udugu zina nguvu na zimekuwa kama laana iliyokipiga chama hicho. Kinachojitokeza hapa katika CHADEMA ni ukosefu wa demokrasia halisi ndani ya chama. Udugu usingeweza kushamiri lau pangelikuwako na taratibu madhubuti za kidemokrasia.
Ninalazimika kukitupia macho chama hicho kwa sababu vituko vya hivi majuzi vya chama hicho vinanilazimisha kufanya hivyo.
Kwanza alijiuzulu nafasi yake ya Makamu Mwenyekiti wa CHADEMA, Said Arfi, ambaye ni mbunge anayeliwakilisha Jimbo la Mpanda Mjini. Arfi alisema kuwa aliamua kujiuzulu nafasi hiyo kwa sababu alichoka kuchaguliwa viongozi na waasisi wa chama hicho.
Siku chache baadaye, Tundu Lissu, ambaye ni mwanasheria wa CHADEMA alitangaza kwamba chama kimewavua nyadhifa zao zote za kichama Zitto Kabwe, aliyekuwa naibu katibu mkuu wa CHADEMA, Dakta Kitila Mkumbo, aliyekuwa mjumbe wa kamati kuu ya CHADEMA na Samson Mwigamba, aliyekuwa mwenyekiti wa chama hicho kwa Mkoa wa Arusha.
Hatua zote hizo zinaashiria kwamba kumechafuka ndani ya CHADEMA na hali ya mambo huko si shwari asilan. Ni wazi kwamba chama hicho kinakabiliwa na matatizo makubwa, ambayo ikiwa busara haitotumiwa kuyatanzua, yanaweza yakakisababisha chama hicho kikadhoofika au hata kikapasuka, ingawa sidhani kwamba hili la pili linaweza likatokea katika kipindi cha hivi karibuni.
CHADEMA ni chama kizito katika siasa za Tanzania. Ni chama ambacho wafuasi wake wengi na hata wasio wafuasi wake wanaamini kwamba endapo kitajiandaa vyema kinaweza kikajinyakulia ushindi katika Uchaguzi Mkuu uliopangwa ufanywe Oktoba 2015.
Fursa yake ya kuupata ushindi huo itazidi kuwa nzuri endapo chama hicho kitashirikiana rasmi na vyama vingine vya upinzani nchini humo. Hilo ndilo tumaini la wenye kutamani kukiona Chama cha Mapinduzi (CCM) kinangolewa madarakani 2015.
Kinachowasikitisha wapenzi wa CHADEMA ni kusikia shutuma za udugu na udini au kama zile zilizotolewa na Kabwe dhidi ya wakuu wa chama. Yeye hakuutaja udugu wala udini lakini aliyoyaelezea yanaonyesha kwamba wakuu wenzake wa CHADEMA hawaelewi nini hasa maana ya demokrasia na kama wanaielewa basi wanaikiuka misingi yake kwa makusudi.
Ikiwa shutuma zote hizo ni za kweli basi wakuu na wafuasi wa CHADEMA wana kazi kubwa. Na kazi yenyewe ni ya kuimarisha demokrasia ndani ya chama chao.
Uimairishwaji huo hauwezi kutokea kwa mkupuo mmoja. Unahitaji mchakato, mchakato wa kuimarisha demokrasia. Mchakato wa namna hiyo hauwezi kuwa mchakato ulio mwepesi au ulio nadhifu. Ni mchakato ulio mgumu na kama si mchafu basi una mazongezonge mengi.
Wala tusitarajie kuzuka miujiza katika mchakato wa aina hiyo wa kuiona demokrasia imeshamiri ghafla bin vu. Mchakato wa kuimarisha demokrasia ndani ya vyama, hasa vya upinzani, unahitaji uvumilivu wa hali ya juu hasa katika nchi kama za kwetu ambako mfumo wa demokrasia ya vyama vingi ni mchanga.
Aghalabu katika nchi kama zetu taasisi za kidemokrasia huwa dhaifu na zisizoweza kutekeleza mambo kama ipasavyo. Nadhani hiyo ndiyo moja ya sababu zinazozifanya serikali zetu ziwe na shida za kupata mafanikio ya kiuchumi au hata ya kijamii.
Lakini sio taasisi za kidemokrasia pekee zilizo na udhaifu huo katika nchi kama za kwetu. Hata vyama vya siasa navyo vimeambukizwa ugonjwa huo.
Ni rahisi kwa vyama vya upinzani, kwa mfano, kuyalenga makombora yao ya lawama kwa vyama vinavyotawala kuliko kujichunguza vyenyewe na kuangalia iwapo vina sifa za uwajibikaji au za kujenga demokrasia.
Vyama vya upinzani katika nchi zenye demokrasia changa mara kwa mara vimethibitisha kwamba ni rahisi kubomoa kwa mwenzako, hasa ikiwa kwake ni Ikulu, kushinda kujenga kwako.
Jambo ambalo mara nyingi tunalisahau ni kwamba demokrasia haihusiki tu na haki za kisiasa na za kiraia bali pia inahusika na taratibu au njia za kuzifikia haki hizo. Wa mwanzo wanaopaswa kulikumbuka hili ni viongozi wa vyama vya siasa, na hasa vile vya upinzani.
Iwapo kweli wanataka kujenga demokrasia wataposhika hatamu za utawala basi lazima tangu sasa wakiwa wapinzani waanze kujizoesha kutumia taratibu za kidemokrasia ili kufikia uamuzi wa ndani ya chama.
Na uamuzi huo ukishakatwa watumie njia au taratibu nyingine za kidemokrasia za kutekeleza uamuzi husika. Huko ndiko kujenga utamaduni wa kidemokrasia.
Demokrasia kwa hakika inaweza kuwa njia ambayo kwayo watawala (na hata viongozi wa vyama) huchaguliwa na uamuzi hukatwa katika mazingira ya ushindani wa kutaka kura za wananchi. Kuna mambo fulani, bila ya shaka, ambayo lazima yawepo kuhakikisha kwamba uchaguzi ni wa haki na umefanywa kwa uwazi.
Muhimu miongoni mwa hayo ni Tume ya Uchaguzi iliyo huru na isiyopendelea upande wowote. Kazi yake iwe ni kuhakikisha kwamba ushindani au mchuano wa kisiasa katika uchaguzi unafanyika kwa haki na bila ya wapigaji kura kusumbuliwa na yeyote yule.
Pamoja na ushindani wa kisiasa kuna suala la uwajibikaji. Huu ni msingi mwingine muhimu wa demokrasia. Mpaka sasa tumekuwa tukizungumzia mchakato na sio matokeo. Tusitaraji kuwa mfumo wa kidemokrasia utaleta manufaa kwa sababu tu mfumo huo ni wa kidemokrasia.
Ili uwe kweli wa kidemokrasia mfumo wa kidemokrasia unahitaji uwe na taratibu za uwajibikaji na nyenzo za kuwachunguza wakubwa. Hayo ni lazima yawepo ili kuwazuia hao wakubwa wasiyatumie vibaya madaraka yao.
Chama kilichozoea kuendesha shughuli zake kimabavu au kwa njia zisizo za uwazi au zisizo za kidemokrasia hakiwezi kuaminika kwamba kipatapo madaraka kitaweza kuendesha nchi kidemokrasia hata kama kinaweza kikaleta maendeleo.
- See more at: Raia Mwema - Laana iliyoipiga CHADEMA