Wiki ya maajabu kwenye ulimwengu wa soka.

Achraf Hakimi

JF-Expert Member
Mar 3, 2010
875
1,779

Mchezo wa soka ni mchezo wa ajabu sana , maajabu yake ndio yanayoleta msisimko na kuufanya kuwa mchezo unaofuatiliwa na mshabiki wengi kuliko mchezo wowote ule.
Gumzo kubwa kwenye ulimwengu wa soka wiki hii ni michuano ya Copa america pamoja na ile ya kombe la dunia la wanawake .
Kwenye Copa America kabla michuano haijaanza majina makubwa yaliyokuwa yakitajwa ni ya wanaume wanne ambao wanalitikisha anga la soka kwa sasa , Lionel Messi na kikosi chake cha Abiceleste kama wajulikanavyo Argentina, Neymar Da Silva toka kwa Seleccao au vijana wa Samba toka huko Brassilia Brazil, Alexis Sanchez toka kwa Mashetani wekundu wa Marekani ya kusini Chile na Radamel Falcao wa Colombia .

Watu hawa wametajwa sana na walidhaniwa kuwa wataipa michuano hii ladha ya aina yake kutokana na uwezo mkubwa walionao wa kusukuma gozi. Hebu mtazame Messi na kikosi chake cha Argentina ambacho ukimuacha yeye kuna watu kama Gonzalo Higuien,Carlos Tevez, Ezequiel Lavezzi, na kwenye benchi unakuta wachezaji ambao wangeanza kwenye kikosi chochote kile ulimwenguni , watu kama Sergio Kun Aguerro, Javier Pastore, Diego Millito na kadhalika . Argentina walianza michuano hii ambayo inafanyika nyumbani kwao kwa sare ya bao moja kwa moja dhidi ya Bolivia . Kama utakumbuka Bolivia aliifumua Argentina bao sita kwenye michuano ya kufuzu kombe la dunia . Ungeweza kuwasamehe Argentina kwa kusema kuwa wamejitahidi kwa kufananisha na dhahma walilokutana nalo awali . Argentina wakajiuliza na wakaingia kwenye mchezo wa pili dhidi ya Colombia wakatoka sare ya bila kufungana, hapo harufu ya hatari ikaanza kunuka taratibu .

Argentina inawezaje kuvuna pointi mbili tu tena kwenye michuano inayofanyika kwako hasa unapokuwa na kikosi kilichosheheni kila mahala wachezaji toka Real Madrid, Barcelona na Inter Milan vilabu ambavyo huwezi kutengeneza "top 5" ya vilabu bora duniani bila kuvitaja.

Argentina wakajipangusa na kuingia kwenye mchezo wa tatu ambako walikutana na kikosi cha Costa Rica, wakashinda mabao matatu bila, japo Costa Rica hii ilikuwa na watu waliotoka kwenye kikosi cha vijana walio na umri wa miaka chini ya 22. Ndipo ilipopangwa ratiba ya robo fainali ambapo Argentina walijikuta mikononi mwa mahasimu wao wa miaka yote Celeste ya Uruguay. Kwa wanaotazama kwa jicho la mbali zaidi walijua kuwa Argentina wangekiona cha mtema kuni. Sababu kuu ni nidhamu ya hali ya juu ya kiufundi na kimfumo ambayo Uruguay wanacheza nayo wakiwa wameiva chini ya upishi wa Oscar Tabarez .

Tatizo kubwa la Argentina halikuwa ukosefu wachezaji wenye kiwango cha juu, kwani wanao mpaka benchi. Issue kubwa ambayo El Checho aka Sergio Batista bado hajapata muda wa kutosha kuifanyia kazi ni mfumo.
Bado anahitaji muda zaidi kuijenga "chemistry" baina ya watu kama kina Messi na wengineo ambao huko wanakocheza soka la vilabu wanaonekana kufanya vyema kuliko timu za taifa .

Kilichowakuta Argentina walipokutana na Uruguay ni kile kile kilichowahukumu dhidi ya Colombia na dhidi ya Bolivia ila tofauti ni kuwa ile ilikuwa hatua ya makundi na hii ni ya mtoano. Baada ya sare ya 1-1 kwenye dakika 120 Uruguay walishinda kwa matuta ambapo Carlos Tevez, mtu ambaye Sergio Batista ni kama alilazimishwa kumuita kikosini ndio aliyekosa penati. Mwanzoni Tevez hakuwemo kwenye mipango yake kwani maskini ya Mungu El Checho alipanga kukijenga kikosi cha Argentina kicheze kwa kumzunguka Lionel Messi na haishangazi kuona kuwa Argentina waliamka katika mchezo ambao Tevez alianzia benchi na mwisho wa siku Tevez ndio amekuja kuiua Argentina .

Ukitazama unaweza kuutazama huu kama mwanzo wa mwisho wa Tevez kwenye kikosi cha Argentina kwani ameshawahi kusema hapo awali kuwa havutiwi na soka la kimataifa na sasa anaweza kuwa amepata sababu ya ziada ya kustaafu mapema, na huo ndio ukawa mwisho wa hadithi ya Argentina katika michuano waliyoandaa wenyewe .


Wakaja mahasimu wa jadi wa Argentina, ulimwengu mzima unawatambua kwa jina "The Samba Boys" huku wao wakipenda kuitwa Seleccao . Kisa chao hakikuwa tofauti na kile cha Argentina. Brazil waliingia kwenye michuano hii wakitafuta kuweka historia ya kutwaa makombe matatu mfulululizo kwani wamelitwaa Copa America mara mbili zilizopita . "On paper" ni nani angesimama mbele ya Brazili? Labda Argentina pekee kwani wao ndio wanaweza kujivunia nyota wanaoweza kusimama kifua kwa kifua na Wana Samba . Utasema nini mbele ya Neymar dogo ambaye ameingia kwenye michuano hii akiwa na lengo la kuudhihirishia ulimwengu kwanini vilabu takribani vitano vinapigania saini yake, kuna watu kama Paulo Henrique Ganso, Lucas Piazon,Robinho , Douglas Maicon ambaye siku hizi anakaa benchi,Dani Alves ,Julio Cesar na wengineo . Brazil walianza kujiuliza kwa Venezuela na matokeo ya sare ya bila kufungana hayakuwaridhisha wengi nyumbani kwenye fukwe za Sao Paolo na Rio De Janeiro. Brazil waliingia kwenye mchezo wa pili kuvaana na Paraguay. Sare nyingine ambayo Brazil walihitaji bao la dakika ya 89 toka kwa Fred aliyeingia kuchukua nafasi ya Neymar ilizidi kuwachanganya na kwenye mcezo dhidi ya Ecuador kama Argentina kwa mara nyingine waliamka na kumpa Ecuador 4-2 .
Machoni pa wengi Brazil walikuwa wamekata kona muhimu kuelekea barabara ya kuweka historia . Lakini nao walipata wasiwasi ratiba ilipotoka na kuonyesha kuwa wanajikuta mikononi mwa Paraguay ile ile ambayo almanusra iwaumbue . Baada ya dakika 120 shughuli iliamuliwa kwa mikwaju ya penati na hapa Brazil walitengeneza historia nyingine kwani haijawahi kutokea timu inashindwa kufunga penati hata moja lakini Brazil walifanya hivyo huku wakiishia kukilaumu kijisehemu cheupe cha mviringo ambacho walikuwa wakijifanya kimewapotezea "timing" za kupiga penati zao kiustadi na wakajikuta waliacha kombe la watu .Kwa wale mashabiki wa soka kama mchezo wataona ajabu lakini maandishi ya hatari yalishaonekana ukutani mwa Brazili tangu mwanzoni .
Hakuna Chemistry na hakuna mipango. Brazil wameshindwa kuzisoma alama za nyakati kama wenzao wa Argentina na kisa chao kikaishia hapo .
Mwanzoni uliona jina la mtu mmoja anayefahamika kama Radamel Falcao. Huyu ni tmu ambaye ndani ya misimu miwili kwenye klabu yake ya Fc Porto ameweza kufunga mabao zaidi ya 70 na kuipa Porto mafanikio ya hatari . Falcao hadi kufikia hatua ya robo fainali alikuwa kashauona wavu mara mbili na kwa nyota wote waliotarajiwa kung'aa ni yeye peke yake ambaye alionyesha ishara za kuwa na kile alichotegemewa kuwa nacho .


Peleka mkanda mbele na Colombia akajikuta kwenye anga za Peru ambao maskini waliingia kwenye michuano hii huku mchezaji wao bora Claudio Pizzaro akiwa jukwaani na si Uwanjani kupigana na wenzie .
Kisa cha Colombia na Peru wala hakikuwa kirefu kama vile vya Brazil na Argentina. Falcao alikosa penati ndani ya dakika 90 na mchezo uligeuka kichwa chini miguu juu wakati wa dakika za nyongeza ambapo Peru waliushangaza ulimwengu kwa kumpa Colombia 2-0 na hapo Kina Falcao na Hugo Rodalega wakajikuta wakikata tiketi mapema na kwenda kucheza soka ufukweni ambako mtu ukishinda huvishwi medali.


Mashetani wekundu wa Chile wakiwa wanachagizwa na Cristiano Ronaldo wa amerika ya kusini na ligi ya Serie A Alexis Sanchez. Baada ya kuwashuhudia kina Brazil, Argentina na Colombia wakiangukia pua dunia nzima ilidhani Chile ndio Bingwa kabla hata ya kufika fainali . Hata baada ya maajabu yote haya ni nani angethubutu kupinga na kuweka rehani fedha zake kwa upande wa Venezuela , wana beki gani ya kumzuia Sanchez? Jibu la swali hili ni jina refu la Osvaldo Vizcarrondo. Huyu ni beki wa kati mwenye roho mbaya ambaye si tu alikuwa kamanda wa meli ya Venezuela bali alipanda mbele kama farasi dume na kuipa timu yake bao la kuongoza, japo nyota mwingine wa Chile Humberto Suazo alisawazisha lakini Gabriel Cichero alikuwa na mawazo mengine na mwishowe ilikuwa kwikwi kwa Alexis Sanchez na Chile .



Ukiachana na Copa America kuna fainali za kombe la dunia la wanawake . Fainali hizi zimetokea kuwa na mvuto wa aina yake kwa mashabiki wa soka ulimwenguni kote .
Fainali iliwakutanisha watu ambao wamestahili kufika pale . Marekani ambao kwa muda mrefu ni wababe wa soka la wanawake na Japan ambao hii ni mara yao ya kwanza kufika kwenye michuano achilia mbali fainali . Mwisho wa siku soka lilichezwa na hakika lilikuwa la kuvutia na hakuna liyekuwa tayari kufa kiurahisi na baada ya dakika 120 matokeo yalikuwa sare ya 2-2 huku kila mmoja akiwa na silaha za hatari , marekani wakiwa na shujaa wao Abby Wambach,Alex Morgan na mwanadada ambaye amesimama imara langoni mwao Hope Solo huku Japan wakiwa na silaha ambazo kwao kimo si tija ila mapambano ndio hasa siri yao wakiongozwa na nahodha Hamare Sawa na mfungaji mahiri Aya Miyama. Japan walitimiza ule msemo wa kingereza usemao "I came , I saw , I conquered" na hakika wamefanikiwa kui-conquer dunia nzima kama walivyoiteka kwa hisia za huzuni wakati walipokumbwa na matetemeko ya ardhi baharini Tsunami miezi michache iliyopita . Kusema kweli baada ya kukumbwa na janga lile watu wa Japan walikuwa wanahitaji kupata faraja ya ukweli na haki ilitendeka kwa kuifunga Marekani kwa mikwaju ya penati

Mwisho wa siku kuna mengi ambayo soka linaondoka nayo kama mafunzo , mchezo huu unaenda ukibadilika na hakika Brazil na Argentina wameshindwa kusoma alama za nyakati
na kutambua kuwa mchezo wa leo si ule wa miaka ile . Hakuna aliye tayari kufa kirahisi eti tu kisa anacheza na mtu ambaye ametoka kuipa Barcelona ubingwa wa ulaya , hakuna aliye tayari kukubali kufungwa eti kisa anamkaba mtu ambaye anatakiwa timu kubwa ulaya , watu wanapaki basi na kama una ubavu basi fanya yale aliyofanya Maradona kwa England mwaka 1986 , hapo sawa lakini sio miaka ya leo.

source: shaffih.blogspot
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom