Afukuzwa kazi kwa kuhifadhi albino – Serikali mko wapi?

Magezi

JF-Expert Member
Oct 26, 2008
3,359
692

na Osoro Nyawangah, Mwanza


ALIYEKUWA mlezi (matron) katika shule maalumu ya msingi ya watoto wenye ulemavu wa mtindio wa ubongo wilayani Misungwi, Anita Issa, ameachishwa kazi kwa sababu mbalimbali, ikiwamo ya kuhifadhi watoto wenye ulemavu wa ngozi (albino).

Taarifa za uhakika zilizolifikia gazeti hili na kuthibitishwa na pande husika, uongozi wa shule hiyo ulifikia uamuzi wa kutoridhika na utendaji wa mlezi huyo na kuishauri serikali ya Wilaya ya Misungwi kumuachisha kazi kwa madai ya kumpenyeza mtoto albino kwenye shule hiyo bila kufuata taratibu zilizowekwa.

Mlezi huyo aliiambia Tanzania Daima kuwa kamati ya shule hiyo ilipendekeza aachishwe kazi kutokana na kuwahifadhi watoto albino shuleni hapo na nyumbani kwake, licha ya serikali kupiga marufuku kuendelea kupokewa kwa watoto hao katika kituo hicho.

“Sababu kubwa iliyosababisha nifukuzwe kazi ni kuwahifadhi watoto albino shuleni na nyumbani kwangu; baada ya kuzuiliwa kuendelea kupokea watoto, mama mmoja kutoka wilayani Geita alifika hapa na mtoto mdogo ambaye maisha yake yalikuwa hatarini kijijini kwao na uongozi ulimwelekeza apate kibali kwa mkuu wa Wilaya ya Misungwi ndipo apokewe,” alisema Anita.

Aliongeza kuwa mama huyo alipokwenda kwenye ofisi ya mkuu wa wilaya hakurudi, hivyo alimuingiza mtoto huyo kwenye mabweni akisubiri uamuzi wa serikali.
Aliema siku kadhaa baadaye uongozi wa shule uligundua kuwapo kwa mtoto huyo na tatizo dhidi yake likaanza na kujumuishwa na hatua ya yeye kukubali kuwahifadhi nyumbani kwake watoto wengine wawili; Semeni Mathias na Shida Mathias, ambao walifukuzwa na wanakijiji cha Butonga wilayani Sengerema baada ya dada yao kuuawa.

Alieleza kuwa watoto hao waliletwa shuleni hapo na waandishi wa habari waliopata kibali kutoka kwa Mkuu wa Wilaya ya Sengerema, lakini uongozi wa Wilaya ya Misungwi ukawakatalia kupokewa shuleni hapo, hivyo akakubali kuwahifadhi kwa muda wakati waandishi hao wakifanya juhudi za kuwatafutia hifadhi mahali pengine.

Akizungumzia hatua hiyo, Mkuu wa Shule hiyo, Juma Abdalla, alithibitisha kufukuzwa kazi kwa mlezi huyo na kudai kuwa uamuzi huo umechukuliwa na kamati ya shule baada ya kuchoshwa na tabia mbaya ya mtumishi huyo licha ya kuonywa mara kadhaa.

Alisema kosa la kumpenyeza mtoto albino shuleni hapo bila ya kibali cha uongozi wa shule au wa wilaya ni sehemu ya sababu zilizosababisha mlezi huyo kuondolewa na kutaja sababu nyingine kuwa ni kutumia vibaya mali na vifaa vya shule, kutumia vifaa vya wanafunzi na kutokuwa na nidhamu kazini.

Source: Tanzania Daima

My take:

Kama haya yametendeka naomba wanaJF mlio Mwanza na Misungwi mjaribu kufuatilia hii kitu huenda baadhi ya watawala ktk serikali wanahusika na mauaji ya albino.
 
Furahia
weekend-15.gif
 
Back
Top Bottom