Rutashubanyuma
JF-Expert Member
- Sep 24, 2010
- 219,470
- 911,173
Waziri Nundu aipa Sumatra siku 7 kuitema Majembe
Imeandikwa na Mwandishi Wetu; Tarehe: 24th December 2010 @ 23:30
KILIO cha Wamiliki wa mabasi yanayofanya safari zake jijini Dar es Salaam na yale yaendayo mikoani, kimesikika na sasa serikali imeiamuru Mamlaka ya Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (SUMATRA) kusitisha haraka mkataba wake na kampuni ya udalali ya Majembe.
Amri hiyo ya serikali ilitolewa jana na Waziri wa Uchukuzi, Omar Nundu aliyeagiza amri hiyo kutekelezwa ndani ya siku saba, akitaja kuwa ni njia mojawapo ya kutekeleza mpango wa kuondoa matatizo ya usafirishaji wa abiria.
Nundu alitoa agizo hilo jijini Dar es Salaam wakati alipokuwa anatoa taarifa ya majibu na mapendekezo ya utekelezaji wa hoja 14 zilizowasilishwa na Chama cha Wamiliki wa Mabasi Tanzania (TABOA) na Chama cha Wamiliki wa Daladala (DARCOBOA).
Alisema Kampuni ya Majembe Auction Mart imekuwa ikifanya kazi za askari wa usalama wa barabarani kinyume cha sheria kwa kukagua matairi, kuangalia leseni ya barabara, bima, taa za magari na vioo wakati hawana ujuzi wala mamlaka ya kufanya hivyo kisheria.
Ili kuondokana na kero hiyo Sumatra wameagizwa kusitisha mkataba wake na Majembe ifikapo Desemba 31 mwaka huu, alisema Nundu.
Nundu alisema wizara yake imepitia kwa makini hoja zote 14 ambapo hoja nne zitaendelea kufanyiwa kazi kwa kina, hoja tatu zimekataliwa na hoja saba zimeanza kutekelezwa kwa kuzingatia maagizo yanayotolewa na Wizara.
Katika maagizo hayo, Majembe imezuiwa kusimamia ukaguzi wa madaraja ya mabasi na kwamba kuanzia Desemba 9, mwaka huu kazi hiyo imekuwa ikifanywa na Sumatra.
Agizo lingine lililotolewa na wizara na kutakiwa kutekelezwa mara moja ni Sumatra kuacha kutoa lugha chafu kwa Taboa na mamlaka zinazohusika kuwaondoa wapiga debe katika vituo vyote vya mabasi nchini.
Nundu ameagiza wafanyakazi na wakala wa mabasi kupewa vitambulisho maalumu na ifikapo Januari 15 mwaka kesho, mamlaka zinazohusika ziwe zimeandaa utaratibu wa kuwatambua wafanyakazi na wakala wa makampuni ya mabasi ili kudhibiti wapiga debe.
Pia Sumatra imetakiwa kukutana na wamiliki wa mabasi kujadili ongezeko la nauli kisha hoja hiyo ipelekwe kwenye kikao cha wadau na ikiwezekana jambo hilo liwe limefanyika ifikapo Januari 31, 2011.
Waziri Nundu alisema hoja zinazoendelea kufanyiwa utafiti kabla ya kutolewa maamuzi ni kuhusu vibali vya kukokota mabasi yanayoharibika, maombi ya kutaka mabasi kuwa bidhaa za mtaji na kulegeza masharti ya leseni na ratiba za mabasi ili gari linaloharibika iwe rahisi kutuma basi jingine kuchukua abiria badala ya kusubiri basi lililoharibika litengenezwe.
Maombi mengine yatakayopitiwa kwa makini kabla ya Serikali kutoa maamuzi ni pamoja na mabasi kuruhusiwa kufanya safari kwa saa 24, yaani na usiku na mchana, kufuta utaratibu wa mabasi kupitia kwenye stendi za mabasi hata kama hakuna abiria anayeshuka wala kupanda ili mabasi hayo yalipe ushuru, na suala la wageni kujihusisha na usafirishaji abiria nchini, ni jambo ambalo linaonekana tishio la kibiashara kwa Taboa.
Nundu alisema maombi ya Taboa kutaka mabasi ya abiria kutopimwa kwenye mizani hayakubaliki kwa kuwa upo uthibitisho kwamba baadhi ya mabasi yamekuwa yakizidisha uzito.
Akijibu hoja ya kuondoa matuta barabarani, Nundu alisema pamoja na kero zinazosababishwa na matuta hayo yataendelea kuwepo ili kuhakikisha madereva wanapunguza mwendo wanapopaswa kufanya hivyo.
Hata hivyo, Wizara ya Uchukuzi kwa kushirikiana na Wizara ya Ujenzi zitachukua hatua mwafaka za kuhakikisha kuwa ujenzi wa matuta barabarani unafuata viwango pamoja na kuweka alama zinazoonesha kuwepo kwa matuta hayo.
Pia Serikali imetupilia mbali malalamiko ya Taboa dhidi ya Sumatra ya kushirikisha katika vikao wajumbe ambao sio wasafirishaji na kueleza kuwa upo umuhimu wa kuendelea na mikutano inayoshirikisha watoa huduma ya usafiri na walaji.
Ndulu alisema anaishukuru Taboa kwa kusitisha mgomo wao na kukubaliana na majibu pia mpango wa utekeleza ji wa kuondoa matatizo ya usafirishaji na kuahidi kuwa Wizara yake itaendelea kufuatilia kwa kina utekelezaji huo ili kuboresha huduma ya usafirishaji.