AG: Ufafanuzi juu ya uteuzi wa wabunge na kupewa uwaziri

Invisible

Robot
Feb 11, 2006
9,075
7,878
Mheshimiwa Rais Jakaya Mrisho Kikwete, tarehe 4 Mei, 2012 alitangaza mabadiliko katika safu ya Baraza la Mawaziri. Katika uteuzi wa Mawaziri na Manaibu Waziri, Mheshimiwa Rais aliwateua Mawaziri wapya kutoka miongoni mwa Wabunge aliokuwa amewateua na kuwatangaza. Baada ya uteuzi huo, kumetolewa maoni kwamba hatua ya Mheshimiwa Rais kuwateua Wabunge Wapya ambao hawajaapishwa Bungeni kuwa Mawaziri ni kitendo cha uvunjaji wa Katiba.

Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali inayachukulia maoni haya kama ni jambo lenye maslahi ya jamii na linalohitaji kufafanuliwa; kwa upande mmoja lakini pia, kutolewa kwa elimu ya Umma; kuhusu Mamlaka ya Rais ya uteuzi wa Wabunge.

Msingi wa Katiba tunaoanza nao ni maelekezo ya masharti yaliyomo kwenye Ibara ya 55(4) kwamba:

"Mawaziri na Naibu Mawaziri wote watateuliwa kutoka miongoni mwa Wabunge"

Pili, ni mamlaka ya Rais ya uteuzi wa Wabunge aliyopewa na masharti ya Ibara ya 66(1)(e) yenye aina ya Wabunge wasiozidi kumi watakaoteuliwa na Rais kutoka miongoni mwa watu wenye sifa zilizotajwa katika aya za (a) na (c) za ibara ya 67 na angalau Wabunge watano kati yao wakiwa Wanawake. Wabunge aliowateuwa Mheshimiwa Rais wanatokana na Ibara hii.

Tatu, baada ya hatua zote hizi ikumbukwe kwamba aliyeteuliwa au kuchaguliwa kuwa Mbunge anakuwa Mbunge ama baada ya kutangazwa na Msimamizi wa Uchaguzi; au baada ya kuteuliwa na Tume ya Uchaguzi kwa wale Wabunge wa viti maalum au anapochaguliwa na Baraza la Wawakilishi au anapoteuliwa na Rais akitumia Mamlaka yake ya uteuzi yanayotokana na Ibara ya 66(1)(e). Hivyo Wabunge wanaohusika hawahitaji kuapishwa kwanza Bungeni ili wawe Wabunge. Kiapo cha Mbunge Bungeni kinamwezesha tu kushiriki katika shughuli za Bunge.

Katiba ya nchi haiweki kwa Rais masharti kwamba kabla ya kumteua Mbunge wa aina hiyo kuwa Waziri au Naibu Waziri Mbunge huyo awe ameapishwa Bungeni kwanza. Masharti mawili muhimu na ya kuzingatia ni kwamba mteule wa nafasi ya uwaziri au Naibu Waziri hatashika madaraka yake ila mpaka kwa mujibu wa Ibara ya 56 ya Katiba, awe ameapa kwanza mbele ya Rais kiapo cha uaminifu na pia kiapo kingine chochote kinachohusika na utendaji wa kazi yake kitakachowekwa kwa mujibu wa Sheria iliyotungwa na Bunge. Sharti la pili, litahusu kiapo cha Uaminifu katika Bunge kabla Mbunge hajaanza kushiriki katika shughuli za Bunge kwa masharti ya Ibara ya 68 ya Katiba. Viapo hivyo havitegemeani na vinaweza kufanyika kwa nyakati tofauti.

Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali inasisitiza kwamba Wabunge ambao hawajaapishwa ndani ya Bunge ni Wabunge na wanapoteuliwa kushika nafasi ya Uwaziri au Naibu Waziri ni halali kwa kuwa uteuzi huo haukiuki masharti yoyote ya Kikatiba au Sheria. Aidha, katika kutekeleza madaraka ya kazi ya Uwaziri au Naibu Waziri Mbunge atahitaji kiapo mbele ya Rais hata kama hajaapishwa Bungeni. Busara ya uandishi wa Katiba na Sheria imetambua kwamba kunaweza kukatokea uteuzi wa aina hiyo wakati Bunge limeahirishwa kama ilivyo sasa. Masharti ya Ibara ya 68 ya Katiba yatazingatiwa katika kikao cha Bunge kijacho.

Bila shaka ufafanuzi huu utaleta uelewa katika jambo hili na kuepusha mikangayiko isiyokuwa ya lazima.



Imetolewa na Jaji Frederick M. Werema (Mb)
MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI
06 Mei, 2012
 
Asante AG,

Tumetambua nani anajua sheria na nani mbumbumbu wa sheria!

Lakini pia tumetambua hitajio la katiba mpya kuondoa mikanganyiko hii

By Tume ya katiba
 
Walewale! Hana jipya. Katumwa kusafisha njia maana kesho wanaapishwa kinyume cha katiba. Tuna viongozi wabovu sana. Mtu anatumwa kukiuka taaluma yake kwa sababu za kisiasa na yupo tayari! Hovyo kabisa!!!?
 
kama katiba imekiukwa ni vyema kukubali na hivyo kurekebisha makosa.
Mbona Obama alirudia kuapa kiapo cha urais,hivyo sioni haja ya AG kuja na utetezi ambao bado utaendeleza malumbano.

KWA HISANI YA MTU WA TANZANIA
 
  • Thanks
Reactions: FJM
shughuli za bunge ni zipi?

KWA HISANI YA MTU WA TANZANIA
Nilitaka kuuliza the same, hivi kuandaa bajeti si shughuli za bunge?, je bajeti haina miongozo ya kuiandaa, je hiyo miongozo inatungwa na kila wizara au inatoka bungeni. Mwenye ufahamu wa haya anijuze.
 
mimi nadhani ifike mahali ndani ya bunge tupige kura ya kutokuwa na imani na rais kwasababu hawa watu ambao rais amewateua akidhani wanaupeo wa kumsaidia ni sifuri kama AG yaani hata tusiyojua sheria kwa upuuzi wake aliyouandika hapa hauhitaji kuwa mwanasheria kujua rais alijichanganya, na hapawnatafuta pakutokea, hakiyamungu tutapambana na nyia mpaka mtajuta kuwa upande wa dhambi, pili wabunge muache unafiki eti kura za kutokuwa na imani na waziri mkuu wakati mnajua kuwa bosi wao ni rais ndiye aliyewateua sasa kwanini msimpigie kura za kutokuwa na imani na bosi wao mkuu mnampigia msimamizi wao? Acheni kufanya siasa laini ndiyo maana mnaanza kusalitiana mnajiita marafiki kumbe wanafiki.
 
Walewale! Hana jipya. Katumwa kusafisha njia maana kesho wanaapishwa kinyume cha katiba. Tuna viongozi wabovu sana. Mtu anatumwa kukiuka taaluma yake kwa sababu za kisiasa na yupo tayari! Hovyo kabisa!!!?
Sijui na huyu ni mkurya wa wapi? Wakurya huwa siyo watu wa kujipendekeza hivi na kukiuka maadili yao ya taaluma.
 
Tumekusikia Jaji, lakini mawaziri watakapoitwa kukutana na kamati za Bunge itakuwaje kwa sababu hizo kwa sisi wenye uelewa mdogo ni shughuli za bunge vile vile. Kwa kifupi, kamati za bunge ni bunge vinginevyo ni wazi kuna matatizo kwenye katiba au wanaotafsiri hiyo katiba.
 
Hakuna mtu aliyetegemea kusikia AG anasema kuwa katiba imekiukwa, after all ni AG huyu huyu aliyeruhusu miswada kama ule wa katiba mpya uende bungeni. Nchi hii na hasa CCM na serikali yake wamejenga utamaduni mbaya sana wa kutokubali makosa.

AG anaweza kusema kuna tofauti gani kati ya mbunge na mbunge-mteule? Hivi rais akishatangazwa na NEC anaweza kuanza kazi kabla ya kula kiapo? Hao mawaziri wataanda bajeti au kujibu kuandaa majibu ya maswali ya wabunge kama nani?

Kufanya kazi za bunge sio lazima ukawa kwenye jengo la Dodoma, sasa wataingia kwenye kamati za bunge kama nani? Kwa nini watu hawakubali kwamba watanzania wa leo wanaelewa mambo?

Sawa, AG katoa ufafanuzi kwa hili, sasa atueleze la Mbunge wa Kwahani Zanzibar kuwa waziri wa AFYA -Tanzania bara? Wizara ambayo si ya muungano.Au na hii ni ruksa chini ya urais wa 'kifamlme?
 
Ndg. AG, nadhani hayupo sahihi, kwanza wabunge hao wateule wangeweza kuapishwa ofisini kwa spika hata katika ofisi ndogo ya bunge jijini dsm. vile vile shughuli za bunge ni pamoja na kamati za bunge, je hawa mawaziri wapya ambao hawajaapishwa na bunge watashiriki vikao vya kamati ambavyo kwa kipindi hiki ni bajeti? Shughuli za bunge ni pamoja na kazi za kamati za bunge na kulipwa mishahara.
Je James Mbatia atalipwa mshahara wa mwezi huu na bunge na wakati bunge bado halijamtambua? Jaji Werema asiwapotoshe Watanzania, huu ni uvunjwaji mkubwa wa Katiba kwa watu walioapa kuilinda na kuitetea katiba.
 
Kitu ambacho Werema amasahau, kwa mujibu wa vifungu alivyotaja hapo, ni wazi kwamba Uwaziri ni kazi za kibunge pia, kwani mtu huyu ni lazima awe mbunge. Au AG ana maana kuwa wateule hawa hivi sasa hawawajibiki kwa bunge, je, hawaandiki chochote kwenda bungeni, je hawatoaandaa majibu ya maswali ya wabunge? je, hawatowasilishwa mwelekeo wa bajeti zao kwenye kamati za bunge? Hapo kweli huyu jamaa amechemka.
 
Rais alipoteua wabunge alisema, "uteuzi huo unaanza mara moja". Ufafanuzi wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali unasema kwamba, "wateule hao hawawezi kushiriki shughuli za kibunge mpaka baada ya kwenda kuapa Bungeni. Kwa hiyo kazi za kibunge haziwezi kuanza mara moja na hivyo hawastahili kulipwa posho na mshahara wa ubunge mpaka baada ya kuapishwa kwenye kikao kijacho.

Je, wabunge hao walioteuliwa watalipwa au hawatalipwa mshahara na posho stahiki za wabunge za kuanzia siku ya uteuzi mpaka siku watakayoapishwa na Spika?

Unawezakuta jamaa wameishaingizwa kwenye payroll na wameishaanza kuvuta stahiki zao zote kabla hata hawajaanza kutekeleza majukumu yao ya kibunge!

Hii Katiba yetu ni bomu sana, na jinsi wanavyotoa ufafanuzi ndivyo wanazidi kuzama kwenye tope zaidi. It is sad kwamba Mwanasheria Mkuu anasema kuwa "Busara ya Waandishi wa Katiba", kwangu mimi sioni busara yoyote zaidi ya utashi wa waandishi wa katiba kuweka mianya kibao ambayo inatuvuruga kila kukicha.

Mtu mwenye busara hawezi kuacha hayo mapengo ili Rais aongoze nchi kwa utashi wake utadhani kwamba anaongoza familia ya nyumba ndogo ambao wanaweza kuburuzwa vyovyote vile bila ku-question kitu kwa kuwa wanajua kuwa wanafanyiwa favor kwa makosa ya mama yao kukubali kuwa nyumba ndogo.
 
Kwanini ufafanuzi huu umechelewa kuwakilishwa kwa umma?Palikuwa na sababu gani kutoa maelezo haya Kama kweli raisi Jakaya hajavunja katiba aliyoapa kuilinda?Nnarudia tena kusema Serikali hii kishikaji itatupeleka pabaya,Kama mnakumbuka Mwanasheria mkuu pana wakati alita sheria ya mikutano au maandamano ibadilidhwe je ilikuwa ni kwa manufaa ya nani Kama sio hao waliompa kula
 
Angetoa mfano basikama imewahi kutojea rais akanwapisha mtu kuwa waziri kabla mtu huyo hajaapishwa kuwa mbunge ingeoneshaana hoja sasa hivi amejaribu kuhalalisha kilichoharimishwa. Na yeye kama wengine wanawekatafsiri yao juu ya "shughuli za bunge"na kuzifunga kwenye kile kinachofanyika ndan ya bungeni. Kuna haja ya kufungua kesi ya kikatiba hapa.
 
Mbona AG pia hajatolea ufafanuzi wa Dk. Mwinyi kupewa Wizara isiyo ya Muungano. Je, napo Rais hajavunja katiba? Mbona hakuna Mtanganyika aliyeshika wizara yoyote Zanzibar?
 
Angetoa mfano basikama imewahi kutojea rais akanwapisha mtu kuwa waziri kabla mtu huyo hajaapishwa kuwa mbunge ingeoneshaana hoja sasa hivi amejaribu kuhalalisha kilichoharimishwa. Na yeye kama wengine wanawekatafsiri yao juu ya "shughuli za bunge"na kuzifunga kwenye kile kinachofanyika ndan ya bungeni. Kuna haja ya kufungua kesi ya kikatiba hapa.

Mzee mwanakijiji kesi ya nini wakati haya ndio mapungufu ambayo mnatakiwa myaseme kwenye mchakato wa katiba mpya?
 
Back
Top Bottom