Na. Exuper Kachenje
TATIZO la ajira kwa vijana nchini limepungua kutoka asilimia 16 mwaka 2001 hadi kufikia asilimia 13 mwaka 2006, imeelezwa.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana Edna Mangesho, alisema hayo hayo jijini Dar es Salaam jana na kuongeza kuwa wizara yake inaridhishwa na juhudi zinazochukuliwa na Serikali na wadau wote katika kukabiliana na tatizo hilo.
"Utafiti uliofanyika mwaka 2006 unaonyesha kupungua kwa tatizo la ajira nchini," alisema Mangesho ambaye hata hivyo hakueleza utafiti huo ulifanywa na nani .
Alibainisha kuwa kwa mujibu wa utafiti huo, mwaka 2001, ukubwa wa tatizo la ajira ulikuwa ni asilimia 12.9 wakati mwaka 2006 tatizo lilipungua na kufikia asilimia 11.7.
Mangesho alifafanua kuwa: "Mwaka 2001 kulikuwa na asilimia 16 ya vijana wasio na ajira, lakini mwaka 2006 utafiti unaonyesha kupungua kwa tatizo hilo kufikia asilimia 13," .
Aliongeza kuwa utafiti huo umebainisha kuwa wanawake wasio na ajira ni wengi kuliko wanaume ambapo asilimia 12.5 ya wanawake hawana ajira huku asilimia 10.5 ya wanaume wakikosa ajira.
Alisema serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali inaendelea na mkakati wa kupambana na tatizo hilo huku kipaumbele cha ajira kikiwa kwa vijana na wanawake.
Kwa mujibu wa naibu Katibu Mkuu huyo, mkazo unawekwa pia katika elimu na vyama vya wafanyakazi.
Alisema kuwa kwa sababu serikali imetangaza kujitoa katikabiashara nafasi hiyo imeachwa kwa sekta binafsi kutengeneza ajira zaidi kupitia huduma za fedha,utalii, madini na kilimo hasa kwa wanawake na vijana.
Kuhusu ajira mbaya kwa watoto Mangeshoo alikiri kuwepo kwa tatizo hilo na kueleza kuwa wizara hiyo ina mikakati kabambe kupiga vita ajira hizo hasa katika madini na mashamba ya chai.
Alisema kwa mijibu wa sheria ya ajira mtoto anaweza kuingia katika ajira akiwa na umri kuanzia miaka 14, lakini bila kumtoa katika masomo bali kwa lengo lakumuendeleza kimaisha na kumpatia ujuzi.
Mangesho alikuwa akizungumza katika kipindi cha Jambo Tanzania kinachorushwa na kituo cha cha Televisheni ya TBC.
Source: Mwananchi
Nilikuwa sijui kuwa Tanzania ni moja kati ya nchi chache zinazoongoza kwa ajira maana kuwa na Unemployment rate ya 13% miongoni mwa vijana ni hatua kubwa. Ila swali langu ni kwa nini uhalifu upo juu na vijana wengi wanashinda vijiweni?, je katibu mkuu wa wizara anaposema ajira anaingiza na wapiga debe na vibaka na dadapoa? au ni ajira gani hasa?