Waziri amfagilia Pinda, awaponda walafi

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797
WAZIRI wa Maliasili na Utalii, Ezekiel Maige, amewataka viongozi wa serikali na wananchi kufuata nyayo za Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kwa kumiliki ardhi ndogo na kuiendeleza na si kujilimbikizia ardhi. Maige alitoa changamoto hiyo mjini hapa jana, wakati alipotembelea nyumbani kwa Waziri Mkuu katika Kijiji cha Kibaoni na kukutana na wazazi wake na kisha kutembelea shamba lake lenye ukubwa wa ekari 170, huku ekari 80 zikiwa zimelimwa mahindi na nyingine zikitumika kwa ajili ya ufugaji wa samaki na nyuki. Alisema baadhi ya viongozi na wananchi wamekuwa wakijilimbikizia ardhi kubwa, huku ikikaa kwa muda mrefu bila kutumika kwa kitu chochote kile, huku wananchi wengine wakiwemo wafugaji wakiwa hawana ardhi kabisa.

Alisema kutokana na wadhifa alionao Waziri Mkuu alikuwa na uwezo wa kuhodhi na kujilimbikizia ardhi kubwa, lakini kutokana na uongozi wake bora na wa kuonesha mfano, anayo ardhi ndogo ambayo ana uwezo wa kuiendeleza. Alibainisha kuwa kuna baadhi ya viongozi na watu mbalimbali wenye uwezo wa kifedha katika maeneo mbalimbali, ikiwemo Dar es Salaam na Kisarawe, wamekuwa wakimiliki ardhi kubwa hadi hekta 5,000, huku wakishindwa kuiendeleza.

"Mimi nafikiri sasa muda umefika wananchi tujifunze kutoka kwa viongozi wetu, kama unamiliki eneo, basi uwe na eneo unaloweza kulitumia.
"Hekta 5,000 kwa kiongozi au mwananchi aliyepo Dar es Salaam….linakaa bila kutumiwa, ni matumizi mabaya ya uwezo wetu wa kifedha, na ni matumizi mabaya ya nafasi zetu za uongozi… sasa wote tujifunze tuwe na maeneo madogo au hata ekari 200 unazoweza kuzitumia,"alisema.

Alisema ni vema wananchi wakamuiga Waziri Mkuu kwa vitendo katika suala zima la kilimo, kwa kutumia ardhi yao kulima kilimo chenye tija, ili waweze kuvuna mazao yanayolingana na ukubwa wa shamba, badala ya kuwa na ardhi kubwa na kukaa bila kuiendeleza.

Alifafanua kuwa kutokana na watu kuhodhi na kujilimbikizia ardhi, baadhi ya wafugaji, wamekuwa wakikosa sehemu ya malisho ya mifugo yao na kusababisha kuvamia maeneo ya hifadhi, misitu na mapori ya akiba na kuharibu mazingira.
 
Back
Top Bottom