Wizara ya ardhi inawafanya wanyonge kuwa maskini zaidi

Andindile

JF-Expert Member
Mar 18, 2009
304
16
Wizara ya ardhi inawafanya wanyonge kuwa maskini zaidi

lC.gif
Mwandishi Wetu​
Aprili 1, 2009
rC.jpg

MWAKA 2009 umewadia, na hivi karibuni tutaanza kusikia tambo za wanasiasa mbali mbali wakijinadi kwa wananchi ili waweze kupigiwa kura katika chaguzi zijazo za Serikali za Mitaa na hatimaye Uchaguzi Mkuu mwakani.
Moja ya silaha za wanasiasa katika kipindi hiki ni sera za vyama vyao ambazo wamezibuni ili kuwaletea wananchi maendeleo; na ndizo ambazo watakuwa wakizinadi ili kupata ridhaa ya wananchi katika maeneo husika kuongoza ili watekeleze sera walizozinadi na hatimaye wananchi wapate maendeleo. Kama wananchi watapata maendeleo au la, hilo hubaki kitendawili.
Ni katika kipindi hiki ambacho utasikia wanasiasa wa kambi moja wakiwaambia wenzao wa kambi nyingine kuwa hawana sera. Ni kauli hizi ndio zimenifanya nijiulize kuna tofauti gani kati ya wanasiasa wasiokuwa na sera na wale wenye sera lakini wakisha kuchaguliwa na kushika hatamu za uongozi hawatekelezi sera walizozinadi kwa wananchi?
Sera ya Uwezeshaji wa Wananchi Kiuchumi ilitolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu mwaka 2004. Katika suala la Ardhi Sera hiyo inatamka bayana: “Serikali itatumia ardhi kama njia ya kuwawezesha wananchi wake kushiriki kikamilifu kiuchumi. Lengo ni kusaidia wananchi watumie ardhi waliyo nayo ama kwa kujipatia hisa katika shughuli za uwekezaji huo au pato lenye kuwanufaisha kushiriki kikamilifu katika shughuli nyingine za kiuchumi”.
Unasema mkakati wa utekelezaji wa tamko hilo ibara ya 4.9.3.(ii): “Kutoa ardhi kwa wawekezaji wakubwa kwa shughuli mbali mbali za kiuchumi. Pale ambapo itabidi Wananchi wahamishwe ili kuwapisha wawekezaji wakubwa. Serikali itawasidia utaalamu wa kuingia katika makubaliano muafaka na wawekezaji kwa nia ya kuwanufaisha”.
Sera hii ni kati ya mihimili iliyotumika kutunga Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2005, katika Ibara ya 48 ya Ilani ya CCM ya 2005 inatamkwa: “utekelezaji wa dhati wa Sera ya Uwezeshaji wa Wananchi Kiuchumi itatuepusha na balaa la kuwa na jamii ambayo ina matajiri wachache walionacho na wananchi wengi wasio nacho”.
Katika miaka ya hivi karibuni limekuwapo ongezeko kubwa la migogoro ya ardhi kati ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi na wananchi. Wananchi wakipinga viwango vidogo vya fidia wanayolipwa ili kupisha miradi mbali mbali ya maendeleo inayopendekezwa na Wizara ya Ardhi.
Kibaya zaidi Wizara ya Ardhi inatumia kutokuelewa kwa wananchi kuhusu thamani halisi ya ardhi na nyumba zao kukiuka kwa makusudi Sheria za Ardhi namba 4 na 5 za mwaka 1999 zinazotamka bayana kuwa “fidia itakuwa ni kwa bei ya soko”; na pia zinaelekeza utaratibu wa kufikia bei ya soko “kuwa itakuwa ni kwa kulinganisha na mauzo ya hivi karibuni ya ardhi au nyumba katika eneo husika”.
Madhumuni ya Wizara ya Ardhi kukiuka Sheria za Ardhi ni kujipatia faida kubwa ya zaidi ya asilimia 1000 kwa kuuza ardhi ilizozipoka kutoka mikononi mwa wananchi wanyonge, ilihali wananchi wanaohamishwa wakipata malipo ya fidia hafifu wakishindwa kujirejeshea viwango vya makazi na maisha waliyokuwa nayo awali kabla ya kuhamishwa kwao. Wengi wao hushindwa kujijengea nyumba bora kama walizokuwa nazo, kujirejeshea huduma za umeme, maji, barabara, ajira n.k na hivyo kurudisha nyuma jitihada za kufikia malengo ya milenia.
Tuchukue mfano wa mradi wa mji wa mfano wa Luguruni ulioanza kutekelezwa na Wizara ya Ardhi Januari mwaka 2007. Tokea mwaka 2005 viwanja katika eneo la Kata ya Kibamba vilikuwa vikiuzwa kwa bei ya sh. milioni sita kwa kiwanja cha meta 20 x 20. Kiwanja cha meta 20 x 20 kina meta mraba 20 x 20= 400.
Ukikokotoa utagundua kuwa ardhi katika Kata ya Kibamba inauzwa kwa bei ya Shs 15,000/= kwa meta mraba tokea mwaka 2005. Cha kushangaza Wizara ya Ardhi, pasipo utu wala ubinadamu, Desemba 2007, iliwalipa fidia wakazi 259 wa eneo la Luguruni waliotakiwa kuhama kupisha mradi huo sh. 300 tu kwa meta ya mraba, sawa na sh. 120,000/= kwa kiwanja cha Mita 20 x 20. Iliwabidi wananchi walioathriwa na mradi huo kuikaba koo Wizara ya Ardhi ndipo ikapandisha kiwango hicho kufikia sh. 1977 tu kwa meta moja ya mraba sawa na fidia ya sh. 790,800 kwa kiwanja cha meta 20 x 20.
Iliwalazimu wananchi waliohamishwa kutoka katika eneo hilo wanunue viwanja kwa bei ya sh. milioni 6 hadi 8, ikimaanisha kuwa walilazimika kuchota fidia za nyumba ili kupata viwanja kwa kuwa fidia ya ardhi haikuweza kuwawezesha kununua viwanja mbadala.
Mara tu baada ya kukamilisha kuwahamisha wananchi kutoka eneo hilo, Wizara ya Ardhi ilitangaza tenda kuuza mapori hayo (pasipo uendelezaji wowote). Nyaraka za tenda zinagharimu sh. 300,000, na bei ya meta moja ya mraba ni sh. 30,000.
Mnunuzi yoyote anayetuma ombi chini ya kiwango hicho hukataliwa kwa kutofikia bei iliyopangwa. Kutokana na bei hiyo, Wizara ya Ardhi inauza kiwanja cha 20 x 20 chenye meta mraba 400 kwa sh. milioni 12, ilihali yenyewe ilimfidia mwananchi sh. 790,800 tu; na hivyo kujipatia faida ya asilimia 1500 (1500%).
Hii ni hali inayothibitisha kuwa maadili ya kitaifa yameporomoka kwa kiwango cha kutisha sana kama taasisi ya Serikali inabuni mpango wa kujipatia faida kubwa sana kiasi hicho kwa kuwanyonya wananchi kwa kukiuka sheria zilizopo kwa makusudi.
Katika lengo hili hilo la kujipatia faida kubwa zaidi Wizara ya Ardhi imewavamia wananchi wa eneo la Kwembe walioko jirani na kituo cha mji wa Luguruni na kupima viwanja vidogo vidogo ndani ya ua wa makazi yao.
Makaro ya maji machafu, matanki ya maji, nyumba za watumishi na mabanda vimemegwa na kuingizwa katika viwanja vipya vilivyotengenezwa kwa ajili ya kuuzwa pasipo kujali hawa binadamu wataishi vipi kuanzia sasa. Wakazi waliokuwa wakipakana na barabara ardhi zao zimemegwa kwa mbele kutengeneza viwanja vya kibiashara kwa ajili ya kuuzwa kwa faida kubwa. Haki za kibanadamu wala utu havijaliwi kabisa, kinachozingatiwa ni idadi ya viwanja vinavyoweza kuzalishwa ili Wizara ya Ardhi iweze kutengeneza fedha zaidi kutokana na mauzo ya viwanja hivyo.
Wakati haya yakitendwa na taasisi ya kiserikali, sera za uwezeshaji wananchi kiuchumi kwa kutumia ardhi zilizonadiwa kwa wananchi mwaka 2005 ziko wapi? Je, wanaopaswa kutekeleza sera hizi wako wapi? Hawaoni yanayotendeka? Wengine ni viongozi waandamizi katika chama tawala. Ni nini kinawafanya wakae kimya kuhusu hali hii ya kinyonyaji? Wanaopaswa kusimamia utekelezaji wa sera hizi wako wapi? Ina maana hawasikii malalamiko ya wananchi katika maeneo yao na katika vyombo vya habari? Kama huu ndio mwendo wenyewe ni afadhali ya kukosa sera kuliko kuwa na sera za kuwadanganyia wananchi na kisha kushindwa kuzitekeleza.
hs3.gif

Mwandishi wa makala hii Chrizant Kibogoyo ni mwanaharakatai wa masuala ya ardhi, aliwasaidia sana waathrika wa mradi wa Luguruni kudai haki yao, na sasa yuko bega kwa bega na wakazi wa Kwembe kuhakikisha kuwa unyonyaji unaoendeshwa na watumishi wa Wizara ya Ardhi unakomeshwa ili ardhi waliyo nayo wananchi itumiwe kuwaendeleza kiuchumi. Anapatikana kwa simu 0787-125599/0719-126575 au chrizant.k@gmail.com
 
Hata ya Kigamboni ya maeneo ya watu kuuzwa kwa wageni kwa kisingizio cha mji mpya nayo ni kichekesho,kwa nini hao wawekezaji wasiende kujenga sehemu ya wazi wang'ang'anie sehemu zenye watu,huu ni unyonyaji mwingine.
 
Back
Top Bottom