Zanzibar iachwe iende

ALEX PETER

Senior Member
Jan 17, 2012
117
23
Hoja yangu

Zanzibar iachwe iende










Lula wa Ndali Mwananzela

Toleo la 241
30 May 2012













KWA nini tunazungusha maneno? Tuseme ukweli tu kwamba endapo Muungano utavunjika wa kulaumiwa si Wazanzibari bali ni Chama cha Mapinduzi (CCM) ambacho kimeshindwa kuonyesha uwezo wa kuutetea Muungano kwa hoja maridhawa na mikakati ya makusudi na badala yake kuendeleza imani ya kuzima hoja za kupinga Muungano kwa mtutu wa bunduki, vitisho, na mabavu.
Ni wakati wa utengano sasa
Tanzania kama nchi ina mambo mengi sana ya kuhangaika nayo ili kuweza kuwainua watu wake kutoka katika laana ya umasikini wa kudumu. Tuna mambo mengi ya kufanya ili kuweza kuwaongoza watu wetu kuelekea uhuru wa kiuchumi na maendeleo yenye kutoa nafasi kwa kila mtu kufanikiwa.
Haiwezekani katika wakati kama huu tuanze kuhangaika na utetezi wa Muungano. Suala la Muungano lilitakiwa liwe limemalizwa miaka 20 iliyopita. Kutokana udhaifu na uongozi mbovu wa CCM leo hii tumefika kwenye ukingo wa kutengana (a precipice of separation).
CCM wameshatuonyesha kuwa hawawezi kuutetea Muungano; hakuna kiongozi yeyote wa CCM mwenye uwezo tena wa kusimama kuutetea Muungano. Si wazee wao na wala si vijana wao; si wasomi wao na wala si wanaharakati wao; si wa Bara na wala si wa Visiwani.
Hakuna mteteziwa Muungano. Si Salim, wala si Bilal; si Makamba na kwa hakika wala si Kikwete. Tusiwaangalie kina Mkapa wala Sumaye kuutetea Muungano. CCM imepoteza ujasiri wa kuutetea Muungano, sasa kwanini tusiseme ukweli?
Huu ni wakati wa kutengana ili kuwe na mataifa mawili yaliyo huru na yenye kuhusiana kama vile mataifa mbalimbali yanavyohusiana duniani kwa kutumia mikataba na nyezo mbalimbali za kimataifa.
Kushindwa kutatua kero za muda mrefu kumetufikisha hapa
Ni lazima tuseme ukweli na ukweli ujulikane. Yanayotokea sasa hayakupaswa kutokea kama viongozi wetu wangeonyesha uwezo wa kuyamaliza matatizo ya ‘kero’ za Muungano.
Ndugu zangu kushindwa kutatuliwa kwa haya kumegeuza kero hizi kuwa ‘matatizo sugu’ ya Muungano. Yaani, ni matatizo yaliyoshindikana. Kwa vile yameshindikana kutatuliwa kwa muda wa miaka hii 50 wakati umefika sasa wa kukubali kushindwa na kusalimu amri kuuachilia Muungano.
Matatizo haya sugu yameonyesha na kudhihirisha pasi ya shaka kikomo cha uwezo wa viongozi wetu. Si mzee Mwinyi wala Mkapa waliokuwa na uwezo wa kuonyesha utatuzi wa matatizo ya Muungano. Kikwete ambaye aliingia kwa ahadi motomoto amethibitisha kuwa na yeye (pamoja na utawala wake wote) hana uwezo wa kutatua matatizo haya sugu.
Ni nani aliyesahau maneno ya kutia moyo ya Rais Kikwete kwenye Bunge la Muungano baada ya kuapishwa kuwa Rais na akilizindua Bunge hilo Desemba 2005?
Ni yeye aliyesema maneno haya “Tunalo jukumu la kihistoria la kuhakikisha kuwa Muungano wetu unadumu na unazidi kuimarika. Nafurahi kusema kuwa Muungano wetu ni imara licha ya changamoto za hapa na pale. Na, kinachonipa faraja zaidi ni ule ukweli kwamba pande zetu zote mbili za Muungano zinayo dhamira ya dhati ya kutatua kero zilizopo kwa lengo la kuuimarisha.”
Miaka sita baada ya maneno haya Muungano wetu ni dhaifu na ‘changamoto za hapa na pale’ zimekuwa matatizo ya kudumu! Kikwete naye kashindwa!
Wanaeneza chuki dhidi ya Wakristu na Watanganyika
Ieleweke kwamba wanaopiga vita Muungano kimsingi kabisa wana tatizo na Wakristu na watu wenye asili ya Bara na hasa wale ambao wanatoka Bara yaani Watanganyika. Baadhi ya viongozi wa mihadhara hii wanatoa kauli ambazo mtu wa kawaida anazichukulia kama kibali na wito wa kuwatendea uovu watu wa Tanganyika.
Maana, kama Watanganyika ndio wanawadhulumu Wazanzibar na Watanganyika hawa wako Zanzibar je si haki kwa Wazanzibari kuwatendea vibaya wadhalimu wao? Maana, kama ni kweli Tanganyika inaikalia Zanzibar kama koloni lake si haki kwa wanaotawaliwa kimabavu na Watanganyika kuinuka dhidi ya Watanganyika?
Na cha kushangaza zaidi (na kuudhi) serikali yao nayo inakuwa kimya kwa vitendo hivi. Hivi makanisa yameanza wiki hii kuchomwa Zanzibar? Hivi baa zimeanza juzi kuchomwa huko Zanzibar au ni kwamba watu wana usahaulifu wa ghafla?
Taarifa iliyotolewa juzi ya kuwahakikishia “watalii” kuwa hali ni shwari haikutaja kabisa kuhusu watu wa Bara ambao siku ya Jumatatu wamekuta vipeperushi vikiwataka waondoke Zanzibar. Hii si mara ya kwanza kwa vipeperushi vya aina hiyo kutokea Zanzibar na inathibitisha kushindwa kwa mfumo wa inteligensia wa nchi yetu!
Lakini Wakristu wa Zanzibar wamekosea nini? Hivi ni kweli wanataka Wakristu wawe wale waliozaliwa Zanzibar tu na wengine wakija na kuhamia huko ni makosa? Kama alivyosema Sheikh Fared mwezi Machi, kama mtu hajakutangazia uadui wowote wala kukuinulia silaha dhidi yako iweje wewe umtangaze adui?
Muda wote makanisa yanapochomwa Zanzibar haijatokea mwendawazimu hata mmoja kufikiria kuchoma msikiti; hivi kweli akatokea mtu wa aina hiyo si ndiyo vita dhidi ya Wakristu itatangazwa?
Tena utaona haihitajiki hata Mkristu kufanya hivyo kwani muhuni mwingine akiamua kuwakorofisha Waislamu kwa kuchoma Msikiti (akijua watalaumiwa Wakristu au Watanganyika) si ndio hawa watoa mihadhara watatangaza vita ya kudumu?
Sasa, hili lazima lidaiwe kwa hawa viongozi – kama hawataki Wakristu Zanzibar kabisa watamke wazi ili Wakristu waondoke Zanzibar kwa amani! Kama wanaitaka Zanzibar ambayo haina dalili ya Ukristu kwa sababu Waislamu ni wengi waseme hivyo badala ya kuwachomea watu makanisa yao na kutishia maisha ya watu.
Ninasema hili nikiamini ya kwamba vitendo vya kuchomewa makanisa na kutishiwa Watanganyika vimevumuliwa mno na havijakemewa kwa uzito unaostahili. Hatujawasikia Wazanzibari maarufu kama kina Dk. Salim, Mzee Mwinyi, Dk. Bilal na wengine kutoa kauli za kuwalinda Wakristu na Watanganyika hawa. Wao wako kimya. Ina maana gani? Hatujawaona hata mmoja wao kutembelea nyumba hizi za Ibada za Wakristu zilizoteketezwa tangia Januari mwaka huu? Wanaogopa nini?
Tuuvunje Muungano vizuri
Kwa watu wanaosoma makala zangu watatambua kuwa msimamo wangu huu wa leo si mgeni. Aprili 27, 2011 niandika makala kwenye gazeti hili toleo la 183 yenye kichwa cha habari “Muungano wetu hauna watetezi tujiandae kuuvunja vizuri”.
Hata hivyo hiyo ilikuwa ni hitimisho la hoja niliyoijenga mwaka mmoja nyuma. Niliandika katika toleo la 147 Augosti 2010 katika makala yenye kichwa cha habari “Wanalivunja Taifa kwa kisingizo cha ‘kuimarisha Muungano’”.
Makala zote zilikuwa zinaonyesha tu kuwa Muungano wetu umefikia mahali tukubali tuuvunje ili tuhusiane kama nchi mbili. Wazanzibari ambao tokea mwanzo lengo lilikuwa ni nchi tumeshawakubalia mengi sana.
Tangu mwanzo wameachwa kuwa Zanzibar bila kulazimishwa kupotea kabisa lakini wanataka zaidi. Sasa Serikali ya CCM imewapa hivi vyote, bendera, wimbo wa taifa, rais wake, baraza lake la mawaziri, bunge lake, vikosi vyake mbalimbali sasa leo wanataka nchi yao tunawakatalia? Kwa vipi tunaweza kuwakatalia?
Hivi mtu kila siku anadai umpe meza, anadai apewe viti na makochi, anadai makabati na mapambano ya ndani, mara anakuja na kudai ukingo wa nyumba na vyote hivyo anapewa leo anaamua kudai nyumba tunashtuka? Hivi tulifikiria hizo meza na makabati alikuwa ayaweke chini ya mwembe?
Tayari CCM imeshakubali kuipa Zanzibar vyote vinavyohitajika kwa nchi, sasa wakati umefika kwa Zanzibar kuwa nchi; watoke kwenye Muungano.
Kwa vile kama nilivyosema mwaka mmoja uliopita, kuwa Muungano wetu hauna watetezi basi mimi nimejichagua kuwa mtetezi wa kuvunja Muungano. Tuuvunje ili tuwe salama.
Bado ninaamini katika umoja wa Afrika kama kanuni ya msingi iliyozaa Tanzania na bado ninaamini ni katika umoja tu vi-nchi vyetu hivi vitaweza kufanikiwa lakini umoja huu kama wa Wazanzibari hatuutaki. Wakati umefika kwa watu wa Bara nao kuanza kujitokeza na kufanya makongamano na maandamano ya kuukataa Muungano.
Si kwa sababu Zanzibar wanatuonea au wanaweza kufanya lolote dhidi ya Tanganyika – hawawezi – bali ni kwa sababu hatutaki kama watu wa Bara kutembea na hatia kuwa tunawaonea Wazanzibari!
Hatutaki kuishi na kujihisi kama wakoloni wakati hakuna lolote ambalo Wazanzibari wanalifanya au kutolifanya linalotudhuru sisi au hata kutuongezea lolote sisi.
Tanzania Bara haiitegemei Zanzibar kwa lolote bali Zanzibar inaitegemea na itaendelea kuitegemea Tanzania Bara! Sasa kama hili ni kweli – na ni kweli – basi Zanzibar iachwe iwe. Mwanafunzi yeyote wa historia anajua kabisa nini kitatokea tena Zanzibar.
Kwa vile CCM na Serikali zake wameshindwa kuutetea Muungano na kutatua matatizo ya Muungano, wakati umefika wa kuiachilia Zanzibar iende.
Tuwaache Wazanzibari waende na warudi kwenye nchi yao yaishe kwa amani. Tunawapenda sana Wazanzibari kiasi kwamba hatuwezi kuwang’ang’ania! Wanataka kwenda waachwe waende. Hadi kitakapokuja kizazi kitakachowahukumu wanasiasa na viongozi uchwara wa dini ambao wanapenda migongano kuliko umoja, chuki kuliko upendo, vurugu kuliko amani. Hawa wanaosimama kutaka kulivunja taifa kipo kizazi kitawahukumu vikali.
Kwa sisi wengine tunasema let Zanzibar go!





SOURCE RAIA MWEMA
 
Back
Top Bottom